Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ujilaumu Mwenyewe Au Chembe Zako za Urithi?

Je, Ujilaumu Mwenyewe Au Chembe Zako za Urithi?

Je, Ujilaumu Mwenyewe Au Chembe Zako za Urithi?

WANASAYANSI wanajitahidi sana kuchunguza kama chembe za urithi ndizo husababisha mazoea kama vile ulevi, watu kufanya ngono na watu wa jinsia zao, kufanya ngono ovyoovyo, jeuri, na mazoea mengineyo yasiyo ya kawaida, na hata kifo chenyewe. Je, hatungefarijika kujua kwamba chembe zetu za urithi ndizo zinazopaswa kulaumiwa kwa mambo ambayo sisi hutenda? Ni kawaida ya binadamu kulaumu mtu au kitu kingine kwa makosa yake.

Ikiwa chembe zetu za urithi ndizo zinazopaswa kulaumiwa, wanasayansi wanasema kuna uwezekano wa kuzibadili na hivyo kuondoa tabia fulani zisizofaa. Matumaini hayo yamechochewa sana na mafanikio ya hivi karibuni katika utafiti wa chembe za urithi za mwanadamu.

Hata hivyo, wanasayansi wanataka kubadili chembe za urithi kwa kuwa wanaamini kwamba chembe hizo ndizo hufanya tutende dhambi na makosa mengine mbalimbali. Je, watafiti wa kisayansi wanaweza kuthibitisha kwamba chembe za urithi ndizo husababisha hali hiyo? Ni wazi kwamba jibu la swali hilo litaathiri sana jinsi tunavyojiona na jinsi tunavyoona wakati wetu ujao. Hata hivyo, tutajifunza mengi zaidi kwa kuchunguza kwanza chanzo cha mwanadamu kabla ya kuchunguza uthibitisho huo.

Chanzo cha Dhambi

Watu wengi wanajua, au hata wamesikia masimulizi juu ya wenzi wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, na jinsi walivyofanya dhambi kwenye bustani ya Edeni. Je, waliumbwa wakiwa na chembe fulani za urithi zenye kasoro ambazo zilifanya watende dhambi na wasiweze kutii?

Muumba wao, Yehova Mungu, ambaye kazi zake zote ni kamilifu, alisema kwamba viumbe hao, ambao ndio waliokuwa wa mwisho kuumbwa, walikuwa ‘wema sana.’ (Mwanzo 1:31; Kumbukumbu la Torati 32:4) Alizidi kuonyesha kwamba aliridhika na kazi yake kwa kuwabariki wenzi hao wawili wa kwanza na kuwaagiza wazaane waijaze dunia na kuitawala. Bila shaka Mungu hangalifanya hivyo kama angalijua kwamba wanadamu hao walikuwa na kasoro.—Mwanzo 1:28.

Kuhusu kuumbwa kwa wenzi wawili wa kwanza, Biblia inatuambia: “Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba.” (Mwanzo 1:27) Hiyo haimaanishi kwamba wanadamu waliumbwa wakiwa wanafanana na Mungu kwa sura, kwa kuwa “Mungu ni Roho.” (Yohana 4:24) Badala yake, inamaanisha kwamba wanadamu walipewa sifa kama za Mungu na uwezo wa kutofautisha mema na mabaya, yaani, dhamiri. (Waroma 2:14, 15) Pia walikuwa na uhuru wa kuchagua na uwezo wa kuchunguza mambo kisha kuamua hatua watakayochukua.

Hata hivyo, wazazi wetu wa kwanza walipewa miongozo, kwa kuwa hata walionywa kuhusu matokeo ya kufanya kosa. (Mwanzo 2:17) Kwa hiyo, mambo ya hakika yanaonyesha kwamba Adamu alipokabili tatizo la kuamua kati ya lililo jema na lililo baya, yeye alichagua kufanya lile aliloona lingemfaidi. Alijiunga na mke wake kufanya kosa badala ya kufikiria uhusiano wake na Muumba wake au matokeo ya baadaye ya kitendo chake. Alijaribu pia kumlaumu Yehova, akisema kwamba alipotoshwa na mke ambaye Yeye alimpa.—Mwanzo 3:6, 12; 1 Timotheo 2:14.

Jinsi Mungu alivyotenda kuhusiana na dhambi ya Adamu na Hawa hufunua jambo fulani. Hakujaribu kurekebisha ‘kasoro fulani’ katika chembe zao za urithi. Badala yake, alitenda yale aliyowaambia yangekuwa matokeo ya matendo yao, ambayo baadaye yalisababisha kifo. (Mwanzo 3:17-19) Masimulizi hayo ya kale yanatusaidia sana kuelewa tabia ya mwanadamu. *

Uthibitisho Kwamba Hatupaswi Kulaumu Chembe za Urithi

Kwa muda mrefu, wanasayansi wamekuwa wakipambana na kazi ngumu ya kujaribu kuona kama chembe za urithi husababisha magonjwa na tabia fulani za kibinadamu na kuona jinsi wanavyoweza kubadili hali hiyo. Baada ya kufanya utafiti kwa muda wa miaka kumi, vikundi sita vya watafiti walitambua chembe ya urithi inayosababisha ugonjwa wa Huntington, ingawa hawajui jinsi ambavyo chembe hiyo husababisha ugonjwa huo. Hata hivyo, likiripoti kuhusu utafiti huo, gazeti Scientific American lilimnukuu Evan Balaban, mwanabiolojia wa Harvard, aliyesema kwamba “ni vigumu hata zaidi kutambua chembe za urithi zinazosababisha kasoro za tabia.”

