Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, inafaa kusali kwa Mungu bila kutumia usemi “katika jina la Yesu”?

Biblia huonyesha kwamba Wakristo wanaotaka kusali kwa Yehova wanapaswa kufanya hivyo katika jina la Yesu. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Hakuna ajaye kwa Baba ila kupitia mimi.” Aliongeza kusema: “Lolote lile mwombalo katika jina langu, hakika nitalifanya, ili Baba apate kutukuzwa kuhusiana na Mwana. Mkiomba jambo lolote katika jina langu, hakika nitalifanya.”—Yohana 14:6, 13, 14.

Kikirejezea cheo cha pekee cha Yesu, kichapo Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature chasema hivi: “Sala zapaswa kutolewa kwa Mungu peke yake, kupitia kwa Mpatanishi Yesu Kristo. Kwa hiyo, sala zozote zinazotolewa kwa watakatifu au malaika hazifai na ni zenye kukufuru. Kuabudu kiumbe yeyote hata awe wa hali ya juu kadiri gani, ni ibada ya sanamu, nayo inakatazwa kabisa katika sheria takatifu ya Mungu.”

Itakuwaje ikiwa baada ya kupata jambo lenye kupendeza, mtu achochewa kusema, “Asante Yehova” bila kuongezea “katika jina la Yesu”? Je, ingekuwa vibaya kufanya hivyo? Sivyo. Namna gani Mkristo akikabili hatari kwa ghafula na apaaze sauti: “Yehova nisaidie!” Mungu hatakataa kumsaidia mtumishi wake kwa sababu tu hakusema “katika jina la Yesu.”

Hata hivyo, twapaswa kutambua kwamba kuzungumza tu na Mungu kwa sauti kubwa hakumaanishi unasali kwake. Kwa mfano, baada ya kuhukumiwa na Yehova kwa kumwua ndugu yake Abeli, Kaini alisema: “Adhabu yangu imenikulia kubwa, haichukuliki. Tazama umenifukuza leo katika uso wa ardhi, nitasitirika mbali na uso wako, nami nitakuwa mtoro na mtu asiye na kikao duniani; hata itakuwa kila anionaye ataniua.” (Mwanzo 4:13, 14) Ingawa Kaini alikuwa akizungumza na Yehova, alikuwa akilalamika kwa hasira kwa sababu ya matokeo mabaya ya dhambi.

Biblia hutuambia: “Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili isiyostahiliwa.” Bila shaka tunakosa unyenyekevu tunapozungumza na Aliye Juu Zaidi kwa njia isiyo rasmi kana kwamba yeye ni mwanadamu. (Yakobo 4:6; Zaburi 47:2; Ufunuo 14:7) Pia lingekuwa jambo lisilo la heshima kujua yale ambayo Neno la Mungu husema kuhusu daraka la Yesu, kisha kukataa kimakusudi kutaja jina la Yesu Kristo katika sala.—Luka 1:32, 33.

Hii haimaanishi kwamba Yehova anatarajia tusali kwa njia fulani maalum. Jambo kuu ni hali ya mtu ya moyoni. (1 Samweli 16:7) Katika karne ya kwanza W.K., Kornelio, ofisa wa jeshi la Roma ‘aliomba dua kwa Mungu kwa kuendelea.’ Kornelio, mtu asiye Myahudi na asiyetahiriwa, hakuwa amejiweka wakfu kwa Yehova. Ingawa yaelekea hakutoa sala zake katika jina la Yesu, sala zake ‘zilipaa kama ukumbuko mbele ya Mungu.’ Kwa nini? Kwa kuwa “mchunguzaji wa moyo,” aliona kwamba Kornelio alikuwa “mtu mstahifu na mwenye kumhofu Mungu.” (Matendo 10:2, 4; Mithali 17:3, NW) Baada ya kupata ujuzi kuhusu “Yesu aliyekuwa ametoka Nazareti,” Kornelio alipokea roho takatifu na kuwa mwanafunzi aliyebatizwa wa Yesu.—Matendo 10:30-48.

Hatimaye, Mungu, wala si wanadamu, ndiye atakayeamua sala atakazosikia. Iwapo katika pindi fulani Mkristo anasali kwa Mungu na kusahau kutumia usemi “katika jina la Yesu,” hapaswi kuhisi kwamba ana hatia. Yehova anafahamu kabisa udhaifu wetu, naye anataka kutusaidia. (Zaburi 103:12-14) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tukidhihirisha imani katika “Mwana wa Mungu . . . , hata iwe ni nini ambacho twaomba kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” (1 Yohana 5:13, 14) Hata hivyo, Wakristo wa kweli wanapowakilisha wengine katika sala zinazotolewa hadharani, wanatambua daraka la Yesu kuhusiana na makusudi ya Yehova kama linavyoonyeshwa katika Maandiko. Nao hujitahidi kumheshimu Yesu kwa kutoa sala kwa Mungu kupitia kwake.