Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanyoofu Huongozwa na Uaminifu-maadili

Wanyoofu Huongozwa na Uaminifu-maadili

Wanyoofu Huongozwa na Uaminifu-maadili

“MWANADAMU aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu,” yasema Biblia. (Ayubu 14:1) Maumivu na kuteseka yamekuwa mambo ya kawaida kwa wanadamu. Kwani maisha ya kila siku yanaweza kuwa na mahangaiko na misukosuko mingi! Ni nini kitakachotuongoza kwa mafanikio na kutusaidia tudumishe msimamo wa uadilifu mbele ya Mungu tunapokabili majaribu?

Mfikirie Yobu, mtu mwenye mali aliyeishi miaka ipatayo 3,500 iliyopita katika sehemu ambayo sasa ni Arabuni. Shetani alimletea maafa yaliyoje mtu huyu mwenye kumhofu Mungu! Alipoteza mifugo yake yote na watoto wake wapendwa wakafa. Muda mfupi baadaye, Shetani alimpiga Yobu kwa majipu kuanzia kichwa hadi wayo. (Ayubu, sura ya 1, 2) Yobu hakujua ni kwa nini alikuwa akipatwa na mambo hayo mabaya. Hata hivyo, ‘Yobu hakufanya dhambi kwa midomo yake.’ (Ayubu 2:10) “Hata nitakapokufa sitajiondolea uelekevu [“uaminifu-maadili,” NW] wangu,” akasema. (Ayubu 27:5) Naam, Yobu aliongozwa na uaminifu-maadili wakati wa majaribu.

Uaminifu-maadili unafafanuliwa kuwa utimamu au ukamili wa maadili na unatia ndani kutokuwa na lawama au kosa mbele ya Mungu. Hata hivyo, haumaanishi kwamba wanadamu wasio wakamilifu na ambao hawawezi kutimiza kabisa viwango vya Mungu watatenda na kunena kwa ukamilifu. Badala yake, uaminifu-maadili wa kibinadamu unamaanisha kujitoa kumtumikia Yehova kwa moyo wote au moyo kamili na kufanya mapenzi na makusudi yake. Kujitoa kumtumikia Mungu kwa njia hiyo huwaongoza waadilifu chini ya hali zozote na nyakati zote. Sehemu ya kwanza ya sura ya 11 ya kitabu cha Biblia cha Mithali inaonyesha jinsi uaminifu-maadili unavyoweza kutuongoza katika sehemu mbalimbali za maisha na kutuhakikishia baraka tutakazopokea. Kwa hiyo, na tuchunguze kwa makini mambo yaliyoandikwa humo.

Uaminifu-Maadili Hutusaidia Kuwa Wanyofu Katika Biashara

Akikazia kanuni inayohusu unyofu, Mfalme Solomoni wa Israeli la kale asema hivi akitumia maneno ya kishairi badala ya maneno ya kisheria: “Mizani ya hadaa ni chukizo kwa BWANA; bali vipimo vilivyo sawasawa humpendeza.” (Mithali 11:1) Mizani na vipimo vyatajwa hapa kwa mara ya kwanza kati ya mara nne katika kitabu cha Mithali na zatumiwa kuonyesha kwamba Yehova anataka waabudu wake wawe wanyofu katika biashara zao.—Mithali 16:11; 20:10, 23.

Huenda mtu akavutiwa na ufanisi wa watu ambao hutumia mizani ya hadaa au wasio wanyofu. Lakini je, tungependa kuvunja viwango vya Mungu vya mema na mabaya kwa kujihusisha na mazoea mabaya ya biashara? Hatutafanya hivyo iwapo tunaongozwa na uaminifu-maadili. Tunajiepusha na ukosefu wa unyofu kwa sababu mizani ya haki na vipimo vya haki huonyesha sisi ni wanyoofu, na humpendeza Yehova.

“Hekima Hukaa na Wanyenyekevu”

Mfalme Solomoni aendelea kusema: “Kijapo kiburi [“kimbelembele,” “NW”] ndipo ijapo aibu; bali hekima hukaa na wanyenyekevu.” (Mithali 11:2) Kimbelembele—hata kiwe kinadhihirishwa kupitia kiburi, kutotii, au wivu—kinaleta aibu. Kwa upande mwingine, ni jambo la hekima kutambua udhaifu wetu. Kuna mifano katika Biblia inayoonyesha kwamba mithali hiyo ni ya kweli.

