Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Huchukia Mwenendo wa Hila

Yehova Huchukia Mwenendo wa Hila

Yehova Huchukia Mwenendo wa Hila

‘Msitendeane mambo ya hiana [“hila,” “NW”].’—MALAKI 2:10.

1. Mungu anataka tufanye nini ili tupokee uhai udumuo milele?

JE, UNGEPENDA kuishi milele? Ikiwa unatumaini ahadi hiyo inayopatikana katika Biblia, huenda ukajibu, ‘Bila shaka.’ Lakini ikiwa unataka Mungu akupatie uhai udumuo milele katika ulimwengu wake mpya, utahitaji kutimiza matakwa yake. (Mhubiri 12:13; Yohana 17:3) Je, tunaweza kutarajia wanadamu wasio wakamilifu wafanye hivyo? Ndiyo, kwa kuwa Yehova anasema maneno haya yenye kutia moyo: “Nataka fadhili wala si sadaka; na kumjua Mungu kuliko sadaka za kuteketezwa.” (Hosea 6:6) Kwa hiyo hata wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kutimiza viwango vya Mungu.

2. Waisraeli wengi walimtendaje Yehova mambo ya hila?

2 Hata hivyo, si wanadamu wote wanaotaka kufanya mapenzi ya Yehova. Hosea anaonyesha kwamba hata Waisraeli wengi hawakutaka kufanya hivyo. Wakiwa taifa, walikuwa wamekubali kufanya agano na Mungu na kutii sheria zake. (Kutoka 24:1-8) Hata hivyo, baada ya muda mfupi, walikuwa ‘wakilivunja hilo agano’ kwa kutotii sheria zake. Kwa hiyo, Yehova alisema kwamba Waisraeli hao ‘walimtenda mambo ya hila.’ (Hosea 6:7, NW) Na tangu wakati huo, watu wengi wamefanya hivyo. Yehova huchukia mwenendo wa hila, iwe ni yeye anayetendwa kwa hila au ni wale wanaompenda na kumtumikia wanaotendwa hivyo.

3. Ni mambo gani yatakayochunguzwa katika funzo hili?

3 Si nabii Hosea peke yake aliyekazia maoni hayo ya Mungu kuhusu hila, maoni ambayo tunapaswa kuwa nayo ikiwa tunatumaini kuishi maisha yenye furaha. Katika makala iliyotangulia, tulichunguza ujumbe wa kiunabii wa Malaki, kuanzia sura ya kwanza ya kitabu chake. Sasa na tufungue sura ya pili ya kitabu hicho, na tuone jinsi maoni ya Mungu kuhusu hila yanavyozidi kukaziwa. Ingawa Malaki alikuwa akishughulika na hali iliyokuwako miongoni mwa watu wa Mungu miongo kadhaa baada ya kurudi kutoka Babiloni, sura hii ya pili ina maana halisi kwetu leo.

Makuhani Wenye Kulaumika

4. Yehova aliwapa makuhani onyo gani?

4 Sura ya 2 inaanza kwa kuonyesha jinsi Yehova anavyowashutumu makuhani Wayahudi kwa sababu ya kuacha njia zake za uadilifu. Makuhani hao wasipotii shauri lake na kurekebisha mwenendo wao, watapatwa na matokeo mabaya sana. Ona mistari miwili ya kwanza: “Enyi makuhani, amri hii yawahusu ninyi. Kama hamtaki kusikia, na kama hamtaki kuitia moyoni, ili kulitukuza jina langu, asema BWANA wa majeshi, basi nitawapelekeeni laana, nami nitazilaani baraka zenu.” Kama makuhani wangewafundisha watu amri za Mungu na kuzitii, wangebarikiwa. Lakini kwa sababu ya kupuuza mapenzi ya Mungu, wangelaaniwa. Hata baraka ambazo makuhani walitangaza zingelaaniwa.

5, 6. (a) Kwa nini makuhani ndio waliolaumika hasa? (b) Yehova alionyeshaje kwamba aliwadharau makuhani?

