Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufaidika na Fadhili-upendo za Yehova

Kufaidika na Fadhili-upendo za Yehova

Kufaidika na Fadhili-upendo za Yehova

‘Ni nani mwenye hekima? Atakaza fikira zake kuelekea matendo ya Yehova ya fadhili-upendo.’—ZABURI 107:43, NW.

1. Usemi “fadhili-upendo” ulitumiwa kwa mara ya kwanza katika Biblia wakati gani, nasi tutachunguza maswali gani kuhusu sifa hiyo?

MIAKA 4,000 hivi iliyopita, Loti, mwana wa ndugu ya Abrahamu alisema hivi kumhusu Yehova: “Umezidisha rehema [“fadhili-upendo,” NW] zako.” (Mwanzo 19:19) Hii ndiyo mara ya kwanza usemi “fadhili-upendo” umetumiwa katika Biblia. Yakobo, Naomi, Daudi, na watumishi wengine wa Mungu pia walitaja sifa hiyo ya Yehova. (Mwanzo 32:10; Ruthu 1:8; 2 Samweli 2:6) Kwa kweli, usemi “fadhili-upendo,” ukiwa katika umoja na katika wingi, unapatikana mara 250 hivi katika Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures. Lakini fadhili-upendo za Yehova ni nini? Ni nani walioonyeshwa sifa hiyo zamani? Nasi hufaidikaje na sifa hiyo leo?

2. Kwa nini ni vigumu sana kueleza maana ya neno la Kiebrania tunalozungumzia, nalo linaweza kutafsiriwaje?

2 Katika Maandiko, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fadhili-upendo” lina maana pana sana hivi kwamba lugha nyingi haziwezi kutumia neno moja kueleza maana kamili ya neno hilo. Hivyo, tafsiri kama “upendo,” “rehema,” na “uaminifu” hazitoi maana sahihi na kamili ya neno hilo. Hata hivyo, kitabu Theological Wordbook of the Old Testament kinasema kwamba usemi “fadhili-upendo” ‘unakaribiana sana na maana kamili ya neno hilo la Kiebrania.’ Kwa kufaa, tafsiri ya New World Translation of the Holy Scriptures—With References inaonyesha kwamba usemi “upendo mwaminifu-mshikamanifu” unaweza kutumiwa kutafsiri neno hilo la Kiebrania badala ya usemi “fadhili-upendo.”—Kutoka 15:13; Zaburi 5:7; kielezi-chini.

Fadhili-Upendo Ni Tofauti na Upendo na Uaminifu-Mshikamanifu

3. Sifa ya fadhili-upendo inatofautianaje na upendo?

3 Sifa ya fadhili-upendo, au upendo mwaminifu-mshikamanifu, inakaribiana sana na sifa ya upendo na ya uaminifu-mshikamanifu. Hata hivyo, sifa ya fadhili-upendo ni tofauti na sifa hizo nyingine katika njia mbalimbali muhimu. Fikiria jinsi fadhili-upendo na upendo zinavyotofautiana. Tunaweza kupenda vitu na pia maoni fulani. Biblia inasema juu ya ‘kupenda mvinyo’ na ‘kupenda hekima.’ (Mithali 21:17; 29:3) Lakini fadhili-upendo hutumiwa kuhusu watu wala si kuhusu maoni au vitu visivyo na uhai. Kwa mfano, andiko la Kutoka 20:6, NW linazungumza juu ya watu linaposema kwamba Yehova ‘huonyesha fadhili-upendo kwa kizazi cha elfu.’

4. Sifa ya fadhili-upendo inatofautianaje na uaminifu-mshikamanifu?

4 Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fadhili-upendo” pia lina maana pana zaidi kuliko usemi “uaminifu-mshikamanifu.” Katika lugha fulani, usemi “uaminifu-mshikamanifu” hutumiwa mara nyingi kuonyesha jinsi mfanyakazi anavyopaswa kutenda kuelekea mkubwa wake. Lakini mtafiti mmoja anasema kwamba ‘mara nyingi Biblia hutumia usemi fadhili-upendo kuonyesha uhusiano ulio tofauti na wa mfanyakazi na mkubwa wake: yaani, mkubwa anakuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa aliye mnyonge na mwenye uhitaji.’ Hivyo mfalme Daudi angeweza kumwomba Yehova hivi: “Umwangaze mtumishi wako kwa nuru ya uso wako. Uniokoe kwa ajili ya fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zako.” (Zaburi 31:16) Yehova, ambaye ndiye mwenye uwezo, anaombwa aonyeshe fadhili-upendo, au upendo mwaminifu-mshikamanifu kwa Daudi mwenye uhitaji. Kwa kuwa wenye uhitaji hawana mamlaka juu ya wenye uwezo, sifa ya fadhili-upendo katika uhusiano kama huo inaonyeshwa kwa nia ya kupenda wala si kwa kulazimishwa.

