Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Waliosafishwa kwa Ajili ya Kazi Zilizo Bora

Watu Waliosafishwa kwa Ajili ya Kazi Zilizo Bora

Watu Waliosafishwa kwa Ajili ya Kazi Zilizo Bora

“Acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na wa roho, tukikamilisha utakatifu katika hofu ya Mungu.”—2 WAKORINTHO 7:1.

1. Yehova anataka wale wanaomwabudu wafanye nini?

“NI NANI atakayepanda katika mlima wa BWANA? ni nani atakayesimama katika patakatifu pake?” Mfalme Daudi wa Israeli la kale aliuliza swali hilo lenye kuamsha fikira kuhusu ibada inayokubaliwa na Yehova. Kisha akatoa jibu: “Mtu aliye na mikono safi na moyo mweupe, asiyeiinua nafsi yake kwa ubatili, wala hakuapa kwa hila.” (Zaburi 24:3, 4) Ili kukubaliwa na Yehova aliye mfano halisi wa utakatifu, lazima mtu awe safi na mtakatifu. Awali, Yehova alikumbusha kutaniko la Israeli hivi: “Takaseni nafsi zenu basi; iweni watakatifu, kwa kuwa mimi ni Mtakatifu.”—Mambo ya Walawi 11:44, 45; 19:2.

2. Paulo na Yakobo walikaziaje umuhimu wa usafi katika ibada ya kweli?

2 Karne kadhaa baadaye, mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake katika jiji lililopotoka kiadili la Korintho: “Kwa kuwa tuna ahadi hizi, wapendwa, acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na wa roho, tukikamilisha utakatifu katika hofu ya Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Kwa mara nyingine tena, andiko hilo laonyesha kwamba ili kuwa na uhusiano na Mungu na kupokea thawabu ambazo ameahidi, lazima mtu awe safi na kujiepusha na uchafu na upotovu wa kimwili na kiroho. Vivyo hivyo, mwanafunzi Yakobo alisema hivi kuhusu ibada inayokubalika kwa Mungu: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyo na unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kutazama mayatima na wajane katika dhiki yao, na kufuliza kujitunza mwenyewe bila doa kutokana na ulimwengu.”—Yakobo 1:27.

3. Ili ibada yetu ikubaliwe na Mungu, twapaswa kuhangaikia sana jambo gani?

3 Kwa kuwa ni muhimu sana kuwa safi, mtakatifu, na bila unajisi katika ibada ya kweli, mtu yeyote anayetaka kupata kibali cha Mungu apaswa kuhangaikia sana kutimiza matakwa hayo. Hata hivyo, kwa sababu leo watu wana maoni na viwango vinavyotofautiana sana kuhusu usafi, tunahitaji kuelewa na kufuata viwango vya usafi vinavyokubalika na Yehova. Tunahitaji kujua Mungu anataka waabudu wake wafanye nini kuhusiana na usafi na mambo ambayo amefanya ili kuwasaidia wabaki wakiwa safi na kukubalika naye.—Zaburi 119:9; Danieli 12:10.

Tumesafishwa kwa Ajili ya Ibada ya Kweli

4. Eleza maoni ya Biblia kuhusu usafi.

4 Kwa watu wengi, usafi unamaanisha kuwa bila uchafu. Hata hivyo, katika Biblia, usafi unafafanuliwa na maneno kadhaa ya Kiebrania na Kigiriki yanayozungumzia usafi wa kimwili na pia usafi wa kiadili na wa kiroho. Kwa hiyo, ensaiklopedia moja ya Biblia inasema: “Maneno ‘safi’ na ‘-sio safi’ hayahusiani na masuala ya usafi wa kimwili tu bali yanahusiana hasa na imani ya kidini. Kupatana na ufafanuzi huo kanuni ya ‘usafi’ inahusu karibu kila jambo maishani.”

