Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Semi Zenye Kupingana za Tertullian

Semi Zenye Kupingana za Tertullian

Semi Zenye Kupingana za Tertullian

‘KUNA ufanano gani kati ya Mkristo na mwanafalsafa? kati ya mtu anayepotosha kweli, na yule anayeitunza na kuifundisha? Kuna upatano gani kati ya Chuo na Kanisa?’ Maswali hayo magumu yaliulizwa na Tertullian, mwandishi wa karne ya pili na ya tatu W.K. Alijulikana kuwa ‘mtu aliyechangia sana historia ya Kanisa na mafundisho ya siku zake.’ Alijua shughuli zote za kidini.

Yaelekea Tertullian alijulikana sana kwa semi zake zenye kupingana, kama hizi: “Mungu ni mkuu hasa, Anapokuwa mdogo.” ‘Tunaamini kabisa kwamba Mwana wa Mungu alikufa, kwa sababu hilo ni jambo lisiloeleweka.’ “[Yesu] alizikwa na kufufuka, na jambo hilo ni hakika, kwa sababu haliwezekani.”

Mbali na semi zenye kupingana za Tertullian, kuna mambo mengine kumhusu ambayo yanatatanisha. Ingawa alitaka maandishi yake yaitetee kweli na kudumisha maadili na mafundisho ya kanisa, hapana shaka kwamba maandishi hayohayo yalipotosha mafundisho ya kweli. Mchango wake mkubwa kwa Jumuiya ya Wakristo ni fundisho ambalo waandishi wa baadaye walilitumia kuanzisha lile fundisho la Utatu. Ili kuelewa vizuri jinsi alivyofanya hivyo, ni vizuri kwanza tupate kumjua Tertullian mwenyewe.

‘Tertullian Alikuwa Mwerevu’

Ni mambo machache sana yanayojulikana kuhusu maisha ya Tertullian. Wasomi wengi wanakubali kwamba alizaliwa wapata mwaka wa 160 W.K. huko Carthage, Afrika Kaskazini. Yaonekana alikuwa amesoma sana na aliwajua vizuri wanafalsafa wa siku zake. Yaelekea alivutiwa na Ukristo alipoona kwamba wale waliodai kuwa Wakristo walikuwa tayari kufia imani yao. Aliuliza hivi kuhusu Wakristo waliofia imani: ‘Je, kuna yeyote anayetafakari juu ya kufia imani na asitake kujua sababu inayofanya watu wafie imani? Na je, ni nani ambaye baada ya kufanya uchunguzi hatakubali mafundisho yetu?’

Baada ya kugeuzwa imani na kuwa Mkristo kwa jina tu, Tertullian alikuwa mwandishi stadi, aliyependa kuandika semi fupi na za akili. ‘Alikuwa mtu mwenye uwezo wa kipekee miongoni mwa wanatheolojia, na alikuwa mwerevu pia,’ kinasema kitabu The Fathers of the Church. Msomi mmoja alisema: ‘Tertullian alikuwa na kipawa cha kutunga semi fupi lakini hakuwa na kipawa cha kutunga sentensi ndefu. Kwa hiyo, ni rahisi zaidi kuelewa semi zake kuliko hoja zake. Labda hiyo ndiyo sababu semi zake fupi zinanukuliwa zaidi ya taarifa zake ndefu.’

Atetea Ukristo

Kitabu maarufu zaidi cha Tertullian kiitwacho, Apology, huonwa kuwa kimojawapo cha vitabu vyenye kutetea sana Ukristo wa jina. Kiliandikwa wakati ambapo Wakristo walikuwa wakishambuliwa na watu wenye ushirikina. Tertullian aliwatetea Wakristo hao na kupinga unyanyasaji huo usio na maana. Alisema: “[Wapinzani] wanafikiri kwamba Wakristo ndio husababisha kila jambo baya linalowapata watu. . . . Ikiwa maji ya Mto Nile si mengi kuweza kunyunyizia mashamba, ikiwa hali ya anga haibadiliki, ikiwa kuna tetemeko la ardhi, njaa, au msiba—mara moja watu hupaaza sauti: ‘Tupeni Wakristo kwa simba!’”

Ingawa mara nyingi Wakristo walishutumiwa kwamba hawakuwa waaminifu kwa Serikali, Tertullian alijitahidi kuonyesha kwamba wao ndio waliokuwa raia waaminifu zaidi kwa Serikali. Baada ya kutaja majaribio kadhaa ya kuipindua serikali, Tertullian aliwakumbusha wapinzani wake kwamba wapagani ndio waliofanya njama hizo wala si Wakristo. Tertullian alisema kwamba Serikali ndiyo iliyopata hasara Wakristo walipouawa.

Vitabu vingine vya Tertullian vilizungumzia maisha ya Kikristo. Kwa mfano, katika kitabu chake cha ufafanuzi kiitwacho, On the Shows, Tertullian alionya juu ya kwenda kwenye sherehe fulani za kujifurahisha, michezo ya kipagani, na michezo mingine ya kuigiza. Yaonekana kulikuwa na waamini wapya ambao hawakuona ubaya wowote kukutana pamoja ili kufunzwa Biblia, kisha kwenda kwenye michezo hiyo ya kipagani. Tertullian aliandika hivi ili kuwachochea wafikiri: “Ni jambo baya kama nini kutoka katika nyumba ya Mungu na kwenda katika nyumba ya ibilisi—kuacha kutenda mema na kuanza kutenda mabaya.” Alisema hivi: ‘Matendo yenu yanapaswa yapatane na maneno yenu.’