Kora, Mlawi mwenye wivu aliongoza umati upinge mamlaka ya Musa na Aroni, watumishi waliowekwa na Mungu. Tendo hilo la kimbelembele lilitokeza nini? ‘Nchi ilifunua kinywa chake na kuwameza’ baadhi ya waasi hao, huku wengine, kutia ndani Kora, wakiteketezwa na moto. (Hesabu 16:1-3, 16-35; 26:10; Kumbukumbu la Torati 11:6) Hiyo ilikuwa fedheha iliyoje! Pia mfikirie Uza, aliyenyosha mkono wake kwa kimbelembele na kushika sanduku la agano ili kulizuia lisianguke. Aliuawa papo hapo. (2 Samweli 6:3-8) Ni jambo muhimu kama nini kuepuka kimbelembele!

Mtu mnyenyekevu na mwenye kiasi hapatwi na aibu hata anapokosea. Ingawa Yobu alikuwa kielelezo kizuri katika mambo mengi, hakuwa mkamilifu. Majaribu yake yalifunua kwamba alikuwa na udhaifu mkubwa na kwamba alifikiri isivyofaa pindi fulani-fulani. Alipokuwa akijitetea mbele ya washtaki wake, Yobu alipoteza usawaziko kwa kadiri fulani. Hata alidokeza kwamba alikuwa mwadilifu zaidi ya Mungu. (Ayubu 35:2, 3) Yehova alisahihishaje maoni ya Yobu?

Akitaja dunia, bahari, anga lililojaa nyota, baadhi ya wanyama, na viumbe wengine wenye kustaajabisha, Yehova alimfundisha Yobu kwamba mwanadamu ni duni sana anapolinganishwa na ukuu wa Mungu. (Yobu, sura ya 38-41) Yehova hakutaja sababu iliyofanya Yobu ateseke. Hakuhitaji kufanya hivyo. Yobu alikuwa mnyenyekevu. Alitambua tofauti kubwa iliyopo kati yake na Mungu, kati ya udhaifu na hali yake ya kutokamilika na uadilifu na nguvu za Yehova. Alisema, “najichukia nafsi yangu, na kutubu katika mavumbi na majivu.” (Ayubu 42:6) Uaminifu-maadili wa Yobu ulifanya akubali karipio. Namna gani sisi? Kwa kuongozwa na uaminifu-maadili, je, tutakuwa tayari kukubali karipio au kusahihishwa inapokuwa lazima?

Musa pia alikuwa mwenye kiasi na mnyenyekevu. Alipolemewa na matatizo ya watu wengine, Yethro, baba-mkwe wake, alimpa suluhisho linalofaa: Wape madaraka fulani baadhi ya wanaume wanaostahili. Kwa kutambua udhaifu wake, kwa hekima Musa alikubali dokezo hilo. (Kutoka 18:17-26; Hesabu 12:3) Mtu mwenye kiasi hasitisiti kuwapa wengine madaraka, wala haogopi kwamba atapoteza mamlaka kwa kuwapa kazi wanaume wengine wanaostahili. (Hesabu 11:16, 17, 26-29) Badala yake, anakuwa na hamu ya kuwasaidia wafanye maendeleo ya kiroho. (1 Timotheo 4:15) Je, hatupaswi kufanya hivyo pia?

‘Njia ya Mtu Mkamilifu Imenyooka’

Akitambua kwamba uaminifu-maadili sikuzote hauwalindi wanyoofu wasipatwe na hatari au maafa, Solomoni asema: “Ukamilifu [“uaminifu-maadili,” “NW”] wao wenye haki utawaongoza bali ukaidi wao wenye fitina utawaangamiza.” (Mithali 11:3) Kwa kweli uaminifu-maadili huongoza wanyoofu wafanye mambo yanayofaa machoni pa Mungu, hata chini ya hali ngumu, nao hunufaika hatimaye. Yobu alidumisha uaminifu-maadili, naye Yehova ‘akaubarikia huo mwisho wa Yobu, zaidi ya mwanzo wake.’ (Ayubu 42:12) Huenda watu wanaotenda kwa hila wakafikiri kwamba wanajinufaisha kwa hasara ya mtu mwingine na hata huenda wakaonekana kuwa wamefanikiwa kwa muda. Lakini mwishowe wataharibiwa kwa sababu ya hila yao.

