Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, lingekuwa jambo la hekima kwa Mkristo wa kweli kuhudhuria ibada ya mazishi au arusi kanisani?

Kushiriki ibada yoyote isiyo ya kweli humchukiza Yehova na lazima kuepukwe. (2 Wakorintho 6:14-17; Ufunuo 18:4) Ibada ya mazishi inayofanywa kanisani ni ibada ya kidini ambayo huenda ikahusisha hotuba inayounga mkono mafundisho yasiyopatana na Maandiko kama vile kutokufa kwa nafsi na kwamba watu wote wazuri wataenda mbinguni. Huenda ikatia ndani mazoea kama vile kufanya ishara ya msalaba na kujiunga na kasisi katika sala. Huenda sala na mazoea mengine ya kidini yanayopingana na mafundisho ya Biblia yakawa sehemu ya sherehe ya arusi ya kidini inayofanywa kanisani au mahali penginepo. Huenda ikawa vigumu kwa Mkristo kustahimili mkazo wa kushiriki ibada isiyo ya kweli anapokuwa miongoni mwa watu wanaoshiriki ibada hiyo. Lingekuwa jambo lisilo la hekima kama nini kujiweka katika hali yenye mkazo kama hiyo!

Namna gani Mkristo akihisi kwamba ni lazima ahudhurie ibada ya mazishi au arusi itakayofanywa kanisani? Kwa mfano, huenda mume asiyeamini akamsihi mke wake Mkristo aandamane naye kwenda kwenye mazishi au arusi hiyo. Je, anaweza kujiunga naye na asishiriki ibada hiyo? Kwa kumheshimu mumewe, huenda mke akaamua kuandamana naye, akiwa ameazimia kutoshiriki sherehe yoyote ya kidini. Kwa upande mwingine, huenda akaamua kutokwenda, akisababu kwamba pengine atakabili mkazo mkubwa wa kihisia-moyo na kushindwa kuvumilia na labda kuvunja kanuni za Mungu. Uamuzi ni wake. Bila shaka angependa kufikia uamuzi unaofaa na kuwa na dhamiri safi.—1 Timotheo 1:19.

Vyovyote vile, ingefaa mke huyo amweleze mumewe kwamba kwa sababu ya dhamiri yake, hawezi kushiriki ibada yoyote ya kidini, kuimba nyimbo, au kuinamisha kichwa sala inapotolewa. Kwa kuzingatia maelezo ya mke wake, huenda mume akaamua kwamba kuwepo kwa mkewe kutatokeza hali inayoweza kumwaibisha. Huenda akaamua kwenda peke yake kwa sababu ya kumpenda mkewe, kuheshimu imani yake, au ili asije akaaibika. Lakini akisisitiza mkewe aandamane naye, anaweza kwenda na akatae kushiriki ibada yoyote ya kidini.

Pia twapaswa kufikiria waabudu wenzetu watakuwa na maoni gani wakituona tukihudhuria ibada ya kidini. Je, jambo hilo laweza kusumbua dhamiri za wengine? Je, lingedhoofisha azimio lao la kujiepusha na ibada ya sanamu? Mtume Paulo atoa shauri hili: ‘Hakikisheni mambo yaliyo ya maana zaidi, ili mpate kuwa bila dosari na kutowakwaza wengine hadi siku ya Kristo.’—Wafilipi 1:10.

Ikiwa ibada hiyo inahusu mshiriki wa karibu wa familia, huenda kukawa na mkazo zaidi kutoka kwa washiriki wa familia. Vyovyote iwavyo, Mkristo apaswa kuchunguza kwa uangalifu mambo yote yanayohusika. Chini ya hali fulani huenda akaamua kwamba kuhudhuria ibada ya mazishi au arusi kanisani bila kushiriki ibada hiyo huenda kusitokeze matatizo yoyote. Hata hivyo, huenda lisiwe jambo la hekima kuhudhuria kwa kuwa kufanya hivyo kunaweza kudhuru dhamiri yako au ya wengine. Hata hali iweje, Mkristo apaswa kuhakikisha kwamba uamuzi wake hautafanya awe na dhamiri mbaya mbele za Mungu na wanadamu.