Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusitawisha Upendo wa Yehova Katika Mioyo ya Watoto Wetu

Kusitawisha Upendo wa Yehova Katika Mioyo ya Watoto Wetu

Simulizi la Maisha

Kusitawisha Upendo wa Yehova Katika Mioyo ya Watoto Wetu

IMESIMULIWA NA WERNER MATZEN

Miaka kadhaa iliyopita mwana wangu mkubwa, Hans Werner, alinipatia Biblia. Aliandika hivi ndani ya jalada yake: “Baba Mpendwa, Neno la Yehova na liendelee kutuongoza katika njia ya uhai tukiwa familia. Shukrani, mwana wako mkubwa.” Wazazi wataelewa jinsi nilivyofurahi sana na kushukuru kusoma maneno hayo. Wakati huo sikujua magumu ambayo tungekabili tukiwa familia.

NILIZALIWA mwaka wa 1924 huko Halstenbek, kilometa 20 hivi kutoka bandari ya Hamburg nchini Ujerumani. Nililelewa na mama na babu yangu. Kwa kuwa nilikuwa nimejifunza kazi ya kutengeneza vifaa, niliandikishwa katika jeshi la Wehrmacht mwaka wa 1942. Siwezi kueleza mambo yenye kutisha niliyojionea katika Vita ya Pili ya Ulimwengu nilipokuwa nikipigana katika mstari wa mbele wa majeshi ya Urusi. Nilishikwa na homa ya matumbo lakini nikarudishwa vitani baada ya kutibiwa. Mnamo Januari 1945, nilikuwa Lodz, Poland, ambako nilijeruhiwa vibaya na kupelekwa katika hospitali ya kijeshi. Bado nilikuwa katika hospitali hiyo vita ilipokwisha. Nikiwa katika hospitali hiyo na baadaye nikiwa kizuizini huko Neuengamme, nilipata wakati wa kutafakari. Nilihangaishwa na maswali haya, Je, kweli Mungu yuko? Ikiwa yuko, kwa nini anaruhusu ukatili mwingi hivyo?

Muda mfupi baada ya kuachiliwa kutoka kizuizini, Septemba 1947, nilimwoa Karla. Tulikulia katika mji mmoja. Karla alikuwa Mkatoliki lakini mimi sikujishughulisha na dini tangu utotoni. Kasisi aliyefunganisha ndoa yetu alipendekeza kwamba tuwe tukisema Sala ya Bwana tukiwa pamoja kila jioni. Tulifanya alivyosema ingawa hatukujua tulikuwa tukiomba nini.

Mwaka mmoja baadaye, Hans Werner akazaliwa. Karibu wakati huohuo, Wilhelm Ahrens, mfanyakazi mwenzangu, alinijulisha kwa Mashahidi wa Yehova. Alinionyesha kutoka kwa Biblia kwamba siku moja vita vitakwisha. (Zaburi 46:9) Mnamo mwaka wa 1950, nilijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Nilifurahi kama nini wakati mke wangu mpendwa alipobatizwa mwaka mmoja baadaye!

Kulea Watoto Katika Njia ya Yehova

Nilisoma katika Biblia kwamba Yehova ndiye mwanzilishi wa ndoa. (Mwanzo 1:26-28; 2:22-24) Kwa kuwa nilikuwepo watoto wetu wakizaliwa—Hans Werner, Karl-Heinz, Michael, Gabriele, na Thomas—niliazimia kuwa mume na baba mzuri. Mimi na Karla tulifurahia kuzaliwa kwa kila mmoja wa watoto wetu.

Kusanyiko la mwaka wa 1953 la Mashahidi wa Yehova huko Nuremberg lilikuwa pindi muhimu sana kwa familia yetu. Ijumaa alasiri, msemaji aliyetoa hotuba yenye kichwa “Kulea Watoto Katika Ulimwengu Mpya,” alisema jambo ambalo hatujalisahau: “Urithi wenye thamani zaidi tunaoweza kuwapa watoto wetu ni tamaa ya kuwa watumishi wa Mungu.” Kwa msaada wa Yehova, mimi na Karla tulitaka kufanya hivyo. Lakini jinsi gani?