Kwa kweli, utafiti unaofanywa kujaribu kuhusianisha chembe za urithi za binadamu na tabia yake umeshindwa. Kwa mfano, ripoti moja katika kichapo, Psychology Today, kuhusu jitihada za kutambua chembe za urithi zinazosababisha kushuka moyo inasema: ‘Habari kuhusu kutokea na kuzuiwa kwa magonjwa ya akili zinaonyesha wazi kwamba magonjwa hayo hayasababishwi tu na chembe za urithi.’ Ripoti hiyo inatoa mfano: “Mmarekani 1 kati ya Wamarekani 100 waliozaliwa kabla ya mwaka wa 1905 alipatwa na mshuko wa moyo kufikia umri wa miaka 75. Wamarekani 6 kati ya Wamarekani 100 waliozaliwa miaka 50 baadaye, walipatwa na mshuko wa moyo kufikia umri wa miaka 24!” Hivyo, ripoti hiyo inamalizia kwa kusema kwamba hali za kijamii wala si chembe za urithi, ndizo zinazoweza kusababisha mabadiliko hayo katika muda mfupi kama huo.

Utafiti huo na utafiti mwingine mbalimbali unatuonyesha nini? Unatuonyesha wazi kwamba si chembe za urithi tu ambazo huathiri utu wetu. Utu wetu huathiriwa sana na mazingira ambayo yamebadilika sana siku hizi. Kuhusu mambo ambayo vijana wanaweza kutazama leo katika vipindi vya kuburudisha vinavyopendwa na wengi, kitabu Boys Will Be Boys kinasema kwamba itakuwa vigumu watoto kuwa na maadili mema ‘ikiwa watakua huku wakitazama kwa muda mrefu televisheni na sinema ambazo huonyesha watu wakishambuliwa, wakipigwa risasi, wakidungwa visu, wakipasuliwa tumbo, au kukatwakatwa, na ikiwa watakua wakisikiliza muziki unaotukuza ubakaji, kujiua, dawa za kulevya, kileo, au ubaguzi.’

Ni wazi kwamba Shetani, “mtawala wa ulimwengu huu,” ametokeza mazingira ambayo hutosheleza tamaa mbovu za mwanadamu. Bila shaka, sote hupata mkazo mkali kutokana na mazingira hayo.—Yohana 12:31; Waefeso 6:12; Ufunuo 12:9, 12.

Kisababishi Kikuu cha Matatizo ya Mwanadamu

Kama tulivyoona, matatizo ya mwanadamu yalianza wakati wenzi wawili wa kwanza walipofanya dhambi. Matokeo yakawa nini? Ingawa wazao wote wa Adamu hawakuhusika katika dhambi yake, wote huzaliwa wakiwa na dhambi, wasio wakamilifu, na wamerithi kifo. Biblia inaeleza: “Hiyo ndiyo sababu, kama vile kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.

Kwa sababu ya kutokamilika, mwanadamu hujikuta katika hali asiyoweza kubadili. Lakini jambo hilo halimaanishi kwamba yeye hana daraka lolote. Biblia huonyesha kwamba wale wanaoweka imani yao katika uandalizi wa Yehova wa kupata uhai, na kuishi kupatana na viwango vya Mungu, watapata kibali chake. Kwa sababu Yehova ni mwenye fadhili-upendo, alifanya uandalizi wa rehema wa kuwakomboa wanadamu, kana kwamba kununua tena, kile kilichopotezwa na Adamu. Uandalizi huo ni dhabihu ya fidia ya Mwanaye mkamilifu, Yesu Kristo, aliyesema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.”—Yohana 3:16; 1 Wakorintho 15:21, 22.

Mtume Paulo alithamini sana uandalizi huo. Alisema: “Mwenye taabu mimi! Ni nani ataniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki? Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Waroma 7:24, 25) Paulo alijua kwamba kama angefanya dhambi kwa sababu ya udhaifu, angeweza kumwomba Mungu amsamehe kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. *

Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo watu wengi walioishi maisha mabaya sana au ambao hali yao ilionekana kuwa bila matumaini, wamepata ujuzi sahihi wa Biblia, wakafanya mabadiliko yanayohitajika, na sasa wanaweza kupata baraka za Mungu. Mabadiliko waliyofanya hayakuwa rahisi, na wengi wao wanalazimika kukabiliana na maelekeo yenye kudhuru. Lakini kwa msaada wa Mungu, wanaweza kudumisha uaminifu-maadili na kufurahia kumtumikia. (Wafilipi 4:13) Fikiria mfano mmoja tu wa mtu aliyefanya mabadiliko makubwa ili kumpendeza Mungu.