5 Kwa nini makuhani ndio waliolaumika hasa? Mstari wa 7 unaonyesha jambo moja lililo wazi: “Yapasa midomo ya kuhani ihifadhi maarifa, tena yawapasa watu kuitafuta sheria kinywani mwake; kwa kuwa yeye ni mjumbe wa BWANA wa majeshi.” Zaidi ya miaka elfu moja mapema, sheria za Mungu ambazo Waisraeli walipewa kupitia Musa zilisema kwamba makuhani walikuwa na daraka la ‘kuwafundisha wana wa Israeli amri zote ambazo Yehova aliwaambia.’ (Mambo ya Walawi 10:11) Kwa kusikitisha, baadaye mwandishi wa 2 Mambo ya Nyakati 15:3 aliripoti hivi: “Tangu siku nyingi Israeli wamekuwa hawana Mungu wa kweli, wala hawana kuhani afundishaye, wala hawana torati.”

6 Wakati wa Malaki, katika karne ya tano K.W.K., hali ya makuhani ilikuwa sawa na hiyo. Walikosa kuwafundisha watu Sheria ya Mungu. Kwa hiyo makuhani hao walipaswa kutozwa hesabu. Ona jinsi Yehova anavyowakemea kwa ukali. Andiko la Malaki 2:3 lasema: “Nitapaka nyuso zenu mavi, naam, mavi ya sadaka zenu.” Hilo ni kemeo kali kama nini! Mavi ya wanyama waliotolewa dhabihu yalipaswa kupelekwa nje ya kambi na kuchomwa. (Mambo ya Walawi 16:27) Lakini Yehova anapowaambia kwamba atapaka nyuso zao mavi, anaonyesha waziwazi kwamba alidharau na kukataa dhabihu zao na wenye kuzitoa.

7. Kwa nini Yehova aliwakasirikia walimu wa Sheria?

7 Karne kadhaa kabla ya siku za Malaki, Yehova aliwapa Walawi kazi ya kutunza tabenakulo na baadaye akawapa kazi ya kutunza hekalu na kufanya utumishi mtakatifu hekaluni. Walikuwa walimu katika taifa la Israeli. Kama wangetimiza mgawo huo, wao na taifa lao wangeendelea kuishi na wangekuwa na amani. (Hesabu 3:5-8) Lakini Walawi waliacha kumwogopa Mungu. Kwa hiyo, Yehova aliwaambia hivi: ‘Mmegeuka mkaiacha njia; mmewakwaza watu wengi katika sheria; mmeliharibu agano la Lawi, hamkuzishika njia zangu.’ (Malaki 2:8, 9) Kwa kushindwa kufundisha kweli na kwa kielelezo chao kibaya, makuhani waliwapotosha Waisraeli wengi, kwa hiyo Yehova alikuwa na sababu nzuri ya kuwakasirikia.

Kutimiza Viwango vya Mungu

8. Je, wanadamu wanaweza kutimiza viwango vya Mungu? Eleza.

8 Tusifikiri kwamba makuhani hao walipaswa kuhurumiwa na kusamehewa kwa sababu walikuwa wanadamu tu wasio wakamilifu na wasioweza kutimiza viwango vya Mungu. Ukweli ni kwamba wanadamu wanaweza kushika amri za Mungu, kwa kuwa Yehova hatazamii wafanye mambo yanayozidi uwezo wao. Huenda ikawa makuhani fulani wa wakati huo walitimiza viwango vya Mungu, na kuna kuhani mmoja aliyevitimiza baadaye. Huyo alikuwa Yesu, “kuhani wa cheo cha juu.” (Waebrania 3:1) Kwa kweli, ingeweza kusemwa hivi kumhusu: “Sheria ya kweli ilikuwa kinywani mwake, wala udhalimu haukuonekana midomoni mwake; alikwenda pamoja nami katika amani na unyofu, na kuwageuza wengi hata wakaacha uovu.”—Malaki 2:6.

