Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuchunguza kwa Makini Mapokeo Fulani Kuhusu Kifo

Kuchunguza kwa Makini Mapokeo Fulani Kuhusu Kifo

Kuchunguza kwa Makini Mapokeo Fulani Kuhusu Kifo

TANGU zamani, mwanadamu ametatanika na kuwa na wasiwasi anapofikiria kifo ambacho ni tukio lenye kuhuzunisha. Zaidi ya hayo, hofu ya kifo huzidishwa na mafundisho ya uwongo, desturi zinazofuatwa na wengi, na imani mbalimbali ambazo watu wameshikilia sana. Kuogopa kifo kunaweza kumnyima mtu furaha maishani na kumfanya asione kusudi la maisha.

Dini kubwa-kubwa zinalaumika hasa kwa kuunga mkono mapokeo kadhaa yanayoshikiliwa na wengi kuhusu kifo. Kwa kuchunguza mapokeo hayo kwa kuyalinganisha na kweli ya Biblia, ona kama utaweza kukielewa kifo vema zaidi.

Pokeo la 1: Kifo ni mwisho wa uhai.

‘Hatuwezi kuepuka kifo,’ kinasema kitabu Death—The Final Stage of Growth. Maneno hayo yanadhihirisha ile imani kwamba kifo ni tukio la kawaida, mwisho wa viumbe wote walio hai. Imani hiyo imefanya watu wawe na tabia ya kutumia fursa yoyote inayotokea ili kujinufaisha.

Lakini je, kwa kweli kifo ni mwisho wa uhai? Si watafiti wote wanaoamini jambo hilo. Kwa mfano, Calvin Harley, mwanabiolojia anayechunguza hali ya kuzeeka kwa binadamu, alisema katika mahojiano fulani kwamba yeye haamini kwamba wanadamu “wamekusudiwa wafe.” Mtaalamu wa kinga ya mwili, William Clark alisema: ‘Si lazima tufe.’ Naye Seymour Benzer kutoka Chuo cha Tekinolojia cha California anasema, ‘hatuwezi kusema kwamba kuzeeka ni jambo lisiloweza kuzuiwa, bali ni mfululizo wa matukio tunayoweza kubadilisha.’

Wanasayansi hushangaa wanapochunguza maumbile ya wanadamu. Wanakuta kwamba tumeumbwa tukiwa na uwezo mwingi sana wa kufanya mambo. Tunatumia tu kiasi kidogo sana cha uwezo huo katika kipindi cha miaka 70 hadi 80 ambacho tunatazamia kuishi. Kwa mfano, wanasayansi wamegundua kwamba ubongo wa binadamu una uwezo mkubwa sana wa kukumbuka mambo. Mtafiti mmoja alikadiria kwamba ubongo wetu unaweza kuhifadhi habari ambazo “zingejaza mabuku milioni ishirini yanayoweza kutoshea mojawapo ya maktaba kubwa zaidi ulimwenguni.” Wataalamu fulani wa mfumo wa neva wanaamini kwamba mwanadamu hutumia sehemu ndogo sana ya ubongo wake katika maisha yake yote. Inafaa kuuliza, ‘Kwa nini tuna ubongo wenye uwezo mkubwa hivyo ilhali sisi hutumia sehemu ndogo sana katika maisha yetu?’

Pia fikiria jinsi ambavyo wanadamu hutenda kwa njia isiyo ya kawaida wanapokabiliwa na kifo! Kwa wengi, kifo cha mke, mume, au mtoto kinaweza kusababisha majonzi makubwa maishani. Mara nyingi, hali ya watu ya kihisia-moyo huvurugika kwa muda mrefu baada ya kifo cha mpendwa. Hata wale ambao hudai kwamba kifo ni tukio la kawaida kwa binadamu hushindwa kukubali wazo la kwamba kifo chao wenyewe kitamaanisha mwisho wa mambo yote. Gazeti British Medical Journal lilitaja ‘maoni ya kitaalamu kwamba kila mtu hutaka kuishi muda mrefu iwezekanavyo.’

Tunapofikiria jinsi mwanadamu anavyokiona kifo, uwezo wake wa pekee wa kukumbuka na kujifunza, na tamaa yake ya moyoni ya kuishi milele, je, si wazi kwamba aliumbwa aishi? Kwa kweli, Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na taraja la kuishi milele, bali si wafe. Ona wakati ujao ambao Mungu aliwaandalia wenzi wawili wa kwanza wa kibinadamu: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.” (Mwanzo 1:28) Huo ulikuwa wakati ujao wa kudumu ulio mzuri kama nini!

Pokeo la 2: Mungu huchukua watu kupitia kifo ili wakakae pamoja naye.