Jambo Lililoonwa Lenye Kutia Moyo

“Nilipokuwa mvulana mdogo katika shule moja ya bweni, nilianza kufanya ngono na wavulana wenzangu, ingawa sikufikiri kamwe kwamba nilikuwa basha (mtu anayefanya ngono na watu wa jinsia yake). Wazazi wangu walikuwa wametalikiana, nao hawakunionyesha upendo ambao nilitamani sana kuonyeshwa. Baada ya kumaliza shule, nilifanya utumishi wa kijeshi uliokuwa wa lazima. Katika kambi ya kijeshi iliyokuwa karibu na yetu, kulikuwa na kikundi cha wanaume mabasha. Nilionea wivu maisha yao ya ubasha, hivyo nikaanza kushirikiana nao. Baada ya kushirikiana nao kwa mwaka mmoja, nilianza kujiona kuwa basha. ‘Nilizaliwa hivyo na siwezi kubadilika,’ nikawaza.

“Nilianza kujifunza misemo ya mabasha hao na kwenda kwenye vilabu vyao ambako dawa za kulevya na vileo vilipatikana kwa urahisi. Maisha hayo yalikuwa yenye kuchukiza sana ingawa kwa nje yalionekana kuwa yenye kusisimua na yenye kuvutia sana. Nilijua moyoni mwangu kwamba uhusiano huo si wa kiasili na kwamba maisha ya ubasha hayakuwa na matumaini ya wakati ujao.

“Katika mji mmoja mdogo, niliona Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova ambapo mkutano ulikuwa ukiendelea. Niliingia ndani na kusikiliza hotuba ambayo ilizungumzia hali zitakazokuwa katika Paradiso. Baadaye nilijuana na Mashahidi fulani walionialika kwenye kusanyiko. Nilienda kwenye kusanyiko hilo na kushangaa kuona familia zenye furaha zikiabudu pamoja. Nilianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi.

“Nilianza kufuata yale niliyokuwa nikijifunza kutoka katika Biblia, ingawa haikuwa rahisi. Niliacha kabisa mazoea yasiyo safi na baada ya kujifunza kwa miezi 14, nikajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Nilipata marafiki wa kweli kwa mara ya kwanza maishani. Nimewasaidia wengine kujifunza kweli ya Biblia, na sasa mimi ni mtumishi wa huduma katika kutaniko la Kikristo. Yehova amenibariki kwelikweli.”

Tunalaumika

Kujaribu kulaumu chembe zetu za urithi kwa makosa yetu hakutatusaidia. Kichapo Psychology Today, kinasema kwamba kulaumu chembe za urithi hakutatusaidia kutatua matatizo yetu, bali ‘huenda kukatukatisha tamaa, hali ambayo ndiyo kisababishi kikuu cha mengi ya matatizo yetu. Pia kufanya hivyo huzidisha matatizo badala ya kuyapunguza.’

Ni kweli kwamba tunalazimika kukabiliana na hali fulani zenye mkazo mkubwa, kutia ndani maelekeo yetu ya kufanya dhambi na jitihada za Shetani za kutukengeusha tusimtii Mungu. (1 Petro 5:8) Ni kweli kwamba chembe zetu za urithi zinaweza kutuathiri kwa njia mbalimbali. Lakini tuna hakika kwamba tutapata msaada. Wakristo wa kweli wana marafiki wenye nguvu—Yehova, Yesu Kristo, roho takatifu ya Mungu, Neno lake Biblia, na kutaniko la Kikristo.—1 Timotheo 6:11, 12; 1 Yohana 2:1.

Kabla ya taifa la Israeli kuingia katika Bara Lililoahidiwa, Musa aliwakumbusha watu daraka lao mbele za Mungu akisema: “Nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako; kumpenda BWANA, Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye.” (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20, italiki ni zetu.) Vivyo hivyo leo, kila mtu ana daraka la kufanya uamuzi wa kibinafsi wa kumtumikia Mungu na kutimiza matakwa yake. Chaguo ni lako.—Wagalatia 6:7, 8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ona gazeti la Amkeni! la Septemba 22, 1996, ukurasa wa 3-8.

^ fu. 19 Ona kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele ukurasa wa 62-69, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Je, Adamu na Hawa walikuwa na kasoro fulani katika chembe zao za urithi ambayo ilifanya watende dhambi?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je, kila mtu anapaswa kuona kuwa ana daraka kuhusiana na maamuzi yake?

[Hisani]

Mtumiaji wa madawa ya kulevya: Godo-Foto

[Picha katika ukurasa wa 11]

Jitihada za kupata chembe za urithi zinazofanya mtu awe na tabia fulani zimeshindwa

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kufuata yale ambayo Biblia husema kunaweza kuwasaidia watu wanyofu wabadilike