5. (a) Ni mambo gani yanayohusiana na fadhili-upendo za Mungu yanayokaziwa katika Neno lake? (b) Tutachunguza mambo gani yanayoonyesha fadhili-upendo za Yehova?

5 “Ni nani mwenye hekima?” akauliza mtunga-zaburi. ‘Atakaza fikira zake kuelekea matendo ya Yehova ya fadhili-upendo.’ (Zaburi 107:43, NW) Tunaweza kukombolewa na kuhifadhiwa kwa sababu ya fadhili-upendo za Yehova. (Zaburi 6:4; 119:88, 159) Sifa hiyo ni ulinzi na huleta kitulizo kutokana na matatizo. (Zaburi 31:16, 21; 40:11; 143:12) Kwa sababu ya sifa hiyo, watu wanaweza kukombolewa kutoka katika dhambi. (Zaburi 25:7) Kwa kuchunguza masimulizi na mistari fulani ya Biblia, tutaona kwamba fadhili-upendo za Yehova huonyeshwa (1) kwa matendo fulani hususa na (2) kwa watumishi wake waaminifu.

Ukombozi—Tendo la Fadhili-Upendo

6, 7. (a) Yehova alizidisha fadhili-upendo zake kwa Loti jinsi gani? (b) Loti alitaja fadhili-upendo za Yehova wakati gani?

6 Labda njia iliyo bora zaidi ya kujua ni kwa kadiri gani Yehova huonyesha sifa ya fadhili-upendo ni kuchunguza masimulizi ya Maandiko yanayohusu sifa hiyo. Katika andiko la Mwanzo 14:1-16, tunaona kwamba Loti, mwana wa ndugu ya Abrahamu, alichukuliwa mateka na majeshi ya adui. Lakini Abrahamu akamwokoa. Uhai wa Loti ulikuwa hatarini tena Yehova alipoamua kuharibu jiji lenye uovu la Sodoma, walikoishi Loti na familia yake.—Mwanzo 18:20-22; 19:12, 13.

7 Muda mfupi kabla ya kuharibiwa kwa Sodoma, malaika wa Yehova walimsindikiza Loti na familia yake kutoka katika jiji hilo. Wakati huo, Loti alisema: “Mtumwa wako ameona kibali machoni pako, nawe umezidisha rehema [“fadhili-upendo,” NW] zako ulizonifanyia kwa kuponya nafsi yangu.” (Mwanzo 19:16, 19) Kwa maneno hayo Loti alikubali kwamba Yehova alimwonyesha fadhili-upendo za pekee kwa kumwokoa. Katika kisa hicho, Mungu alionyesha fadhili-upendo zake kwa kumkomboa na kumhifadhi Loti.—2 Petro 2:7.

Fadhili-Upendo za Yehova na Mwongozo Wake

8, 9. (a) Mtumishi wa Abrahamu alipewa mgawo gani? (b) Kwa nini mtumishi huyo alisali kwa Mungu amwonyeshe fadhili-upendo, na kulitokea nini alipokuwa akisali?

8 Katika kitabu cha Mwanzo sura ya 24, tunasoma kuhusu tendo lingine linaloonyesha fadhili-upendo au upendo mwaminifu-mshikamanifu wa Mungu. Masimulizi hayo yanaonyesha kwamba Abrahamu alimtuma mtumishi wake asafiri kwenda nchi ya watu wa jamaa ya Abrahamu ili kumtafutia mwanawe Isaka mke. (Mstari wa 2-4) Huo ulikuwa mgawo mgumu, lakini mtumishi huyo alihakikishiwa kwamba malaika wa Yehova angemwongoza. (Mstari wa 7) Mwishowe, mtumishi huyo alifika kwenye kisima kimoja nje ya “mji wa Nahori” (ama Harani au mji mwingine uliokuwa karibu) wakati wanawake walipokuwa wakija kuchota maji. (Mstari wa 10, 11) Alipoona wanawake hao wakikaribia, alijua kwamba huo ulikuwa wakati muhimu zaidi kuhusiana na mgawo wake. Lakini angechaguaje mwanamke atakayefaa?

