Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sheria za Mungu Hutufaidi

Sheria za Mungu Hutufaidi

Sheria za Mungu Hutufaidi

“Sheria yako naipenda mno ajabu.”—ZABURI 119:97.

1. Watu wengi wana maoni gani kuhusu kutii sheria za Mungu?

LEO watu wengi hawapendi kutii sheria za Mungu. Wengi hawaoni haja ya kunyenyekea mamlaka fulani ya juu isiyoonekana. Tunaishi katika enzi ambapo watu wengi wanaamini kwamba hakuna sheria dhahiri kuhusu mema na mabaya, lakini maadili hutegemea hali zilizopo. Si rahisi kuelewa au kupambanua mema na mabaya. (Mithali 17:15; Isaya 5:20) Uchunguzi mmoja wa hivi karibuni kuhusu jinsi watu wengi wa ulimwengu wanavyoona mambo ulisema kwamba “Waamerika wengi wanataka kujiamulia ni mambo gani yaliyo sawa, mema, na muhimu kwao.” Wangetaka “Mungu mpole na sheria legevu. Hawangependa viongozi wenye nguvu nyingi ambao hushikilia sana maoni yao, iwe ni kuhusu maadili au mambo mengine.” Mchunguzi mmoja wa mambo ya kijamii alisema kwamba leo “watu wanatarajiwa wajiamulie maana ya kuishi maisha mema yenye maadili.” Aliendelea kusema hivi: ‘Mamlaka yoyote ya juu inalazimika kubadili sheria zake ili zifaane na mahitaji ya watu.’

2. Masimulizi ya Biblia yanayotaja sheria kwa mara ya kwanza yanaonyeshaje uhusiano uliopo kati ya sheria na kupata baraka na kibali cha Mungu?

2 Kwa kuwa watu wengi wanatilia shaka faida ya kufuata sheria za Yehova, tunahitaji kuamini kabisa kwamba viwango vya Mungu vinatufaidi. Inafaa kuchunguza masimulizi ya Biblia yanayotaja sheria kwa mara ya kwanza. Katika andiko la Mwanzo 26:5, tunasoma maneno haya ya Mungu: ‘Abrahamu aliyahifadhi maagizo yangu, na amri zangu, na hukumu zangu, na sheria zangu.’ Maneno hayo yalitamkwa karne nyingi kabla Yehova hajawapa wazao wa Abrahamu Sheria ya Musa. Mungu alimthawabishaje Abrahamu kwa sababu ya kutii, kutia ndani kutii amri Zake? Yehova Mungu alimwahidi hivi: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.” (Mwanzo 22:18) Kwa hiyo, kutii sheria za Mungu kunahusiana sana na kupata baraka na kibali chake.

3. (a) Mtunga-zaburi mmoja alikuwa na maoni gani kuhusu sheria ya Yehova? (b) Ni maswali gani tunayopaswa kufikiria?

3 Mtunga-zaburi mmoja—yaelekea mwana-mfalme ambaye angekuja kuwa mfalme wa Yuda—alikuwa na maoni ya pekee kuhusu sheria. Alimwambia Mungu hivi: “Sheria yako naipenda mno ajabu.” (Zaburi 119:97, italiki ni zetu.) Hakutamka maneno hayo kwa kuchochewa tu na hisia. Alisema hivyo kuonyesha jinsi alivyopenda mapenzi ya Mungu yaliyoelezwa katika sheria yake. Yesu Kristo, Mwana mkamilifu wa Mungu, alikuwa na maoni kama hayo. Yesu anaelezwa kwa njia ya kiunabii kuwa ndiye aliyesema hivi: “Kuyafanya mapenzi yako, Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu; naam, sheria yako imo moyoni mwangu.” (Zaburi 40:8; Waebrania 10:9) Namna gani sisi? Je, tunafurahia kufanya mapenzi ya Mungu? Je, tunasadiki kwamba sheria za Yehova zinatusaidia na kutufaidi? Kutii sheria za Mungu kuna umuhimu gani katika ibada yetu, maisha yetu ya kila siku, maamuzi tunayofanya, na uhusiano wetu pamoja na wengine? Ili tuipende sheria ya Mungu tunapaswa kwanza kuelewa ni kwa nini Mungu ana haki ya kutunga sheria na kuhakikisha zinafuatwa.

