Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waonyeshe Fadhili-upendo Wenye Uhitaji

Waonyeshe Fadhili-upendo Wenye Uhitaji

Waonyeshe Fadhili-upendo Wenye Uhitaji

‘Tendeaneni kwa fadhili-upendo.’—ZEKARIA 7:9, NW.

1, 2. (a) Kwa nini tunapaswa kuonyesha fadhili-upendo? (b) Tutazungumzia maswali gani?

NENO la Yehova Mungu hututia moyo kupenda “rehema [“fadhili-upendo,” NW].” (Mika 6:8) Na pia hutupatia sababu za kufanya hivyo. Hiyo ni kwa sababu “mwenye rehema [“fadhili-upendo,” NW] huitendea mema nafsi yake.” (Mithali 11:17) Maneno hayo ni ya kweli kabisa! Tunapoonyesha fadhili-upendo, tunasitawisha urafiki wa karibu na wenye kudumu pamoja na wengine. Hivyo, tutakuwa na marafiki waaminifu-washikamanifu—ambao ni zawadi yenye thamani kubwa!—Mithali 18:24.

2 Zaidi ya hayo, Maandiko yanatuambia: “Aandamaye haki na fadhili [“fadhili-upendo,” NW] ataona uhai.” (Mithali 21:21) Naam, tukifuata fadhili-upendo tutapendwa na Mungu na tutakuwa na taraja la kufurahia baraka za wakati ujao zinazotia ndani uhai udumuo milele. Lakini tunaweza kuonyeshaje fadhili-upendo? Tuonyeshe nani fadhili-upendo? Na je, fadhili-upendo ni tofauti na fadhili ambazo kwa kawaida wanadamu huonyesha?

Fadhili Ambazo Wanadamu Huonyesha na Fadhili-Upendo

3. Sifa ya fadhili-upendo inatofautianaje na fadhili ambazo wanadamu huonyesha?

3 Sifa ya fadhili-upendo inatofautiana kwa njia mbalimbali na fadhili ambazo kwa kawaida wanadamu huonyesha. Kwa mfano, mara nyingi mtu anayeonyesha fadhili hufanya hivyo bila kujihusisha kibinafsi, au kuwa na uhusiano na watu anaowaonyesha fadhili. Hata hivyo, tunapoonyesha mtu fadhili-upendo tunashikamana naye kwa upendo. Katika Biblia, matendo ya fadhili-upendo kati ya wanadamu huenda yakategemea uhusiano uliopo tayari. (Mwanzo 20:13; 2 Samweli 3:8; 16:17) Au huenda yakategemea uhusiano unaotokana na matendo ya fadhili-upendo ambayo mtu alikuwa ametendewa hapo awali. (Yoshua 2:1, 12-14; 1 Samweli 15:6; 2 Samweli 10:1, 2) Ili kuonyesha tofauti hiyo, na tulinganishe mifano miwili ya Biblia inayoonyesha fadhili-upendo na fadhili ambazo wanadamu huonyesha.

4, 5. Mifano miwili inayotajwa katika Biblia inaonyeshaje tofauti kati ya fadhili ambazo wanadamu huonyesha na fadhili-upendo?

4 Mfano mmoja wa fadhili ambazo wanadamu huonyesha unahusu watu fulani walioharibikiwa na meli. Mtume Paulo alikuwa mmoja wao. Watu hao walipelekwa na maji hadi ufuo wa kisiwa cha Malta. (Matendo 27:37–28:1) Watu wa Malta hawakuwa na uhusiano na wasafiri hao waliokuwa taabani. Na zaidi, wasafiri hao hawakuwa wamewatendea watu wa Malta jambo lolote ambalo lingewafanya wahisi wakiwa na daraka la kuwasaidia. Hata hivyo, wakazi hao wa visiwani waliwakaribisha wageni hao vizuri na kuwaonyesha “fadhili ya kibinadamu isiyo ya kawaida.” (Matendo 28:2, 7) Ukaribishaji huo ulikuwa tendo la fadhili kwa wageni ambalo halikutazamiwa. Kwa hiyo ukaribishaji wao ulikuwa fadhili ambazo wanadamu huonyesha.