9 Kwa kuwa alijua kwamba alihitaji msaada wa Mungu, mtumishi wa Abrahamu alisali: “Ee BWANA, Mungu wa bwana wangu [Abrahamu] nakuomba mambo yangu uyajalie yawe heri leo, ukamfadhili [“ukamwonyeshe fadhili-upendo,” NW] bwana wangu [Abrahamu].” (Mstari wa 12) Yehova angeonyeshaje fadhili-upendo zake? Mtumishi huyo aliomba apewe ishara hususa ya kumtambua mwanamke ambaye Mungu amechagua. (Mstari wa 13, 14) Mwanamke mmoja alitenda sawasawa na vile mtumishi huyo alivyomwomba Yehova. Alitenda kana kwamba alikuwa amesikia sala yake! (Mstari 15-20) Hivyo, mtumishi huyo ‘akamkazia macho kwa mshangao.’ Lakini kuna mambo fulani muhimu aliyohitaji kujua. Je, mwanamke huyo mrembo alikuwa wa jamaa ya Abrahamu? Na je, alikuwa bado hajaolewa? Kwa hiyo mtumishi huyo “akanyamaza, ili ajue kwamba BWANA ameifanikisha safari yake ama sivyo.”—Mstari wa 16, 21.

10. Kwa nini mtumishi wa Abrahamu alisema kwamba Yehova alimwonyesha bwana wake fadhili-upendo?

10 Muda mfupi baadaye, mwanamke huyo kijana alijitambulisha kuwa “binti wa Bethueli mwana wa Milka, aliyemzalia Nahori [ndugu ya Abrahamu].” (Mwanzo 11:26; 24:24) Papo hapo mtumishi huyo akatambua kwamba Yehova alikuwa amejibu sala yake. Kwa furaha, aliinama chini na kusema: “Na atukuzwe BWANA, Mungu wa bwana wangu [Abrahamu], ambaye hakuacha rehema [“fadhili-upendo,” NW] zake na kweli yake kwa bwana wangu. BWANA akaniongoza mimi nami njiani hata nyumba ya nduguze bwana wangu.” (Mstari wa 27) Kwa kutoa mwongozo, Mungu alionyesha fadhili-upendo kwa Abrahamu, bwana wa mtumishi huyo.

Fadhili-Upendo za Mungu Huleta Kitulizo na Ulinzi

11, 12. (a) Yehova alimwonyesha Yosefu fadhili-upendo wakati wa majaribu gani? (b) Mungu alimwonyeshaje Yosefu fadhili-upendo?

11 Sasa, na tuchunguze kitabu cha Mwanzo sura ya 39. Sura hiyo inazungumza juu ya Yosefu, kitukuu wa Abrahamu, ambaye aliuzwa utumwani Misri. Hata hivyo, “BWANA akawa pamoja na [Yosefu].” (Mstari wa 1, 2) Kwa kweli, hata Potifa, Mmisri ambaye alikuwa bwana-mkubwa wa Yosefu, aliona kwamba Yehova alikuwa pamoja na Yosefu. (Mstari wa 3) Hata hivyo, Yosefu alipatwa na jaribu kali sana. Alishtakiwa isivyo kweli kwamba alitaka kumbaka mke wa Potifa na akafungwa gerezani. (Mstari wa 7-20) Akiwa “gerezani,” “walimwumiza miguu yake kwa pingu, akatiwa katika minyororo ya chuma.”—Mwanzo 40:15; Zaburi 105:18.

12 Ni nini kilichotokea wakati wa jaribu hilo kali sana? “BWANA akawa pamoja na [Yosefu], akamfadhili [“akamwonyesha fadhili-upendo,” NW].” (Mstari wa 21a) Tendo moja hususa la fadhili-upendo lilisababisha mfululizo wa matukio ambayo baadaye yalimletea Yosefu kitulizo kutokana na matatizo yake. Yehova alimwezesha Yosefu kupata “kibali machoni pa mkuu wa gereza.” (Mstari wa 21b) Kwa hiyo, mkuu huyo akampa Yosefu madaraka makubwa. (Mstari wa 22) Halafu, Yosefu akakutana na mtu aliyefanya ajulikane kwa Farao, mtawala wa Misri. (Mwanzo 40:1-4, 9-15; 41:9-14) Baadaye, mfalme alimpandisha Yosefu cheo akawa mtawala wa pili wa Misri. Cheo hicho kilimwezesha kuokoa uhai wakati nchi ya Misri ilipopatwa na njaa kali. (Mwanzo 41:37-55) Mateso ya Yosefu yalianza alipokuwa na umri wa miaka 17 na kuendelea kwa miaka zaidi ya 12! (Mwanzo 37:2, 4; 41:46) Lakini katika miaka hiyo yote ambayo Yosefu aliteseka na kutaabika, Yehova Mungu alimwonyesha fadhili-upendo kwa kumlinda asipatwe na madhara makubwa na kwa kumhifadhi ili kutimiza daraka la pekee katika kusudi la Mungu.

