Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pendezwa na Uadilifu wa Yehova

Pendezwa na Uadilifu wa Yehova

Pendezwa na Uadilifu wa Yehova

‘Aandamaye uadilifu na fadhili, ataona uhai na uadilifu na heshima.’—MITHALI 21:21.

1. Watu wamefuata mwenendo gani leo ambao umeleta matokeo mabaya?

“IKO njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu; lakini mwisho wake ni njia za mauti.” (Mithali 16:25) Mithali hii ya Biblia hufafanua vizuri mwenendo wa watu wengi leo. Kwa ujumla, watu hujishughulisha tu na mambo wanayoona kuwa sawa na kupuuza mahitaji ya lazima ya wengine. (Mithali 21:2) Wanadai kwamba wanaheshimu sheria na viwango vya nchi lakini wanapinda sheria inapowezekana. Kwa sababu hiyo, jamii imegawanyika na kuvurugika.—2 Timotheo 3:1-5.

2. Wanadamu wanahitaji nini kwa haraka ili wanufaike?

2 Ili tunufaike—na wanadamu wote wawe na amani na usalama—tunahitaji kwa haraka sheria au kiwango cha uadilifu ambacho watu wote watakubali na kutii. Bila shaka, hakuna sheria au kiwango kilichowekwa na wanadamu ambacho kinaweza kutimiza uhitaji huo, hata kama waliokiweka ni wenye hekima au ni wanyofu kadiri gani. (Yeremia 10:23; Waroma 3:10, 23) Ikiwa kiwango hicho kipo, kinaweza kupatikana wapi nacho kikoje? Labda swali muhimu ni: Ikiwa kuna kiwango kama hicho, je, ungekipenda na kukifuata?

Kupata Kiwango cha Uadilifu

3. Ni nani anayestahili kutoa kiwango kinachokubalika na chenye kunufaisha watu wote, na kwa nini?

3 Ili kupata kiwango kitakachokubaliwa na wote na kuwanufaisha wote, tutahitaji kumgeukia mtu asiyeweza kuzuiwa na vikwazo vya kijamii, kitamaduni, siasa, udhaifu wa kibinadamu, na ambaye anaweza kufikiria mambo ya baadaye. Bila shaka, Yehova Mungu, Muumba mweza yote, ndiye pekee anayestahili kuweka kiwango hicho, naye anasema: “Kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.” (Isaya 55:9) Zaidi ya hayo, Biblia humfafanua Yehova kuwa “Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, Yeye ndiye mwenye haki [“uadilifu,” NW] na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Usemi “Yehova ni mwadilifu,” unapatikana katika Biblia nzima. (Kutoka 9:27; 2 Mambo ya Nyakati 12:6; Zaburi 11:7; 129:4; Maombolezo 1:18; Ufunuo 19:2; NW, kielezi-chini) Naam, Yehova anaweza kutupatia kiwango bora zaidi kwa sababu yeye ni mwaminifu, ni mwenye haki, na ni mwadilifu.

4. Neno “uadilifu” linamaanisha nini?

4 Bila shaka, neno “uadilifu” halipendwi sana na watu wengi leo. Watu wengi wana maoni mabaya au hata hulidharau neno hilo kwa sababu wao hulihusianisha na watu wanaojiona kuwa watakatifu kuliko wengine. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba uadilifu unahusisha haki, unyoofu, wema wa adili; kutokuwa na hatia, kutokuwa na dhambi, kutimiza kanuni za sheria ya Mungu au viwango vya adili vinavyokubalika, kutenda kwa haki. Je, hungependezwa na sheria au kiwango kinachotia ndani sifa nzuri kama hizo?

5. Eleza jinsi ambavyo Biblia hufafanua sifa ya uadilifu.

5 Kichapo Encyclopaedia Judaica chasema: ‘Uadilifu si sifa ya kuwaziwa tu bali ni sifa inayotegemea kufanya mambo ya haki na yanayofaa katika mahusiano yote.’ Kwa mfano, uadilifu wa Mungu si sifa tu ambayo Mungu anayo kama vile utakatifu na usafi. Badala yake, uadilifu ni wonyesho wa utu wake katika njia za haki na zinazofaa. Huenda tukasema kwamba kwa sababu Yehova ni mtakatifu na safi, kila kitu anachofanya au kinachotoka kwake ni chenye uadilifu. Kama Biblia inavyosema, “BWANA ni mwenye haki [“mwadilifu,” NW] katika njia zake zote, na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.”—Zaburi 145:17.

