Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimethawabishwa kwa Ujitoaji-Kimungu

Nimethawabishwa kwa Ujitoaji-Kimungu

Simulizi la Maisha

Nimethawabishwa kwa Ujitoaji-Kimungu

LIMESIMULIWA NA WILLIAM AIHINORIA

Niliamka usiku wa manane na kukuta Baba akipiga kite kama ilivyokuwa kawaida yake. Alikuwa akigaagaa sakafuni huku ameshika tumbo lake. Mimi, Mama, na dadangu mkubwa, tulikusanyika karibu naye. Maumivu yalipotulia kidogo, aliketi wima, akavuta pumzi na kusema: “Mashahidi wa Yehova ndio tu wenye amani katika dunia hii.” Maneno hayo yalinishangaza na pia kunigusa moyo sana kwa sababu sikuwa nimewahi kusikia juu ya Mashahidi wa Yehova. Hivyo nikataka kujua Baba alimaanisha nini.

JAMBO hilo lilitukia mwaka wa 1953 nilipokuwa na umri wa miaka sita. Nilikulia katika familia yenye desturi ya kuoa wake wengi na tuliishi katika kijiji cha wakulima cha Ewossa, kilichoko magharibi ya kati ya Nigeria. Nilikuwa mtoto wa pili, lakini mtoto wa kwanza wa kiume katika familia ambayo mwishowe ilipanuka ikatia ndani wake 3 wa Baba na watoto 13. Sote tuliishi katika nyumba ya udongo ya Babu yenye vyumba vinne, ambayo ilikuwa imeezekwa kwa nyasi. Familia hiyo pia ilitia ndani Nyanya na ndugu watatu wa Baba, na familia zao.

Maisha yangu ya utotoni yalikuwa yenye huzuni. Huzuni hiyo ilizidishwa hasa na afya mbaya ya Baba. Alikuwa na maumivu ya tumbo yaliyomsumbua hadi alipokufa miaka mingi baadaye. Ugonjwa huo usiojulikana haungeweza kutibika kwa miti shamba au kwa madawa mengine ya kiasili, ambayo familia ya hali ya chini ya Kiafrika ingeweza kulipia. Mara nyingi tulilia usiku kucha kando ya Baba aliyekuwa akigaagaa sakafuni kwa maumivu. Baba na Mama walisafiri mara nyingi kwenda kutafuta dawa. Waliposafiri, mimi na ndugu zangu tulitunzwa na Nyanya.

Familia yetu ilijiruzuku kwa kulima na kuuza viazi vikuu, mihogo, na njugu za kola. Pia tuligema umajimaji unaotumiwa kutengeneza mpira ili kuongezea mapato yetu madogo. Chakula chetu kikuu kilikuwa viazi vikuu. Tulikula viazi vikuu asubuhi, mchana, vikiwa vimepondwa-pondwa, na jioni vilevile. Mara kwa mara tulikula ndizi zilizochomwa.

Kuabudu wazazi wetu wa kale kulizingatiwa sana katika maisha yetu. Watu wa familia yetu waliwatolea chakula wazazi wao waliokufa kwa kukiweka mbele ya miti iliyokuwa imefungiwa magamba ya kauri. Baba pia aliabudu sanamu fulani ili kujikinga na roho waovu na wachawi.

Nilipokuwa na umri wa miaka mitano, tulihama kijijini mwetu kwa muda mfupi na kwenda katika kambi moja ya wakulima, umbali wa kilometa 11 hivi. Huko, Baba alipatwa na minyoo iliyofanya ugonjwa wake wa tumbo uwe mbaya hata zaidi. Hangeweza kufanya kazi mchana, nalo tumbo lilimwuma sana usiku. Nilipatwa na homa inayosababishwa na aina fulani ya funza, ambao hujipenyeza chini ya ngozi. Kwa sababu hiyo, tulitegemea misaada kutoka kwa watu wetu wa ukoo. Badala ya kufa kwa umaskini, tulirudi kijijini mwetu huko Ewossa. Baba hakutaka mimi, mtoto wake wa kiume wa kwanza, niwe mkulima. Aliona kwamba elimu nzuri ingeniwezesha kuinua hali ya maisha ya familia yetu na ingenisaidia kulea ndugu na dada zangu.

Napata Kujua Dini Mbalimbali

Nilianza kwenda shuleni baada ya kurudi kijijini mwetu. Kwa hiyo nikapata kujua dini mbalimbali za Jumuiya ya Wakristo. Katika miaka ya 1950 elimu ya serikali za kikoloni iliambatanishwa na dini. Kwa kuwa shule ya msingi niliyosomea ilikuwa ya Wakatoliki, nililazimika kuwa Mkatoliki.