Fadhili-Upendo za Mungu Hazishindwi

13. (a) Ni maneno gani yanayohusu fadhili-upendo za Yehova yanayopatikana kwenye Zaburi ya 136? (b) Fadhili-upendo ni nini hasa?

13 Yehova aliwaonyesha Waisraeli fadhili-upendo mara nyingi sana. Zaburi ya 136 inasema kwamba kwa sababu ya fadhili-upendo zake aliwakomboa (Mstari wa 10-15, NW), akawaongoza (Mstari wa 16, NW), na kuwalinda. (Mstari wa 17-20, NW) Mungu pia amewaonyesha watu mmoja-mmoja fadhili-upendo zake. Mtu anayewaonyesha wanadamu wenzake fadhili-upendo hufanya hivyo kwa kujitolea kufanya mambo fulani ili kutimiza uhitaji fulani muhimu. Kuhusu fadhili-upendo, kitabu kimoja kinachozungumza juu ya Biblia kinasema: ‘Ni sifa ambayo hufanya maisha yawe bora zaidi. Inasaidia wale waliopatwa na mabaya au taabu.’ Msomi mmoja anaeleza fadhili-upendo kuwa “upendo unaoonyeshwa kwa matendo.”

14, 15. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Loti alikuwa mtumishi wa Mungu aliyekubaliwa?

14 Masimulizi ya kitabu cha Mwanzo ambayo tumechunguza yanatuonyesha kwamba Yehova hashindwi kuwaonyesha fadhili-upendo wale wanaompenda. Loti, Abrahamu, na Yosefu waliishi katika hali tofauti na walipatwa na majaribu yaliyotofautiana kabisa. Walikuwa wanadamu wasio wakamilifu, lakini walikuwa watumishi waliokubalika machoni pa Yehova, nao walihitaji msaada wake. Tunapata faraja kujua kwamba Baba yetu wa mbinguni huwaonyesha watu kama hao fadhili-upendo.

15 Loti alifanya maamuzi fulani yasiyo ya hekima yaliyomletea matatizo. (Mwanzo 13:12, 13; 14:11, 12) Lakini alionyesha sifa fulani nzuri. Wakati malaika wawili wa Mungu walipofika Sodoma, Loti aliwakaribisha vizuri. (Mwanzo 19:1-3) Kwa imani aliwaonya wakwe zake wa kiume kuhusu uharibifu wa Sodoma uliokuwa unakaribia. (Mwanzo 19:14) Maoni ya Mungu kuhusu Loti yanapatikana katika 2 Petro 2:7-9, ambapo tunasoma: “[Yehova] alimkomboa Loti mwadilifu, aliyetaabishwa sana na kujitia mno kwa watu wanaokaidi sheria katika mwenendo mlegevu—kwa maana mtu huyo mwadilifu kwa yale ambayo aliona na kusikia alipokuwa akikaa miongoni mwao kutoka siku hadi siku alikuwa akitesa-tesa nafsi yake yenye uadilifu kwa sababu ya vitendo vyao vya kuasi sheria—Yehova ajua jinsi ya kukomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.” Naam, Loti alikuwa mtu mwadilifu, na andiko hilo linaonyesha kwamba alikuwa mtu mwenye ujitoaji-kimungu. Kama yeye, sisi hufurahia fadhili-upendo za Mungu tunapofanya “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.”—2 Petro 3:11, 12.

