Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Atakayeokoka Siku ya Yehova?

Ni Nani Atakayeokoka Siku ya Yehova?

Ni Nani Atakayeokoka Siku ya Yehova?

“Siku ile inakuja, inawaka kama tanuru.”—MALAKI 4:1.

1. Malaki anafafanuaje mwisho wa mfumo huu mwovu?

NABII Malaki alipuliziwa na Mungu kuandika unabii unaohusu mambo yenye kutisha yatakayotokea hivi karibuni. Mambo hayo yataathiri kila mtu duniani. Andiko la Malaki 4:1 linatabiri hivi: “Angalieni, siku ile inakuja, inawaka kama tanuru; na watu wote wenye kiburi, nao wote watendao uovu, watakuwa makapi; na siku ile inayokuja itawateketeza, asema BWANA wa majeshi; hata haitawaachia shina wala tawi.” Uharibifu wa mfumo huu mwovu wa mambo utakuwa kamili kadiri gani? Utakuwa kama mti ambao mizizi yake imeharibiwa kabisa ili usipate kukua tena.

2. Maandiko fulani yanafafanuaje ile siku ya Yehova?

2 Huenda ukauliza, ‘Ni “siku” gani hiyo inayotabiriwa na nabii Malaki?’ Ni siku ileile inayotajwa katika andiko la Isaya 13:9, linalosema: “Tazama, siku ya BWANA inakuja, siku kali, ya hasira na ghadhabu kuu, ili iifanye nchi kuwa ukiwa, na kuwaharibu watu wake, wenye dhambi, wasikae ndani yake.” Andiko la Sefania 1:15 linatoa ufafanuzi huu linaposema: “Siku ile ni siku ya ghadhabu, siku ya fadhaa na dhiki, siku ya uharibifu na ukiwa, siku ya giza na utusitusi, siku ya mawingu na giza kuu.”

“Dhiki Kubwa”

3. ‘Siku ya Yehova’ ni nini?

3 Katika utimizo mkubwa wa unabii wa Malaki, ‘siku ya Yehova’ ni wakati wa “dhiki kubwa.” Yesu alitabiri hivi: “Maana ndipo kutakuwa na dhiki kubwa ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu hadi sasa, la, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21) Ebu fikiria jinsi ulimwengu ulivyopata dhiki, hasa tangu mwaka wa 1914. (Mathayo 24:7-12) Watu zaidi ya milioni 50 walikufa katika Vita ya Pili ya Ulimwengu! Hata hivyo, “dhiki kubwa” itafanya matukio hayo kuwa duni. Dhiki kubwa sawa na siku ya Yehova itaisha wakati wa Har–Magedoni, na kukomesha siku za mwisho za mfumo huu mwovu.—2 Timotheo 3:1-5, 13; Ufunuo 7:14; 16:14, 16.

4. Ni nini kitakachotokea mwishoni mwa siku ya Yehova?

4 Mwishoni mwa siku hiyo ya Yehova, ulimwengu wa Shetani na wale wanaouunga mkono watakuwa wameangamizwa. Dini isiyo ya kweli ndiyo itakayoharibiwa kwanza. Kisha Yehova atatekeleza hukumu yake dhidi ya mfumo wa Shetani wa kisiasa na wa kiuchumi. (Ufunuo 17:12-14; 19:17, 18) Ezekieli atabiri hivi: “Watatupa fedha yao katika njia kuu za mji, na dhahabu yao itakuwa kama kitu cha unajisi; fedha yao na dhahabu yao hazitaweza kuwaokoa siku ya ghadhabu ya BWANA.” (Ezekieli 7:19) Andiko la Sefania 1:14 lasema hivi kuhusu siku hiyo: “Hiyo siku ya BWANA iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka sana.” Kwa kuzingatia yale ambayo Biblia inasema kuhusu siku ya Yehova, twapaswa kuazimia kutenda kupatana na matakwa ya Mungu ya uadilifu.

