Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutimiza Matakwa ya Mungu Humtukuza Yehova

Kutimiza Matakwa ya Mungu Humtukuza Yehova

Kutimiza Matakwa ya Mungu Humtukuza Yehova

“Nitamtukuza kwa shukrani.”—ZABURI 69:30.

1. (a) Kwa nini Yehova anastahili kutukuzwa? (b) Tunamtukuzaje kwa shukrani?

YEHOVA ndiye Mungu mweza yote, Bwana Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu, na Muumba. Kwa sababu hiyo, jina lake na makusudi yake yanapaswa kutukuzwa. Kumtukuza Yehova kunamaanisha kumheshimu sana, kumsifu na kumhimidi kwa maneno na matendo. Kufanya hivyo “kwa shukrani” kwataka tuwe tukishukuru sikuzote kwa mambo anayotufanyia sasa na yale atakayotufanyia wakati ujao. Tunapaswa kuwa na maoni kama yale yanayoonyeshwa katika andiko la Ufunuo 4:11, ambapo viumbe waaminifu wa roho huko mbinguni wanatangaza hivi: “Wewe wastahili, Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.” Tunamtukuzaje Yehova? Kwa kujifunza juu yake kisha kufanya mambo anayotaka tufanye. Twapaswa kuhisi kama mtunga-zaburi aliposema: “Unifundishe kuyatenda mapenzi yako, kwa maana ndiwe Mungu wangu.”—Zaburi 143:10.

2. Yehova hushughulikaje na wale wanaomtukuza, na wale wasiomtukuza?

2 Yehova huthamini watu wanaomtukuza. Ndiyo sababu yeye ni “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Anawathawabishaje? Yesu alisema hivi katika sala aliyotoa kwa Baba yake wa kimbingu: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Naam, wale ‘wanaomtukuza Yehova kwa shukrani’ “watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29) Kwa upande mwingine, ‘mtu mbaya hatapata thawabu.’ (Mithali 24:20) Katika siku hizi za mwisho, tunahitaji kuanza kumtukuza Yehova bila kupoteza wakati kwa kuwa hivi karibuni ataharibu waovu na kukomboa waadilifu. “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17; Mithali 2:21, 22.

3. Kwa nini tuzingatie kitabu cha Malaki?

3 Mapenzi ya Yehova yanapatikana katika Biblia, kwa kuwa “Andiko lote limepuliziwa na Mungu.” (2 Timotheo 3:16) Neno hilo la Mungu lina masimulizi mengi yanayoonyesha jinsi ambavyo Yehova hubariki wale wanaomtukuza na kinachowapata wale wasiomtukuza. Mojawapo ya masimulizi hayo linahusu mambo yaliyotukia Israeli siku za nabii Malaki. Nabii Malaki aliandika kitabu chake yapata mwaka wa 443 K.W.K., Nehemia alipokuwa liwali wa Yuda. Kitabu hiki muhimu na chenye kuvutia, kina habari na unabii ambao ‘uliandikwa kuwa onyo kwetu sisi ambao juu yetu miisho ya mifumo ya mambo imewasili.’ (1 Wakorintho 10:11) Kuzingatia maneno ya Malaki kwaweza kutusaidia tujitayarishe kwa ajili ya “siku ile ya BWANA, iliyo kuu na kuogofya,” wakati Atakapoharibu mfumo huu mwovu.—Malaki 4:5.

4. Ni mambo gani sita yanayokaziwa katika Malaki sura ya 1?

4 Kitabu cha Malaki kilichoandikwa zaidi ya miaka 2,400 iliyopita hutusaidiaje katika karne hii ya 21 tujitayarishe kwa ajili ya siku ya Yehova iliyo kuu na itishayo? Sura ya kwanza inafanya tukazie fikira angalau mambo sita muhimu yanayotusaidia kumtukuza Yehova kwa shukrani ili tupate kibali chake na uhai udumuo milele: (1) Yehova anawapenda watu wake. (2) Tunahitaji kuonyesha kwamba tunathamini mambo matakatifu. (3) Yehova anatarajia tumpe kilicho bora zaidi. (4) Ibada ya kweli huchochewa na upendo usio na ubinafsi, haichochewi na pupa. (5) Utumishi unaokubalika kwa Mungu si takwa gumu. (6) Lazima kila mmoja wetu atoe hesabu mbele za Mungu. Hivyo basi, katika makala hii ya kwanza kati ya makala tatu zinazohusu kitabu cha Malaki, na tufikirie kila moja ya mambo hayo tunapochunguza Malaki sura ya 1.