Yehova Ndiye Mwenye Haki ya Kutoa Sheria

4. Kwa nini Yehova ndiye mwenye haki kamili ya kutoa sheria?

4 Kwa kuwa yeye ndiye Muumba, Yehova ana haki kamili ya kutoa sheria katika ulimwengu wote. (Ufunuo 4:11) Nabii Isaya alisema: “BWANA ndiye mfanya sheria [“Mtoaji-sheria,” NW] wetu.” (Isaya 33:22) Ametoa sheria za asili zinazoongoza uumbaji wenye uhai na usio na uhai. (Ayubu 38:4-38; 39:1-12; Zaburi 104:5-19) Kwa kuwa aliumbwa na Mungu, mwanadamu yuko chini ya sheria za asili za Yehova. Na ingawa mwanadamu ana uhuru wa kuchagua na ana uwezo wa kutumia akili, anakuwa na furaha tu anapotii sheria za Mungu zinazohusu maadili na ibada yetu kwa Mungu.—Waroma 12:1; 1 Wakorintho 2:14-16.

5. Kanuni iliyo katika andiko la Wagalatia 6:7 inathibitikaje kuwa kweli kuhusiana na sheria za Mungu?

5 Kama tujuavyo, sheria za Yehova za asili hazibadiliki. (Yeremia 33:20, 21) Mtu akitenda kinyume cha sheria fulani za asili, kwa mfano, akipanda juu ya jengo kubwa na kuruka, atapatwa na madhara. Vivyo hivyo, sheria za Mungu za maadili hazibadiliki na mtu hawezi kuzikwepa au kuzivunja na kufikiri kwamba ataepuka matokeo yake. Sheria za Mungu za maadili zinapaswa kufuatwa kama vile sheria zake za asili, ingawa huenda kutofuata sheria hizo za maadili kusiwe na matokeo ya papo hapo. “Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia.”—Wagalatia 6:7; 1 Timotheo 5:24.

Sheria ya Yehova Inatia Ndani Nini?

6. Sheria za Mungu zinatia ndani mambo gani?

6 Sheria ya Musa ilikuwa mfano bora wa sheria ya Mungu. (Waroma 7:12) Baadaye, Yehova Mungu alitoa “sheria ya Kristo” * ichukue mahali pa Sheria ya Musa. (Wagalatia 6:2; 1 Wakorintho 9:21) Tukiwa Wakristo walio chini ya “sheria kamilifu iliyo ya uhuru,” tunaelewa kwamba maagizo ya Mungu hayahusu tu mambo fulani katika maisha yetu, kama vile mafundisho ya kidini au taratibu za ibada. Viwango vyake vinahusu sehemu zote za maisha yetu, kutia ndani maisha ya familia, shughuli za kibiashara, jinsi tunavyopaswa kujiendesha kuhusiana na watu wa jinsia tofauti, maoni yetu kuelekea Wakristo wenzetu, na kushiriki katika ibada ya kweli.—Yakobo 1:25, 27.

7. Toa mifano ya sheria muhimu za Mungu.

7 Kwa mfano Biblia inasema: “Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume watunzwao kwa makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume walalao pamoja na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawatarithi ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10) Naam, uzinzi na uasherati si ‘mahusiano tu ya kimapenzi,’ wala ngono za wanawake kwa wanawake au wanaume kwa wanaume, si ‘mtindo tofauti tu wa maisha.’ Vitendo hivyo sawa na vitendo kama vile kuiba, kusema uwongo, na kuchongea, ni uvunjaji wa sheria za Yehova. (Zaburi 101:5; Wakolosai 3:9; 1 Petro 4:15) Yakobo alishutumu kujigamba, naye Paulo akatushauri tuepuke maongezi ya kipumbavu na mzaha wenye aibu. (Waefeso 5:4; Yakobo 4:16) Wakristo huziona amri hizo zote zinazohusu mwenendo kuwa sehemu ya sheria kamilifu ya Mungu.—Zaburi 19:7.