5 Kwa kulinganisha, fikiria jinsi Mfalme Daudi alivyomkaribisha Mefiboshethi, mwana wa Yonathani rafiki yake. Daudi alimwambia hivi Mefiboshethi: “Utakula chakula mezani pangu daima.” Akimweleza sababu ya kufanya hivyo, Daudi alimwambia: “Nitakutendea mema; kwa ajili ya Yonathani, baba yako.” (2 Samweli 9:6, 7, 13) Kwa kufaa, ukaribishaji huo wa Daudi unatajwa kuwa fadhili-upendo, si fadhili tu, kwa kuwa alionyesha uaminifu-mshikamanifu kwa uhusiano uliokuwa tayari umeanzishwa. (1 Samweli 18:3; 20:15, 42) Vivyo hivyo leo, watumishi wa Mungu huwaonyesha fadhili wanadamu kwa ujumla. Lakini wanaonyesha fadhili-upendo zenye kudumu, au upendo mwaminifu-mshikamanifu kwa wenzao ambao wana uhusiano wenye kukubalika kwa Mungu.—Mathayo 5:45; Wagalatia 6:10.

6. Ni mambo gani yanayohusiana na fadhili-upendo zinazoonyeshwa kati ya wanadamu ambayo yamekaziwa katika Neno la Mungu?

6 Ili kufahamu mambo mengine yanayohusiana na fadhili-upendo, tutachunguza kwa ufupi masimulizi matatu ya Biblia yanayokazia sifa hiyo. Kutokana na masimulizi hayo tutaona kwamba wanadamu huonyesha fadhili-upendo kwa (1) matendo hususa, (2) kwa nia ya kupenda, na (3)  hasa kwa wale walio na uhitaji. Zaidi ya hayo, masimulizi hayo yanaonyesha jinsi tunavyoweza kuonyesha fadhili-upendo leo.

Baba Aonyesha Fadhili-Upendo

7. Mtumishi wa Abrahamu alimwambia nini Bethueli na Labani, na mtumishi huyo alizusha suala gani?

7 Andiko la Mwanzo 24:28-67 linamalizia masimulizi kuhusu mtumishi wa Abrahamu, aliyetajwa katika makala iliyotangulia. Baada ya kukutana na Rebeka, mtumishi huyo alialikwa nyumbani kwa Bethueli, babake Rebeka. (Mstari wa 28-32) Huko mtumishi huyo alisimulia kwa undani mgawo wake wa kumtafutia mwana wa Abrahamu mke. (Mstari wa 33-47) Alikazia kwamba aliona kufanikiwa kwake kufikia wakati huo kuwa ishara kutoka kwa Yehova, “aliyeniongoza njiani, nimtwalie mwana wa bwana wangu binti wa ndugu yake.” (Mstari wa 48) Yaelekea mtumishi huyo alitumaini kwamba maelezo yake ya kutoka moyoni kuhusu tukio hilo yangemhakikishia Bethueli na mwanawe Labani kwamba Yehova alibariki mgawo huo. Mwishowe mtumishi huyo alisema: “Kama mnataka kumfanyia rehema [“fadhili-upendo,” NW] na kweli bwana wangu, niambieni kama sivyo, niambieni; ili nigeuke upande wa kuume au wa kushoto.”—Mstari wa 49.

8. Bethueli aliitikiaje katika kisa hiki kinachomhusu Rebeka?

8 Tayari Yehova alikuwa amemwonyesha Abrahamu fadhili-upendo. (Mwanzo 24:12, 14, 27) Je, Bethueli angekuwa tayari kufanya vivyo hivyo kwa kumruhusu Rebeka aende na mtumishi wa Abrahamu? Je, yeye pia angeonyesha fadhili-upendo kama zile zilizoonyeshwa na Mungu? Au safari ndefu ya mtumishi huyo ingekuwa ya bure? Ni lazima mtumishi huyo wa Abrahamu awe alifarijika sana kusikia Labani na Bethueli wakisema: “Neno hili limetoka kwa BWANA.” (Mstari wa 50) Walitambua kwamba Yehova alikuwa anahusika katika jambo hilo na wakakubali uamuzi wake bila kusita. Kisha, Bethueli akaonyesha fadhili-upendo zake kwa kuendelea kusema: “Rebeka huyu hapa; mchukue uende. Na awe mke wa mwana wa bwana wako kama Mwenyezi-Mungu alivyosema.” (Mstari wa 51, BHN) Rebeka alikubali kwenda na mtumishi wa Abrahamu na muda si muda akawa mke mpendwa wa Isaka.—Mstari wa 49, 52-58, 67.

Mwana Aonyesha Fadhili-Upendo

9, 10. (a) Yakobo alimwomba mwanawe Yosefu amfanyie nini? (b) Yosefu alimwonyeshaje babake fadhili-upendo?