6. Paulo alisema nini kuhusu Wayahudi fulani wasioamini walioishi siku zake, na kwa nini?

6 Mtume Paulo alikazia jambo hilo katika barua yake kwa Wakristo huko Roma. Aliandika hivi kuhusu Wayahudi fulani wasioamini: “Kwa sababu ya kutojua uadilifu wa Mungu bali wakitafuta sana kusimamisha ulio wao wenyewe, hawakujitiisha wenyewe kwa uadilifu wa Mungu.” (Waroma 10:3) Kwa nini Paulo alisema kwamba watu hao ‘hawakujua uadilifu wa Mungu’? Je, hawakufundishwa Sheria, ambayo ni viwango vya uadilifu vya Mungu? Bila shaka walifundishwa. Hata hivyo, wengi wao waliona uadilifu kuwa wema wa kibinafsi, ambao mtu husitawisha kwa kushika kwa makini sana sheria za dini, badala ya kuuona kuwa kiwango cha kuwaongoza katika kushughulika na wanadamu wenzao. Watu hao walikuwa sawa na viongozi wa kidini wa siku za Yesu ambao hawakuelewa maana halisi ya haki na uadilifu.—Mathayo 23:23-28.

7. Uadilifu wa Yehova hudhihirishwaje?

7 Tofauti na watu hao, uadilifu wa Yehova hudhihirishwa na kuonekana waziwazi katika matendo yake yote. Ingawa kwa sababu ya uadilifu wake Mungu hataachilia wanaotenda dhambi kimakusudi, hilo halimaanishi kwamba yeye hajali, ni mwenye kudai mno, na anapaswa kuogopwa. Kinyume cha hilo, matendo yake ya uadilifu yameandaa msingi ambao wanadamu wanaweza kumfikia na kuokolewa kutoka kwa matokeo mabaya ya dhambi. Kwa hiyo, kwa kufaa Yehova anatajwa kuwa “Mungu mwenye haki [“mwadilifu,” NW], mwokozi.”—Isaya 45:21.

Uadilifu na Wokovu

8, 9. Sheria ilidhihirisha uadilifu wa Mungu katika njia zipi?

8 Ili kuelewa uhusiano uliopo kati ya uadilifu wa Mungu na tendo lake la upendo la wokovu, fikiria Sheria aliyolipa taifa la Israeli kupitia Musa. Bila shaka, Sheria hiyo ilikuwa ya uadilifu. Katika maneno yake ya mwisho, Musa aliwakumbusha Waisraeli hivi: “Liko taifa gani kubwa, lililo na amri na hukumu zenye haki [“adilifu,” NW] kama torati hii yote, ninayoiweka mbele yenu leo”? (Kumbukumbu la Torati 4:8) Karne kadhaa baadaye, Mfalme Daudi wa Israeli alisema: “Hukumu za BWANA ni kweli, zina haki [“adilifu,” NW] kabisa.”—Zaburi 19:9.

9 Yehova alidhihirisha waziwazi viwango vyake vya mema na mabaya kupitia Sheria. Sheria ilionyesha waziwazi jinsi Waisraeli walivyopaswa kujiendesha katika mambo yanayohusu dini, biashara, ndoa, vyakula na usafi, na bila shaka hukumu. Pia Sheria ilitia ndani adhabu kali kwa waliokosa kuifuata, na hata nyakati nyingine kulikuwa na hukumu ya kifo. * Lakini je, matakwa ya Mungu yaliyoonyeshwa katika Sheria, yalikuwa mzigo wenye kulemea watu na kuwanyima uhuru na furaha, kama wanavyodai watu wengi leo?

