Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unakionaje Kifo?

Unakionaje Kifo?

Unakionaje Kifo?

HATA tuwe wenye afya au tuwe matajiri kadiri gani, kifo hutuvunja moyo tunapoendelea na shughuli zetu za kila siku. Tunaweza kufa tunapovuka barabara au hata tukiwa tumelala kitandani. Misiba kama lile shambulio la magaidi la Septemba 11, 2001, huko New York City na Washington, D.C., hutukumbusha kwamba “adui wa mwisho” kifo, huua watu wa aina zote na wa umri mbalimbali. Mara nyingine adui huyo huua maelfu ya watu katika muda wa dakika chache tu.—1 Wakorintho 15:26.

Hata hivyo, inaonekana kwamba watu hutaka sana kujua habari za kifo. Ripoti za vifo vya watu wengi, hasa wanaokufa katika hali zenye kutisha, hufanya magazeti yanunuliwe kwa wingi na watu wengi kutazama televisheni. Watu hawachoki kupata ripoti za kifo, kiwe kinasababishwa na vita, misiba ya kiasili, uhalifu, au ugonjwa. Hisia ambazo watu huonyesha hasa mtu mashuhuri anapokufa hudhihirisha kwa njia yenye kushangaza kwamba wao hutaka sana kujua habari za kifo.

Ni kweli kwamba ripoti za kifo huathiri watu kwa njia mbalimbali. Watu hutaka sana kujua habari za kifo cha watu wengine. Hata hivyo, wanapokabiliwa na kifo chao wenyewe, wao hujikunyata kwa hofu. Wengi wetu hata hatupendi kufikiria kifo chetu wenyewe.

Je, Kifo Hukushangaza?

Hatupendi hata kidogo kuwazia kwamba tutakufa siku moja. Kwa nini? Kwa sababu Mungu ameweka ndani yetu tamaa kubwa ya kuishi milele. “Ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao,” linasema andiko la Mhubiri 3:11. Kwa hiyo, hali ya kutoweza kuepuka kifo imeendelea kutatanisha wanadamu. Ili kutatua tatizo hilo na kuridhisha tamaa ya kiasili ya kutaka kuendelea kuishi, wanadamu wamebuni mafundisho mbalimbali, kama vile fundisho la kutokufa kwa nafsi na la kuzaliwa upya katika umbo jingine.

Vyovyote vile, kifo ni tukio linalotisha na kuleta wasiwasi mwingi, na watu kwa ujumla huogopa kufa. Kwa hiyo, hatupaswi kushangaa kwamba watu kwa ujumla hungojea kifo kwa wasiwasi mwingi. Kwanza, kifo huonyesha kwamba haifai kabisa kutumia maisha yetu kufuatia mali au kutaka kuongoza wengine.

Wengine Hufia Hospitalini

Zamani, watu walikuwa na desturi ya kumwacha mtu mwenye ugonjwa au majeraha yasiyoweza kupona afe katika mazingira ya nyumbani aliyoyajua na kuyapenda. Desturi hiyo ilifuatwa mara nyingi nyakati za Biblia, na bado jamii fulani huifuata. (Mwanzo 49:1, 2, 33) Katika jamii hizo, familia hukutana pamoja, na watoto hushirikishwa katika mazungumzo. Jambo hilo hufanya kila mshiriki wa familia kuona kwamba haombolezi peke yake, naye hufarijika kujua kwamba kila mshiriki wa familia ana daraka kuhusiana na kifo hicho.

Desturi hiyo ni tofauti kabisa na yale ambayo hutukia katika jamii ambazo huona kifo kuwa tukio lenye kuhuzunisha sana, lisilopaswa kuzungumziwa au hata kuambiwa watoto, kwa kuwa inasemekana kwamba ‘hawawezi kustahimili.’ Siku hizi watu hufa katika mazingira mbalimbali na mara nyingi wao hufa wakiwa peke yao. Watu wengi wangependa kufa kwa amani wakiwa nyumbani, huku wakitunzwa kwa upendo na familia zao. Lakini wengi hufia hospitalini, mara nyingi wakiwa na maumivu, wametengwa na familia zao, na wamezungukwa na mashine nyingi zenye kuogopesha. Kwa upande mwingine, kuna mamilioni wengi wasiotambulika ambao hufa kutokana na mauaji ya kikabila, njaa, UKIMWI, vita vya wenyewe kwa wenyewe, au ufukara tu.

Jambo la Kufikiria

Biblia haitukatazi kufikiri kuhusu kifo. Hata andiko la Mhubiri 7:2 hutuambia hivi: “Heri kuiendea nyumba ya matanga, kuliko kuiendea nyumba ya karamu. Kwa maana huo ndio mwisho wa wanadamu wote.” Tunapotambua kwamba tunaweza kufa wakati wowote, huenda tukaacha shughuli zetu za kawaida na kutafakari juu ya ufupi wa maisha. Huenda jambo hilo likatusaidia kuishi maisha yetu kwa njia inayofaa zaidi badala ya kuishi ovyoovyo bila kusudi.

Unakionaje kifo? Je, umechunguza hisia zako, imani, matumaini, na wasiwasi ulio nao kuhusu kifo chako?

Mwanadamu hawezi kueleza wala kuelewa hali halisi ya uhai au ya kifo. Muumba wetu tu ndiye anayeweza kutoa habari yenye kutegemeka kuhusu mambo hayo. Kwake “iko chemchemi ya uzima,” na ‘njia za kutoka mautini zina yeye.’ (Zaburi 36:9; 68:20) Huenda ukashangaa kuona kwamba utapata faraja na kitia-moyo unapochunguza yale ambayo Neno la Mungu linasema juu ya imani ya wengi kuhusu kifo. Neno la Mungu litaonyesha kwamba kifo si mwisho wa mambo yote.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Kujua kwamba tunaweza kupatwa na kifo hutusaidia kuishi maisha yetu kwa njia inayofaa zaidi