5. Wale wanaohofu jina la Yehova wanapata nini?

5 Baada ya kutabiri mambo yatakayoupata ulimwengu wa Shetani katika siku ya Yehova, andiko la Malaki 4:2 lamnukuu Yehova akisema: “Kwenu ninyi mnaolicha [“mnaolihofu,” NW] jina langu, jua la haki litawazukia, lenye kuponya katika mbawa zake; nanyi mtatoka nje, na kuchezacheza kama ndama wa mazizini.” “Jua la haki” ni Yesu Kristo. Yeye ndiye ‘nuru ya kiroho ya ulimwengu.’ (Yohana 8:12) Yesu anaangaza kwa kuponya—kwanza kwa uponyaji wa kiroho tunaoshuhudia leo, kisha uponyaji kamili wa kimwili katika ulimwengu mpya. Kama Yehova asemavyo, walioponywa ‘watatoka nje, na kuchezacheza kama ndama wa mazizini’ ambao wamesisimuka na kufurahia kuachiliwa kutoka kifungoni.

6. Watumishi wa Yehova watashiriki sherehe gani ya ushindi?

6 Namna gani watu wanaopuuza matakwa ya Yehova? Andiko la Malaki 4:3 linasema hivi: “Nanyi, [watumishi wa Mungu] mtawakanyaga waovu; maana watakuwa majivu chini ya nyayo za miguu yenu; katika siku ile niifanyayo, asema BWANA wa majeshi.” Wanadamu wanaomwabudu Mungu hawatashiriki kuharibu ulimwengu wa Shetani. Badala yake, ‘watawakanyaga waovu’ kwa njia ya mfano kwa kushiriki sherehe ya ushindi mkubwa baada ya siku ya Yehova. Kulikuwa na sherehe kubwa baada ya Farao na majeshi yake kuangamizwa katika Bahari Nyekundu. (Kutoka 15:1-21) Vivyo hivyo, kutakuwa na sherehe ya ushindi baada ya Shetani na ulimwengu wake kuondolewa wakati wa dhiki kubwa. Waaminifu watakaookoka siku ya Yehova watasema: “Na tushangilie na kuufurahia wokovu wake.” (Isaya 25:9) Kutakuwa na shangwe iliyoje kuona enzi kuu ya Yehova ikitetewa na dunia kusafishwa ili ikaliwe kwa amani!

Jumuiya ya Wakristo Yaiga Israeli

7, 8. Eleza jinsi hali ya kiroho ya Israeli ilivyokuwa katika siku za Malaki.

7 Wale wanaopata kibali cha Yehova ni wale tu wanaomtumikia. Ndivyo ilivyokuwa Malaki alipoandika kitabu chake. Mnamo mwaka wa 537 K.W.K., mabaki wa Israeli walikuwa wamerudishwa baada ya kuwa utekwani miaka 70 huko Babiloni. Hata hivyo, miaka 100 iliyofuata, taifa hilo lililorudishwa lilianza kuasi imani na kutenda maovu tena. Watu wengi walikuwa wakilidharau jina la Yehova, wakipuuza sheria zake za uadilifu; kuchafua hekalu lake kwa kuleta wanyama walio vipofu, walemavu, na wagonjwa ili watolewe kuwa dhabihu; na kutaliki wake wa ujana wao.

8 Kwa hiyo, Yehova aliwaambia hivi: “Nitawakaribieni ili kuhukumu; nami nitakuwa shahidi mwepesi juu ya wachawi, na juu ya wazinzi, na juu yao waapao kwa uongo; na juu yao wamwoneao mwenye kuajiriwa, kwa ajili ya mshahara wake, wamwoneao mjane na yatima, na kumpotosha mgeni asipate haki yake, wala hawaniogopi mimi, . . . Kwa kuwa mimi, BWANA, sina kigeugeu.” (Malaki 3:5, 6) Hata hivyo, Yehova aliwaalika watu ambao huenda wangeacha njia zao mbaya: “Nirudieni mimi, nami nitawarudia ninyi.”—Malaki 3:7.