Mfalme mwenye hekima asema: “Mali hazifaidii kitu siku ya ghadhabu; bali haki huokoa na mauti.” (Mithali 11:4) Ni jambo la kipumbavu kama nini kufuatia vitu vya kimwili na kupuuza mambo ya kiroho kama vile funzo la kibinafsi, kusali, kuhudhuria mikutano, na kushiriki huduma ya shambani—mambo ambayo huzidisha upendo wetu kwa Mungu na kuimarisha ujitoaji wetu kwake! Mali haitaweza kuokoa yeyote wakati wa ile dhiki kubwa inayokuja. (Mathayo 24:21) Wanyoofu tu ndio watakaookolewa kwa sababu ya uadilifu wao. (Ufunuo 7:9, 14) Kwa hiyo, ni jambo la hekima kutii ombi hili la Sefania: “Kabla haijawajilia siku ya hasira ya BWANA. Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu.” (Sefania 2:2, 3) Kwa sasa, na tuazimie ‘kumheshimu Yehova kwa mali zetu.’—Mithali 3:9.

Akikazia zaidi umuhimu wa kufuatia uadilifu, Solomoni atofautisha mambo yatakayowapata wakamilifu na yatakayowapata waovu, asemapo: “Haki yake mtu mkamilifu itamwongoza njia yake; bali mtu mwovu ataanguka kwa uovu wake. Haki yao wenye haki itawaokoa; bali wafanyao fitina watanaswa kwa hila yao wenyewe. Mtu mwovu atakapokufa, taraja lake lapotea; na matumaini ya uovu huangamia. Mwenye haki huokolewa katika dhiki, na mtu mwovu ataiingia badala yake.” (Mithali 11:5-8) Mtu mkamilifu haanguki katika njia zake wala hanaswi katika shughuli zake. Njia yake imenyooka. Mwishowe, wanyoofu huokolewa kutoka kwa taabu. Huenda waovu wakaonekana kuwa wenye nguvu, lakini hawataokoka.

‘Mji Wafurahi’

Watu wengine huathiriwa pia na uaminifu-maadili wa wanyoofu na uovu wa watenda maovu. Mfalme wa Israeli asema: “Asiyemcha Mungu humpoteza jirani yake kwa kinywa chake; bali wenye haki watapona kwa maarifa.” (Mithali 11:9) Hakuna awezaye kukana kwamba uchongezi, porojo yenye kudhuru, maongezi yenye aibu, na maongezi ya kipuuzi hudhuru wengine. Kwa upande mwingine, maneno ya mwadilifu ni safi, hufikiriwa kwa uangalifu, na ni ya fadhili. Ujuzi humwokoa mwadilifu kwa sababu uaminifu-maadili wake humsaidia kupata uthibitisho unaohitajiwa kuonyesha kwamba washtaki wake wanasema uwongo.

Mfalme aendelea kusema: “Wenye haki wasitawipo, mji hufurahi; waovu waangamiapo, watu hupiga kelele.” (Mithali 11:10) Kwa kawaida watu waadilifu hupendwa na wengine, nao huwafurahisha jirani zao. Hakuna mtu anayependezwa na “waovu.” Waovu wanapokufa, kwa kawaida watu hawaombolezi. Bila shaka hakutakuwa na huzuni yoyote wakati Yehova ‘atakapotenga waovu na nchi na kung’oa wafanyao hila.’ (Mithali 2:21, 22) Badala yake, kutakuwa na furaha kwa sababu wameondolewa kabisa. Lakini namna gani sisi? Twapaswa kufikiria iwapo tunachangia furaha ya wengine kwa namna tunavyojiendesha.

“Mji Hutukuzwa”

Akiendelea kuonyesha jinsi ambavyo mtu mnyoofu na mwovu huathiri jamii, Solomoni asema: “Mji hutukuzwa kwa mbaraka wa mwenye haki; bali mji hupinduliwa kwa kinywa cha mwovu.”Mithali 11:11.