16. Biblia inatumia maneno gani ya sifa inapozungumza juu ya Abrahamu na Yosefu?

16 Masimulizi ya kitabu cha Mwanzo sura ya 24 yanaeleza wazi uhusiano wa karibu kati ya Abrahamu na Yehova. Mstari wa kwanza unasema kwamba ‘BWANA alimbariki Abrahamu katika vitu vyote.’ Mtumishi wa Abrahamu alimwita Yehova ‘Mungu wa bwana wangu Abrahamu.’ (Mstari wa 12, 27) Naye mwanafunzi Yakobo anasema kwamba Abrahamu ‘alitangazwa kuwa mwadilifu’ na “akaja kuitwa ‘rafiki ya Yehova.’” (Yakobo 2:21-23) Yosefu pia alikuwa na uhusiano wa karibu na Yehova ambao unakaziwa katika sura yote ya Mwanzo 39. (Mstari wa 2, 3, 21, 23) Zaidi ya hayo, mwanafunzi Stefano alisema hivi kumhusu Yosefu: “Mungu alikuwa pamoja naye.”—Matendo 7:9.

17. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya Loti, Abrahamu, na Yosefu?

17 Watu waliopokea fadhili-upendo za Mungu ambazo tumetoka tu kuzungumzia walikuwa na uhusiano mzuri na Yehova Mungu nao walitimiza kusudi lake katika njia mbalimbali. Walikabili vizuizi ambavyo hawangeweza kuvishinda kwa nguvu zao. Mambo haya yalikuwa hatarini: Maisha ya Loti, kuendelezwa kwa ukoo wa Abrahamu, na daraka ambalo Yosefu angetimiza. Yehova tu ndiye angeweza kutimiza mahitaji ya wanaume hao wenye kumwogopa, naye alifanya hivyo kwa matendo ya fadhili-upendo. Ili Yehova atuonyeshe fadhili-upendo milele, ni lazima tudumishe uhusiano wa karibu pamoja naye na kuendelea kufanya mapenzi yake.—Ezra 7:28; Zaburi 18:50.

Watumishi wa Mungu Wana Kibali

18. Maandiko mbalimbali ya Biblia huonyesha nini kuhusu fadhili-upendo za Yehova?

18 Fadhili-upendo za Yehova ‘zimejaa duniani,’ nasi tunathamini kama nini sifa hiyo ya Mungu! (Zaburi 119:64) Tunaitikia kwa moyo wote maneno haya yenye kurudiwa-rudiwa ya mtunga-zaburi: “Na wamshukuru BWANA, kwa fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zake, na maajabu yake kwa wanadamu.” (Zaburi 107:8, 15, 21, 31) Tunafurahi kwamba Yehova huwaonyesha fadhili-upendo watumishi wake wanaokubalika machoni pake—wawe watu mmoja-mmoja au kikundi. Danieli alimtaja Yehova katika sala kuwa “[Mungu wa kweli], Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake.” (Danieli 9:4) Mfalme Daudi alisali: “Uwadumishie wakujuao fadhili [“fadhili-upendo,” NW].” (Zaburi 36:10) Tunashukuru kama nini kwamba Yehova huwaonyesha watumishi wake fadhili-upendo!—1 Wafalme 8:23; 1 Mambo ya Nyakati 17:13.

19. Tutachunguza maswali gani katika makala inayofuata?

19 Kwa kweli Yehova anatukubali sisi watu wake! Tunafaidika na upendo ambao Mungu anaonyesha wanadamu kwa ujumla na pia kufurahia baraka za pekee zinazotokana na fadhili-upendo au upendo mwaminifu-mshikamanifu wa Baba yetu wa mbinguni. (Yohana 3:16) Tunanufaika zaidi na sifa hiyo nzuri ya Yehova, hasa tunapokuwa na uhitaji. (Zaburi 36:7) Lakini tunaweza kuigaje fadhili-upendo za Yehova Mungu? Je, sisi mmoja-mmoja tunaonyesha sifa hiyo ya pekee? Maswali hayo na mengine yanayohusiana nayo yatazungumziwa katika makala ifuatayo.

Je, Unakumbuka?

• Tumejifunza nini kuhusu neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fadhili-upendo”?

• Sifa ya fadhili-upendo inatofautianaje na upendo na uaminifu-mshikamanifu?

• Ni katika njia zipi Yehova alionyesha fadhili-upendo kwa Loti, Abrahamu, na Yosefu?

• Tunaweza kupata uhakikisho gani kutokana na jinsi Yehova alivyoonyesha fadhili-upendo hapo zamani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Je, unajua jinsi Mungu alivyomwonyesha Loti fadhili-upendo?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yehova alimwongoza mtumishi wa Abrahamu kwa fadhili-upendo

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yehova alionyesha fadhili-upendo kwa kumlinda Yosefu