Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Ni Nani?

Mungu Ni Nani?

Mungu Ni Nani?

KICHAPO The Encyclopedia Americana chasema kwamba ‘kwa kawaida jina Mungu hupewa mtu mwenye mamlaka kuu zaidi ulimwenguni na anayepaswa kuabudiwa na wanadamu.’ Kamusi ya Kiswahili Sanifu yafafanua jina “Mungu” kuwa ‘mwenye kuumba ulimwengu na vyote vilivyomo ndani yake.’ Mungu huyo mwenye kutia kicho ana utu wa aina gani?

Je, Mungu ana utu au ni nguvu tu? Je, ana jina? Je, yeye ni sehemu ya Utatu kama watu wengi wanavyoamini? Tunawezaje kumjua Mungu? Biblia hutoa majibu ya kweli na yenye kuridhisha kwa maswali hayo. Kwa kweli, inatutia moyo tumtafute Mungu, isemapo: “Yeye hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:27.

Je, Mungu Ana Utu au Ni Nguvu Tu?

Wengi wanaoamini Mungu hufikiri kwamba yeye ni nguvu fulani tu, wala hana utu. Kwa mfano, katika tamaduni fulani, miungu inahusianishwa na nguvu za asili. Watu fulani ambao wamechunguza matokeo ya utafiti wa kisayansi kuhusu ulimwengu na asili ya uhai duniani, wameona kwamba lazima kuwe na Mwanzilishi wa vitu vyote. Hata hivyo, wanasita kuamini kwamba Mwanzilishi huyo ana utu.

Hata hivyo, je, utata wa uumbaji hauonyeshi kwamba Mwanzilishi huyo alikuwa na akili nyingi? Akili inahitaji ubongo. Mungu ndiye Mwanzilishi huyo mwenye akili aliyeumba vitu vyote. Naam, Mungu ana mwili wa roho ulio tofauti na wetu. Biblia husema: “Ikiwa kuna mwili wa nyama, kuna wa kiroho pia.” (1 Wakorintho 15:44) Ikieleza jinsi Mungu alivyo, Biblia husema hivi waziwazi: “Mungu ni Roho.” (Yohana 4:24) Mwili wa roho ni tofauti kabisa na miili yetu na wanadamu hawawezi kuuona. (Yohana 1:18) Vilevile kuna viumbe wa roho wasioonekana. Wao ni malaika—“wana wa Mungu.”—Ayubu 1:6; 2:1.

Kwa kuwa Mungu hakuumbwa na mtu yeyote na ana mwili wa roho, ni wazi kwamba ana mahali anapoishi. Kuhusiana na makao ya roho, Biblia hutuambia kwamba mbingu ni “makao” ya Mungu. (1 Wafalme 8:43) Pia, mwandishi wa Biblia Paulo asema: ‘Kristo aliingia, mbinguni kwenyewe, ili sasa aonekane mbele ya uso wa Mungu kwa ajili yetu.’— Waebrania 9:24.

Katika Biblia neno “roho” hutumiwa katika maana nyingine pia. Akisali kwa Mungu, mtunga-zaburi alisema hivi: “Waipeleka roho yako, wanaumbwa.” (Zaburi 104:30) Roho hiyo si Mungu mwenyewe, bali ni nguvu ambayo Mungu hutumia kufanya anachotaka. Mungu alitumia roho hiyo kuumba mbingu halisi, dunia, na vitu vyote vilivyo hai. (Mwanzo 1:2; Zaburi 33:6) Roho yake inaitwa roho takatifu. Mungu alitumia roho yake takatifu kupulizia waandikaji wa Biblia. (2 Petro 1:20, 21) Kwa hiyo, roho takatifu ni nguvu isiyoonekana ambayo Mungu hutumia kutimiza makusudi yake.