Yehova Anawapenda Watu Wake

5, 6. (a) Kwa nini Yehova alimpenda Yakobo? (b) Tunaweza kutazamia nini tukiiga uaminifu wa Yakobo?

5 Upendo wa Yehova unafafanuliwa katika mistari ya kwanza-kwanza ya unabii wa Malaki. Kitabu hicho kinaanza kwa kusema: “Ufunuo wa neno la BWANA kwa Israeli.” Zaidi ya hayo, Mungu anasema: “Nimewapenda ninyi.” Akitaja mfano katika mstari huohuo, Yehova anasema: “Nimempenda Yakobo.” Yakobo alikuwa na imani katika Yehova. Baada ya muda, Yehova alibadili jina la Yakobo kuwa Israeli, naye akawa babu wa taifa la Israeli. Yehova alimpenda Yakobo kwa sababu alikuwa mwanamume mwenye imani. Yehova aliwapenda pia wana wa Yakobo ambao walikuwa na maoni kama ya baba yao.—Malaki 1:1, 2.

6 Tukimpenda Yehova na kushikamana na watu wake kwa uaminifu, tunaweza kupata faraja kutokana na maneno yanayopatikana katika andiko la 1 Samweli 12:22: “BWANA hatawaacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu.” Yehova anawapenda watu wake na mwishowe atawapa thawabu ya uhai udumuo milele. Kwa hiyo twasoma: “Umtumaini BWANA ukatende mema, ukae katika nchi, upendezwe na uaminifu. Nawe utajifurahisha kwa BWANA, naye atakupa haja za moyo wako.” (Zaburi 37:3, 4) Kumpenda Yehova kwahusisha jambo la pili tunalopaswa kuzingatia katika Malaki sura ya 1.

Onyesha Kwamba Unathamini Mambo Matakatifu

7. Kwa nini Yehova alimchukia Esau?

7 Kama tunavyosoma katika Malaki 1:2, 3, baada ya Yehova kusema, “nimempenda Yakobo,” asema, “Esau nimemchukia.” Kwa nini ilikuwa hivyo? Yakobo alimtukuza Yehova, lakini Esau ndugu yake pacha hakufanya hivyo. Esau pia aliitwa Edomu. Katika Malaki 1:4, nchi ya Edomu inaitwa mpaka wa uovu, na wakazi wake wanashutumiwa. Esau alipewa jina Edomu (linalomaanisha “-ekundu”) kwa sababu alimwuzia Yakobo haki yake yenye thamani ya mzaliwa wa kwanza ili apewe mchuzi wa chakula chekundu. Andiko la Mwanzo 25:34 linasema kwamba ‘Esau aliidharau haki yake ya mzaliwa wa kwanza.’ Mtume Paulo aliwahimiza waamini wenzake wawe waangalifu ili kwamba “kusipate kuwa na mwasherati wala yeyote asiyethamini mambo matakatifu, kama Esau, ambaye kwa kubadilishana na mlo mmoja alitoa haki zake za kuwa mzaliwa wa kwanza.”—Waebrania 12:14-16.