5. Sheria ya Musa ilitia ndani mambo mengi kadiri gani katika maisha ya Waisraeli?

5 Kwa kweli, Sheria ya Musa ilitia ndani sheria na kanuni zilizohusu kila sehemu ya maisha ya Waisraeli, ikionyesha kihususa mambo yaliyokuwa safi na ya kukubalika na yale yasiyokubalika. Kwa mfano, katika Mambo ya Walawi sura ya 11 hadi 15, tunapata maagizo kamili kuhusu mambo yaliyo safi na yasiyo safi. Wanyama fulani hawakuwa safi, nao Waisraeli hawakupaswa kuwala. Baada ya kujifungua mwanamke angekuwa najisi kwa kipindi fulani hususa. Magonjwa fulani ya ngozi, hasa ukoma, na mtiririko wa umajimaji kutoka katika viungo vya uzazi vya wanaume na wanawake pia ungemfanya mtu kuwa najisi. Pia Sheria ilionyesha waziwazi jambo lililopaswa kufanywa mtu alipotiwa unajisi. Kwa mfano, twasoma hivi katika andiko la Hesabu 5:2: “Waamrishe wana wa Israeli kwamba wamtoe kila mwenye ukoma maragoni, na kila mtu aliye na kisonono [“anayetiririkwa na umajimaji,” NW], na kila aliye najisi kwa ajili ya wafu.”

6. Sheria za usafi zilitolewa kwa kusudi gani?

6 Bila shaka, sheria hizo pamoja na sheria nyingine kutoka kwa Yehova zilitia ndani kanuni zinazohusu tiba na maisha. Kanuni hizo ziliwanufaisha wale waliozifuata muda mrefu kabla ya wanasayansi kugundua manufaa yake. Hata hivyo, kanuni hizo hazikutolewa tu kuwa sheria za kitiba, au kutoa mwongozo katika mambo ya kitiba tu. Zilikuwa sehemu ya ibada ya kweli. Kwa kuwa sheria hizo zilihusu maisha ya watu ya kila siku—kula, kuzaa watoto, uhusiano wa ndoa, na kadhalika—zilikazia kwamba Mungu wao, Yehova alikuwa na haki ya kuwaamulia mambo yaliyofaa na yasiyofaa katika sehemu zote za maisha yao, ambayo walikuwa wameyaweka wakfu kwa Yehova.—Kumbukumbu la Torati 7:6; Zaburi 135:4.

7. Taifa la Israeli lingepata baraka gani kwa kushika Sheria?

7 Pia agano la Sheria liliwalinda Waisraeli na mazoea yenye kutia unajisi ya mataifa yaliyowazunguka. Kwa kutii Sheria hiyo kwa uaminifu, kutia ndani matakwa yote ya kubaki wakiwa safi machoni pa Yehova, Waisraeli wangeweza kumtumikia Mungu kwa njia inayokubalika na kupata kibali chake. Kwa habari hiyo, Yehova aliliambia hivi taifa hilo: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, nanyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.”—Kutoka 19:5, 6; Kumbukumbu la Torati 26:19.

8. Kwa nini Wakristo leo wapaswa kuzingatia mambo yanayosemwa katika Sheria kuhusu usafi?

8 Kwa kuwa Yehova alitia ndani mambo hayo katika Sheria ili kuwafundisha Waisraeli jinsi ya kuwa safi, watakatifu, na watu wenye kukubalika kwake, je, haingefaa Wakristo leo kufikiria kwa makini iwapo wanatimiza matakwa hayo? Hata ingawa Wakristo hawako chini ya Sheria, wanapaswa kukumbuka kwamba mambo yote yaliyo katika Sheria “ni kivuli cha mambo yajayo, bali uhalisi ni wa Kristo,” kama Paulo alivyosema. (Wakolosai 2:17; Waebrania 10:1) Ikiwa Yehova Mungu, ambaye anasema “mimi sibadiliki,” aliona usafi na kutotiwa unajisi kuwa mambo muhimu sana katika ibada ya kweli wakati huo, je, iwapo tunataka kibali na baraka zake, haitupasi kuchukua kwa uzito usafi wa kimwili, kiadili, na kiroho?—Malaki 3:6, BHN; Waroma 15:4; 1 Wakorintho 10:11, 31.

Usafi wa Kimwili Hutupendekeza

9, 10. (a) Kwa nini usafi wa kimwili ni muhimu kwa Mkristo? (b) Ni mambo gani ambayo mara nyingi husemwa kuhusu makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova?