Tulianza kwa kusali pamoja kwa ukawaida tukiwa familia. Watoto wakaona umuhimu wa sala. Wakiwa wangali wachanga, watoto wote walijua kwamba sikuzote tulisali kabla ya chakula. Hata walipokuwa wachanga sana, mara tu walipoona chupa yao, waliinamisha vichwa vyao vidogo na kukunja mikono yao midogo. Pindi moja, tulialikwa kwenye arusi ya watu wa jamaa wa mke wangu, ambao hawakuwa Mashahidi. Baada ya sherehe, wazazi wa bibi-arusi waliwaalika wageni nyumbani kwao wakapate viburudisho. Kila mtu alitaka kula mara hiyo. Lakini mtoto wetu Karl-Heinz mwenye umri wa miaka mitano aliona kuwa haifai kufanya hivyo. Alisema, “tafadhali toeni sala kwanza.” Wageni walimtazama, kisha wakatutazama, hatimaye wakamtazama mkaribishaji. Ili kuepuka aibu, nilijitolea kutoa sala ya chakula, naye mkaribishaji akakubali.

Kisa hicho kilinikumbusha maneno haya ya Yesu: “Kutoka kinywani mwa vitoto na watoto wanyonyao umetoa sifa.” (Mathayo 21:16) Tuna hakika kwamba sala zetu za kutoka moyoni zilizotolewa kwa ukawaida ziliwasaidia watoto kumwona Yehova kuwa Baba yao wa kimbingu mwenye upendo.

Daraka Letu Mbele ya Yehova

Kufundisha watoto wampende Mungu kwahusisha kusoma na kujifunza Neno lake kwa ukawaida. Kwa kuzingatia jambo hilo, tulifanya funzo la familia kila juma, hasa Jumatatu jioni. Kwa kuwa mtoto wa kwanza na wa mwisho waliachana kwa miaka tisa, mahitaji ya watoto yalitofautiana sana, kwa hiyo hatungeweza kuchunguza habari ileile na wote.

Kwa mfano, tulirahisisha sana mafundisho kwa ajili ya watoto ambao hawakuwa wameanza kwenda shuleni. Karla alizungumza nao andiko moja tu la Biblia, au alitumia picha za vichapo vinavyozungumzia habari ya Biblia. Ningali nakumbuka jinsi nilivyokuwa nikiamshwa asubuhi na watoto wachanga wakipanda juu ya kitanda chetu kutuonyesha picha walizopenda zaidi katika kitabu The New World. *

Karla alisitawisha ustadi wa kufundisha watoto kwa saburi waelewe sababu nyingi zinazofanya tumpende Yehova. Huenda kazi hiyo ikasikika kuwa rahisi, lakini kwa kweli, ilikuwa kazi yenye kuchosha kimwili na kihisia-moyo na ilichukua muda wetu mwingi. Hata hivyo, hatukukata tamaa. Tulitaka kusitawisha upendo huo katika mioyo yao michanga kabla hawajaathiriwa na watu wengine wasiomjua Yehova. Kwa hiyo, tulisisitiza kwamba watoto wetu wahudhurie funzo la familia mara tu walipoanza kuketi.

Tukiwa wazazi, mimi na Karla tulitambua umuhimu wa kuwekea watoto wetu kielelezo kizuri kuhusiana na ibada. Tulipokuwa tukila, tukilima, au tukitembea, tulijaribu kuimarisha uhusiano wa kila mtoto pamoja na Yehova. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Tulihakikisha kwamba kila mtoto ana Biblia yake tangu utotoni. Isitoshe, nilipopokea magazeti, niliandika jina la kila mshiriki wa familia katika nakala zao. Kwa hiyo watoto walijua vitabu vyao. Tulianza kuwapatia watoto mgawo wa kusoma makala fulani za Amkeni! Baada ya chakula cha mchana Jumapili, walitueleza jinsi walivyoelewa habari hiyo.

Kuwapa Watoto Uangalifu Waliohitaji

Bila shaka, mambo hayakuwa shwari wakati wote. Kadiri watoto walivyokua, tulitambua kwamba ili kuwasaidia wasitawishe upendo mioyoni mwao tulihitaji kujua ni nini kilicho mioyoni mwao. Hiyo ilimaanisha kuwasikiliza. Nyakati nyingine watoto wetu walitulalamikia, kwa hiyo mimi na Karla, tuliketi chini na kuzungumza pamoja nao. Tulitenga wakati hususa wa nusu saa baada ya funzo la familia. Kila mtu alipewa ruhusa ya kutoa maoni yake waziwazi.