8. Ni nini kilichofanya Paulo amlinganishe Esau na mwasherati?

8 Kwa nini Paulo alimlinganisha Esau na mwasherati? Kwa sababu mtu akiwa na maoni kama ya Esau anaweza kukosa kuthamini mambo matakatifu. Kisha jambo hilo linaweza kufanya mtu atende dhambi nzito, kama vile uasherati. Kwa hiyo, huenda tukajiuliza hivi: ‘Je, nyakati nyingine ninashawishiwa kubadilisha urithi wangu wa Kikristo yaani, uhai udumuo milele na kitu cha muda tu kama vile mchuzi wa dengu? Je, huenda ikawa ninadharau mambo matakatifu pasipo kujua?’ Esau alitaka sana kutimiza tamaa ya kimwili. Alimwambia Yakobo hivi: “Harakisha tafadhali, nipe hicho chakula chekundu nile.” (Mwanzo 25:30, NW) Kwa kusikitisha, baadhi ya watumishi wa Mungu, wamesema: “Harakisha! Kwa nini ningojee kufunga ndoa yenye kuheshimika?” Tamaa yao ya kutimiza hamu ya ngono bila kujali matokeo imekuwa ndiyo bakuli yao ya mchuzi wa dengu.

9. Tunawezaje kudumisha hofu yenye staha kwa Yehova?

9 Na tusidharau kamwe mambo matakatifu kwa kupuuza usafi wa kiadili, uaminifu-maadili, na urithi wetu wa kiroho. Badala ya kuwa kama Esau, na tuwe kama Yakobo aliyekuwa mwaminifu na tudumishe hofu yenye staha kwa Mungu kwa kuonyesha kwamba tunathamini sana mambo matakatifu. Twaweza kufanyaje hivyo? Kwa kuhakikisha kwamba tunatimiza matakwa ya Yehova. Hilo linatuongoza kwenye jambo la tatu linalotajwa katika Malaki sura ya 1. Jambo gani?

Kumpa Yehova Kilicho Bora Zaidi

10. Makuhani walidharau meza ya Yehova jinsi gani?

10 Makuhani wa Yuda waliokuwa wakitumikia hekaluni huko Yerusalemu siku za Malaki hawakuwa wakimtolea Yehova dhabihu zilizo bora zaidi. Andiko la Malaki 1:6-8 linasema: “Mwana humheshimu baba yake, na mtumishi humcha bwana wake; basi, kama mimi ni baba yenu, heshima yangu iko wapi? na kama mimi ni bwana wenu, kicho changu ki wapi? BWANA wa majeshi awauliza ninyi, enyi makuhani, mnaolidharau jina langu.” Makuhani waliuliza hivi: “Tumelidharau jina lako kwa jinsi gani?” Yehova akawajibu: ‘Kwa kutoa chakula kilichotiwa unajisi juu ya madhabahu yangu,’ Kisha makuhani wakauliza, “Sisi tumekutia unajisi kwa jinsi gani?” Naye Yehova akawajibu: “Kwa sababu mwasema, meza ya BWANA ni kitu cha kudharauliwa.” Makuhani hao waliidharau meza ya Yehova kila mara walipotoa dhabihu ya mnyama aliye kilema, huku wakisema: “Si vibaya.”

11. (a) Yehova alisema nini kuhusu dhabihu zisizokubalika? (b) Ni katika njia gani watu kwa ujumla walikuwa na hatia?

11 Basi, Yehova akasababu nao kuhusu dhabihu hizo zisizokubalika kwa kuwaambia: “Haya! mtolee liwali wako; je! atakuwa radhi nawe? au atakukubali nafsi yako?” La, liwali wao hangefurahia zawadi ya namna hiyo. Bila shaka, Bwana Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu hangekubali matoleo yenye kasoro! Si makuhani peke yao waliokuwa na lawama. Ni kweli kwamba walikuwa wakimdharau Yehova kwa kudhabihu wanyama hao wagonjwa. Lakini, je, watu kwa ujumla walikuwa bila hatia? La. Watu hao walichagua wanyama vipofu, vilema, na wagonjwa na kuwaleta kwa makuhani watolewe kuwa dhabihu. Ilikuwa dhambi iliyoje!

