Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upanuzi wa Haraka Wahitajiwa kwa Sababu ya Ongezeko Kubwa

Upanuzi wa Haraka Wahitajiwa kwa Sababu ya Ongezeko Kubwa

“Njoni Kwangu, . . . Nami Hakika Nitawaburudisha Ninyi”

Upanuzi wa Haraka Wahitajiwa kwa Sababu ya Ongezeko Kubwa

“NJONI kwangu, . . . nami hakika nitawaburudisha nyinyi,” akasema Yesu Kristo. (Mathayo 11:28) Huo ni mwaliko wenye kusisimua kama nini kutoka kwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo! (Waefeso 5:23) Tukichunguza maneno hayo kwa uangalifu, tutathamini sana chanzo muhimu cha burudiko—kushirikiana na ndugu na dada zetu wa kiroho katika mikutano ya Kikristo. Bila shaka, twakubaliana na mtunga-zaburi aliyeimba: “Jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja.”—Zaburi 133:1.

Kwa kweli, tunapata marafiki bora zaidi kwenye mikutano hiyo ambapo hali ya kiroho ni salama na yenye kupendeza. Akiwa na sababu nzuri kijana mmoja Mkristo alisema: “Mimi hushinda shuleni, nami huchoka sana. Lakini mikutano ni kama maji yanayopatikana jangwani, ambapo mimi huburudishwa na kupata nguvu za kukabiliana na siku nyingine shuleni.” Kijana mmoja kutoka Nigeria alisema: “Nimeona kwamba kushirikiana kwa ukaribu na watu wanaompenda Yehova hunisaidia kubaki karibu naye.”

Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova popote pale yalipo hutimiza uhitaji mkubwa katika jamii yakiwa vituo vya ibada ya kweli. Katika sehemu nyingi, angalau mara mbili kwa juma kuna mikutano kwenye Jumba la Ufalme, nao wanafunzi wa Biblia hutiwa moyo kuhudhuria mikutano hiyo upesi iwezekanavyo ili wanufaike na burudiko linalotokana na ushirika huo.—Waebrania 10:24, 25.

Uhitaji wa Haraka

Hata hivyo, si Mashahidi wote wa Yehova walio na Jumba zuri la Ufalme. Ongezeko kubwa la watangazaji wa Ufalme ulimwenguni pote limefanya kuwe na uhitaji huo wa haraka. Maelfu ya Majumba ya Ufalme yangali yanahitajiwa, hasa katika nchi zinazoendelea.—Isaya 54:2; 60:22.

Kwa mfano: Kulikuwa na Majumba ya Ufalme 10 tu kwa ajili ya makutaniko 290 katika jiji kuu la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Nchi hiyo ilihitaji sana Majumba mengi ya Ufalme. Nchini Angola, makutaniko mengi hukutania nje kwa kuwa Majumba ya Ufalme ni machache. Nchi nyingine pia zinahitaji Majumba ya Ufalme.

Kwa hiyo, tangu mwaka wa 1999, mipango ilianzishwa ya kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme katika nchi ambazo zimepungukiwa kifedha. Mashahidi fulani wenye uzoefu wamejitolea kusaidia katika miradi ya ujenzi katika nchi hizo. Wanapoungwa mkono na wafanyakazi wa kujitolea katika nchi hizo, kunakuwa na matokeo mazuri sana. Mashahidi katika nchi hizo wananufaika pia na mazoezi wanayopata. Mipango hii yote inasaidia kujengwa kwa Majumba ya Ufalme katika nchi zinazohusika.

Kwa hiyo msaada unaofaa unatolewa na Majumba ya Ufalme yanajengwa kwa kutumia mbinu na vifaa vinavyopatikana katika maeneo mbalimbali kulingana na mahitaji ya huko. Lengo si kujenga tu Majumba mengi ya Ufalme, bali ni kuanzisha mpango wa udumishaji unaofaa katika kila eneo.—2 Wakorintho 8:14, 15.

Maendeleo Yanayotia Moyo

Jitihada za kujenga sehemu hizo za ibada zimekuwa na matokeo gani? Mwanzoni mwa mwaka wa 2001, ripoti moja kutoka Malawi ilisema: “Mambo ambayo yametimizwa katika nchi hii yanavutia kwelikweli. Miezi miwili ijayo, tutakamilisha Majumba ya Ufalme zaidi.” (Picha ya 1 na ya 2) Nchini Togo, wafanyakazi wa kujitolea walijenga Majumba mazuri ya Ufalme katika miezi ya hivi majuzi. (Picha ya 3) Kazi nzuri inayofanywa na wafanyakazi wa kujitolea inasaidia pia kujengwa kwa Majumba ya Ufalme nchini Mexico, Brazili, na nchi nyinginezo.

Makutaniko yameona kwamba Jumba la Ufalme linapojengwa, wenyeji hutambua kwamba Mashahidi wa Yehova watadumu mahali hapo. Yaonekana kwamba wengi walikuwa wakisitasita kushirikiana na Mashahidi hadi mahali panapofaa pa ibada palipojengwa. Kutaniko la Nafisi nchini Malawi laripoti: “Sasa tuna Jumba zuri la Ufalme linalotoa ushahidi mzuri. Kwa hiyo, ni rahisi kuanzisha mafunzo ya Biblia.”