8. (a) Sheria ya Yehova ni nini hasa? (b) Ni nini maana ya msingi ya neno la Kiebrania linalotafsiriwa “sheria”?

8 Kanuni hizo za msingi za Neno la Yehova zinafunua kwamba sheria yake si orodha tu ya amri zinazopaswa kufuatwa bila kufikiri. Sheria hiyo inafanya maisha yetu kwa ujumla yawe na usawaziko na yenye kunufaisha. Sheria ya Mungu inajenga, ni ya maadili, na yenye kuelimisha. (Zaburi 119:72) Neno “sheria” ambalo mtunga-zaburi ametumia, limetafsiriwa kutoka kwa neno la Kiebrania toh·rahʹ. Msomi mmoja wa Biblia anasema: ‘Neno hilo linatokana na kitenzi kinachomaanisha kuelekeza, kuongoza, kulenga, kupiga mshale. Hivyo basi, neno hilo linamaanisha kanuni ya mwenendo.’ Mtunga-zaburi aliiona sheria kuwa zawadi kutoka kwa Mungu. Nasi pia twapaswa kuiheshimu vivyo hivyo na kuiruhusu ituongoze maishani.

9, 10. (a) Kwa nini tunahitaji mwongozo wenye kutegemeka? (b) Ni kwa njia gani tu tunaweza kufanikiwa maishani na kuwa wenye furaha?

9 Viumbe wote wanahitaji mwongozo wenye kutegemeka na mwelekezo wenye kutumainika. Yesu na malaika pia wanahitaji mambo hayo ingawa wao ni viumbe wa hali ya juu kuliko wanadamu. (Zaburi 8:5; Yohana 5:30; 6:38; Waebrania 2:7; Ufunuo 22:8, 9) Ikiwa viumbe hao wakamilifu wanaweza kufaidika na mwongozo wa Mungu, basi sisi wanadamu wasio wakamilifu tunaweza kufaidika hata zaidi na mwongozo huo. Historia ya mwanadamu na mambo ambayo hutupata yamethibitisha kwamba maoni haya ya nabii Yeremia ni ya kweli: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23.

10 Ikiwa tunataka tufanikiwe maishani na tuwe na furaha, ni lazima tutafute mwongozo wa Mungu. Mfalme Solomoni alitambua hatari ya kukataa mwongozo wa Mungu na kufuata viwango vyetu wenyewe: “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, lakini mwisho wake ni njia za mauti.”—Mithali 14:12.

Sababu Zinazofanya Tupende Sheria ya Yehova

11. Kwa nini tutamani kuielewa sheria ya Mungu?

11 Tunapaswa kusitawisha tamaa nyingi ya kuielewa sheria ya Yehova. Mtunga-zaburi alionyesha tamaa hiyo aliposema: “Unifumbue macho yangu niyatazame maajabu yatokayo katika sheria yako.” (Zaburi 119:18) Kadiri ujuzi wetu juu ya Mungu na njia zake uongezekavyo, ndivyo tuzidivyo kuelewa ukweli wa maneno haya ya Isaya: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata. Laiti ungalisikiliza amri zangu!” (Isaya 48:17, 18) Yehova anataka sana watu wake wasikilize amri zake ili waepuke msiba na wafurahie maisha. Na tuchunguze sababu fulani kuu zinazofanya tupende sheria ya Mungu.