12. Tunasaidiwaje kumpa Yehova kilicho bora zaidi?

12 Njia moja ya kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kwelikweli ni kwa kumpa kilicho bora zaidi. (Mathayo 22:37, 38) Tofauti na makuhani wasiotii wa siku za Malaki, leo tengenezo la Yehova hutoa mafundisho mazuri ya Kimaandiko ambayo hutusaidia kumtukuza Yehova kwa shukrani na kutimiza matakwa yake. Hilo linahusiana na jambo la nne linalopatikana katika Malaki sura ya 1.

Ibada ya Kweli Huchochewa na Upendo, Haichochewi na Pupa

13. Makuhani walikuwa wakifanya nini kuonyesha kwamba walichochewa na pupa?

13 Makuhani wa siku za Malaki walikuwa wenye ubinafsi, wasio na upendo, na wenye pupa ya pesa. Twajuaje hivyo? Andiko la Malaki 1:10 linasema: “Laiti angekuwapo kwenu mtu mmoja wa kuifunga milango; msije mkawasha moto bure madhabahuni pangu! Sina furaha kwenu, asema BWANA wa majeshi, wala sitakubali dhabihu yo yote mikononi mwenu.” Naam, makuhani hao wenye pupa walidai walipwe kwa ajili ya utumishi mdogo waliofanya hekaluni. Walidai walipwe kwa kufunga milango na kuwasha mioto ya madhabahu! Basi haishangazi kwamba Yehova hakukubali dhabihu yo yote mikononi mwao!

14. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Mashahidi wa Yehova huchochewa na upendo?

14 Pupa na ubinafsi wa makuhani wenye dhambi katika Yerusalemu la kale zinatukumbusha kwamba, kulingana na Neno la Mungu, watu wenye pupa hawatarithi Ufalme wa Mungu. (1 Wakorintho 6:9, 10) Tunapokumbuka kwamba makuhani hao walitaka tu kujifaidi wenyewe, tutathamini zaidi kazi ya kuhubiri inayofanywa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Kazi hii ni ya kujitolea, na tunatoa huduma yetu bila malipo. La, “sisi si wachuuzi wa neno la Mungu.” (2 Wakorintho 2:17) Kama Paulo, kila mmoja wetu anaweza kwa kweli kusema hivi: “Bila gharama nilitangaza kwenu kwa mteremo habari njema ya Mungu.” (2 Wakorintho 11:7) Ona kwamba Paulo ‘alitangaza kwa mteremo habari njema.’ Hilo linadokeza jambo la tano linalokaziwa katika Malaki sura ya 1.

Utumishi kwa Mungu Si Takwa Gumu

15, 16. (a) Makuhani walikuwa na maoni gani kuhusu kutoa dhabihu? (b) Mashahidi wa Yehova hutoaje dhabihu zao?

15 Makuhani wasio na imani katika Yerusalemu la kale waliona kutoa dhabihu kuwa takwa gumu. Ilikuwa mzigo kwao. Mungu aliwaambia hivi kama inavyoonyeshwa katika Malaki 1:13: “Mwasema, Tazama, jambo hili linatuchokesha namna gani! nanyi mmelidharau.” Makuhani hao walidharau mambo matakatifu ya Mungu. Na tusali kwa bidii tusije tukawa kama wao. Badala yake, sikuzote na tuwe na mtazamo unaoonyeshwa katika andiko la 1 Yohana 5:3: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.”

16 Na tufurahie kumtolea Mungu dhabihu za kiroho, bila kuona jambo hilo kuwa mzigo wenye kulemea kamwe. Na tutii maneno haya ya kiunabii: ‘Mkamwambie [Yehova], Ondoa maovu yote, uyatakabali yaliyo mema; na hivyo ndivyo tutakavyotoa sadaka za midomo yetu kana kwamba ni ng’ombe.’ (Hosea 14:2) Usemi “midomo yetu kana kwamba ni ng’ombe” unaonyesha dhabihu za kiroho, yaani, maneno tunayosema kumsifu Yehova na yanayohusu makusudi yake. Andiko la Waebrania 13:15 linasema hivi: “Kupitia yeye [Yesu Kristo] acheni sikuzote tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani.” Tunafurahi kama nini kwamba dhabihu zetu za kiroho si matakwa tu, bali ni udhihirisho wa moyo wote kwamba tunampenda Mungu! Hilo latuongoza kwenye jambo la sita linalopatikana katika Malaki sura ya 1.