Washiriki wa Kutaniko la Krake nchini Benin walivumilia dhihaka kali hapo zamani kwa sababu Jumba lao la Ufalme la zamani lilikuwa la hali ya chini likilinganishwa na makanisa fulani. (Picha ya 4) Sasa kutaniko hilo lina Jumba zuri la Ufalme linalowakilisha ibada ya kweli kwa njia nzuri na ya heshima. (Picha ya 5) Kutaniko hilo lilikuwa na wahubiri wa Ufalme 34 na hudhurio la wastani wa watu 73 kwenye mikutano ya Jumapili. Hata hivyo, watu 651 walihudhuria kuwekwa wakfu kwa Jumba la Ufalme. Wengi waliohudhuria walitoka mjini na walivutiwa kuona jinsi Mashahidi walivyojenga jumba hilo kwa muda mfupi. Ofisi ya tawi nchini Zimbabwe iliandika hivi kuhusu mambo ambayo yametokea kwa sababu ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme: “Mwezi mmoja baada ya Jumba la Ufalme kujengwa, kwa kawaida hudhurio huongezeka maradufu.”—Picha ya 6 na ya 7.

Bila shaka, Majumba mengi mapya ya Ufalme yanawaandalia Wakristo waliojiweka wakfu na watu wanaopendezwa mahali pa kupata burudiko la kiroho. “Tunafurahi sana,” akasema Shahidi mmoja huko Ukrainia baada ya kutaniko moja la kwao kuanza kutumia Jumba jipya la Ufalme. “Tulijionea jinsi Yehova anavyowasaidia watu wake.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10, 11]

Michango ya Ukarimu Inathaminiwa

Mashahidi wa Yehova hufurahi sana kuona maendeleo ya haraka ambayo yamefanywa ili kutimiza uhitaji wa haraka wa kuwa na Majumba mapya ya Ufalme ulimwenguni pote. Idadi inayozidi kuongezeka ya waabudu wa Yehova katika nchi mbalimbali yaonyesha kwamba kuna uhitaji wa Majumba mapya ya Ufalme wakati ujao. Kwani, katika mwaka wa utumishi wa 2001 kwa wastani makutaniko mapya 32 yalianzishwa kila juma! Makutaniko hayo yanahitaji mahali pa kukutania na kuabudu.

Huenda swali likazuka, ‘Tutapata wapi pesa za kujenga Majumba mapya ya Ufalme, hasa katika nchi ambazo akina ndugu wana mapato madogo?’ Jibu la swali hilo lahusisha msaada kutoka kwa Mungu na ukarimu wa wanadamu.

Kupatana na ahadi yake, Yehova huwamwagia watumishi wake roho yake takatifu, na kuwawezesha “kufanya mema, kuwa matajiri katika kazi zilizo bora, kuwa wakarimu, tayari kushiriki.” (1 Timotheo 6:18) Roho ya Mungu huwachochea Mashahidi wa Yehova kuunga mkono kazi ya kuhubiri kwa kila njia—huku wakidhabihu wakati wao, nguvu zao, kazi zao, na mali nyingine katika utendaji wa Kikristo.

Roho ya ukarimu huchochea Mashahidi na watu wengine wasaidie upanuzi na ujenzi huo kifedha. Mbali na kusaidia kulipia gharama za kawaida za makutaniko, wao hutoa michango kwa ajili ya kazi ya ujenzi katika sehemu nyingine za dunia.

Katika kila kutaniko kuna masanduku yaliyoandikwa “Michango kwa Ajili ya Kazi ya Ulimwenguni Pote—Mathayo 24:14.” Watu wanaweza kutumbukiza michango yao ya hiari katika masanduku hayo. (2 Wafalme 12:9) Michango yote inathaminiwa, iwe ya kiasi kikubwa au kidogo. (Marko 12:42-44) Pesa hizo hutumiwa kwa njia mbalimbali ikitegemea uhitaji, kutia ndani kujenga Majumba ya Ufalme. Pesa hizo hazitumiwi kulipa wakubwa wao kwa kuwa Mashahidi wa Yehova hawana wakubwa.

Je, michango ya kazi ya ulimwenguni pote hutimiza kusudi lake? Ndiyo. Ofisi ya tawi ya Liberia—nchi inayokumbwa na vita ya wenyewe kwa wenyewe—yaripoti kwamba Mashahidi wengi hawana kazi na wanakabili matatizo makubwa sana ya kiuchumi. Watu wa Yehova katika nchi hiyo wanawezaje kupata mahali panapofaa pa ibada? “Michango ya ukarimu ya akina ndugu katika nchi nyingine itatumiwa kufanya kazi hiyo,” yasema ofisi ya tawi. “Ni mpango wa upendo na hekima kama nini!”

Ndugu wenyeji pia hutoa michango, licha ya mapato yao madogo. Nchi ya Sierra Leone, Afrika yaripoti: “Ndugu wenyeji wanaunga mkono mpango huo nao wanafurahia kujitolea kufanya kazi na kutoa michango wanayoweza ili kusaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme.”

Jambo la maana hata zaidi ni kwamba jitihada hizo za ujenzi humletea Yehova sifa. Ndugu kutoka Liberia wanasema hivi kwa furaha: “Kujengwa kwa majumba mazuri ya ibada kote nchini kutasaidia watu wajue kwamba ibada ya kweli itadumu na kutasaidia pia kutukuza na kuremba jina kuu la Mungu wetu.”