Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumtukuza Mungu Katika Milima ya Filipino

Kumtukuza Mungu Katika Milima ya Filipino

Kumtukuza Mungu Katika Milima ya Filipino

Hujakosea kufikiri kwamba Filipino ni nchi yenye visiwa. Lakini Filipino pia ni nchi yenye milima inayovutia. Mashahidi wa Yehova wamehubiri kwa urahisi katika miji na sehemu za nyanda za chini na kupata matokeo. Hata hivyo, hali ni tofauti katika maeneo ya milimani.

MILIMA yenye kuvutia inatofautiana sana na fuo za mchanga, matumbawe, vijiji vya kuvua samaki, na miji yenye pilikapilika iliyo kwenye nyanda za kisiwa hicho. Ni vigumu pia kuhubiri “habari njema” za Ufalme wa Mungu kwenye milima hiyo.—Mathayo 24:14.

Visiwa vya Filipino viko mahali ambapo mabamba yaliyo kwenye tabaka la nje la dunia hukutana. Kuporomoka kwa ardhi katika eneo hili kumetokeza milima yenye miinuko mikali kwenye visiwa vikubwa zaidi. Zaidi ya visiwa 7,100 vinavyofanyiza nchi ya Filipino viko kwenye tao la magharibi mwa Eneo la Volkeno la Pasifiki. Kwa hiyo visiwa hivyo vina volkeno ambayo huchangia pia kuwepo kwa mandhari ya milima-milima. Ardhi hiyo yenye mawemawe inawatenganisha watu wa milimani. Ni vigumu kuwafikia watu hao kwa sababu kuna barabara chache sana za magari.

Licha ya vizuizi hivyo, Mashahidi wa Yehova wanaona uhitaji wa kufikia “watu wa namna zote.” (1 Timotheo 2:4) Kwa hiyo, Mashahidi nchini Filipino wamefanya kazi kupatana na andiko la Isaya 42:11, 12: “Na waimbe wenyeji wa Sela, wapige kelele toka vilele vya milima. Na wamtukuze BWANA, na kutangaza sifa zake visiwani.”

Jitihada kali ya kuhubiria watu wanaokaa milimani zilianza miaka zaidi ya 50 iliyopita. Baada ya Vita ya Pili ya Ulimwengu, mishonari walisaidia kusongeza mbele kazi hiyo. Wenyeji wengi walikubali kweli ya Biblia, kisha wakasaidia kueneza kweli hiyo katika vijiji vilivyo juu ya milima. Kazi hiyo ikawa na matokeo mazuri. Kwa mfano, kuna watangazaji wa habari njema zaidi ya 6,000 katika milima ya Cordillera Central iliyo kaskazini mwa Luzon. Wengi wao ni wenyeji na wanatia ndani Waibaloi, Waifugao, na Wakalinga.

Hata hivyo, bado kuna maeneo fulani ya milimani ambayo hayafikiki kwa urahisi. Watu wanaoishi huko hawajasahaulika. Baadhi yao wamefikiwaje, nao wameitikiaje?

Imani Halisi Yachukua Mahali pa Mapokeo

Kwenye kisiwa cha kaskazini cha Luzon, maeneo ya mlimani ya mkoa wa Abra yanakaliwa na Watinggi. Huenda neno hilo lilitokana na neno la zamani la Kimalay tinggi, linalomaanisha “mlima.” Neno hilo linafaa kwelikweli! Watu hao hujiita Itneg na lugha yao inaitwa vivyo hivyo. Wanaamini mungu aitwaye Kabunian, nao ni washirikina sana. Kwa mfano, ikiwa mtu anayepanga kwenda mahali fulani anapiga chafya, hiyo ni dalili ya kupatwa na mabaya. Lazima asubiri kwa muda wa saa kadhaa ili hali hiyo isimletee balaa.

Mnamo mwaka wa 1572, Wahispania walileta Ukatoliki, lakini hawakuwafundisha Watinggi Ukristo wa kweli. Wale waliokubali kuwa Wakatoliki waliendelea kumwamini mungu Kabunian na kufuata desturi zao. Watu hao walipata ujuzi sahihi wa Biblia kwa mara ya kwanza katika miaka ya 1930 wakati Mashahidi wa Yehova walipoanza kueneza ujumbe wa Ufalme katika milima hiyo. Tangu wakati huo, Watinggi wengi wameanza kumtukuza Yehova “toka vilele vya milima.”