Mama mmoja mwenye umri wa miaka 27 aliyekuwa karibu kufa na kuacha watoto wake watatu alimwambia hivi mtawa Mkatoliki: ‘Usije hapa kuniambia eti haya ni mapenzi ya Mungu kwangu. Ninaudhika sana mtu anaponiambia hivyo.’ Lakini, hivyo ndivyo dini nyingi hufundisha kuhusu kifo—kwamba Mungu huchukua watu ili wakakae pamoja naye.

Je, Muumba ni mkatili sana hivi kwamba angetuua bila kujali, huku akijua kwamba kifo hutuhuzunisha? La, Mungu wa Biblia hawezi kufanya hivyo. Kulingana na andiko la 1 Yohana 4:8, “Mungu ni upendo.” Ona kwamba andiko hilo halisemi Mungu ana upendo wala halisemi Mungu anapenda, bali linasema Mungu ni upendo. Upendo wa Mungu ni mwingi, halisi, na mkamilifu. Upendo huo hudhihirishwa sana katika utu na matendo ya Mungu hivi kwamba tunaweza kusema kwa kufaa kwamba yeye ni mfano halisi wa sifa ya upendo. Mungu kama huyo hawezi kuchukua watu kupitia kifo ili wakakae pamoja naye.

Dini zisizo za kweli zimefanya watu wasielewe hali ya wafu na mahali wanapoenda baada ya kufa. Inaaminika kwamba watu huenda mbinguni, motoni, purgatori, au Limbo baada ya kufa. Baadhi ya sehemu hizo hazieleweki na huogopesha sana. Lakini Biblia hutuambia kwamba wafu hawajui neno lolote; ni kana kwamba wamelala usingizi. (Mhubiri 9:5, 10; Yohana 11:11-14) Hivyo, hakuna haja ya kuwa na wasiwasi kuhusu kinachotupata tunapokufa, kama vile tu hatungekuwa na wasiwasi kuona mtu amelala fofofo. Yesu alitaja wakati ambapo “wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho” ‘wangetoka’ kuishi maisha mapya katika dunia paradiso.—Yohana 5:28, 29; Luka 23:43.

Pokeo la 3: Mungu huchukua watoto wadogo ili wawe malaika.

Elisabeth Kübler-Ross, aliyewachunguza watu wenye magonjwa yasiyotibika, alitaja maoni mengine yanayoshikiliwa na wengi katika dini. Akieleza tukio fulani halisi, alisema kwamba si ‘hekima kumwambia mtoto aliyefiwa na ndugu yake kwamba Mungu anawapenda sana wavulana wadogo na ndiyo sababu alimchukua Johnny, ndugu yake mdogo, kwenda mbinguni.’ Maneno kama hayo hufanya Mungu aeleweke vibaya na hayaonyeshi utu wake wala sifa zake. Dakt. Kübler-Ross anaendelea kusema: ‘Msichana mdogo aliyeambiwa maneno hayo alimchukia Mungu hata alipokuwa mtu mzima na jambo hilo likafanya ashuke moyo sana alipofiwa na mtoto wake wa kiume miaka thelathini baadaye.’

Mbona Mungu amchukue mtoto ili kupata malaika mwingine—kana kwamba Mungu anamhitaji mtoto huyo zaidi ya vile wazazi wake wanavyomhitaji? Iwapo ni kweli kwamba Mungu huchukua watoto, je, jambo hili halingemfanya awe Muumba asiye na upendo na mwenye ubinafsi? Tofauti na maoni hayo, Biblia inasema: “Upendo ni wa kutoka kwa Mungu.” (1 Yohana 4:7) Je, Mungu wa upendo angesababisha kifo kama hicho ambacho hata wanadamu walio na kiasi fulani cha maadili wangekiona kuwa jambo lisilofaa kabisa?

Hivyo, kwa nini watoto hufa? Sehemu ya jibu hilo linapatikana katika Biblia kwenye Mhubiri 9:11, NW: “Wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” Nalo andiko la Zaburi 51:5 linatuambia kwamba sote ni watu wasio wakamilifu, waliozaliwa katika dhambi, na kwamba mwishowe sote tutakufa kwa sababu mbalimbali. Mara kwa mara, watoto hufa hata kabla hawajazaliwa. Nyakati nyingine wao hufa kwa sababu ya misiba fulani au aksidenti. Hatuwezi kumlaumu Mungu kwa vifo hivyo.

Pokeo la 4: Watu fulani huteswa baada ya kufa.

Dini nyingi hufundisha kwamba waovu wataenda motoni wakateswe milele. Je, fundisho hilo linapatana na akili na ni la Kimaandiko? Mwanadamu anatarajiwa kuishi muda wa miaka 70 au 80 hivi. Hata mtu awe alifanya mambo mabaya kadiri gani alipokuwa hai, je, kuteswa milele kungekuwa adhabu ya haki? La. Halingekuwa jambo la haki hata kidogo kutesa mtu milele kwa sababu ya dhambi alizofanya kwa muda mfupi alipokuwa hai.