12. Ujuzi wa Yehova kutuhusu unamfanyaje kuwa Mtoaji-sheria bora?

12 Sheria ya Mungu inatoka kwa Yule anayetujua vizuri kabisa. Kwa kuwa Yehova ni Muumba wetu, ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba anatujua vizuri sana. (Zaburi 139:1, 2; Matendo 17:24-28) Marafiki wa karibu, watu wa ukoo, na hata wazazi hawawezi kutujua vizuri jinsi Yehova anavyotujua. Kwani, Mungu anatujua vizuri kuliko vile tujijuavyo! Mfanyi wetu anajua kabisa mahitaji yetu ya kiroho, kihisia-moyo, kiakili, na kimwili. Anaposhugulika nasi, yeye huonyesha kwamba anaelewa vizuri sana maumbile yetu, tamaa zetu, na malengo yetu. Yehova anaelewa udhaifu wetu, lakini anajua pia tuna uwezo wa kutimiza mambo yenye manufaa. Mtunga-zaburi anasema: “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:14) Kwa hiyo, tunaweza kuhisi salama kiroho tunapojitahidi kufuata sheria ya Mungu, tukijitiisha kwa hiari chini ya mwongozo wake.—Mithali 3:19-26.

13. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anajali sana hali yetu?

13 Sheria ya Mungu hutoka kwa Yule anayetupenda. Mungu anajali sana hali yetu. Je, haikumgharimu sana kumtoa Mwana wake kuwa “fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi”? (Mathayo 20:28) Yehova ameahidi kwamba ‘hataacha tushawishwe kupita vile tuwezavyo kuhimili.’ (1 Wakorintho 10:13) Nayo Biblia inatuhakikishia kwamba ‘anatujali.’ (1 Petro 5:7) Hakuna yeyote anayependezwa sana kuwatolea wanadamu miongozo yenye kuwanufaisha kuliko Yehova. Anajua mambo yanayoweza kutuletea faida, furaha, au huzuni. Ingawa sisi si wakamilifu na hufanya makosa, tukifuatia uadilifu, yeye hutuonyesha upendo katika njia zitakazotuletea uhai na baraka.—Ezekieli 33:11.

14. Sheria ya Mungu hutofautiana na maoni ya wanadamu katika njia gani muhimu?

14 Sheria ya Mungu kwa hakika haibadiliki. Katika nyakati hizi zetu zenye msukosuko, Yehova ni mwamba imara, ambaye amekuwako tangu milele hata milele. (Zaburi 90:2) Alisema hivi kujihusu: “Mimi ni mwenyezi-Mungu, mimi sibadiliki.” (Malaki 3:6, BHN) Viwango vya Mungu vilivyoandikwa katika Biblia vinategemeka kabisa—tofauti na maoni ya mwanadamu ambayo hubadilika daima. (Yakobo 1:17) Kwa mfano, kwa miaka mingi wanasaikolojia walipendekeza kwamba watoto walelewe kwa kuendekezwa, lakini baadaye wakabadili maoni yao na kukiri kwamba walikuwa wamekosea. Viwango na miongozo ya wanadamu kuhusu jambo hilo hubadilika-badilika sana. Hata hivyo, Neno la Yehova halibadiliki. Kwa karne nyingi Biblia imetoa ushauri kuhusu kulea watoto kwa upendo. Mtume Paulo aliandika: “Akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Inatia moyo kama nini kujua kwamba tunaweza kutumaini viwango vya Yehova ambavyo havibadiliki!

Wanaotii Sheria za Mungu Hubarikiwa

15, 16. (a) Kutakuwa na matokeo gani tukifuata viwango vya Yehova? (b) Sheria za Mungu zinawezaje kuwa mwongozo mzuri katika ndoa?

15 Mungu alisema hivi kupitia nabii wake Isaya: “Neno langu, litokalo katika kinywa changu .  . . litafanikiwa.” (Isaya 55:11) Tuna uhakika huohuo kwamba tukijitahidi kabisa kufuata viwango vya Neno lake, tutafanikiwa na kutimiza mambo yanayofaa. Tutapata furaha pia.