9. Ni nani wanaoandaa kwa uaminifu kweli za Biblia wakati wetu?

9 Hali kadhalika, kwa muda unaozidi karne moja sasa, ndugu watiwa-mafuta wa Kristo ambao wana tumaini la kuishi mbinguni, wametumikia wakiwa “ukuhani mtakatifu, ili kutoa dhabihu za kiroho zenye kukubalika kwa Mungu.” (1 Petro 2:5) Wanaongoza katika kuandalia wengine kweli za Biblia. Wewe mwenyewe umejionea kutokana na kweli ambazo wanafundisha kwamba sheria ya kweli iko kinywani mwao. Sivyo? Wamesaidia wengi waache mafundisho ya dini isiyo ya kweli, na sasa kuna mamilioni ya watu ulimwenguni pote ambao wamejifunza kweli za Biblia na ambao wana tumaini la kuishi milele. Watu hao nao wana pendeleo la kufundisha mamilioni ya wengine sheria ya kweli.—Yohana 10:16; Ufunuo 7:9.

Kwa Nini Tuwe Macho?

10. Kwa nini twapaswa kuwa macho?

10 Hata hivyo, tunapaswa kuwa macho. Tunaweza kukosa kufahamu masomo tunayofundishwa kwenye Malaki 2:1-9. Je, tuko macho udhalimu usionekane midomoni mwetu? Kwa mfano, je, washiriki wa familia yetu wanaweza kuamini kabisa yale tusemayo? Je, ndugu na dada zetu wa kiroho katika kutaniko wanaweza kuamini tusemayo? Inaweza kuwa rahisi sana kuzoea kusema mambo yanayosikika kuwa kweli kumbe unataka kuwapotosha wengine kimakusudi. Au huenda mtu akatilia chumvi au akaficha habari fulani katika shughuli za kibiashara. Je, Yehova hataona jambo hilo? Tukiwa na mazoea kama hayo, je, atakubali dhabihu za sifa kutoka vinywani mwetu?

11. Ni nani hasa wanaohitaji kuwa macho?

11 Andiko la Malaki 2:7 linapasa kuwa onyo kwa ndugu walio na pendeleo la kufundisha Neno la Mungu katika makutaniko leo. Linasema kwamba midomo yao ‘yapaswa kuhifadhi maarifa, tena yawapasa watu kuitafuta sheria’ vinywani mwao. Walimu hao wana daraka zito kwa kuwa andiko la Yakobo 3:1 linaonyesha kwamba ‘watapokea hukumu nzito zaidi.’ Ingawa ndugu hao wanapaswa kufundisha kwa shauku na bidii, lazima mafundisho yao yategemee kabisa Neno la Mungu lililoandikwa na maagizo yanayopatikana kupitia tengenezo la Yehova. Kwa kufanya hivyo, “watakuwa na sifa za ustahili wa kutosha kufundisha wengine.” Kwa hiyo wanashauriwa: “Fanya yote uwezayo kabisa ili ujionyeshe mwenyewe kuwa mwenye kukubaliwa na Mungu, mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli.”—2 Timotheo 2:2, 15.

12. Wanaofundisha wanapaswa kuwa waangalifu kuhusu jambo gani?

12 Tusipokuwa waangalifu, tunaweza kushawishiwa kutia ndani mapendezi au maoni yetu tunapofundisha. Jambo hilo linaweza kuwa hatari kwa mtu anayeshikilia sana maoni yake hata maoni hayo yanapopingana na mafundisho ya tengenezo la Yehova. Lakini Malaki sura ya 2 inaonyesha kwamba tunapaswa kutarajia walimu kutanikoni wafundishe tu ujuzi kutoka kwa Mungu wala si mawazo yao wenyewe yanayoweza kuwakwaza kondoo. Yesu alisema hivi: “Yeyote yule akwazaye mmoja wa wadogo hawa wawekao imani katika mimi, ni jambo lenye manufaa zaidi kwake jiwe la kusagia kama lile lizungushwalo na punda lining’inizwe kuzunguka shingo yake na kuzamishwa katika bahari pana, iliyo wazi.”—Mathayo 18:6.

Kufunga Ndoa na Mtu Asiyeamini

13, 14. Ni mwenendo gani wa hila ambao Malaki alielekezea fikira?

