Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Makasisi Wawili Waliothamini Vitabu vya Russell

Makasisi Wawili Waliothamini Vitabu vya Russell

Makasisi Wawili Waliothamini Vitabu vya Russell

KATIKA mwaka wa 1891, Charles Taze Russell, aliyefanya kazi kubwa sana miongoni mwa waabudu wa kweli wa Yehova, alizuru Ulaya kwa mara ya kwanza. Kulingana na ripoti fulani, alipofika Pinerolo, Italia, Russell alikutana na Profesa Daniele Rivoire, aliyekuwa kasisi wa dini ya Wawaldo. * Ingawa Rivoire aliendelea kushirikiana kwa ukaribu na Wawaldo baada ya kuacha ukasisi, alikuwa tayari kujifunza mambo mapya na alisoma vichapo vingi vilivyoandikwa na C. T. Russell.

Katika mwaka wa 1903, Rivoire alitafsiri kitabu cha Russell The Divine Plan of the Ages katika Kiitalia na kulipia gharama za uchapishaji. Hii ilikuwa kabla Mashahidi wa Yehova hawajachapisha kitabu hicho katika Kiitalia. Katika dibaji ya kitabu hicho, Rivoire aliandika hivi: “Twaacha tafsiri hii ya kwanza ya Kiitalia chini ya ulinzi wa Bwana. Na aibariki licha ya makosa yaliyomo ili ichangie kutukuzwa kwa jina lake lililo takatifu sana na kufanya watoto wake wanaozungumza Kiitalia wajitoe kabisa kwa Mungu. Wote ambao kwa kusoma kitabu hiki wanathamini kina cha utajiri, hekima, na ujuzi wa mipango na upendo wa Mungu, na wachochewe kumshukuru Mungu mwenyewe ambaye kupitia wema wake amewezesha kuchapishwa kwa kichapo hiki.”

Rivoire pia alianza kutafsiri gazeti Zion’s Watchtower and Herald of Christ’s Presence katika Kiitalia. Gazeti hilo ambalo lilikuja kuitwa Mnara wa Mlinzi, lilichapishwa mara nne mwaka wa 1903. Hata ingawa Profesa Rivoire hakupata kuwa Mwanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, alipendezwa sana kueneza ujumbe wa Biblia kama ulivyoelezwa katika vichapo vya Wanafunzi wa Biblia.

“Ilionekana Kama Magamba Yameanguka Kutoka kwa Macho Yangu”

Kasisi mwingine wa Wawaldo aliyethamini vichapo vya Russell alikuwa Giuseppe Banchetti. Giuseppe alifundishwa mafundisho ya Wawaldo na babake aliyeacha Ukatoliki. Mwaka wa 1894, Giuseppe akawa kasisi na akahudumia jumuiya kadhaa za Wawaldo huko Apulia na Abruzzi na katika visiwa vya Elba na Sicily.

Mashahidi wa Yehova walichapisha kitabu cha Russell, Divine Plan of the Ages, katika Kiitalia mwaka wa 1905. Banchetti aliandika maoni yenye kusisimua kuhusu kitabu hicho. Maoni yake yalichapishwa katika jarida la Waprotestanti La Rivista Cristiana. Banchetti aliandika: ‘Kwa upande wetu, kitabu cha Russell ndiyo njia nyangavu na hakika zaidi ya kuongoza Mkristo yeyote kujifunza Maandiko Matakatifu kwa njia yenye kunufaisha na kuthawabisha. Punde tu baada ya kukisoma, ilionekana kana kwamba magamba yameanguka kutoka kwa macho yangu, na kwamba njia ya kumjua Mungu ilikuwa imenyooka zaidi na kuwa rahisi zaidi. Hata sikuona mambo ambayo hapo awali yalionekana kuwa yanapingana. Mafundisho ambayo hapo awali yalionekana kuwa magumu kueleweka yalionekana rahisi na yenye kukubalika kabisa. Mambo ambayo hayakueleweka hapo awali yakawa wazi zaidi. Nilielewa kwa urahisi mpango wenye kuvutia sana wa kuokoa ulimwengu kupitia Kristo hivi kwamba nilichochewa kusema maneno haya ya Mtume: Lo! kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi!’—Waroma 11:33.

