Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yohana aliona “umati mkubwa” ukimtolea Yehova utumishi mtakatifu katika sehemu gani ya hekalu?—Ufunuo 7:9-15.

Ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba umati mkubwa humwabudu Yehova katika mojawapo ya nyua za kidunia za hekalu lake kubwa la kiroho, hasa ua unaofananishwa na ua wa nje wa hekalu la Solomoni.

Hapo awali, ilisemekana kwamba mkutano mkubwa uko katika hali ya kiroho inayofananishwa na Ua wa wasio Wayahudi uliokuwepo katika siku za Yesu. Hata hivyo, utafiti zaidi umeonyesha sababu tano hivi zinazoonyesha kwamba hivyo sivyo ilivyo. Kwanza, si sehemu zote za hekalu la Herode zilizo na ufananisho katika hekalu kubwa la kiroho la Yehova. Kwa mfano, hekalu la Herode lilikuwa na Ua wa Wanawake na Ua wa Waisraeli. Wanaume kwa wanawake wangeweza kuingia katika Ua wa Wanawake, lakini ni wanaume peke yao walioruhusiwa kuingia katika Ua wa Waisraeli. Katika nyua za kidunia za hekalu kubwa la kiroho la Yehova, wanaume kwa wanawake wanaabudu pamoja. (Wagalatia 3:28, 29) Kwa hiyo, hakuna kitu kinachofananisha Ua wa Wanawake na Ua wa Waisraeli katika hekalu la kiroho.

Pili, hakukuwa na Ua wa wasio Wayahudi katika plani zilizotolewa na Mungu za kujenga hekalu la Solomoni au hekalu ambalo Ezekieli aliona katika maono; wala hakukuwa na Ua wa wasio Wayahudi katika hekalu lililojengwa upya na Zerubabeli. Kwa hiyo, hakuna sababu ya kuamini kwamba Ua wa wasio Wayahudi una ufananisho wa kiroho katika mpango wa ibada katika hekalu kubwa la kiroho la Yehova, hasa tunapofikiria jambo linalofuata.

Tatu, Ua wa wasio Wayahudi ulijengwa na Mfalme Herode wa Edomu ili kujitukuza mwenyewe na kupata kibali cha Waroma. Herode alianza kurekebisha hekalu lililojengwa na Zerubabeli labda katika mwaka wa 18 au 17 K.W.K. Kichapo The Anchor Bible Dictionary chasema hivi: ‘Watawala wa Roma ya kale walitaka hekalu kubwa zaidi ya mahekalu yaliyojengwa katika majiji ya mashariki.’ Hata hivyo, vipimo vya hekalu tayari vilikuwa vimewekwa. Kamusi hiyo yatoa maelezo haya: “Ingawa Hekalu lenyewe lingetoshana kwa ukubwa na [hekalu lililojengwa na Solomoni na Zerubabeli], Hekalu la Mlimani lingekuwa na ukubwa wowote.” Kwa hiyo, Herode alipanua eneo la hekalu kwa kuongezea sehemu ambayo sasa inaitwa Ua wa wasio Wayahudi. Inawezekanaje basi hekalu lililojengwa chini ya hali hizo liwe na ufananisho fulani katika mpango wa kumwabudu Yehova katika hekalu la kiroho?

Nne, karibu kila mtu—vipofu, vilema, na watu wasio Wayahudi na wasiotahiriwa—wangeweza kuingia katika Ua wa wasio Wayahudi. (Mathayo 21:14, 15) Ni kweli kwamba, ua huo ulitumiwa na watu wengi wasio Wayahudi na wasiotahiriwa ambao wangetaka kumtolea Mungu matoleo. Nyakati fulani Yesu alitumia ua huo kuhutubia umati na mara mbili akawafukuza wabadili-fedha na wafanyabiashara, na kuwaambia kwamba hawakuheshimu nyumba ya Baba yake. (Mathayo 21:12, 13; Yohana 2:14-16) Hata hivyo, kichapo The Jewish Encyclopedia chasema: “Kwa kweli ua huo wa nje, haukuwa sehemu ya hekalu. Ardhi yake haikuwa takatifu, na mtu yeyote angeweza kuingia humo.”

Tano, neno la Kigiriki (hi.e.·e·ron’) linalotafsiriwa “hekalu” ambalo limetumiwa kurejezea Ua wa wasio Wayahudi “linarejezea jengo lenyewe na maeneo yote yaliyolizunguka wala si Hekalu peke yake,” chasema kichapo A Handbook on the Gospel of Matthew cha Barclay M. Newman na Philip C. Stine. Kwa kutofautisha, neno la Kigiriki (na.·os’) linalotafsiriwa “hekalu” katika maono ya Yohana ya umati mkubwa lina maana hususa zaidi. Kuhusiana na hekalu la Yerusalemu, mara nyingi neno hilo hurejezea Patakatifu Zaidi, jengo lenyewe, au maeneo yanayozunguka hekalu. Nyakati nyingine neno hilo hutafsiriwa “patakatifu.”—Mathayo 27:5, 51; Luka 1:9, 21; Yohana 2:20.

Umati mkubwa hudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. Wao ni safi kiroho, kwa kuwa “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Kwa hiyo, wanatangazwa kuwa waadilifu na wana tumaini la kuwa rafiki za Mungu na kuokoka dhiki kubwa. (Yakobo 2:23, 25) Katika mambo mengi, wanafanana na wageuzwa-imani katika Israeli ambao walitii agano la Sheria na kuabudu pamoja na Waisraeli.

Bila shaka, wageuzwa-imani hao hawakutumikia katika ua wa ndani ambapo makuhani walifanya kazi zao. Nao washiriki wa umati mkubwa hawamo katika ua wa ndani wa hekalu kubwa la kiroho la Yehova. Ua huo wa ndani unafananisha hali kamilifu na adilifu ya wana wa kibinadamu ambao wanakuwa sehemu ya “ukuhani mtakatifu” wa Yehova wanapokuwa hapa duniani. (1 Petro 2:5) Lakini, kama vile mzee wa mbinguni alivyomwambia Yohana, kwa kweli umati mkubwa uko hekaluni, si nje ya hekalu halisi, mahali panapoonwa kuwa Ua wa wasio Wayahudi. Hilo ni pendeleo lililoje! Nalo linakazia uhitaji wa kila mmoja wetu kudumisha usafi wa kiroho na wa kiadili nyakati zote!

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 31]

 

Hekalu la Solomoni

1. Hekalu

2. Ua wa Ndani

3. Ua wa Nje

4. Ngazi za Ua wa Hekalu