9 Yakobo, mjukuu wa Abrahamu pia alionyeshwa fadhili-upendo. Kama Mwanzo sura ya 47 inavyoeleza, Yakobo alikuwa akiishi Misri wakati huo na ‘siku za kufa kwake zikakaribia.’ (Mstari wa 27-29) Alikuwa na wasiwasi kwa kuwa angekufa nje ya nchi ambayo Mungu alimwahidi Abrahamu. (Mwanzo 15:18; 35:10, 12; 49:29-32) Hata hivyo, Yakobo hakutaka kuzikwa Misri, hivyo akapanga mwili wake upelekwe katika nchi ya Kanaani. Hakuna mtu mwingine ambaye angeweza kuhakikisha kwamba tamaa yake imetimizwa isipokuwa tu mwanawe Yosefu aliyekuwa na uwezo.

10 Masimulizi hayo yanasema: “Yakobo akamwita mwanawe [Yosefu], akamwambia, Kama nimeona kibali machoni pako, . . . ukanifanyie rehema [“fadhili-upendo,” NW] na kweli; nakusihi usinizike katika Misri. Lakini nitakapolala pamoja na baba zangu, unichukue toka Misri, unizike katika kaburi lao.” (Mwanzo 47:29, 30) Yosefu aliahidi kutimiza ombi hilo, na muda mfupi baadaye Yakobo akafa. Yosefu na wana wengine wa Yakobo walibeba mwili wake ‘mpaka nchi ya Kanaani, nao wakamzika katika pango ya shamba la Makpela, aliyoinunua Abrahamu.’ (Mwanzo 50:5-8, 12-14) Hivyo, Yosefu akamwonyesha babake fadhili-upendo.

Binti-Mkwe Aonyesha Fadhili-Upendo

11, 12. (a) Ruthu alimwonyeshaje Naomi fadhili-upendo? (b) Ni katika njia gani Ruthu alionyesha fadhili-upendo nyingi zaidi wakati wa “mwisho” kuliko “mwanzo”?

11 Kitabu cha Ruthu kinasimulia jinsi Naomi alivyoonyeshwa fadhili-upendo na Ruthu, binti-mkwe wake aliyekuwa Mmoabu. Wote wawili walikuwa wajane. Naomi alipoamua kurudi Bethlehemu huko Yuda, Ruthu alionyesha fadhili-upendo na nia thabiti aliposema: “Wewe uendako nitakwenda, na wewe ukaapo nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” (Ruthu 1:16) Baadaye Ruthu alionyesha fadhili-upendo alipokubali kuolewa na Boazi, aliyekuwa mzee kutoka ukoo wa Naomi. * (Kumbukumbu la Torati 25:5, 6; Ruthu 3:6-9) Boazi alimwambia Ruthu hivi: “Umezidi kuonyesha fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zako mwisho kuliko mwanzo, kwa vile usivyowafuata vijana, kama ni maskini kama ni matajiri.”—Ruthu 3:10.

12 Ruthu alionyesha fadhili-upendo zake “mwanzo” alipowaacha watu wao na kuandamana na Naomi. (Ruthu 1:14; 2:11) Tendo la “mwisho” la fadhili-upendo lilikuwa bora kuliko la “mwanzo” kwa kuwa Ruthu alikubali kuolewa na Boazi. Kwa kuwa Naomi alikuwa amepita umri wa kuzaa, sasa Ruthu angeweza kumzalia mrithi. Boazi na Ruthu walioana, na baadaye Ruthu alipopata mtoto, wanawake wa Bethlehemu wakapaaza sauti: “Naomi amezaliwa mwana.” (Ruthu 4:14, 17) Kwa kweli Ruthu alikuwa “mwanamke mwema,” aliyethawabishwa na Yehova kwa kupewa pendeleo zuri la kuwa nyanya ya Yesu Kristo.—Ruthu 2:12; 3:11; 4:18-22; Mathayo 1:1, 5, 6.

Zaonyeshwa kwa Matendo

13. Bethueli, Yosefu, na Ruthu walionyeshaje fadhili-upendo?

13 Je, umeona jinsi Bethueli, Yosefu, na Ruthu walivyoonyesha fadhili-upendo? Walifanya hivyo kwa maneno yenye fadhili na kwa matendo hususa. Bethueli hakusema tu, “Rebeka huyu hapa” bali ‘alimwacha Rebeka aende.’ (Mwanzo 24:51, 59, BHN) Yosefu hakusema tu, “Nitafanya kama ulivyosema” bali yeye na ndugu zake walimfanyia Yakobo “kama alivyowaagiza.” (Mwanzo 47:30; 50:12, 13) Naye Ruthu hakusema tu, “Wewe uendako nitakwenda,” lakini aliwaacha watu wao na kuandamana na Naomi, “wakaendelea wote wawili hata walipofika Bethlehemu.” (Ruthu 1:16, 19) Huko Yuda, Ruthu pia ‘alifanya yote kama vile mkwewe alivyomwagiza.’ (Ruthu 3:6) Naam, fadhili-upendo za Ruthu, kama za wale wengine, zilionyeshwa kwa matendo.

