Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unafahamu Upendo wa Mungu?

Je, Unafahamu Upendo wa Mungu?

Je, Unafahamu Upendo wa Mungu?

WAKATI fulani, Yobu alieleza hali ya wanadamu wasio wakamilifu kwa maneno haya: “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu. Yeye huchanua kama vile ua, kisha hukatwa; hukimbia kama kivuli, wala hakai kamwe.” (Ayubu 14:1, 2) Maisha ya Yobu wakati huo yalikuwa yamejaa maumivu na majonzi. Je, umewahi kuhisi hivyo?

Hata hivyo, licha ya magumu na matatizo tunayoweza kukabili, tuna tumaini thabiti linalotegemea huruma na upendo wa Mungu. Kwanza kabisa, Baba yetu wa kimbingu mwenye rehema ameandaa dhabihu ya fidia ili kukomboa wanadamu kutoka katika hali yao ya dhambi. Kulingana na andiko la Yohana 3:16, 17, Yesu Kristo alisema: “Kwa maana Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu] sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele. Kwa maana Mungu alimtuma Mwana wake [Yesu] kuingia katika ulimwengu, si ili ahukumu ulimwengu, bali ili ulimwengu uokolewe kupitia yeye.”

Pia fikiria jinsi Mungu alivyotuonyesha fadhili sisi wanadamu wasio wakamilifu. Mtume Paulo alisema: “Alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso mzima wa dunia, naye aliagiza nyakati zilizowekwa na mipaka iliyowekwa ya makao ya watu, ili wao wamtafute Mungu, ikiwa wangeweza kupapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate, ijapokuwa, kweli, yeye hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:26, 27) Ebu wazia hilo linamaanisha nini kwetu! Ingawa sisi ni wanadamu wasio wakamilifu, bado twaweza kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova Mungu, Muumba wetu mwenye upendo.

Kwa hiyo, basi, tunaweza kutazamia wakati ujao kwa uhakika, tukijua kwamba Mungu anatujali naye amechochewa na upendo kutupatia maandalizi yatakayotunufaisha milele. (1 Petro 5:7; 2 Petro 3:13) Kwa hiyo, basi, tuna sababu nzuri za kujua mengi zaidi kumhusu Mungu wetu mwenye upendo kwa kujifunza Neno lake, Biblia.