Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Ulemavu Utakavyokoma

Jinsi Ulemavu Utakavyokoma

Jinsi Ulemavu Utakavyokoma

EBU wazia vipofu wakiona, viziwi wakisikia, mabubu wakiimba kwa shangwe, na miguu ya vilema ikiwa imara na kuweza kutembea! Hatuzungumzii maendeleo ya kisayansi kuhusu tiba, bali kuhusu jinsi hali itakavyokuwa wakati Mungu mwenyewe atakapochukua hatua kwa niaba ya wanadamu. Biblia inatabiri hivi: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.” (Isaya 35:5, 6) Lakini tunawezaje kuwa na uhakika kwamba unabii huu wa ajabu utatimizwa?

Kwanza, alipokuwa duniani, Yesu Kristo aliponya watu magonjwa na ulemavu wa kila aina. Na zaidi ya hayo, miujiza mingi aliyofanya ilionekana na watu wengi, hata na maadui wake. Kwa hakika katika pindi moja, wapinzani wenye shaka walichunguza kwa makini uponyaji mmoja ili kumharibia Yesu sifa. Lakini waliudhika kwa sababu uchunguzi wao ulithibitisha muujiza wake. (Yohana 9:1, 5-34) Baada ya Yesu kufanya muujiza mwingine wasioweza kupinga, walisema hivi kwa kukata tamaa: “Twapaswa kufanya nini, kwa sababu mtu huyu hufanya ishara nyingi?” (Yohana 11:47) Hata hivyo, watu wa kawaida hawakuwa na maoni kama hayo, bali waliitikia na wengi wakaanza kumwamini Yesu.—Yohana 2:23; 10:41, 42; 12:9-11.

Miujiza ya Yesu Inaonyesha Maponyo Atakayofanya Ulimwenguni Pote

Miujiza ya Yesu haikuwa uthibitisho tu wa kwamba Yesu alikuwa Mesiya na Mwana wa Mungu. Iliandaa msingi wa imani katika ahadi za Biblia kwamba wanadamu watiifu wataponywa wakati ujao. Ahadi hizo zatia ndani unabii wa Isaya sura ya 35 uliotajwa kwenye fungu la kwanza. Isaya 33:24 husema hivi kuhusu afya ya wakati ujao ya wanadamu wanaomwogopa Mungu: “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” Ufunuo 21:4 pia huahidi: “[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani [majaribu na mateso ya wakati huu] yamepitilia mbali.”

Mara nyingi watu husali kuhusu kutimizwa kwa unabii huu wanaporudia sala ya Yesu ya kielelezo, isemayo hivi kwa sehemu: “Ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:10) Ndiyo, mapenzi ya Mungu yanatia ndani dunia na wanadamu. Hivi karibuni, magonjwa na ulemavu, ijapokuwa yameruhusiwa kwa sababu fulani, hayatakuwapo tena, wala hayataharibu milele mahali pa Mungu pa ‘kuweka miguu.’—Isaya 66:1. *

Waliponywa Bila Maumivu Wala Malipo

Yesu aliponya watu bila maumivu, na bila malipo, hata magonjwa yao yawe yalikuwa ya aina gani. Bila shaka, habari za maponyo hayo zilijulikana upesi, na punde si punde, “umati mkubwa ukamkaribia yeye, ukiwa pamoja na watu waliokuwa vilema, walioharibika viungo, walio vipofu, mabubu, na wengi wa hali tofauti, nao wakawatupa kabisa miguuni pake, naye akawaponya.” Watu waliitikiaje? Mathayo aliyeshuhudia aendelea kusema: “Umati ukahisi mshangao ulipoona mabubu wakisema na vilema wakitembea na vipofu wakiona, nao ukatukuza Mungu wa Israeli.”—Mathayo 15:30, 31.

Ona kwamba walioponywa na Yesu hawakuchaguliwa kwa ujanja kutoka kwa umati kama wafanyavyo walaghai. Bali, watu wa ukoo na marafiki wa wale waliokuwa wagonjwa ‘waliwatupa kabisa miguuni pake [Yesu], naye akawaponya.’ Ebu sasa tuone mifano kadhaa hususa ya uwezo wa Yesu wa kuponya.

