Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Twapaswa Kumjua Mungu

Twapaswa Kumjua Mungu

Twapaswa Kumjua Mungu

JE, HUSISIMUKI kuona anga lililojaa nyota usiku usiokuwa na mawingu? Je, huvutiwi na harufu nzuri ya maua yenye kupendeza? Je, hufurahi kusikiliza nyimbo za ndege na sauti za majani yakipeperushwa na upepo mwanana? Nao nyangumi wakubwa na viumbe wengine wa baharini wanavutia wee! Kisha kuna wanadamu wenye dhamiri na ubongo tata. Vitu vyote vyenye kuvutia vinavyotuzunguka vilitoka wapi?

Watu fulani hufikiri kwamba vitu hivyo vyote vilijitokeza vyenyewe. Lakini ikiwa ni kweli, kwa nini wanadamu wanaamini kwamba kuna Mungu? Kemikali mbalimbali zingewezaje kuungana kiaksidenti na kutokeza viumbe wanaofahamu mahitaji yao ya kiroho?

‘Wanadamu wana uhitaji wa asili wa kuabudu bila kujali hali yao ya kiuchumi au ya kielimu.’ Taarifa hiyo inatoa muhtasari wa utafiti uliofanywa na Profesa Alister Hardy na kuchapishwa katika kitabu chake The Spiritual Nature of Man. Majaribio ya ubongo yaliyofanywa hivi karibuni yamefanya wanasayansi fulani wa mfumo wa neva kudokeza kwamba huenda wanadamu waliumbwa wakiwa na uwezo wa kuabudu. Kitabu chenye kichwa Is God the Only Reality? chasema: ‘Tangu waumbwe, watu wa tamaduni na enzi zote wamekuwa wakitafuta kusudi la maisha kupitia dini.’

Fikiria jinsi mtu fulani mwenye elimu alivyosema miaka 2,000 iliyopita. Aliandika hivi: “Kila nyumba imejengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyejenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4) Kwa kweli, mstari wa kwanza kabisa wa Biblia husema: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.”—Mwanzo 1:1.

Hata hivyo, Mungu ni nani? Wanadamu wana majibu tofauti-tofauti kwa swali hilo. Tineja mmoja Mjapani anayeitwa Yoshi alipoulizwa Mungu ni nani alijibu: “Sina hakika. Mimi ni Mbudha, nami sijali sana kujua Mungu ni nani.” Hata hivyo, Yoshi alikiri kwamba watu wengi huamini kuwa Buddha ni mungu. Nick, ambaye ni mfanyabiashara mwenye umri wa miaka sitini na kitu anaamini kuna Mungu mwenye nguvu kupita wote. Alipoulizwa aeleze Mungu ni nani, Nick alitua kwa muda mrefu kisha akasema: “Hilo ni swali gumu sana rafiki yangu. Naweza kusema tu kwamba Mungu yuko.”

Watu fulani “wanaheshimu na kuabudu kiumbe badala ya Muumba mwenyewe.” (Waroma 1:25, Biblia Habari Njema) Mamilioni ya watu huabudu wazazi waliokufa, huku wakiamini kwamba hawawezi kumfikia Mungu. Katika dini ya Wahindu, kuna miungu mingi ya kiume na ya kike. Katika siku za mitume wa Yesu, watu waliabudu miungu mbalimbali kama vile Zeusi na Hermesi. (Matendo 14:11, 12) Makanisa mengi ya Jumuiya ya Wakristo hufundisha kwamba Mungu ni Utatu yaani kuna Mungu Baba, Mungu Mwana, na Mungu Roho Mtakatifu.

Kwa kweli, Biblia husema, ‘kuna miungu mingi na mabwana wengi.’ Hata hivyo, inaongeza kusema: “Kwa kweli kwetu kuna Mungu mmoja Baba, ambaye kutokana naye vitu vyote vipo.” (1 Wakorintho 8:5, 6) Naam, kuna Mungu mmoja tu wa kweli. Lakini yeye ni nani? Anafananaje? Ni muhimu kujua majibu ya maswali hayo. Yesu alisema hivi aliposali kwa Mungu: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Tuna sababu ya kuamini kwamba hali yetu njema ya milele yategemea kujua kweli kuhusu Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Viumbe hawa walitoka wapi?

[Hisani]

Nyangumi: Courtesy of Tourism Queensland

[Picha katika ukurasa wa 2 zimeandaliwa na]

COVER: Index Stock Photography © 2002