Nilipofikisha miaka 19 mwaka wa 1966, nilijiunga na Shule ya Upili ya Pilgrim Baptist katika mji wa Ewohinmi, umbali wa kilometa 8 kutoka Ewossa. Huko nilianza kufunzwa imani tofauti ya kidini. Kwa sababu sasa nilikuwa ninasomea shule ya Kiprotestanti, makasisi Wakatoliki walinizuia nisishiriki Misa Jumapili.

Nilipata fursa ya kusoma Biblia kwa mara ya kwanza wakati nilipojiunga na shule hiyo ya Baptist. Ingawa sikuacha kanisa Katoliki, nilisoma Biblia peke yangu kila Jumapili baada ya kutoka kanisani. Nilipendezwa sana na mafundisho ya Yesu Kristo na yalinichochea kutaka kuishi maisha yenye kusudi na ya ujitoaji-kimungu. Kadiri nilivyosoma Biblia ndivyo nilivyozidi kuchukizwa na unafiki wa viongozi fulani wa dini na maisha machafu ya watu wa kawaida. Watu hao waliodai kuwa Wakristo walifanya mambo yaliyokuwa tofauti sana na yale ambayo Yesu na wanafunzi wake walifundisha na kufanya.

Kuna mambo fulani hasa yaliyonishtua. Pindi moja nilipoenda kununua tasbihi kwenye duka ambapo mkatekista mmoja (mwalimu afundishaye imani ya dini) alikuwa akiuza bidhaa fulani, niliona kinyago cha uchawi kikining’inia mlangoni. Pindi nyingine mkuu wa shule ya Baptist alijaribu kuninajisi. Baadaye nilipata kujua kwamba alikuwa na zoea la kufanya ngono na wanaume wenzake na alikuwa amewanajisi wengine. Nilifikiria mambo hayo na kujiuliza, ‘Je, Mungu hukubali dini ambazo washiriki wake na hata viongozi wake huachiliwa tu waendelee kufanya dhambi nzito?’

Nabadili Dini

Hata hivyo, nilifurahia sana yale niliyosoma katika Biblia na nikaamua kuendelea kuisoma. Wakati huo ndipo nilipoanza kufikiria maneno ya Baba aliyokuwa amesema miaka 15 hivi iliyokuwa imepita: “Mashahidi wa Yehova ndio tu wenye amani katika dunia hii.” Lakini nilikuwa na wasiwasi kwa sababu vijana Mashahidi shuleni mwetu walidhihakiwa na nyakati nyingine hata kuadhibiwa kwa kukataa kushiriki ibada ya asubuhi. Baadhi ya mambo waliyoamini yalionekana kuwa yasiyo ya kawaida. Kwa mfano, ilikuwa vigumu kuamini kwamba watu 144,000 tu ndio wanaoenda mbinguni. (Ufunuo 14:3) Kwa kuwa nilitamani sana kwenda mbinguni, nilitaka kujua kama idadi hiyo ilikuwa imekamilika kabla sijazaliwa.

Ilikuwa wazi kwamba mwenendo na mtazamo wa Mashahidi ulikuwa tofauti. Hawakuhusika katika mwenendo mchafu kingono au vitendo vya jeuri vya wanafunzi wengine shuleni. Nilikuwa nimesoma katika Biblia kwamba wafuasi wa dini ya kweli wanapaswa kujitenga kabisa na ulimwengu, na niliona Mashahidi hao walikuwa wamefanya hivyo.—Yohana 17:14-16; Yakobo 1:27.

Niliamua kufanya uchunguzi zaidi. Mnamo Septemba 1969, nilipata kitabu “Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele.” Mwezi uliofuata, painia mmoja, kama wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova wanavyoitwa, akaanza kujifunza nami. Baada ya kujifunza mara ya kwanza nilichochewa kusoma kitabu hicho. Nilianza kukisoma Jumamosi usiku na kukimaliza alasiri siku iliyofuata. Mara nikaanza kuwaelezea wanafunzi wenzangu mambo mazuri niliyokuwa nikisoma. Wanafunzi na walimu walifikiri kwamba imani yangu mpya ingefanya nirukwe na akili. Lakini nilijua kwamba sikuwa ninarukwa na akili.—Matendo 26:24.

Habari kwamba nilikuwa ninahubiri dini mpya ziliwafikia wazazi wangu. Waliniomba nirudi nyumbani mara moja ili wachunguze nilikuwa na tatizo gani. Hakuna yeyote ambaye angenipa ushauri, kwa kuwa Mashahidi wote walikuwa wameenda kwenye mojawapo ya makusanyiko yao huko Ilesha. Niliporudi nyumbani, nilishambuliwa kwa maswali na kushutumiwa na mama na watu wengine wa ukoo. Nilijaribu niwezavyo kutetea yale niliyokuwa nikijifunza katika Biblia.—1 Petro 3:15.