Lazima Kila Mmoja Atoe Hesabu

17, 18. (a) Kwa nini Yehova alimlaani “mtu mwenye kudanganya”? (b) Watu wenye kudanganya walikosa kufikiria jambo gani?

17 Kama vile watu walioishi katika siku za Malaki walivyopaswa kutoa hesabu kwa sababu ya matendo yao, ndivyo na sisi. (Waroma 14:12; Wagalatia 6:5) Kupatana na hilo, Malaki 1:14 linasema: “Na alaaniwe mtu mwenye kudanganya, ambaye katika kundi lake ana mume, akaweka nadhiri, ila amtolea Bwana kitu kilicho na kilema.” Mtu yeyote aliyekuwa na kundi la wanyama, alikuwa na wanyama kadhaa. Hakuwa na mnyama mmoja tu—kwa mfano, kondoo mmoja tu—hivi kwamba hangekuwa na mwingine wa kumtoa dhabihu. Alipochagua mnyama wa kutolewa kuwa dhabihu, haingekuwa lazima achague mnyama aliye kipofu, kilema, au mgonjwa. Ikiwa angechagua mnyama mwenye kasoro, hilo lingeonyesha kwamba alidharau mpango wa Yehova wa kutoa dhabihu. Bila shaka mtu aliyekuwa na kundi la wanyama angeweza kupata mnyama asiye na kasoro yoyote!

18 Kwa hiyo, Yehova alikuwa na sababu nzuri ya kumlaani mtu mwenye kudanganya, mtu aliyekuwa na mnyama mzuri wa kiume lakini akaleta au labda akakokota mnyama aliye kipofu, kilema, au mgonjwa hadi kwa kuhani ili atolewe kuwa dhabihu. Katika unabii wa Malaki, hatusomi jambo lolote linaloonyesha kwamba kuhani fulani alinukuu sheria ya Mungu na kueleza kwamba mnyama mwenye kasoro hakubaliki. (Mambo ya Walawi 22:17-20) Mtu yeyote mwenye kufikiri alijua kwamba matokeo yangekuwa mabaya kama angejaribu kumtolea liwali zawadi kama hiyo na kudai kwamba inafaa. Kwa hakika, walikuwa wakishughulika na Yehova, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu, ambaye ni mkuu kuliko liwali yeyote. Unabii wa Malaki 1:14 unasema hivi: “Mimi ni Mfalme mkuu, asema BWANA wa majeshi, na jina langu latisha katika Mataifa.”

19. Tunatamani nini, nasi twapaswa kuwa tukifanya nini?

19 Tukiwa watumishi waaminifu wa Mungu, tunatamani sana kuona siku ambayo wanadamu wote watamheshimu Mfalme Mkuu, Yehova. Wakati huo, “dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:9) Kwa sasa, na tufanye yote tuwezayo kutimiza viwango vya Yehova kwa kumwiga mtunga-zaburi aliyesema hivi: “Nitamtukuza kwa shukrani.” (Zaburi 69:30) Ili kutimiza hilo, Malaki ana shauri lingine linaloweza kutunufaisha sana. Na tuchunguze kwa uangalifu sehemu nyingine za kitabu cha Malaki katika makala mbili zifuatazo.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini tumtukuze Yehova?

• Kwa nini Yehova alikataa dhabihu za makuhani siku za Malaki?

• Tunamtoleaje Yehova dhabihu ya sifa?

• Ni nini kinachopaswa kutuchochea katika ibada ya kweli?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Unabii wa Malaki unahusu siku zetu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Esau hakuthamini mambo matakatifu

[Picha katika ukurasa wa 11]

Makuhani na watu kwa ujumla walitoa dhabihu zisizokubalika

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote hutoa dhabihu za sifa bila malipo