Upofu: Yesu alipokuwa Yerusalemu, alifungua macho ya mtu aliyekuwa “kipofu tangu kuzaliwa.” Mwanamume huyo alijulikana sana jijini kuwa mwombaji kipofu. Kwa hivyo, unaweza kuwazia msisimko na makelele yaliyokuwako wakati watu walipomwona akitembea huko na huko akiwa anaona! Hata hivyo, si wote waliofurahi. Wakiwa wamekasirika sana kwa sababu hapo awali Yesu alikuwa amefunua uovu wao, baadhi ya washiriki wa madhehebu mashuhuri ya Kiyahudi yaliyoitwa Mafarisayo, walitaka kutumia ujanja ili kupata jambo la kumsingizia Yesu. (Yohana 8:13, 42-44; 9:1, 6-31) Kwa sababu hiyo, walimhoji mtu huyo aliyeponywa, kisha wakawahoji wazazi wake, na baadaye wakamhoji tena. Lakini mafarisayo hao walikasirika kwa sababu uchunguzi wao ulithibitisha muujiza wa Yesu. Akishangazwa na uovu wa watu hao wanafiki wa kidini, mwanamume huyo aliyeponywa alisema: “Kutoka zamani za kale haijasikiwa kamwe kwamba yeyote alifungua macho ya mtu aliyezaliwa kipofu. Kama mtu huyu hangekuwa atoka kwa Mungu, hangeweza kufanya lolote hata kidogo.” (Yohana 9:32, 33) Kwa sababu ya kueleza imani yake kwa unyoofu na kwa njia inayofaa, Mafarisayo, ‘wakamfukuza nje,’ kuonyesha kwamba walimfukuza mtu huyo aliyekuwa kipofu kutoka katika sinagogi.—Yohana 9:22, 34.

Uziwi: Yesu alipokuwa Dekapolisi, eneo lililo mashariki ya Mto Yordani, ‘watu huko walimletea mtu kiziwi na aliye na kizuizi cha usemi.’ (Marko 7:31, 32) Mbali na kumponya mtu huyo, Yesu alionyesha kwamba anajali kikweli hisia za viziwi ambao huenda wakaaibika wanapokuwa mbele ya watu wengi. Biblia inatuambia kwamba Yesu alimchukua mtu huyo kiziwi “kutoka katika umati kwa faragha,” na kumponya. Tena watazamaji “walikuwa wakistaajabishwa kwa njia izidiyo zaidi sana iliyo ya kawaida” na kusema: “Amefanya mambo yote vema. Afanya hata viziwi wasikie na wasiosema waseme.”—Marko 7:33-37.

Kupooza: Yesu akiwa Kapernaumu, watu walimletea mtu aliyepooza akiwa amelala kitandani. (Mathayo 9:2) Mistari ya 6 hadi 8 yaeleza kilichotendeka. “[Yesu] akamwambia mwenye kupooza: ‘Inuka, chukua kitanda chako, na kwenda nyumbani kwako.’ Naye akainuka na kwenda zake nyumbani kwake. Kwa kuona hilo umati ukaingiwa na hofu, nao ukamtukuza Mungu, aliyewapa wanadamu mamlaka ya namna hiyo.” Muujiza huu pia ulifanywa wakiwepo wanafunzi wa Yesu na maadui wake. Ona kwamba kwa kuwa wanafunzi wa Yesu hawakupofushwa na chuki na ubaguzi,‘walimtukuza Mungu’ kwa yale waliyoona.

Ugonjwa: “Huko pia mwenye ukoma akaja kwake [Yesu], akimsihi sana hata kwa kukunja magoti, akimwambia: “Ikiwa tu wewe wataka, waweza kunifanya safi.” Ndipo akasukumwa na sikitiko, naye akanyoosha mkono wake akamgusa, akamwambia: ‘Mimi nataka. Fanywa safi.’ Na mara hiyo ule ukoma ukamtoka, naye akawa safi.” (Marko 1:40-42) Ona kwamba Yesu hakumponya mtu huyo shingo upande bali alichochewa na huruma ya kweli. Ebu wazia kwamba wewe ni mwenye ukoma. Ungehisije kama ungeponywa mara moja na bila maumivu ugonjwa huo wenye kuhofiwa ambao hatua kwa hatua unaharibu viungo vya mwili wako na kukufanya utengwe na jamii? Bila shaka unaweza kuelewa ni kwa nini mtu mmoja mwenye ukoma aliyeponywa kimuujiza ‘alianguka kifudifudi kwenye miguu ya Yesu, akimshukuru.’—Luka 17:12-16.

Jeraha: Muujiza wa mwisho wa Yesu kabla ya kukamatwa na kutundikwa ulikuwa wa uponyaji. Akichukua hatua ya haraka kuwashambulia wale waliokuwa wanamchukua Yesu, mtume Petro “kwa kuwa alikuwa na upanga, akaufuta na kumpiga mtumwa wa kuhani wa cheo cha juu.” (Yohana 18:3-5, 10) Katika kitabu cha Luka, masimulizi hayohayo yanatuambia kwamba Yesu ‘alimgusa sikio na kumponya.’ (Luka 22:50, 51) Kwa mara nyingine tena tendo hilo la fadhili lilifanywa mbele ya rafiki za Yesu na vilevile maadui wake ambao wakati huu, walitaka kumkamata.