10. Watu waliompenda Yehova walizionaje sheria zake?

10 Watu waliompenda Yehova walipendezwa sana na sheria na maagizo yake ya uadilifu. Kwa mfano, kama tulivyoona Mfalme Daudi hakusema tu kwamba hukumu za Yehova ni za kweli na za uadilifu, bali alizipenda na kuzithamini sana pia. Kuhusu sheria na hukumu za Yehova aliandika hivi: ‘Ni za kutamanika kuliko dhahabu, kuliko wingi wa dhahabu safi. Nazo ni tamu kuliko asali, kuliko sega la asali. Tena mtumishi wako huonywa kwazo, katika kuzishika kuna thawabu nyingi.’—Zaburi 19:7, 10, 11.

11. Sheria ilithibitikaje kuwa ‘mfunzi ikiongoza kwa Kristo’?

11 Karne kadhaa baadaye, Paulo alitaja jambo lililofanya Sheria iwe yenye manufaa hata zaidi. Aliandika hivi katika barua yake kwa Wagalatia: “Hiyo Sheria imekuwa mfunzi wetu ikiongoza kwa Kristo, ili tupate kutangazwa kuwa waadilifu kwa sababu ya imani.” (Wagalatia 3:24) Katika siku za Paulo, mfunzi alikuwa mtumishi au mtumwa katika nyumba kubwa. Alikuwa na wajibu wa kuwalinda watoto na kuandamana nao hadi shuleni. Sawa na mfunzi, Sheria iliwalinda Waisraeli na mazoea mapotovu ya kiadili na ya kidini ya mataifa yaliyowazunguka. (Kumbukumbu la Torati 18:9-13; Wagalatia 3:23) Kwa kuongezea, Sheria ilifanya Waisraeli watambue hali yao yenye dhambi na kwamba walihitaji msamaha na wokovu. (Wagalatia 3:19) Mpango wa kutoa dhabihu ulikazia uhitaji wa dhabihu ya fidia na ulikuwa mfano wa kiunabii ambao ungesaidia kumtambua Mesiya wa kweli. (Waebrania 10:1, 11, 12) Kwa hiyo, ingawa Yehova alidhihirisha uadilifu wake kupitia Sheria, alifanya hivyo kwa kufikiria hali njema na wokovu wa milele wa wanadamu.

Wale Wanaoonwa Kuwa Waadilifu na Mungu

12. Waisraeli wangepata nini kwa kutii Sheria kwa makini?

12 Waisraeli wangekuwa waadilifu mbele za Mungu kama wangetii Sheria yake ambayo ilikuwa adilifu kabisa. Musa aliwakumbusha Waisraeli maneno haya kabla hawajaingia katika Bara Lililoahidiwa: “Itakuwa haki [“uadilifu,” NW] kwetu, tukitunza kufanya maagizo haya yote mbele ya BWANA, Mungu wetu, kama alivyotuagiza.” (Kumbukumbu la Torati 6:25) Kwa kuongezea, Yehova alikuwa ameahidi: “Mtazishika amri zangu na hukumu zangu; ambazo mtu akizitumia ataishi kwa hizo; mimi ndimi BWANA.”—Mambo ya Walawi 18:5; Waroma 10:5.

13. Je, Yehova alitenda kwa njia isiyo ya haki kwa kuwataka watu wake wafuate Sheria adilifu? Eleza.

13 Inasikitisha kwamba Waisraeli walishindwa “kufanya maagizo haya yote mbele ya BWANA” na hivyo wakakosa baraka walizoahidiwa. Walishindwa kushika amri zote za Mungu kwa sababu Sheria ya Mungu ilikuwa kamilifu lakini wao hawakuwa wakamilifu. Je, hii yamaanisha kwamba Mungu si mwenye haki au si mwadilifu? Sivyo. Paulo aliandika hivi: “Basi, tutasema nini? Je, kwa Mungu kuna ukosefu wa haki? Hilo lisipate kuwa hivyo kamwe!” (Waroma 9:14) Ukweli ni kwamba Mungu aliwaona watu walioishi kabla na hata baada ya Sheria kutolewa kuwa waadilifu ingawa walikuwa wenye dhambi na wasio wakamilifu. Baadhi ya watu hao wenye kumwogopa Mungu ni Noa, Abrahamu, Yobu, Rahabu, na Danieli. (Mwanzo 7:1; 15:6; Ayubu 1:1; Ezekieli 14:14; Yakobo 2:25) Kwa hiyo swali ni: Watu hao walionwa kuwa waadilifu na Mungu chini ya msingi gani?