9. Unabii wa Malaki ulitimizwaje kwa mara ya kwanza?

9 Maneno hayo yalitimia pia katika karne ya kwanza W.K. Mabaki wa Wayahudi walimtumikia Yehova na wakawa sehemu ya “taifa” jipya la Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho. Baadaye taifa hilo lilitia ndani watu wasio Wayahudi. Lakini Waisraeli wengi wa asili walimkataa Yesu. Kwa hiyo, Yesu aliliambia hivi taifa hilo la Israeli “Tazameni! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:38; 1 Wakorintho 16:22) Katika mwaka wa 70 W.K., kama ilivyotabiriwa kwenye Malaki 4:1, ‘siku inayowaka kama tanuru’ iliwajilia Waisraeli wa asili. Yerusalemu na hekalu lake liliharibiwa, na watu zaidi ya milioni moja wakafa kwa sababu ya njaa, kung’ang’ania mamlaka, na mashambulizi yaliyofanywa na majeshi ya Roma. Hata hivyo, wale waliomtumikia Yehova hawakupatwa na dhiki hiyo.—Marko 13:14-20.

10. Watu wa kawaida na makasisi wameigaje taifa la Israeli la karne ya kwanza?

10 Wanadamu, na hasa Jumuiya ya Wakristo wameiga taifa la Israeli la karne ya kwanza. Viongozi na watu wa kawaida wanazidi kupendelea imani za dini isiyo ya kweli badala ya ile kweli kuhusu Mungu ambayo Yesu alifundisha. Makasisi ndio wanaolaumika hasa. Wanakataa kutumia jina la Yehova, na hata wameliondoa katika tafsiri mbalimbali za Biblia. Wanamdharau Yehova kwa mafundisho yasiyopatana na Maandiko, kama vile mafundisho ya kipagani ya kuteswa milele katika moto wa mateso, Utatu, kutokufa kwa nafsi, na mageuzi. Kwa hiyo, sawa na makuhani katika siku za Malaki, wanakosa kumpa Yehova sifa anayostahili.

11. Dini za ulimwengu zinaonyeshaje mungu wanayemtumikia hasa?

11 Siku za mwisho zilipoanza mwaka wa 1914, dini za ulimwengu huu zikiongozwa na zile zinazodai kuwa za Kikristo, zilionyesha ni mungu yupi wanayemtumikia hasa. Wakati wa Vita ya Kwanza na ya Pili ya Ulimwengu, waliwatia wafuasi wao moyo waende vitani kwa sababu ya mizozo ya kitaifa hata kama kufanya hivyo kungemaanisha kuua watu wa dini zao. Neno la Mungu linatambulisha waziwazi wale wanaomtii Yehova na wale wasiomtii linaposema: “Watoto wa Mungu na watoto wa Ibilisi ni dhahiri kwa jambo hili: Kila mtu ambaye haendelezi uadilifu hatokani na Mungu, wala yeye ambaye hapendi ndugu yake. Kwa maana huu ndio ujumbe ambao mmesikia tangu mwanzo, kwamba twapaswa tupendane; si kama Kaini, ambaye alitokana na yule mwovu akamchinja ndugu yake.”—1 Yohana 3:10-12.

Kutimiza Unabii

12, 13. Ni unabii gani ambao umetimizwa na watumishi wa Mungu sasa?

12 Kufikia mwisho wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu mwaka wa 1918, watumishi wa Yehova wangeweza kutambua kwamba Mungu alikuwa amehukumia uharibifu Jumuiya ya Wakristo pamoja na dini zote zisizo za kweli. Kuanzia wakati huo na kuendelea, mwito ulitolewa kwa watu wenye mioyo minyofu: “Tokeni kwake, watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake, na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya tauni zake. Kwa maana dhambi zake zimetungamana pamoja hadi mbinguni, na Mungu amekumbuka matendo yake yasiyo ya haki.” (Ufunuo 18:4, 5) Wale waliotamani kwelikweli kumtumikia Yehova walianza kusafishwa na kuondolewa madoa yote ya dini isiyo ya kweli, kisha wakaanza kuhubiri ulimwenguni pote habari njema ya Ufalme uliosimamishwa, kazi ambayo ingekamilishwa kabla ya mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo.—Mathayo 24:14.