14. (a) Watumishi wa Yehova wa siku hizi wanaonyeshaje fadhili-upendo kwa matendo? (b) Ni matendo gani ya fadhili-upendo yanayofanywa na Wakristo katika eneo lako?

14 Inachangamsha moyo kuona jinsi watumishi wa Mungu leo wanavyoendelea kuonyesha fadhili-upendo kwa matendo. Kwa mfano, fikiria wale wanaoendelea kuwategemeza kihisia-moyo waamini wenzao walio wagonjwa, walioshuka moyo, au wenye huzuni. (Mithali 12:25) Au fikiria Mashahidi wengi wa Yehova ambao kwa uaminifu hutumia magari yao kuwapeleka wazee-wazee kwenye Jumba la Ufalme ili kuhudhuria mikutano ya kila juma ya kutaniko. Wengi wana maoni kama haya ya Anna mwenye umri wa miaka 82 ambaye ana ugonjwa wa yabisi kavu: “Kupelekwa kwa gari kwenye mikutano yote ni baraka kutoka kwa Yehova. Ninamshukuru kutoka moyoni kwa kunipatia ndugu na dada kama hao wenye upendo.” Je, unafanya vivyo hivyo katika kutaniko lako? (1 Yohana 3:17, 18) Ikiwa unafanya hivyo, uwe na uhakika kwamba fadhili-upendo zako zinathaminiwa sana.

Zaonyeshwa kwa Nia ya Kupenda

15. Ni sifa gani inayohusiana na fadhili-upendo ambayo pia inakaziwa na masimulizi matatu ya Biblia ambayo tumechunguza?

15 Masimulizi ya Biblia ambayo tumechunguza yanaonyesha pia kwamba fadhili-upendo zinaonyeshwa kwa nia ya kupenda, pasipo kulazimishwa. Bethueli na Rebeka walishirikiana na mtumishi wa Abrahamu kwa nia ya kupenda. (Mwanzo 24:51, 58) Yosefu alionyesha fadhili-upendo bila kusukumwa na yeyote. (Mwanzo 50:4, 5) Ruthu “alikaza nia yake kufuatana na [Naomi].” (Ruthu 1:18) Naomi alipomshauri Ruthu azungumze na Boazi, Mmoabi huyo alichochewa na fadhili-upendo kusema: “Hayo yote unenayo mimi nitayafanya.”—Ruthu 3:1-5.

16, 17. Ni nini kinachofanya fadhili-upendo za Bethueli, Yosefu, na Ruthu ziwe na umuhimu wa kipekee, nao walichochewa na nini kuonyesha sifa hiyo?

16 Fadhili-upendo zilizoonyeshwa na Bethueli, Yosefu, na Ruthu zina umuhimu wa kipekee kwa sababu Abrahamu, Yakobo, na Naomi hawangeweza kuwalazimisha kutenda jinsi walivyotenda. Kwani, hakuna sheria ambayo ingemlazimisha Bethueli aache binti yake aende. Ingekuwa rahisi kwake kumwambia mtumishi wa Abrahamu hivi: ‘La, sitaki binti yangu anayefanya kazi kwa bidii awe mbali nami.’ (Mwanzo 24:18-20) Vivyo hivyo, Yosefu alikuwa huru kuamua kama atatimiza au hatatimiza ombi la babake, kwa kuwa Yakobo angekuwa amekufa na hangeweza kumlazimisha alitimize. Naomi mwenyewe alisema kwamba Ruthu alikuwa huru kukaa Moabu. (Ruthu 1:8) Ruthu pia alikuwa huru kuolewa na mmoja wa “vijana” badala ya kuolewa na Boazi aliyekuwa mzee.

17 Bethueli, Yosefu, na Ruthu walionyesha fadhili-upendo kwa nia ya kupenda; walichochewa kufanya hivyo kutoka moyoni. Walihisi wana daraka la kuwaonyesha fadhili-upendo watu waliokuwa na uhusiano nao, kama vile baadaye Mfalme Daudi alivyohisi ana wajibu wa kuonyesha sifa hiyo kwa Mefiboshethi.

18. (a) Wazee Wakristo ‘huchunga kundi’ wakiwa na mtazamo gani? (b) Mzee mmoja alisema anahisije kuhusu kuwasaidia waamini wenzake?