Mungu Ana Jina la Kipekee

Mwandishi wa Biblia Aguri aliuliza hivi: “Ni nani aliyekamata upepo kwa makonzi yake? Ni nani aliyeyafunga maji ndani ya nguo yake? Ni nani aliyefanya imara ncha zote za nchi? Jina lake ni nani? Na ni nani jina la mwanawe?” (Mithali 30:4) Kwa kweli, Aguri alikuwa akiuliza, ‘Je, unajua jina au ukoo wa mtu aliyefanya mambo haya?’ Ni Mungu peke yake anayeweza kudhibiti nguvu za asili. Ingawa uumbaji unathibitisha wazi kwamba Mungu yuko, haufunui jina lake. Kwa kweli, hatungeweza kujua jina la Mungu kama Mungu mwenyewe hangetufunulia jina hilo. Naye ametufunulia. “Mimi ni YEHOVA,” asema Muumba.—Kutoka 6:2.

Jina la Mungu la kipekee, Yehova, linapatikana karibu mara 7,000 katika Maandishi ya awali ya Kiebrania. Yesu Kristo aliwajulisha watu jina hilo na kulisifu mbele yao. (Yohana 17:6, 26) Jina hilo linapatikana katika kitabu cha mwisho cha Biblia likiwa sehemu ya usemi “Haleluya,” unaomaanisha “msifuni Yah.” Nalo jina “Yah” ni ufupisho wa “Yehova.” (Ufunuo 19:1-6, kielezi-chini, NW) Hata hivyo, Biblia nyingi za kisasa hazitumii jina hilo. Mara nyingi Biblia hizo hutumia neno “BWANA” au “MUNGU,” kwa herufi kubwa ili kulitofautisha na mitajo ya kawaida ya cheo kama “Bwana” na “Mungu.” Wasomi fulani wanasema kwamba huenda jina la Mungu lilitamkwa Yahweh.

Kwa nini kuna maoni yanayopingana kuhusu jina la Aliye mkuu zaidi ulimwenguni? Tatizo hilo lilianza karne kadhaa zilizopita wakati Wayahudi waliacha kutamka jina la Mungu kwa sababu za kishirikina na badala yake wakaanza kutumia usemi wa Kiebrania “Bwana Mwenye Enzi Kuu” mahali popote jina la Mungu lilipotumiwa katika Maandiko. Kwa kuwa Kiebrania kilichotumiwa kuandika Biblia hakikuwa na vokali, hatuwezi kujua kwa usahihi jinsi Musa, Daudi na watu wengine wa kale walivyotamka herufi zinazofanyiza jina la Mungu. Hata hivyo, jina la Kiingereza Jehovah, limetumiwa kwa karne nyingi na tafsiri yake imetumiwa sana katika lugha nyingi leo.—Kutoka 6:3; Isaya 26:4.

Ingawa haijulikani waziwazi jinsi jina la Mungu lilivyotamkwa na yWaebrania wa kale, maana ya jina hilo inajulikana. Jina lake lamaanisha “Yeye Husababisha Iwe.” Kwa hiyo, Yehova Mungu hujitambulisha kuwa Mkusudiaji Mkuu. Yeye hutimiza ahadi na makusudi yake sikuzote. Mungu wa pekee wa kweli, aliye na uwezo wa kufanya hivyo, ndiye peke yake mwenye haki ya kuitwa Yehova.—Isaya 55:11.

Bila shaka, jina Yehova humtofautisha Mungu Mweza Yote na miungu mingine yote. Ndiyo sababu jina hilo linapatikana mara nyingi sana katika Biblia. Ingawa tafsiri nyingi hazitumii jina la Mungu, andiko la Zaburi 83:18 husema hivi waziwazi: “Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” Wakati wa huduma yake, Yesu Kristo aliwafundisha wafuasi wake hivi: “Basi, nyinyi lazima msali kwa njia hii: ‘Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe.’” (Mathayo 6:9) Kwa hiyo twapaswa kutumia jina la Mungu tunaposali, tunapozungumza juu yake, na tunapomsifu mbele za wengine.

Je, Yesu Ni Mungu?

Yehova Mungu anamtambulisha waziwazi Mwana wake. Simulizi la Injili ya Mathayo lasema kwamba baada ya Yesu kubatizwa, “kulikuwa na sauti kutoka katika mbingu iliyosema: ‘Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.’” (Mathayo 3:16, 17) Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu.