Baada ya kushindwa kuthibitisha kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa walimu wa uwongo, mjomba wangu alijaribu mbinu tofauti. Alinisihi hivi: “Kumbuka kwamba ulienda shuleni kusoma. Ukiacha shule uende kuhubiri, hutamaliza masomo yako. Kwa hiyo, ungengoja umalize shule kwanza kisha ujiunge na dini hiyo mpya.” Wakati huo ushauri huo ulionekana unafaa, kwa hiyo nikaacha kujifunza na Mashahidi.

Mnamo Desemba 1970, mara tu baada ya kumaliza shule, nilienda moja kwa moja kwenye Jumba la Ufalme, na tangu wakati huo nimekuwa nikihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Nilibatizwa Agosti 30, 1971, kuonyesha wakfu wangu kwa Mungu. Jambo hilo liliwashtua wazazi wangu na pia watu wa kijiji kwa ujumla. Walisema kwamba nilikuwa nimewakatisha tamaa kwa kuwa mimi ndiye niliyekuwa mtu wa kwanza katika kijiji cha Ewossa kupata msaada wa masomo wa serikali. Wengi walikuwa na matumaini makubwa kunihusu. Walitumaini kwamba ningetumia elimu yangu kuboresha maisha katika kijiji hicho.

Matokeo ya Kubadili Dini

Familia yangu na wazee wa kijiji walituma watu fulani kuja kunishawishi niache dini yangu. Walijaribu kufanya hivyo huku wakinilaani. “Ikiwa hutaacha dini hii hutafaulu maishani,” wakasema. “Hutapata kazi wala hutaweza kujenga nyumba yako mwenyewe. Hutaweza kuoa wala kuwa na familia.”

Kinyume cha matabiri yao mabaya, niliajiriwa kazi ya ualimu miezi kumi tu baada ya kumaliza shule. Kisha mnamo Oktoba 1972, nikamwoa mke wangu mpendwa, Veronica. Baadaye, serikali ilinizoeza kazi ya afisa wa kilimo. Nilinunua gari langu la kwanza, na nikaanza kujenga nyumba. Binti yetu Victory, alizaliwa Novemba 5, 1973, na katika miaka iliyofuata, Lydia, Wilfred, na Joan wakazaliwa. Micah, mtoto wetu wa mwisho, alizaliwa mwaka wa 1986. Wote wamekuwa urithi wenye thamani sana kutoka kwa Yehova.—Zaburi 127:3.

Ninapokumbuka maisha yangu, ninaweza kusema kwamba laana za watu wa kijiji chetu ziligeuka kuwa baraka. Hiyo ndiyo sababu nilimwita binti yangu wa kwanza Victory (Ushindi). Hivi karibuni watu wa kijiji chetu waliniandikia barua, wakisema: “Tafadhali, tunataka urudi nyumbani na kushiriki katika maendeleo ya kijiji chetu kwa kuwa sasa Mungu anakubariki.”

Kulea Watoto Katika Njia za Mungu

Mimi na mke wangu tulijua kwamba ingekuwa vigumu kuendelea kufuatia vitu vya kimwili na wakati huohuo kutimiza daraka letu la kulea watoto. Hivyo, tumejifunza kuridhika na maisha sahili. Tunaona ni afadhali kuishi hivyo kuliko kukabili magumu yanayoweza kutokana na mtindo tofauti wa maisha.

Ni jambo la kawaida nchini mwetu kwa familia kadhaa kuishi katika nyumba moja na kutumia bafu moja, kupikia mahali pamoja, na kadhalika. Katika miji yote niliyoishi nikiwa mfanyakazi wa serikali, tulifurahi kupata nyumba yenye vitu hivyo ndani. Ni kweli kwamba kodi ya nyumba hizo ilikuwa ya juu, lakini zilisaidia kukinga watoto wetu na uvutano usiofaa. Ninamshukuru Yehova kwamba katika miaka ambayo imepita, tumeweza kulea watoto wetu katika mazingira mazuri kiroho.

Zaidi ya hayo, mke wangu hukaa nyumbani ili kutunza watoto. Ninapomaliza kazi, sisi hujitahidi kufanya mambo yote kwa ushirikiano tukiwa familia. Mambo hayo hutia ndani funzo la Biblia la familia, kutayarisha na kuhudhuria mikutano ya kutaniko, kushiriki katika huduma ya Kikristo, na kushiriki katika tafrija mbalimbali.