18 Sifa ya fadhili-upendo inatambulisha watu wa Mungu kutia ndani wale wanaochunga kundi lake. (Zaburi 110:3; 1 Wathesalonike 5:12) Wazee hao, au waangalizi, wanahisi wana daraka la kutimiza mambo wanayotazamiwa kutimiza wanapowekwa kuwa wazee. (Matendo 20:28) Hata hivyo, wao hufanya uchungaji na matendo mengine ya fadhili-upendo kwa ajili ya kutaniko, “si kwa kushurutishwa, bali kwa nia ya kupenda.” (1 Petro 5:2) Wazee huchunga kundi kwa sababu wana daraka hilo na wanatamani kufanya hivyo. Wanawaonyesha kondoo wa Kristo fadhili-upendo kwa sababu wanapaswa kufanya hivyo nao pia wanataka kufanya hivyo. (Yohana 21:15-17) “Ninapenda kutembelea akina ndugu nyumbani au kuwapigia simu ili kuwaonyesha tu nilikuwa ninawafikiria,” anasema mzee mmoja Mkristo. “Kuwasaidia akina ndugu huniletea furaha na uradhi mwingi!” Wazee wote wanaojali wanakubaliana na maneno hayo kabisa.

Waonyeshe Fadhili-Upendo Wenye Uhitaji

19. Masimulizi ya Biblia yaliyozungumziwa katika makala hii yanakazia nini kuhusu fadhili-upendo?

19 Masimulizi ya Biblia tuliyozungumzia pia yanakazia kwamba fadhili-upendo zinapaswa kuonyeshwa wale ambao hawawezi kujitimizia mahitaji yao. Abrahamu alihitaji msaada wa Bethueli ili kuendeleza ukoo wake. Naye Yakobo alihitaji msaada wa Yosefu ili mwili wake upelekwe Kanaani. Naomi pia alihitaji msaada wa Ruthu ili kupata mrithi. Abrahamu, Yakobo, na Naomi hawangeweza kutimiza mahitaji yao bila kusaidiwa. Vivyo hivyo leo, fadhili-upendo zinapaswa hasa kuonyeshwa wale wenye uhitaji. (Mithali 19:17) Tunapaswa kumwiga mzee wa ukoo Yobu, ambaye alijali ‘maskini aliyelilia msaada, yatima asiyekuwa na wa kumsaidia’ na pia wale “waliokuwa karibu kuangamia.” Yobu pia ‘aliwafanya wajane waone tena furaha moyoni’ na akawa ‘macho kwa kipofu na miguu kwa viwete.’—Ayubu 29:12-15, BHN.

20, 21. Ni nani tunaohitaji kuwaonyesha fadhili-upendo, na sote tunapaswa kuazimia kufanya nini?

20 Kwa kweli, kuna ‘maskini wanaolilia msaada’ katika kila kutaniko la Kikristo. Huenda kilio chao kikasababishwa na upweke, kuvunjika moyo, kuhisi hawafai, kukatishwa tamaa na wengine, ugonjwa mbaya sana, au kifo cha mpendwa. Hata sababu iwe nini, Wakristo hao wapendwa wana mahitaji ambayo yanaweza na yanapaswa kutimizwa kwa matendo yetu ya fadhili-upendo tunayofanya kwa nia ya kupenda na kwa kuendelea.—1 Wathesalonike 5:14.

21 Hivyo basi, na tuendelee kumwiga Yehova Mungu, ambaye ni “mwingi wa rehema [“fadhili-upendo,” NW].” (Kutoka 34:6; Waefeso 5:1) Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwatendea jambo fulani hususa hasa wale wenye uhitaji. Na bila shaka tutamtukuza Yehova na kupata furaha nyingi ‘tunapotendeana kwa fadhili-upendo.’—Zekaria 7:9, NW.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Ili upate kujua zaidi kuhusu aina ya ndoa kati ya Boazi na Ruthu, ona ukurasa wa 370 katika Buku la Kwanza la Insight on the Scriptures, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Ungejibuje?

• Fadhili-upendo hutofautianaje na fadhili ambazo wanadamu huonyesha?

• Bethueli, Yosefu, na Ruthu walionyesha fadhili-upendo katika njia zipi?

• Tunapaswa kuonyesha fadhili-upendo tukiwa na mtazamo gani?

• Ni nani tunaohitaji kuwaonyesha fadhili-upendo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Bethueli alionyeshaje fadhili-upendo?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Upendo mwaminifu-mshikamanifu wa Ruthu ulikuwa baraka kwa Naomi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wanadamu huonyesha fadhili-upendo kwa nia ya kupenda, kwa matendo hususa, na kwa wale walio na uhitaji