Kwa mfano, Lingbaoan alikuwa kiongozi wa kabila hilo aliyeheshimiwa sana. Alijishughulisha sana na utamaduni wa Watinggi. “Nilifuata mapokeo ya Watinggi kwa dhati. Mtu alipouawa, tulicheza dansi baada ya maziko, na kupiga kengele. Pia tulitoa dhabihu za wanyama. Tuliamini mungu Kabunian, nami sikumjua Mungu wa Biblia.” Alifanya mambo hayo yote licha ya kwamba alijiona kuwa Mkatoliki.

Walipokuwa wakihubiri eneo hilo, Mashahidi wa Yehova walikutana na Lingbaoan na wakamtia moyo asome Biblia. Akumbuka hivi: “Biblia ndiyo iliyonisadikisha kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.” Baadaye, Lingbaoan alijifunza Biblia na Shahidi mmoja, naye akaamua kumtumikia Mungu wa kweli. Aliacha mazoea yake ya zamani, kutia ndani cheo chake akiwa kiongozi wa kabila, jambo lililowakasirisha marafiki wake wa zamani na kasisi wa eneo hilo. Hata hivyo, Lingbaoan alikuwa ameazimia kufuata kweli aliyopata katika Biblia. Sasa anatumikia akiwa mzee wa kutaniko.

Safari ya Siku Saba

Ijapokuwa sasa habari njema zinahubiriwa kwa ukawaida katika sehemu fulani za Abra, sehemu nyingine ziko mbali sana kwa hiyo zinahubiriwa mara chache sana. Wakati fulani uliopita, jitihada ilifanywa kufika katika mojawapo ya sehemu hizo. Kikundi cha Mashahidi 35 walifunga safari kwenda kuhubiri eneo lisilogawiwa mtu huko Tineg, Abra, ambalo halikuwa limetembelewa kwa muda wa miaka 27.

Walisafiri kwa miguu, kwenda kuhubiri na safari hiyo ilichukua muda unaozidi siku saba. Hebu wazia kuvuka daraja zinazoning’inia na mito yenye kina kirefu na kutembea kwa saa nyingi kwenye milima ukiwa umebeba vifaa vyako—ili tu kuwahubiria habari njema watu ambao hawahubiriwi kwa ukawaida! Wakati wa safari hiyo ya siku saba, tulilala nje siku nne.

Ijapokuwa Mashahidi hao wajasiri waliofunga safari hiyo walibeba chakula, hawangeweza kubeba chakula cha kuwatosha safari nzima. Hata hivyo, hakukuwa na tatizo lolote kwa sababu watu wa eneo hilo walifurahi sana kubadilisha chakula na vichapo vinavyotegemea Biblia. Mashahidi walipewa vyakula vingi sana vya shambani, samaki, na nyama ya mbawala. Ijapokuwa kulikuwa na magumu fulani, kikundi hicho kilisema: “Kujidhabihu kwetu kulithawabishwa na shangwe nyingi tuliyopata.”

Katika siku hizo saba, wahudumu hao walihubiri katika vijiji kumi, wakawaachia watu vitabu 60, magazeti 186, broshua 50 na trakti nyingi. Walianzisha mafunzo ya Biblia na vikundi 74. Katika mji wa Tineg, maofisa wa mji huo pamoja na raia fulani mashuhuri waliomba kuwe na mkutano wa kutaniko. Mkutano huo ulihudhuriwa na watu 78. Wengi waliohudhuria walikuwa walimu na polisi. Tunatumaini kwamba Watinggi wengi watajiunga na wale ‘wanaopiga kelele’ na kumsifu Yehova toka vilele vya milima.

Kitu Kilicho Bora Kuliko Dhahabu

Wahispania walipata dhahabu katika visiwa vilivyoko kusini ya Filipino. Visiwa hivyo viliitwa Mindoro, ufupisho wa neno la Kihispania mina de oro, au “mgodi wa dhahabu.” Hata hivyo, kitu kilicho bora kuliko dhahabu sasa kinapatikana katika visiwa hivyo—watu wanaotaka kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova.

Wenyeji wapatao 125,000 wanaoitwa Wamangya huishi kwenye msitu ulio sehemu za ndani-ndani za eneo la Mindoro. Wanaishi maisha sahili, hawashirikiani sana na watu wengine, na wana lugha yao. Wengi wao huabudu uumbaji na miungu mingi, nao huamini kwamba kuna viumbe wa roho katika mimea, wanyama, na vitu vya asili.

Wanapokosa chakula au vitu vingine, mara kwa mara Wamangya huenda kwenye maeneo ya pwani kutafuta kazi. Pailing, anayetoka katika kikundi kidogo cha Wamangya wanaoitwa Wabatanga alienda kutafuta kazi pwani. Alikulia miongoni mwa watu wa kwao katika misitu iliyo milimani, naye aliamini desturi na mazoea ya Wabatanga. Alijifunga shuka ambayo ndiyo vazi la kawaida la Wabatanga. Ili kupata mazao ya kutosha, Wabatanga waliamini kwamba lazima waue kuku, na kuacha damu itonetone kwenye maji wanaposali.