Naam, tunapochunguza miujiza ya Yesu zaidi, tunafahamu waziwazi zaidi mambo yanayothibitisha miujiza hiyo kuwa ya kweli. (2 Timotheo 3:16) Na kama ilivyotangulia kutajwa, funzo hilo lapaswa kuimarisha imani yetu katika ahadi ya Mungu ya kuponya wanadamu watiifu. Biblia hueleza imani ya Kikristo kuwa “taraja lililohakikishwa la mambo yatumainiwayo, wonyesho dhahiri wa mambo halisi ingawa hayaonwi.” (Waebrania 11:1) Ni wazi kwamba Mungu anatutia moyo tuwe na imani yenye nguvu badala ya kuamini bila kufikiri au kutumaini tu kwamba mambo hayo yatatokea. (1 Yohana 4:1) Tukiwa na imani kama hiyo, tutakuwa wenye nguvu na afya kiroho, na wenye furaha nyingi zaidi.—Mathayo 5:3; Waroma 10:17.

Ni Lazima Uponyaji wa Kiroho Uje Kwanza!

Watu wengi walio na afya ya kimwili hawana furaha. Baadhi yao hata hujaribu kujiua kwa sababu hawana tumaini la wakati ujao au wanahisi wamelemewa na matatizo. Kwa njia hiyo, wamekuwa walemavu kiroho—hali ambayo Mungu anaona kuwa mbaya zaidi kuliko ulemavu wa kimwili. (Yohana 9:41) Kwa upande mwingine, wengi ambao ni walemavu kimwili kama Christian na Junior waliotajwa katika makala iliyotangulia, wanaishi maisha yenye furaha na yenye kuridhisha. Kwa nini? Kwa sababu wana afya bora kiroho na wanatiwa nguvu na tumaini hakika linalotegemea Biblia.

Akitaja uhitaji pekee wa mwanadamu, Yesu alisema: “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4) Naam tofauti na wanyama, wanadamu wanahitaji mengi zaidi ya chakula cha kimwili. Tukiwa tumeumbwa kwa “mfano” wa Mungu, tunahitaji chakula cha kiroho—kumjua Mungu na kujua jinsi kusudi lake linavyotuhusu na vilevile kufanya mapenzi yake. (Mwanzo 1:27; Yohana 4:34) Kumjua Mungu hutupatia kusudi maishani na hutuchochea kumtumikia. Pia hutuwekea msingi wa kuwa na uhai udumuo milele katika dunia paradiso. ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’—Yohana 17:3.

Ni wazi kwamba watu wa siku za Yesu walimwita “Mwalimu” na wala si “Mponyaji.” (Luka 3:12; 7:40) Kwa nini? Kwa sababu Yesu aliwafundisha kuhusu Ufalme wa Mungu ambao ndiyo suluhisho la kudumu kwa matatizo ya wanadamu. (Luka 4:43; Yohana 6:26, 27) Yesu Kristo akiwa mtawala katika serikali hiyo ya kimbingu, atatawala dunia yote na kutimiza ahadi zote za Biblia za kuifanya dunia kuwa mpya na wanadamu waadilifu kuwa wakamilifu kama Biblia inavyoahidi. (Ufunuo 11:15) Ndiyo sababu katika sala yake ya kielelezo, Yesu alihusianisha kuja kwa Ufalme wa Mungu na kufanywa kwa mapenzi ya Mungu duniani.—Mathayo 6:10.

Watu wengi walio walemavu wanapojifunza kuhusu tumaini hili lenye kusisimua, wao hushangilia badala ya kuhuzunika. (Luka 6:21) Kwa hakika, Mungu hataondoa tu magonjwa na ulemavu, bali pia atafutilia mbali kile kinachosababisha kuteseka kwa wanadamu—dhambi. Bila shaka maandiko ya Isaya 33:24 na Mathayo 9:2-7 yaliyonukuliwa awali, yanahusisha magonjwa na hali yetu yenye dhambi. (Waroma 5:12) Hivyo, dhambi ikiwa imeshindwa, wanadamu watafurahia “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu,” uhuru unaotia ndani ukamilifu wa akili na mwili.—Waroma 8:21.

Huenda wale wanaofurahia afya bora kwa kiasi fulani wakachukulia hali yao kivivihivi tu. Lakini sivyo ilivyo na wale wanaosumbuliwa na ulemavu. Wanajua thamani ya kuwa na afya nzuri, kuwa hai na jinsi mambo yanavyoweza kubadilika kwa ghafula, bila kutazamiwa. (Mhubiri 9:11) Basi, tunatumaini kwamba wale walio walemavu miongoni mwa wasomaji wetu watafikiria kwa makini ahadi bora za Mungu kama zilivyoandikwa katika Biblia. Yesu alitoa uhai wake ili kuhakikisha kutimizwa kwa ahadi hizo. Huu ndio uhakikisho bora kabisa.—Mathayo 8:16, 17; Yohana 3:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kwa habari zaidi kuhusu sababu inayofanya Mungu aruhusu kuteseka, ona broshua Je, Kweli Mungu Anatujali?, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.