Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Aipata Kweli Mahali Asipotazamia

Aipata Kweli Mahali Asipotazamia

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

Aipata Kweli Mahali Asipotazamia

NI MAPENZI ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:3, 4) Ili kutimiza hilo, Mashahidi wa Yehova wamechapisha na kugawanya Biblia na vichapo vingi sana vya kusaidia watu kujifunza Biblia. Nyakati nyingine, vichapo hivyo vimewasaidia watu wenye mioyo minyofu wajifunze kweli kupitia njia wasizotazamia kabisa. Kuhusiana na jambo hilo, watangazaji wa Ufalme huko Freetown, Sierra Leone, wanaripoti jambo lililoonwa lifuatalo.

Osman ni mtoto wa pili wa kiume katika familia yenye watoto tisa. Kwa kuwa familia yao ilikuwa ya kidini, Osman alikuwa akiandamana na babake kwenda kuabudu. Hata hivyo, Osman alisumbuliwa sana na mambo ambayo dini yake ilifundisha kuhusu moto wa mateso. Hakuelewa jinsi ambavyo Mungu mwenye rehema angetesa waovu kwa kuwachoma motoni. Nayo mambo aliyoelezwa ili kumsaidia aelewe fundisho la moto wa mateso hayakumtuliza.

Siku moja, alipokuwa na umri wa miaka 20, Osman aliona kitabu cha buluu ndani ya pipa la takataka kilichokuwa kimefunikwa kidogo na takataka. Kwa kuwa alipenda vitabu, Osman alikiokota, akakisafisha, ndipo akaona kichwa chake—Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. *

‘Ni kweli gani hii,’ Osman akajiuliza. Kwa kutaka kujua kweli hiyo, Osman alichukua kitabu hicho, akaenda nacho nyumbani na kukisoma chote mara moja. Alifurahi kama nini kujifunza kwamba jina la Mungu ni Yehova! (Zaburi 83:18) Osman pia alijifunza kwamba sifa kuu ya Mungu ni upendo na hata wazo la kutesa watu motoni Humchukiza sana. (Yeremia 32:35; 1 Yohana 4:8) Mwishowe, Osman alijifunza kwamba hivi karibuni Yehova ataleta paradiso duniani ambapo watu wataweza kuishi milele. (Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4) Hizo ni kweli nzuri kama nini kutoka kwa Mungu mwenye upendo! Osman alimshukuru Yehova sana kwa kumwezesha kupata kweli mahali asipotazamia.

Siku kadhaa baadaye, Osman alisaidiwa na marafiki fulani kupata Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, kisha akahudhuria mkutano kwa mara ya kwanza. Akiwa huko, alimwomba Shahidi mmoja ajifunze Biblia pamoja naye. Ingawa alipingwa sana na familia yao, Osman alifanya maendeleo ya kiroho na kubatizwa. (Mathayo 10:36) Leo, anatumikia akiwa mzee wa kutaniko. Inafurahisha kama nini kwamba mambo hayo yote yalitokana na kuokota kichapo cha Biblia katika pipa la takataka!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1968.