14. Biblia inamaanisha nini inaposema kwamba mwanadamu ni “mwadilifu”?

14 Biblia inapotaja wanadamu kuwa “waadilifu,” haimaanishi kwamba hawana dhambi au ni wakamilifu. Badala yake, inamaanisha kwamba wanatimiza wajibu wao mbele za Mungu na wanadamu wenzao. Kwa mfano, Noa aliitwa “mtu wa haki [“mwadilifu,” NW]” na “mkamilifu katika vizazi vyake” kwa sababu alifanya “sawasawa na vyote alivyomwamuru Mungu, hivyo ndivyo alivyofanya.” (Mwanzo 6:9, 22; Malaki 3:18) Zekaria na Elizabeti, wazazi wa Yohana Mbatizaji, “walikuwa waadilifu mbele ya Mungu kwa sababu ya kutembea bila lawama kwa kupatana na amri zote na matakwa ya kisheria ya Yehova.” (Luka 1:6) Pia mtu fulani asiye Mwisraeli, ofisa wa jeshi la Italia aliyeitwa Kornelio, alitajwa kuwa “mwanamume mwadilifu na mwenye kumhofu Mungu.”—Matendo 10:22.

15. Uadilifu unahusiana sana na nini?

15 Zaidi ya hayo, uadilifu wa wanadamu unahusiana sana na mambo yaliyo moyoni mwa mtu—imani ya mtu na jinsi anavyothamini upendo na ahadi za Yehova—wala si kufanya tu mambo ambayo Mungu anataka. Maandiko yanasema kwamba Abrahamu ‘alimwamini Yehova, naye akamhesabia jambo hili kuwa haki [“uadilifu,” NW].’ (Mwanzo 15:6) Abrahamu aliamini kwamba Mungu yuko na pia aliamini ahadi yake kuhusu “mbegu.” (Mwanzo 3:15; 12:2; 15:5; 22:18, NW) Kwa sababu ya imani hiyo na pia matendo yaliyopatana nayo, Yehova angeweza kuwa na uhusiano na Abrahamu na kumbariki pamoja na waaminifu wengine hata ingawa hawakuwa wakamilifu.—Zaburi 36:10; Waroma 4:20-22.

16. Kuwa na imani katika dhabihu kumewatolea watu fursa gani?

16 Mwishowe, uadilifu wa wanadamu unategemea kuwa na imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Paulo aliandika hivi kuhusu Wakristo katika karne ya kwanza: “Ni kama zawadi ya bure kwamba wao wanatangazwa kuwa waadilifu kwa fadhili [ya Mungu] isiyostahiliwa kupitia kuachiliwa kwa njia ya fidia iliyolipwa na Kristo Yesu.” (Waroma 3:24) Paulo alikuwa akizungumza kuhusu wale waliochaguliwa kuwa warithi pamoja na Kristo katika Ufalme wa mbinguni. Lakini dhabihu ya fidia ya Yesu iliwapa mamilioni wengine fursa ya kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Mungu. Katika maono, mtume Yohana aliona “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, . . . wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo, wamevaa kanzu nyeupe.” Kanzu nyeupe zaonyesha kwamba wao ni safi na ni waadilifu mbele za Mungu kwa sababu “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.”—Ufunuo 7:9, 14.

Pendezwa na Uadilifu wa Yehova

17. Ni hatua gani zinazopaswa kuchukuliwa ili kufuatia uadilifu?

17 Hata ingawa Yehova alimtoa kwa upendo Mwana wake, Yesu Kristo, ili wanadamu wawe na msimamo wa uadilifu mbele zake, wao hawawezi kupata msimamo huo bila kufanya jambo lolote. Mtu anapaswa kudhihirisha imani katika fidia, kupatanisha maisha yake na mapenzi ya Mungu, kujiweka wakfu kwa Yehova, na kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji. Kisha, mtu anapaswa kuendelea kufuatia uadilifu na vilevile sifa nyingine za kiroho. Timotheo, Mkristo aliyebatizwa na aliyekuwa na tumaini la kwenda mbinguni, alitiwa moyo hivi na Paulo: “Fuatia uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, tabia-pole.” (1 Timotheo 6:11; 2 Timotheo 2:22) Pia Yesu alikazia uhitaji wa kuendelea kujitahidi aliposema: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake.” Huenda tukajitahidi sana kupata baraka za Ufalme wa Mungu, lakini je, tunajitahidi vivyo hivyo kufuatia njia za uadilifu za Yehova?—Mathayo 6:33.