16 Fikiria jinsi sheria za Mungu zinavyotoa mwongozo mzuri wa kuwa na ndoa yenye mafanikio. Paulo aliandika: “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila kutiwa unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Inawapasa wenzi wa ndoa waheshimiane na kupendana: “Acheni kila mtu mmoja-mmoja kati yenu ampende hivyo mke wake kama yeye mwenyewe; kwa upande mwingine, mke apaswa kuwa na staha yenye kina kirefu kwa mume wake.” (Waefeso 5:33) Upendo unaohitajiwa unaelezwa katika 1 Wakorintho 13:4-8: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujitutumui, haujiendeshi bila adabu, hautafuti masilahi yao wenyewe, haupati kuwa wenye kuchokozeka. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.” Ndoa yenye upendo wa aina hiyo haitavunjika.

17. Tunafaidikaje kwa kufuata viwango vya Yehova kuhusu utumiaji wa vileo?

17 Jambo jingine linalothibitisha kwamba viwango vya Yehova hutufaidi ni kwamba yeye anakataza ulevi. Hata anachukia “kujitoa kwa divai nyingi.” (1 Timotheo 3:3, 8; Waroma 13:13) Wengi wanaopuuza viwango vya Mungu kuhusu jambo hilo hupatwa na magonjwa yanayosababishwa au kuzidishwa na kunywa kupita kiasi. Kwa kupuuza ushauri wa Biblia kuhusu kiasi, wengine wamekuwa na mazoea ya kunywa sana ili “waweze kustarehe.” Matatizo yanayotokana na kunywa kupita kiasi ni mengi, kutia ndani kutojiheshimu, kuharibika kwa mahusiano ya familia au kuvunjika kwa familia, kutumia vibaya mapato, na kupoteza kazi. (Mithali 23:19-21, 29-35) Kwa kweli viwango vya Yehova kuhusu utumiaji wa vileo ni ulinzi.

18. Je, sheria za Mungu zinaweza kutumika katika mambo ya kifedha? Eleza.

18 Imethibitika kwamba viwango vya Mungu pia vinaweza kutumika katika mambo ya kifedha. Biblia huwahimiza Wakristo wawe wanyofu na wenye bidii. (Luka 16:10; Waefeso 4:28; Wakolosai 3:23) Kwa kuwa wanafuata ushauri huo, Wakristo wengi wamepandishwa cheo au kuendelea na kazi huku watu wengine wakifutwa. Mtu hunufaika kifedha pia akiepuka mazoea yasiyopatana na Maandiko kama vile kucheza kamari, kuvuta sigara, na kutumia dawa za kulevya. Hapana shaka kwamba unaweza kukumbuka mifano mingine ya jinsi viwango vya Mungu vinavyoweza kutufaidi kifedha.

19, 20. Kwa nini ni jambo la hekima kukubali na kushika sheria za Mungu?

19 Ni rahisi kwa wanadamu wasio wakamilifu kukiuka sheria na viwango vya Mungu. Fikiria Waisraeli kwenye Mlima Sinai. Mungu aliwaambia: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu.” Nao wakajibu: “Hayo yote aliyoyasema BWANA tutayatenda.” Lakini walitenda kinyume kama nini! (Kutoka 19:5, 8; Zaburi 106:12-43) Tofauti na hao, na tukubali na kushika viwango vya Mungu.

20 Ni jambo la hekima na la furaha kushikamana kabisa na sheria zisizo na kifani ambazo Yehova ametupatia zituongoze maishani. (Zaburi 19:7-11) Ili kufanikiwa kufanya hivyo, tunahitaji kuelewa na kuthamini faida ya kanuni za Mungu. Habari hiyo itazungumziwa katika makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ili kupata habari zaidi kuhusu “sheria ya Kristo,” ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1996, ukurasa wa 14-24.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba sheria za Mungu zinatufaidi?

• Ni sababu zipi zinazofanya tupende sheria ya Yehova?

• Sheria za Mungu hutufaidi katika njia zipi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Abrahamu alibarikiwa sana kwa kutii sheria ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mahangaiko ya maisha ya leo yenye shughuli nyingi hukengeusha watu wasifuate sheria ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kama mnara wa taa juu ya mwamba, sheria ya Mungu ni imara na haibadiliki