Pailing haamini tena mapokeo hayo. Kwa nini? Alipoenda kwenye nyanda za chini, aliajiriwa kazi na familia za Mashahidi wa Yehova. Mojawapo ya familia hizo iliamua kumweleza Pailing kweli ya Biblia. Aliitikia vizuri na kutambua umuhimu wa kujifunza makusudi ya Yehova kwa mwanadamu na dunia. Walimpeleka katika shule ya msingi na vilevile kumfunza Biblia. Pailing alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova akiwa na umri wa miaka 24. Alikuwa na umri wa miaka 30 akiwa katika kidato cha pili. Alifanya shule kuwa eneo lake la kuhubiri. Sasa wanamwita Rolando (jina la watu wa nyanda za chini).

Sasa Rolando ni mhubiri wa wakati wote aliye nadhifu na mwenye furaha. Anatumikia akiwa mtumishi wa huduma katika mojawapo ya makutaniko ya Mindoro. Hivi karibuni Rolando alirudi milimani, si kujiunga na Wabatanga katika desturi zao, bali kuwaeleza kweli za Biblia zenye kuokoa uhai.

Wanatamani Kupata Jumba la Ufalme

Mkoa wa Bukidnon—yaani, “Watu wa Milimani” huko Cebuano—uko kusini mwa kisiwa cha Mindanao. Eneo hilo lina milima, makorongo, mabonde yenye mito, na nyanda za juu. Ardhi hiyo yenye rutuba inafaa sana kwa kilimo cha mananasi, mahindi, kahawa, mpunga, na ndizi. Makabila ya milimani ya Watalaandigi na Wahigaoni huishi huko. Watu hao pia wanahitaji kufundishwa kuhusu Yehova. Hivi karibuni, fursa hiyo ilijitokeza kwa njia yenye kupendeza karibu na mji wa Talakag.

Mashahidi waliokwea milima hiyo walipata halihewa yenye baridi lakini walikaribishwa kwa uchangamfu. Wenyeji walidai kwamba wanamwamini Baba, Mungu mweza yote, lakini hawakujua jina lake. Kwa kuwa wanaishi msituni, hiyo ilikuwa mara yao ya kwanza kukutana na Mashahidi wa Yehova. Walielezwa jina la Mungu na vilevile kusudi lake zuri kuhusiana na Ufalme. Watu hao walifurahi sana, kwa hiyo ikaamuliwa kwamba ziara zaidi zifanywe katika kijiji chao.

Ziara kadhaa zilifanywa. Kufuatia ziara hizo, wenyeji walitoa uwanja wa kujenga “nyumba” ya Mashahidi wa Yehova. Mashahidi walikubali uwanja huo kwa furaha. Uwanja huo ulikuwa juu ya kilima kirefu zaidi katika eneo hilo, upande wa pili wa barabara. Jengo hilo lilijengwa kwa mbao, mianzi, na majani ya mchikichi. Ilichukua muda wa miezi mitatu na siku kumi kulikamilisha. Kibao kilichoandikwa “Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova” kilionekana waziwazi mbele ya jengo hilo. Hebu wazia, Jumba la Ufalme lililojengwa kabla kutaniko halijaanzishwa!

Tangu wakati huo, mzee mmoja wa kutaniko ambaye ni mhudumu wa wakati wote, pamoja na mtumishi wa huduma, wamehamia huko. Wakiwa na Mashahidi kutoka maeneo jirani, waliweka mradi wa kuanzisha kutaniko. Walitimiza mradi huo mnamo Agosti 1998. Sasa kutaniko dogo linatumia kikamili Jumba hilo la Ufalme kusaidia watu wa milimani wajifunze kweli za Biblia.

Kwa kweli, Yehova amewatumia sana watumishi wake waliojitoa ambao wanaishi Filipino kueneza kweli ya Ufalme hata katika maeneo ya milimani ambayo si rahisi kufikika. Tunakumbushwa maneno ya andiko la Isaya 52:7, linalosema: “Jinsi ilivyo mizuri juu ya milima miguu yake aletaye habari njema.”

[Ramani katika ukurasa wa  11]

 

ABRA

MINDORO

BUKIDNON

[Hisani]

Dunia: Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wanaohubiri maeneo ya milimani hutumia muda wa saa nyingi kukwea milima yenye mawemawe

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kubatizwa katika kijito cha mlimani