18. (a) Kwa nini si rahisi kufuatia uadilifu? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na kielelezo cha Loti?

18 Kwa kweli, si rahisi kufuatia uadilifu. Hii ni kwa sababu sote ni wanadamu wasio wakamilifu nasi huwa na mwelekeo wa kutenda mambo yasiyo ya uadilifu. (Isaya 64:6) Zaidi ya hayo, tunazungukwa na watu wasiojali njia za uadilifu za Yehova. Hali zetu zafanana sana na za Loti, aliyeishi katika jiji la Sodoma lenye uovu mwingi. Mtume Petro alieleza ni kwa nini Yehova aliona inafaa kumkomboa Loti kutokana na uharibifu uliokuwa ukikaribia. Petro alisema: “Mtu huyo mwadilifu kwa yale ambayo aliona na kusikia alipokuwa akikaa miongoni mwao kila siku alikuwa akitesa-tesa nafsi yake yenye uadilifu kwa sababu ya vitendo vyao vya kuasi sheria.” (2 Petro 2:7, 8) Kwa hiyo, kila mmoja wetu apaswa kujiuliza: ‘Je, mimi hufurahia kimoyomoyo mambo yasiyo ya adili yanayotuzunguka? Je, mimi huona vitumbuizo au michezo yenye jeuri inayopendwa na wengi kuwa tu mambo yasiyopendeza? Au je, ninateseka nafsi kama Loti kwa sababu ya mambo hayo yasiyo ya adili?’

19. Tutapata thawabu gani kwa kupendezwa na uadilifu wa Mungu?

19 Tunaweza kupata ulinzi na usalama katika siku hizi zenye hatari na msukosuko kwa kupendezwa na uadilifu wa Yehova. Wakati swali hili lilipoulizwa: “BWANA, ni nani atakayekaa katika hema yako? Ni nani atakayefanya maskani yake katika kilima chako kitakatifu?” Mfalme Daudi alijibu: “Ni mtu aendaye kwa ukamilifu, na kutenda haki [“uadilifu,” NW].” (Zaburi 15:1, 2) Kwa kufuatia uadilifu wa Mungu na kupendezwa nao, tunaweza kudumisha uhusiano mzuri pamoja naye na kuzidi kupata kibali na baraka zake. Kwa hiyo, tunapata uradhi maishani, tunajistahi, na kuwa na amani ya akili. ‘Aandamaye uadilifu na fadhili, ataona uhai na uadilifu na heshima,’ linasema Neno la Mungu. (Mithali 21:21) Zaidi ya hayo, tukijitahidi kadiri tuwezavyo kufanya yanayofaa, tutakuwa na uhusiano wenye furaha na maisha bora—kiadili na kiroho. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Heri washikao hukumu, na kutenda haki [“uadilifu,” NW] sikuzote.”—Zaburi 106:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kwa maelezo kamili kuhusu mambo yaliyohusika katika Sheria ya Musa, ona makala yenye kichwa “Some Features of the Law Covenant,” kwenye ukurasa wa 214-220 katika kichapo Insight on the Scriptures buku la 2, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Uadilifu ni nini?

• Wokovu unahusianaje na uadilifu wa Mungu?

• Wanadamu huonwa kuwa waadilifu na Mungu chini ya msingi gani?

• Tunawezaje kupendezwa na uadilifu wa Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mfalme Daudi alipendezwa sana na sheria za Mungu

[Picha katika ukurasa wa 16]

Mungu aliwaona Noa, Abrahamu, Zekaria na Elizabeti, na Kornelio kuwa waadilifu. Je, unajua sababu?