Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, mtu aliye na tatizo kubwa la afya ambaye anataka kubatizwa ni lazima azamishwe kabisa katika maji, hata ingawa ingekuwa vigumu kumzamisha?

Neno “batiza” latokana na kitenzi cha Kigiriki baʹpto, kinachomaanisha “kuchovya.” (Yohana 13:26) Katika Biblia, “kubatiza” ni sawa na “kuzamisha.” Kichapo The Emphasised Bible cha Rotherham chasema hivi kuhusu ubatizo wa towashi Mwethiopia uliofanywa na Filipo: “Wote wawili wakateremka kwenda kuingia katika maji, Filipo na pia towashi,—naye akamzamisha.” (Matendo 8:38) Kwa hiyo mtu anayebatizwa huchovywa katika maji.—Mathayo 3:16; Marko 1:10.

Yesu aliwaagiza hivi wanafunzi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza.” (Mathayo 28:19, 20) Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova hubatiza watu katika vidimbwi, maziwa, mito, au sehemu nyingine zenye maji ya kutosha kuzamisha watu kabisa. Kwa kuwa kubatizwa kwa kuzamishwa kabisa ni takwa la Kimaandiko, hakuna mwanadamu aliye na mamlaka ya kumzuia mtu asibatizwe. Kwa hiyo, mtu apaswa kubatizwa hata inapokuwa lazima kuchukua hatua zisizo za kawaida kwa sababu ya hali yake. Kwa mfano, watu wenye umri mkubwa au wenye afya mbaya, wamebatizwa kwenye bafu kubwa. Maji ya bafu yaweza kupashwa moto, anayetaka kubatizwa aweza kuingizwa kwa utaratibu ndani ya maji, kisha baada ya mwili wake kuyazoea, anaweza kubatizwa.

Hata watu walio na matatizo mabaya sana ya afya wamebatizwa. Kwa mfano, watu fulani ambao walifanyiwa upasuaji wa koo, na hivyo kuachwa na tundu kooni, au wale wanaohitaji kutumia mashine ya kuwasaidia kupumua, wamezamishwa. Bila shaka, ili kubatiza watu wenye matatizo hayo, matayarisho mazuri yapasa kufanywa. Lingekuwa jambo la hekima muuguzi au daktari awepo ikiwezekana. Hata hivyo, karibu kila mtu mwenye tatizo la afya anaweza kubatizwa ikiwa hatua ya uangalifu au tahadhari itachukuliwa. Ikiwa mtu yuko tayari kukabiliana na hatari yoyote inayoweza kutokea, jitihada yapasa kufanywa ili abatizwe katika maji.