13 Kuanzia mstari wa 10 na kuendelea, Malaki sura ya 2 yaelekezea fikira hila kwa njia iliyo wazi zaidi. Malaki akazia mienendo miwili inayohusiana, naye atumia neno “hila” mara kadhaa. Ona kwamba Malaki alianza kutoa shauri lake kwa kuuliza maswali haya: “Je! sisi sote hatuna baba mmoja? Mungu aliyetuumba siye mmoja tu? Basi, mbona kila mmoja wetu anamtenda ndugu yake mambo ya hiana [“hila,” NW], tukilinajisi agano la baba zetu?” Kisha katika mstari wa 11, aliongeza kusema kwamba mwenendo wa hiana [“hila,” NW] wa Waisraeli ulikuwa sawa na ‘kunajisi utakatifu wa Yehova.’ Ni jambo gani baya walilokuwa wakifanya? Mstari huo unataja zoea fulani baya—walikuwa ‘wamemwoa binti ya mungu mgeni.’

14 Yaani, baadhi ya Waisraeli waliokuwa raia wa taifa lililokuwa wakfu kwa Yehova, walikuwa wamefunga ndoa na watu wasioamini. Muktadha unatusaidia kufahamu sababu iliyofanya jambo hilo liwe baya sana. Mstari wa 10 unasema kwamba walikuwa na baba mmoja tu. Baba huyo si Yakobo (aliyepewa jina Israeli), wala si Abrahamu, wala Adamu. Andiko la Malaki 1:6 linaonyesha kwamba ‘baba huyo mmoja tu’ ni Yehova. Taifa la Israeli lilikuwa na uhusiano pamoja na Mungu, nao walihusishwa katika agano alilofanya na baba zao. Mojawapo ya sheria katika agano hilo inasema: “Usioane nao, binti yako usimpe mwanawe mume, wala usimtwalie mwanao mume binti yake.”—Kumbukumbu la Torati 7:3.

15. (a) Huenda watu fulani wakatoa sababu gani ya kutaka kufunga ndoa na mtu asiyeamini? (b) Yehova ana maoni gani kuhusu ndoa?

15 Huenda baadhi ya watu leo wakasababu hivi: ‘Mtu ninayevutiwa naye ni mzuri sana. Labda baadaye atakubali ibada ya kweli.’ Kufikiri kwa njia hiyo kunathibitisha onyo hili lililopuliziwa: “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha.” (Yeremia 17:9) Maoni ya Mungu kuhusu kufunga ndoa na mtu asiyeamini, yanaonyeshwa katika Malaki 2:12: “BWANA atamtenga mtu atendayo hayo.” Kwa hiyo, Wakristo wanahimizwa wafunge ndoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Katika mpango wa Kikristo, mtu anayeamini ‘hatengwi’ kwa sababu ya kufunga ndoa na mtu asiyeamini. Hata hivyo, mtu asiyeamini akikataa kuwa mwamini atapatwa na nini hivi karibuni, Mungu atakapoharibu mfumo huu?—Zaburi 37:37, 38.

Kumtendea Vibaya Mwenzi wa Ndoa

16, 17. Watu fulani walifuata mwenendo gani wa hila?

16 Kisha Malaki ataja kosa la pili la hila: kumtendea vibaya mwenzi wa ndoa, hasa kwa kumtaliki bila sababu nzuri. Mstari wa 14 wa sura ya 2 wasema: “BWANA amekuwa shahidi kati ya wewe na mke wa ujana wako, uliyemtenda mambo ya hiana [“hila,” NW], angawa yeye ni mwenzako, na mke wa agano lako.” Kwa kuwatendea wake zao kwa hila, waume Wayahudi walifanya madhabahu ya Yehova ‘ifunikwe kwa machozi.’ (Malaki 2:13) Wanaume hao walikuwa wakiwataliki wake zao kwa sababu mbalimbali zisizo na msingi, wakiwaacha wake wa ujana wao isivyofaa, labda ili waoe wanawake wachanga zaidi au wanawake wapagani. Nao makuhani wafisadi waliruhusu jambo hilo! Hata hivyo, andiko la Malaki 2:16 linasema: “Nakuchukia kuachana, asema BWANA, Mungu wa Israeli.” Baadaye, Yesu alionyesha kwamba msingi pekee wa talaka ambao ungefanya mwenzi asiye na hatia awe huru kufunga ndoa, ni uasherati.—Mathayo 19:9.