Tumejitahidi kufuata ushauri wa andiko la Kumbukumbu la Torati 6:6, 7, unaowatia wazazi moyo wawafundishe watoto wao si nyumbani tu bali kwenye kila fursa. Jambo hilo limefanya watoto wawe na ukaribu na Mashahidi badala ya watu wa ulimwengu. Wamejifunza kutokana na mfano wetu kuwa waangalifu wanapochagua marafiki kwa sababu mimi na Veronica hatushirikiani sana na watu ambao si Mashahidi.—Mithali 13:20; 1 Wakorintho 15:33.

Bila shaka, kuna jambo jingine ambalo limewasaidia watoto wetu mbali na mwongozo wetu na mafundisho yetu. Tumekuwa tukiwakaribisha na bado tunaendelea kuwakaribisha Wakristo wenye bidii, hasa waangalizi wasafirio wa Mashahidi wa Yehova. Wakristo hao wakomavu wanapokuwa na familia yetu, watoto wetu huona na pia hujifunza kutokana na maisha yao ya kujidhabihu. Hilo limekazia mambo tunayowafunza na kufanya wathamini kweli ya Biblia.

Nimethawabishwa kwa Ujitoaji-Kimungu

Leo, mimi na mke wangu, pamoja na watoto wetu wanne, tu wahudumu wa wakati wote. Nilianza kufanya upainia mwaka wa 1973. Katika miaka iliyopita, nimelazimika kuacha huduma ya wakati wote mara kwa mara kwa sababu ya hali za kiuchumi. Pia, mara kwa mara nimepata pendeleo la kufunza Shule ya Huduma ya Ufalme, ambayo huwazoeza waangalizi Wakristo wa Mashahidi wa Yehova. Sasa ninafurahi kutumikia katika Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali na pia kutumikia nikiwa mwangalizi wa jiji la Uhonmora.

Binti zangu wawili wa kwanza, Victory na Lydia, wamefunga ndoa nao wanaishi kwa furaha na waume zao ambao ni wazee Wakristo. Wanatumika pamoja na waume zao katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Igieduma, Nigeria. Mtoto wetu wa kiume wa kwanza, Wilfred, ni mtumishi wa huduma, naye mtoto wetu wa mwisho, Micah, hufanya upainia msaidizi mara kwa mara. Katika mwaka wa 1997, Joan alimaliza shule ya upili na kuanza upainia wa kawaida.

Nimefurahi sana kuwasaidia wengine, kutia ndani watu fulani wa ukoo wangu, kumtumikia Yehova Mungu. Babangu alishindwa kumtumikia Yehova kwa sababu alikuwa na wake wengi. Tangu ujanani, mimi nimependa watu. Mimi sijali sana matatizo yangu wakati ninapoona wengine wakiteseka. Ninatumaini kwamba wanaelewa kwamba tamaa yangu ya kuwasaidia ni ya moyo mweupe, na hilo hufanya iwe rahisi kwao kuzungumza nami.

Mmoja kati ya wale niliosaidia kujifunza makusudi ya Mungu ni mwanamume mmoja kijana asiyeweza kutoka kitandani kwa sababu ni mlemavu. Alikuwa akifanya kazi na kampuni moja ya umeme alipopatwa na mshtuko mbaya wa umeme na kulemaa kuanzia kifua kwenda chini. Alikubali kujifunza Biblia na hatua kwa hatua akaanza kuitikia yale aliyokuwa akijifunza. Alibatizwa Oktoba 14, 1995, katika kijito kimoja karibu na nyumbani kwetu. Hiyo ilikuwa mara yake ya kwanza kutoka kitandani kwa muda wa miaka 15. Alisema hiyo ndiyo iliyokuwa siku yenye furaha zaidi maishani mwake. Sasa yeye ni mtumishi wa huduma kutanikoni.

Sijuti kabisa kwamba kwa miaka 30 hivi iliyopita nilifanya uamuzi wa kumtumikia Yehova kwa kushirikiana na watu wake waliojiweka wakfu na wenye umoja. Nimeona upendo halisi ambao wanaonyesha kwa matendo. Hata kama uhai udumuo milele haungekuwa sehemu ya thawabu ambayo Yehova angewapa watumishi wake waaminifu, bado ningetamani kuishi maisha ya ujitoaji-kimungu. (1 Timotheo 6:6; Waebrania 11:6) Ujitoaji-kimungu umeniongoza maishani na kunitia nguvu. Kwa sababu hiyo, mimi na familia yangu tumekuwa wenye furaha na kuridhika.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na mke wangu na watoto mwaka wa 1990

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na mke wangu, watoto, na wakwe zangu wawili wa kiume