Kama Remigio Cuminetti alivyotaja katika mwaka wa 1925, Banchetti alionyesha “anakubaliana kabisa” na vitabu vya Wanafunzi wa Biblia na “alisadiki kabisa” mafundisho yaliyofafanuliwa na wanafunzi hao. Pia Banchetti alijitahidi sana kujulisha watu mafundisho hayo.

Maandishi ya Banchetti yanaonyesha wazi kwamba yeye aliamini mafundisho ya Biblia kwamba kutakuwa na ufufuo hapa duniani sawa na wanavyoamini Mashahidi wa Yehova. Pia alikubaliana na Wanafunzi wa Biblia alipoeleza kwamba Mungu alikuwa ameweka na kufunua mwaka ambao Yesu angekufa katika unabii wa Danieli wa yale majuma 70. (Danieli 9:24-27) Alipinga mafundisho ya kanisa lake mara kadhaa na aliamini kwamba Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo wapaswa kuadhimishwa mara moja tu kwa mwaka, “tarehe ileile ambayo alikufa.” (Luka 22:19, 20) Alikataa nadharia ya mageuzi ya Darwin, na kusisitiza kwamba Wakristo wa kweli hawapaswi kwenda vitani.—Isaya 2:4.

Pindi moja, Banchetti alikuwa akizungumza na mtu fulani anayeitwa J. Campbell Wall kuhusu vitabu vya Russell. Akijibu uchambuzi wa Wall, Banchetti alisema: “Nina hakika kwamba ukisoma mabuku sita ya Russell, utapata shangwe nyingi, nawe utanishukuru sana. Mimi sijionyeshi kuwa nafahamu sana mafundisho; lakini nilisoma vitabu hivyo miaka kumi na moja iliyopita, nami namshukuru Mungu kila siku kwa kuniangazia nuru hiyo na kunipa faraja hiyo kupitia vitabu ambavyo vinategemea kabisa Maandiko Matakatifu.”

“Sikilizeni, Sikilizeni, Sikilizeni”

Ni jambo la maana sana kwamba makasisi hao wawili Wawaldo—Daniele Rivoire na Giuseppe Banchetti—walikubaliana na jinsi Russell alivyoieleza Biblia. Banchetti aliandika hivi: “Nasema kwamba hakuna mmoja kati yetu sisi Waevanjeli, hata makasisi wetu, au maprofesa wa theolojia anayejua kila kitu. Tuna mambo mengi sana ya kujifunza. . . . [Twapaswa] . . . kutulia na kusikiliza, bila kufikiri tunajua kila kitu, na tusikatae kuchunguza mambo tunayohitaji kuchunguza. Badala yake, sikilizeni, sikilizeni, sikilizeni.”

Kila mwaka, maelfu husikiliza ujumbe wa Ufalme wanaopelekewa nyumbani kwao na Mashahidi wa Yehova. Kila mahali, watu wenye kiu ya Biblia na ambao wako tayari kukubali maoni mapya, wanakubali mwaliko wa Yesu: “Uje uwe mfuasi wangu.”—Marko 10:17-21; Ufunuo 22:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Wawaldo walipewa jina la Pierre Vaudès, au Peter Waldo, mfanyabiashara wa karne ya 12 aliyeishi Lyons, Ufaransa. Waldo alitengwa na ushirika wa Kanisa Katoliki kwa sababu ya imani yake. Kwa habari zaidi kuhusu Wawaldo, ona makala “Wawaldo—Waacha Uzushi na Kuwa Waprotestanti” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 2002.

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 28]

Profesa Daniele Rivoire

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 29]

Giuseppe Banchetti

[Hisani]

Banchetti: La Luce, April 14, 1926