13 Walifanya hivyo ili kutimiza unabii unaopatikana katika andiko la Malaki 4:5 ambapo Yehova alisema: “Angalieni, nitawapelekea Eliya nabii, kabla haijaja siku ile ya BWANA, iliyo kuu na kuogofya.” Unabii huo ulitimizwa kwanza kupitia kazi iliyofanywa na Yohana Mbatizaji, aliyefananishwa na Eliya. Yohana alifanya kazi kama ya Eliya alipowabatiza Wayahudi waliokuwa wametubu dhambi walizokuwa wamefanya dhidi ya agano la Sheria. Jambo la maana hata zaidi ni kwamba Yohana alikuwa mtangulizi wa Mesiya. Hata hivyo, kazi ya Yohana ilikuwa utimizo mdogo tu wa unabii wa Malaki. Yesu akizungumza kuhusu Yohana kuwa Eliya wa pili, alionyesha kwamba kazi ya “Eliya” bado ingefanywa wakati ujao.—Mathayo 17:11, 12.

14. Ni kazi gani muhimu inayopaswa kufanywa kabla mfumo huu haujaisha?

14 Unabii wa Malaki ulionyesha kwamba kazi hiyo kubwa ya Eliya ingefanywa kabla ya ‘siku ya Yehova iliyo kuu na kuogofya.’ Siku hiyo yamalizika wakati wa vita inayokaribia sana ya siku kuu ya Mungu Mweza Yote, kwenye Har–Magedoni. Hiyo yamaanisha kwamba kabla ya mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo na kabla ya kuanza kwa Utawala wa Miaka Elfu wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu chini ya Yesu Kristo aliyetawazwa, kazi inayofanana na ya Eliya ingefanywa. Kupatana na unabii huo, kabla Yehova hajaharibu mfumo huu mwovu, jamii ya kisasa ya Eliya, ikiungwa mkono na mamilioni ya Wakristo wenzao wenye tumaini la kuishi duniani, kwa shauku wanafanya kazi ya kurudisha ibada safi, wakilihimidi jina la Yehova na kufundisha watu wenye mfano wa kondoo kweli za Biblia.

Yehova Hubariki Watumishi Wake

15. Yehova huwakumbukaje watumishi wake?

15 Yehova hubariki wale wanaomtumikia. Andiko la Malaki 3:16 linasema: “Ndipo wale waliomcha BWANA waliposemezana wao kwa wao. Naye BWANA akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha BWANA, na kulitafakari jina lake.” Kuanzia Abeli na kuendelea, ni kana kwamba Mungu amekuwa akiandika majina ya wale ambao atawakumbuka na kuwapa uhai udumuo milele. Yehova anasema hivi kuwahusu: “Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, asema BWANA wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la.”—Malaki 3:10.

16, 17. Yehova amewabarikije watu wake na kazi yao?

16 Kwa kweli Yehova amewathawabisha wale wanaomtumikia. Jinsi gani? Njia moja ni kwa kuwapa ufahamu zaidi wa makusudi yake. (Mithali 4:18; Danieli 12:10) Njia nyingine ni kwa kuwawezesha wapate matokeo mazuri katika kazi yao ya kuhubiri. Watu wengi wenye mioyo minyofu wamejiunga nao katika ibada ya kweli, nao wanafanyiza “umati mkubwa . . . kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha, . . . nao wafuliza kulia kwa sauti kubwa, wakisema: ‘Sisi tunawiwa wokovu na Mungu wetu, aketiye juu ya hicho kiti cha ufalme, na kwa Mwana-Kondoo.’” (Ufunuo 7:9, 10) Umati huo mkubwa umedhihirishwa kwa njia ya kustaajabisha, na wale wanaomtumikia Yehova sasa ni zaidi ya milioni sita katika makutaniko zaidi ya 93,000 duniani pote!