Wakazi wa mjini wanaoishi kwa unyoofu huchangia amani na furaha na kufanya wengine wawe na maadili bora katika jamii. Kwa hiyo, mji hutukuzwa—husitawi. Wale wanaosema maneno ya uchongezi, yasiyo ya fadhili, na yasiyofaa husababisha mvurugo, ukosefu wa furaha, migawanyiko, na matatizo. Hali huwa hivyo hasa watu wanaofanya mambo hayo wanapokuwa na mamlaka. Mji kama huo huwa na mvurugo, ufisadi, nao huzorota kiadili na pengine kiuchumi.

Kanuni inayotajwa katika andiko la Mithali 11:11 inawahusu pia watu wa Yehova wanaposhirikiana katika makutaniko yao yaliyo kama miji. Kutaniko lenye watu wa kiroho,wanyoofu wanaoongozwa na uaminifu-maadili, huwa na watu wenye furaha, bidii, na wanaojali, ambao humletea Mungu utukufu. Yehova hubariki kutaniko kama hilo, nalo husitawi kiroho. Pindi kwa pindi kunakuwa na watu wachache wasiotosheka, wakosoaji na wanaolalamika kuhusu jinsi mambo yanavyofanywa. Watu hao ni kama ‘mzizi wenye sumu’ unaoweza kuenea na kutia wengine sumu ambao hapo awali hawakuwa na tatizo lolote. (Waebrania 12:15) Mara nyingi watu kama hao hutaka mamlaka zaidi na umashuhuri. Wao huchochea uvumi kwamba kuna upendeleo, ubaguzi wa kikabila, au mambo kama hayo katika kutaniko au miongoni mwa wazee. Kwa kweli, maneno yao yaweza kusababisha mgawanyiko katika kutaniko. Hatupaswi kusikiliza mazungumzo ya watu kama hao, badala yake twapaswa kujitahidi kuwa watu wa kiroho wanaochangia amani na umoja katika kutaniko.

Solomoni aendelea kusema: “Asiye na akili humdharau mwenziwe; bali mtu aliye na ufahamu hunyamaza. Mwenye kitango akisingizia hufunua siri; bali mwenye roho ya uaminifu husitiri mambo.”Mithali 11:12, 13.

Mtu asiye na ufahamu au “asiye na akili” husababisha madhara makubwa kwelikweli! Yeye huzungumza pasipo kujizuia na kuwachongea au kuwadharau wengine waziwazi. Wazee waliowekwa rasmi wapaswa kukomesha mara moja uvutano huo usiofaa. Tofauti na “asiye na akili,” mtu mwenye ufahamu anajua wakati wa kunyamaza. Badala ya kufunua siri, yeye husitiri mambo. Mtu mwenye ufahamu anajua kwamba ulimi usiozuiwa unaweza kusababisha madhara makubwa, kwa hiyo yeye ni mwenye “roho ya uaminifu.” Yeye ni mwaminifu-mshikamanifu kwa waabudu wenzake naye hafunui siri zinazoweza kuwahatarisha. Watu hao wanaoshika uaminifu-maadili ni baraka kama nini kwa kutaniko!

Ili kutusaidia tutembee katika njia ya wanyoofu, Yehova huandaa chakula kingi cha kiroho chini ya mwelekezo wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Pia tunapokea msaada kutoka kwa wazee Wakristo katika makutaniko yetu yaliyo kama miji. (Waefeso 4:11-13) Kwa kweli tunashukuru sana kwa maandalizi hayo, kwa kuwa “pasipo mashauri taifa huanguka; bali kwa wingi wa washauri huja wokovu.” (Mithali 11:14) Hata kutokee nini, na tuazimie kabisa ‘kwenda kwa ukamilifu [“uaminifu-maadili,” NW] wetu.’—Zaburi 26:1.

[Blabu katika ukurasa wa 26]

Ni jambo la kipumbavu kama nini kufuatia vitu vya kimwili na kupuuza mambo ya kiroho!

[Picha katika ukurasa wa 24]

Yobu aliongozwa na uaminifu-maadili, naye Yehova alimbariki

[Picha katika ukurasa wa 25]

Uza alikufa kwa sababu ya kimbelembele chake