Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Mwana Alivyomsaidia Baba Yake

Jinsi Mwana Alivyomsaidia Baba Yake

Jinsi Mwana Alivyomsaidia Baba Yake

JAMES, mwenye umri wa miaka 32, anayeishi Uingereza ana ugonjwa mbaya sana wa akili na pia ule ugonjwa wa akili unaowapata watoto wachanga. Hata hivyo, kwa miaka mingi amehudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova akiwa na mama yake na dada yake. Lakini, baba yake hakuwahi kupendezwa na imani yao. Jioni moja, baada ya mkutano ulioonyesha jinsi ya kualika mtu unayemfahamu kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo, James alienda haraka chumbani mwake. Mama yake alimfuata kwa wasiwasi na kumkuta akipekua-pekua kwa haraka magazeti ya zamani ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Alichagua moja lililokuwa na mwaliko wa Ukumbusho kwenye ukurasa wake wa nyuma, akamwendea baba yake haraka. Kwanza, alielekeza kidole chake kwenye picha na kisha kwa baba yake na kusema “Wewe!” Mama yake na baba yake walitazamana kwa mshangao walipotambua kwamba James alikuwa anataka kumwalika baba yake kwenye Ukumbusho. Baba yake alisema kwamba huenda angehudhuria.

Jioni ile ya Ukumbusho, James alikwenda kwa kabati la nguo za baba yake akachagua suruali moja, akampelekea na kumwonyesha kwa ishara aivae. Baba yake alimwambia kwamba hataenda mkutanoni. Basi, James na mama yake wakaondoka kwenda kwenye Jumba la Ufalme.

Hata hivyo, baadaye, James alianza kuwa na tabia ya kukataa-kataa kumtii mama yake alipojaribu kumtayarisha ili wahudhurie mikutano ya kutaniko, akichagua kubaki nyumbani na baba yake. Halafu Jumapili moja asubuhi, James alikataa tena mama yake alipojaribu kumtayarisha kwa ajili ya mkutano. Mama yake alipigwa butaa wakati baba ya James alipomgeukia na kusema, “James, iwapo nitaenda mkutanoni leo, je, utaenda?” James alitabasamu, kisha akamkumbatia baba yake na kusema, “Ndiyo!” na wote watatu wakaenda kwenye Jumba la Ufalme.

Tangu siku hiyo, baba ya James aliendelea kuhudhuria mikutano yote ya Jumapili kisha akasema kwamba iwapo anataka kufanya maendeleo, anapaswa kuhudhuria mikutano mingine pia. (Waebrania 10:24, 25) Alifanya hivyo akahudhuria mikutano yote, na miezi miwili baadaye akaanza kujifunza Biblia kwa ukawaida. Alifanya maendeleo haraka na kufanya mabadiliko katika maisha yake, na punde si punde akaanza kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme. Mwaka mmoja baada ya kuanza kujifunza Biblia, alijiweka wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu huo kwa ubatizo wa maji. Sasa yeye anatumikia akiwa mtumishi wa huduma kutanikoni. Sasa wote katika familia wanamtumikia Yehova kwa umoja.