Kwa mfano, Thomas na Gabriele, watoto wetu wachanga zaidi, walihisi kwamba tulikuwa tukimpendelea ndugu yao mkubwa. Wakati mmoja walitueleza maoni yao waziwazi kwa kusema: “Baba, twaona kwamba wewe na Mama sikuzote humruhusu Hans Werner afanye apendavyo.” Mwanzoni, nilishangaa. Hata hivyo, baada ya kufikiria jambo hilo pasipo kupendelea upande wowote, mimi na Karla tulikiri kwamba watoto wetu walikuwa wamesema kweli. Kwa hiyo tukajitahidi kuwatendea sawa watoto wote.

Nyakati fulani, niliwaadhibu watoto haraka-haraka au isivyo haki. Tulipofanya hivyo, tukiwa wazazi tulijifunza kuomba msamaha. Baada ya hapo tulisali kwa Yehova. Ilifaa watoto waone kwamba baba yao alikuwa tayari kumwomba Yehova msamaha na vilevile kuwaomba watoto wake msamaha. Kwa sababu hiyo, tukawa na uhusiano mchangamfu na wa kirafiki pamoja nao. Mara nyingi walituambia, “Nyinyi ndio rafiki zetu bora zaidi.” Tulifurahi sana kusikia hivyo.

Kufanya kazi pamoja hufanya familia iwe na umoja. Ili kuwe na umoja, kila mmoja alifanya kazi za kawaida za nyumbani. Hans Werner alipewa mgawo wa kwenda dukani na kununua vitu mara moja kwa juma, kwa hiyo alipewa pesa pamoja na orodha ya ununuzi. Juma moja, hatukumpa orodha wala pesa zozote. Alimwuliza mama yake, naye akamwambia hatukuwa na pesa zozote. Watoto walianza kunong’onezeana kisha kila mmoja akaleta kisanduku chake cha pesa na kuweka pesa hizo mezani. Kisha wote wakasema, “Mama, sasa twaweza kwenda dukani!” Naam, watoto walijifunza kusaidia hali ya dharura ilipotokea, na jambo hilo lilifanya familia iwe na uhusiano wa karibu zaidi.

Kadiri walivyokua, wavulana wetu walianza kupendezwa na wasichana. Kwa mfano, Thomas alianza kuvutiwa sana na msichana fulani mwenye umri wa miaka 16. Msichana huyo alikuwa Shahidi. Nilimwambia kwamba ikiwa anapendezwa kikweli na msichana huyo, lazima awe tayari kumwoa na kuchukua daraka la kutunza mke na watoto. Thomas aling’amua kwamba hakuwa tayari kuoa, kwa kuwa alikuwa na umri wa miaka 18 tu.

Kufanya Maendeleo Tukiwa Familia

Watoto wetu wakiwa bado wachanga walijiunga na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi mmoja baada ya mwingine. Tulisikiliza kwa makini hotuba zao, na tulitiwa moyo kwa sababu tuliona kwamba watoto wetu walimpenda Mungu kutoka moyoni. Waangalizi wa mzunguko na wa wilaya ambao walikaa nasi mara kwa mara walitusimulia mambo waliyojionea au wakatusomea Biblia. Wanaume hao pamoja na wake zao walisaidia familia yetu ipendezwe na huduma ya wakati wote.

Tulitazamia kwa hamu kuhudhuria makusanyiko. Yalisaidia sana watoto wetu wasitawishe tamaa ya kuwa watumishi wa Mungu. Watoto waliona pindi hiyo kuwa muhimu walipovalia beji zao kabla ya kusafiri kwenda kwenye kusanyiko. Tuliguswa mioyo Hans Werner alipobatizwa akiwa na umri wa miaka kumi. Watu kadhaa walihisi kwamba ni mchanga mno asiweze kujiweka wakfu kwa Yehova. Hata hivyo, akiwa na umri wa miaka 50, aliniambia kwamba anashukuru kwa kumtumikia Yehova kwa miaka 40.

Tuliwaonyesha watoto wetu kwamba uhusiano wa karibu pamoja na Yehova ni jambo muhimu, lakini hatukuwalazimisha kujiweka wakfu. Hata hivyo, tulifurahi wengine walipofanya maendeleo hadi wakabatizwa walipokuwa tayari kufanya hivyo.

Twajifunza Kumtwika Yehova Mizigo Yetu

Tulifurahi sana mwaka wa 1971, wakati Hans Werner alipohitimu kutoka darasa la 51 la Shule ya Gileadi ya Watchtower na kupewa mgawo wa kutumikia akiwa mishonari nchini Hispania. Watoto hao wengine, mmoja baada ya mwingine, walitumikia wakiwa watumishi wa wakati wote, na jambo hilo lilitufurahisha sana. Ni karibu na wakati huo ndipo Hans Werner aliponipatia ile Biblia iliyotajwa mwanzoni mwa makala hii. Tulifurahi sana tukiwa familia.