Mungu peke yake ndiye anayeweza kufunua kile ambacho hutokea watu wanapokufa, naye amefanya hivyo katika Neno lake lililoandikwa, Biblia. Biblia inasema hivi: “Anavyokufa huyu [mnyama] ndivyo anavyokufa huyu [mwanadamu]; naam, wote wanayo pumzi moja . . . Wote huendea mahali pamoja; wote hutoka katika mavumbi; na hata mavumbini hurudi tena.” (Mhubiri 3:19, 20) Andiko hilo halitaji moto wa mateso. Wanadamu hurudi mavumbini—hali ya kutokuwepo—wanapokufa.

Ili mtu ateswe ni lazima awe na fahamu. Je, wafu wana fahamu? Kwa mara nyingine Biblia inajibu: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote, wala hawana ijara tena; maana kumbukumbu lao limesahauliwa.” (Mhubiri 9:5) Haiwezekani kwa wafu, ambao “hawajui neno lolote,” wahisi uchungu hata wawe wapi.

Pokeo la 5: Kifo humaanisha kwamba hatutapata kuwa hai tena.

Uhai hukoma tunapokufa, lakini hilo halimaanishi kwamba hatuna matumaini ya kuwa hai tena. Yobu, aliyekuwa mtu mwaminifu, alijua kwamba angeenda Sheoli, yaani kaburini, baada ya kufa. Lakini sikiliza sala yake kwa Mungu: “Laiti ungenificha [Sheoli], ukanilinda kwa siri, hata ghadhabu zako zitakapopita, na kuniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka! Mtu akifa, je! atakuwa hai tena? . . . Wewe ungeita, nami ningekujibu.”—Ayubu 14:13-15.

Yobu aliamini kwamba kama angekuwa mwaminifu hadi kifo, baadaye Mungu angemkumbuka na kumfufua. Watumishi wa zamani wa Mungu waliamini hivyo. Yesu alithibitisha tumaini hilo na kuonyesha kwamba Mungu angemtumia kufufua wafu. Kristo mwenyewe anatuhakikishia hivi: ‘Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti ya Yesu na kutoka, wale waliofanya mambo mema kwenye ufufuo wa uhai, wale waliozoea kufanya mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.’—Yohana 5:28, 29.

Hivi karibuni Mungu ataondoa uovu wote na kuleta ulimwengu mpya chini ya utawala wa mbinguni. (Zaburi 37:10, 11; Danieli 2:44; Ufunuo 16:14, 16) Utawala huo utafanya dunia yote kuwa paradiso, ambayo itakaliwa na watu wenye kumtumikia Mungu. Tunasoma hivi katika Biblia: “Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’”—Ufunuo 21:3, 4.

Kuishi Bila Woga

Inafariji kujua kwamba kuna tumaini la ufufuo na ni Nani anayetoa tumaini hilo. Yesu aliahidi: “Nanyi mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru.” (Yohana 8:32) Ahadi hiyo inatia ndani kutuweka huru na hofu ya kifo. Yehova peke yake ndiye anayeweza kuzuia tusizeeke na kufa na kutupatia uhai wa milele. Je, unaweza kuamini ahadi za Mungu? Ndiyo, kwa sababu Neno la Mungu hutimizwa sikuzote. (Isaya 55:11) Tunakutia moyo ujifunze mengi zaidi kuhusu makusudi ya Mungu kwa wanadamu. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Kuogopa kifo kunaweza kumnyima mtu furaha maishani

[Chati katika ukurasa wa 7]

MAPOKEO FULANI YA KAWAIDA MAANDIKO YANASEMA NINI?

KUHUSU KIFO

Kifo ni mwisho wa uhai Mwanzo 1:28; 2:17;

Waroma 5:12

Mungu huchukua watu kupitia Ayubu 34:15; Zaburi 37:11, 29;

kifo ili wakakae pamoja naye Zaburi 115:16

Mungu huchukua watoto wadogo Zaburi 51:5; 104:1, 4;

ili wawe malaika Waebrania 1:7, 14

Watu fulani huteswa baada ya kifo Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5, 10; Waroma 6:23

Kifo humaanisha kwamba Ayubu 14:14, 15;

hatutapata kuwa hai tena Yohana 3:16; 17:3;

Matendo 24:15

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kujua kweli kuhusu kifo hutuondolea hofu

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

Barrators—Giampolo/The Doré Illustrations For Dante’s Divine Comedy/Dover Publications Inc.