Apotosha Kweli Huku Akiitetea

Katika makala yake yenye kichwa, Against Praxeas, Tertullian alianza kwa kusema: “Ibilisi amepinga kweli kwa njia mbalimbali. Mara kwa mara, lengo lake limekuwa kupotosha kweli huku akiitetea.” Mwanamume Praxeas anayetajwa katika maandishi hayo hatambulishwi vizuri, lakini Tertullian alipinga mafundisho yake kuhusu Mungu na Kristo. Alimwona Praxeas kuwa kibaraka wa Shetani aliyejaribu kupotosha Ukristo kwa hila.

Uhusiano kati ya Mungu na Kristo ndilo suala lililokuwa limepamba moto miongoni mwa wale waliokuwa Wakristo kwa jina wakati huo. Baadhi yao, hasa Wagiriki, walikuwa na tatizo la kuelewa jinsi imani katika Mungu mmoja inavyohusiana na daraka la Yesu akiwa Mwokozi na Mkombozi. Praxeas alijaribu kutatua tatizo lao kwa kufundisha kwamba Yesu ni Baba aliyeonekana katika umbo tofauti na kwamba hakuna tofauti kati ya Baba na Mwana. Fundisho hilo linaloitwa modalism linasema kwamba Mungu alijifunua ‘kuwa Baba wakati wa Uumbaji na wakati alipotoa Sheria, akajifunua kuwa Mwana katika Yesu Kristo, kisha akajifunua kuwa Roho Takatifu baada ya Kristo kupaa mbinguni.’

Tertullian alionyesha kwamba Maandiko yalieleza wazi tofauti kati ya Baba na Mwana. Baada ya kunukuu 1 Wakorintho 15:27, 28, alisababu hivi: ‘Kwa kuwa kuna yule aliyevitiisha vitu vyote, na pia kuna Yule ambaye kwake vitu hivyo vilitiishwa, basi ni lazima watu hawa wawe wawili.’ Tertullian alikazia maneno ya Yesu mwenyewe: “Baba ni mkubwa zaidi kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Akitumia sehemu fulani za Maandiko ya Kiebrania, kama vile andiko la Zaburi 8:5, alionyesha jinsi Biblia inavyoeleza “cheo cha chini” cha Mwana. “Hivyo Baba ni tofauti na Mwana na ni mkuu zaidi kuliko Mwana,” Tertullian akamalizia. ‘Kuna tofauti kati ya Anayezaa na anayezaliwa; anayetumana na anayetumwa; pia anayeumba na yule ambaye kupitia kwake kitu kinaumbwa.’

Tertullian alimwona Mwana kuwa na cheo cha chini kuliko Baba. Hata hivyo, katika jitihada zake za kupinga fundisho la modalism, Tertullian ‘aliyapita mambo ambayo yameandikwa.’ (1 Wakorintho 4:6) Tertullian alibuni fundisho lingine kujaribu kuthibitisha kimakosa kwamba Yesu ni Mungu. Katika ufafanuzi wake wa fundisho hilo Tertullian akawa mtu wa kwanza kutumia neno la Kilatini la “utatu” kueleza uhusiano kati ya Baba, Mwana, na roho takatifu.

Jihadhari na Falsafa ya Kilimwengu

Tertullian aliwezaje kubuni fundisho hilo? Tunapata jibu kutokana na maoni yake yenye kutatanisha kuhusu falsafa. Tertullian aliita falsafa “‘mafundisho’ ya watu na ya ‘roho waovu.’” Alishutumu waziwazi mazoea ya kutumia falsafa kuthibitisha kweli za Kikristo. “Na tuepuke kabisa kutokeza Ukristo uliopotoshwa kwa mafundisho ya Wastoa, Plato, na maneno ya kubuniwa,” akasema. Hata hivyo, Tertullian alitumia sana falsafa ya kilimwengu ilipopatana na maoni yake.—Wakolosai 2:8.

Kitabu kimoja kinachozungumzia utatu kinasema: ‘Theolojia ya utatu ilihitaji kutegemezwa na mafundisho ya Wagiriki ili isitawi.’ Nacho kitabu The Theology of Tertullian kinasema: ‘Tertullian alichanganya maneno na maoni ya wanasheria na wanafalsafa kubuni fundisho lake kuhusu Mungu, mwana, na roho takatifu ambalo licha ya kasoro zake, liliandaa msingi wa kuzungumzia fundisho hilo katika Baraza la Nicaea.’ Hivyo, fundisho la Tertullian likasaidia sana kueneza mafundisho yenye makosa katika Jumuiya yote wa Wakristo.

Tertullian aliwalaumu wengine kwa kuipotosha kweli huku wakiitetea. Hata hivyo, yeye alifanya kosa hilohilo kwa kuchanganya kweli ya Biblia iliyopuliziwa na Mungu na falsafa ya wanadamu. Hivyo, na tufikirie kwa makini onyo la Kimaandiko juu ya ‘kukazia uangalifu matamko yaliyopuliziwa yenye kuongoza vibaya na mafundisho ya roho waovu.’—1 Timotheo 4:1.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Tertullian alishutumu falsafa lakini akaitumia kueneza maoni yake

[Hisani]

Ukurasa wa 29 na 30: © Cliché Bibliothèque nationale de France, Paris

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wakristo wa kweli huepuka kuchanganya kweli ya Biblia na falsafa ya wanadamu