17 Fikiria kwa uzito maneno ya Malaki na uone jinsi yanavyogusa mioyo na kuchochea huruma. Anataja “mwenzako, na mke wa ujana wako.” Kila mwanamume anayehusika alikuwa ameoa mwabudu mwenzake, mwanamke Mwisraeli, aliyekuwa amemchagua kuwa mwenzi mpendwa wa maisha. Ingawa huenda wote wawili walifunga ndoa walipokuwa wachanga, kuzeeka na kupita kwa wakati hakukupaswa kubatilisha agano walilokuwa wamefanya, yaani, ndoa.

18. Unabii wa Malaki kuhusu hila unatuhusuje leo?

18 Bila shaka, shauri hilo kuhusu masuala hayo linatuhusu leo. Ni jambo la kusikitisha kwamba watu fulani hupuuza mwongozo wa Mungu wa kufunga ndoa katika Bwana tu. Pia inasikitisha kwamba wengine hukosa kujitahidi kuimarisha ndoa yao. Badala yake, wao hutoa udhuru na kufuata mwenendo unaochukiwa na Mungu kwa kuwapa wenzi wao talaka zisizo za Kimaandiko ili kufunga ndoa na mtu mwingine. Kwa kufanya mambo hayo yote, wao ‘humchokesha Yehova.’ Katika siku za Malaki, wale waliopuuza mashauri ya Mungu hata walihisi kwa ushupavu kwamba maoni ya Yehova hayafai. Ni kama walisema: “Mungu mwenye kuhukumu yuko wapi?” Walikuwa na mawazo yaliyopotoka kama nini! Na tusinaswe na mtego huo.—Malaki 2:17.

19. Waume na wake wanawezaje kupokea roho ya Mungu?

19 Jambo lenye kutia moyo ni kwamba Malaki anaonyesha kuwa wanaume fulani walioishi siku zake hawakuwatendea wake zao kwa hila. ‘Walikuwa na roho takatifu ya Mungu kwa kiasi fulani.’ (Mstari wa 15, NW) Jambo lenye kufurahisha ni kwamba leo katika tengenezo la Mungu, kuna wanaume wengi kama hao ambao ‘wanawapa heshima wake zao.’ (1 Petro 3:7) Hawawapigi wake zao, au kuwatukana, hawawalazimishi wake zao wafanye nao ngono zilizopotoka, na hawawavunjii heshima wake zao kwa kuchezacheza kimahaba na wanawake wengine au kwa kutazama ponografia. Pia tengenezo la Yehova limebarikiwa kuwa na wake wengi Wakristo walio waaminifu kwa Mungu na sheria zake. Wanaume na wanawake hao wanajua mambo ambayo Mungu huchukia, nao hujiendesha na kufikiri kulingana na maoni ya Mungu kuhusu mambo hayo. Na uendelee kuwaiga, ‘ukimtii Mungu kuwa mtawala,’ na utabarikiwa kupokea roho yake takatifu.—Matendo 5:29.

20. Wanadamu watapatwa na nini hivi karibuni?

20 Hivi karibuni, Yehova atauhukumu ulimwengu mzima. Kila mtu atatoa hesabu kwake kuhusiana na imani na matendo yake. “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Waroma 14:12) Kwa hiyo swali lenye kuvutia ni hili: Ni nani atakayeokoka siku ya Yehova? Makala ya tatu na ya mwisho katika mfululizo huu itazungumzia habari hiyo.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini hasa Yehova aliwashutumu makuhani wa Israeli?

• Kwa nini viwango vya Mungu si vya juu sana kwa wanadamu kutimiza?

• Kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu tunapofundisha leo?

• Ni mazoea gani mawili hasa yaliyoshutumiwa na Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Katika siku za Malaki makuhani walilaumiwa kwa kutoshika njia za Yehova

[Picha katika ukurasa wa 16]

Twapaswa kuwa waangalifu kufundisha njia za Yehova, si kuendeleza mapendezi yetu wenyewe

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yehova aliwashutumu Waisraeli waliowataliki wake zao bila sababu nzuri na kuoa wanawake wapagani

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wakristo leo huheshimu agano lao la ndoa