Hata hivyo, watu fulani wa dini husema kwamba Yesu ni Mungu. Wengine husema kwamba Mungu ni Utatu. Kulingana na fundisho hilo, “Baba ni Mungu, Mwana ni Mungu, na Roho Takatifu ni Mungu, hata hivyo hawa si Miungu watatu bali Mungu mmoja.” Inaaminika kwamba hao watatu “ni wa umilele na wana cheo sawa.” (The Catholic Encyclopedia) Je, maoni hayo ni sahihi?

Maandiko yaliyopuliziwa yasema hivi kuhusu Yehova: “Tangu milele hata milele ndiwe Mungu.” (Zaburi 90:2) Yeye ni “Mfalme wa umilele”—asiye na mwanzo wala mwisho. (1 Timotheo 1:17) Kwa upande mwingine, Yesu ni “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote,” “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Wakolosai 1:13-15; Ufunuo 3:14) Akimrejezea Mungu kuwa Baba yake, Yesu alisema: “Baba ni mkubwa zaidi kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Pia Yesu alisema kwamba kuna mambo fulani ambayo wala yeye wala malaika hawakuyajua ila Mungu peke yake. (Marko 13:32) Isitoshe, Yesu alisali kwa Baba yake, akisema: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” (Luka 22:42) Yesu alikuwa akisali kwa nani ikiwa si kwa Aliye mkuu zaidi yake? Naye Yesu hakujifufua, alifufuliwa na Mungu.—Matendo 2:32.

Kwa hiyo, Biblia yaonyesha kwamba Yehova ndiye Mungu Mweza Yote, naye Yesu ni Mwana wake. Wote wawili hawakuwa na cheo sawa kabla ya Yesu hajaja duniani au wakati wa maisha yake duniani na wala Yesu hakuwa sawa na Baba yake baada ya kufufuliwa na kurudi mbinguni. (1 Wakorintho 11:3; 15:28) Kama tulivyoona, mungu wa tatu katika fundisho la Utatu, yaani roho takatifu, si mtu, bali ni nguvu anazotumia Mungu kufanya chochote anachotaka. Kwa hiyo, fundisho la Utatu si la Kimaandiko. * Biblia husema, “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.”—Kumbukumbu la Torati 6:4, NW.

Mjue Mungu Vizuri

Ili kumpenda Mungu na kumpa ujitoaji usiohusisha wengine ambao ni haki yake, twapaswa kumjua vizuri. Tunaweza kumjuaje Mungu vizuri? Biblia husema, “sifa zake zisizoonekana zaonwa waziwazi tangu uumbaji wa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zafahamiwa kwa vitu vilivyofanywa, hata nguvu zake za milele na Uungu.” (Waroma 1:20) Njia moja ya kumjua Mungu vizuri ni kutazama na kutafakari kwa shukrani vitu alivyoumba.

Hata hivyo, uumbaji hautuelezi mambo yote tunayopaswa kujua kuhusu Mungu. Kwa mfano, ili kuelewa kwamba Mungu ana utu halisi, ana mwili wa roho na jina la kipekee, twahitaji kuchunguza Biblia. Kwa kweli, kujifunza Biblia ndiyo njia bora ya kumjua Mungu vizuri. Katika Maandiko, Yehova hutuambia yeye ni Mungu wa aina gani. Yeye pia hutufunulia makusudi yake na kutuelimisha katika njia zake. (Amosi 3:7; 2 Timotheo 3:16, 17) Twaweza kuwa na furaha kama nini kujua kwamba Mungu anataka ‘tuje kwenye ujuzi sahihi wa kweli’ ili tunufaike na maandalizi yake ya upendo! (1 Timotheo 2:4) Kwa hiyo, na tujitahidi kabisa kujifunza yote tuwezayo kumhusu Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Kwa habari zaidi, ona broshua Je! Uamini Utatu?, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mungu alitumia roho yake takatifu kuumba dunia na kupulizia wanadamu kuiandika Biblia

[Picha katika ukurasa wa 5]

Sauti kutoka mbinguni ilisema: “Huyu ni Mwana wangu”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu alisali kwa Mungu Aliye mkuu kuliko yeye

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu aliwajulisha watu jina la Mungu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Tunaweza kumjua Mungu vizuri