17 Yehova amethawabisha Mashahidi wa Yehova pia kwa vichapo vinavyozungumzia habari ya Biblia ambavyo vimegawanywa kwa wingi zaidi katika historia yote. Sasa nakala zipatazo milioni 90 za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! huchapishwa kila mwezi; Mnara wa Mlinzi huchapishwa katika lugha 144 na Amkeni! katika lugha 87. Nakala milioni 107 za kitabu cha kujifunzia Biblia, Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, kilichochapishwa mwaka wa 1968, ziligawanywa katika lugha 117. Nakala milioni 81 za kitabu, Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kilichotolewa mwaka wa 1982, ziligawanywa katika lugha 131. Nakala zaidi ya milioni 85 za kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichotolewa mwaka wa 1995, zimegawanywa katika lugha 154. Kufikia sasa nakala zipatazo milioni 150 za broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? iliyochapishwa mwaka wa 1996 tayari zimegawanywa katika lugha 244.

18. Kwa nini tunafurahia ufanisi wa kiroho licha ya upinzani?

18 Kumekuwa na ufanisi wa kiroho licha ya upinzani mkali na wenye kuendelea kutoka kwa ulimwengu wa Shetani. Ufanisi huo unaonyesha ukweli wa maneno ya Isaya 54:17: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa BWANA, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema BWANA.” Watumishi wa Yehova wanafarijika kama nini kujua kwamba unabii wa Malaki 3:17, unatimia kwao kwa kiwango kikubwa: “Nao watakuwa wangu, asema BWANA wa majeshi, katika siku ile niifanyayo; naam, watakuwa hazina yangu hasa.”

Kumtumikia Yehova kwa Shangwe

19. Wale wanaomtumikia Yehova wanatofautianaje na wale wasiomtumikia?

19 Tofauti iliyopo kati ya watumishi waaminifu wa Yehova na wale walio katika ulimwengu wa Shetani inazidi kudhihirika kila siku. Andiko la Malaki 3:18 lilitabiri: “Ndipo mtakaporudi, nanyi mtapambanua kati ya wenye haki na waovu, na kati ya yeye amtumikiaye Mungu na yeye asiyemtumikia.” Mojawapo ya tofauti zilizopo ni kwamba wale wanaomtumikia Yehova hufanya hivyo kwa shangwe kuu. Kati ya mambo yanayowaletea shangwe ni tumaini zuri walilo nalo. Wanamwamini Yehova kabisa anaposema: “Mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo.”—Isaya 65:17, 18; Zaburi 37:10, 11, 29; Ufunuo 21:4, 5.

20. Kwa nini sisi ni wenye shangwe?

20 Tunaamini ahadi ya Yehova kwamba watu wake wote waaminifu wataokoka siku hiyo kuu na kuingia katika ulimwengu mpya. (Sefania 2:3; Ufunuo 7:13, 14) Na hata ingawa wengine kwa sababu ya umri, ugonjwa, au aksidenti huenda wakafa kabla ulimwengu mpya haujaja, Yehova anawahakikishia kwamba atawafufua, wakiwa na taraja la kupata uhai udumuo milele. (Yohana 5:28, 29; Tito 1:2) Kwa hiyo ingawa sote tuna matatizo na magumu, tunapokaribia siku hiyo ya Yehova, tuna kila sababu ya kuwa watu wenye shangwe zaidi duniani.

Ungejibuje?

• ‘Siku ya Yehova’ ni nini?

• Dini za ulimwengu zinaigaje Israeli la kale?

• Watumishi wa Yehova hutimiza unabii gani?

• Yehova amewabarikije watu wake?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Yerusalemu ya karne ya kwanza ‘iliwaka kama tanuru’

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yehova huwatimizia mahitaji wale wanaomtumikia

[Picha katika ukurasa wa 24]

Watumishi wa Yehova ni wenye shangwe kwelikweli kwa sababu ya tumaini lao zuri