Kisha tukagundua kwamba tulihitaji kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Yehova. Kwa nini? Kwa sababu tuliona baadhi ya watoto wetu wakipatwa na matatizo yaliyojaribu sana imani yao. Kwa mfano, binti yetu mpendwa Gabriele alipatwa na dhiki nyingi. Aliolewa na Lothar mwaka wa 1976 ambaye alipatwa na ugonjwa muda mfupi baada ya arusi yao. Alipozidi kudhoofika, Gabriele alimtunza hadi alipokufa. Kuona mshiriki wa familia aliyekuwa na afya nzuri akipatwa na ugonjwa na kufa kulitukumbusha jinsi tunavyohitaji msaada wenye upendo wa Yehova.—Isaya 33:2.

Mapendeleo Katika Tengenezo la Yehova

Nilipowekwa rasmi kuwa mtumishi wa kutaniko (sasa ni mwangalizi-msimamizi) mwaka wa 1955, sikuwa tayari kwa daraka hilo. Nilikuwa na kazi nyingi na siku fulani nililazimika kuamka saa kumi asubuhi ili kushughulikia mambo ya kutaniko. Mke na watoto wangu walinisaidia sana, huku wakihakikisha kwamba sikusumbuliwa jioni ambazo nilikuwa na kazi za kufanya.

Hata hivyo, tukiwa familia, tulitumia wakati mwingi pamoja kadiri tulivyoweza. Nyakati fulani mwajiri wangu aliniruhusu nitumie gari lake ili nikatembeze familia yangu. Watoto walifurahia pindi ambazo tulijifunza gazeti Mnara wa Mlinzi tukiwa msituni. Pia tulisafiri kwa miguu pamoja, huku nyakati nyingine tukiimba nyimbo kwa kufuatanisha na ala inayoitwa hamonika tukiwa katikati ya msitu.

Mwaka wa 1978 niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko wa badala (mhudumu asafiriye). Nilihisi mgawo huo ulikuwa mzito kwa hiyo nilisali hivi: “Yehova nahisi kwamba siwezi mgawo huu. Lakini ukitaka nijaribu, nitafanya yote niwezayo.” Miaka miwili baadaye, nikiwa na umri wa miaka 54, nilimwachia mwana wetu mdogo Thomas biashara yangu.

Watoto wetu wote walikuwa wakubwa, hivyo mimi na Karla tulipata fursa ya kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova. Mwaka huohuo, niliwekwa rasmi kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko na nikagawiwa eneo la Hamburg na eneo lote la Schleswig-Holstein. Kwa sababu tulikuwa tumelea watoto, tuliwaelewa wazazi vizuri zaidi pamoja na watoto wao.

Baada ya kuandamana nami katika kazi ya mzunguko kwa miaka kumi, Karla alihitaji kufanyiwa upasuaji. Mwaka huohuo, madaktari waligundua kwamba nina uvimbe wa ubongo. Kwa hiyo, niliacha kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko na kufanyiwa upasuaji wa ubongo. Baada ya miaka mitatu nikawa mwangalizi wa mzunguko wa badala. Mimi na Karla tuna umri wa miaka 70 na kitu, na tumeacha kazi ya kuzunguka. Yehova alitusaidia kuona kwamba hakuna haja ya kung’ang’ania mgawo ambao singeweza kuufanya.

Tunapokumbuka yaliyopita, Mimi na Karla tunamshukuru Yehova kwa kutuwezesha tuwasaidie watoto wetu wasitawishe upendo kwa ile kweli katika mioyo yao. (Mithali 22:6) Katika miaka yote, Yehova ametuongoza na kutuzoeza, huku akitusaidia tutekeleze majukumu yetu. Ingawa tumezeeka nasi tu dhaifu, tungali twampenda Yehova kama zamani.—Waroma 12:10, 11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, lakini sasa hakipatikani.

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 26]

Familia yetu, ikitembea kandokando ya Mto Elbe, Hamburg, mwaka wa 1965

[Malezo ya picha katika ukurasa wa 28]

Baadhi ya washiriki wa familia kwenye kusanyiko la kimataifa huko Berlin mwaka wa 1998

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 29]

Mimi na mke wangu, Karla