9 Je, usafi wa kimwili bado ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli? Ingawa usafi wa kimwili pekee haumfanyi mtu kuwa mwabudu wa kweli wa Mungu, bila shaka inafaa sana mwabudu wa kweli awe safi kimwili kulingana na hali zake. Wakati huu tunamoishi watu wengi hawajali kuoga, kufua mavazi yao, au kudumisha mazingira safi. Kwa hiyo, wale ambao hudumisha usafi hutambuliwa kwa urahisi na watu walio karibu nao. Kama Paulo alivyowaambia Wakristo huko Korintho, kudumisha usafi kwaweza kuwa na matokeo mazuri: “Katika njia yoyote sisi hatutoi sababu yoyote ya kukwaza, ili huduma yetu isitafutiwe kosa; bali katika kila njia twajipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu.”—2 Wakorintho 6:3, 4.

10 Mara nyingi Mashahidi wa Yehova wamesifiwa na maofisa wa umma kwa sababu ya kuwa safi, wenye utaratibu, na wanaojiendesha kwa heshima, hasa katika makusanyiko yao makubwa. Kwa mfano, gazeti La Stampa lilisema hivi kuhusu kusanyiko lililofanywa katika mkoa wa Savona, Italia: “Jambo ambalo mtu anatambua mara moja kuhusu watu wanaotumia uwanja huu ni usafi na utaratibu wao.” Baada ya kusanyiko la Mashahidi lililofanywa katika uwanja wa São Paulo, Brazili, ofisa mmoja wa uwanja huo alimwambia hivi msimamizi wa watu waliofanya kazi ya usafi: “Kuanzia sasa na kuendelea tunataka uwanja usafishwe kama vile Mashahidi wa Yehova walivyousafisha.” Ofisa mwingine katika uwanja uo huo alisema: “Mashahidi wa Yehova wanapotaka kukodisha uwanja huu, sisi huhangaikia tu tarehe ambazo watauhitaji. Hatuhangaikii jambo jingine lolote.”

11, 12. (a) Ni kanuni gani ya Biblia tunayopaswa kukumbuka kuhusiana na usafi wa kibinafsi? (b) Tunaweza kujiuliza maswali gani kuhusu mazoea na maisha yetu?

11 Ikiwa usafi na utaratibu katika mahali petu pa ibada unaweza kuleta sifa kwa Mungu tunayeabudu, bila shaka ni jambo muhimu kudhihirisha sifa hizo katika maisha yetu ya kibinafsi. Hata hivyo, huenda tukahisi kwamba tukiwa nyumbani mwetu, tuna haki ya kufanya lolote tupendalo na kutojali usafi. Bila shaka tuna uhuru wa kuchagua mavazi na mapambo yanayotupendeza! Hata hivyo, kwa kiwango kikubwa uhuru huo una mipaka. Kumbuka kwamba Paulo aliwaonya hivi Wakristo wenzake alipozungumza kuhusu chakula ambacho mtu angeamua kula: “Fulizeni kuangalia kwamba mamlaka yenu hii isipate kwa njia fulani kuwa kipingamizi chenye kukwaza kwa wale walio dhaifu.” Kisha akataja kanuni hii muhimu: “Mambo yote yaruhusika kisheria; lakini si mambo yote yenye faida. Mambo yote yaruhusika kisheria; lakini si mambo yote yajengayo.” (1 Wakorintho 8:9; 10:23) Shauri la Paulo linatuhusuje katika suala la usafi?

12 Ni jambo linalopatana na akili kutazamia mhudumu wa Mungu awe safi na mwenye utaratibu maishani. Kwa hiyo, tunapaswa kuhakikisha kwamba usafi wa makao na mazingira yetu unapatana na dai letu kwamba sisi ni wahudumu wa Neno la Mungu. Makao yetu yanatoa ushuhuda gani kutuhusu sisi na imani yetu? Je, yanaonyesha kwamba tunatamani kwelikweli kuishi katika dunia safi yenye utaratibu na uadilifu, ambayo tunawapendekezea wengine kwa bidii? (2 Petro 3:13) Hali kadhalika, sura yetu—iwe ni wakati wa mapumziko au tunapokuwa katika huduma—inaweza ama kufanya watu wavutiwe ama wasivutiwe na ujumbe tunaohubiri. Kwa mfano, ona maelezo ya ripota wa gazeti fulani nchini Mexico: “Kwa kweli, kuna vijana wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, na jambo lenye kutokeza kuwahusu ni mitindo yao ya nywele, usafi, na mavazi mazuri.” Tunafurahi kama nini kuwa na vijana kama hao!

13. Tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba tunadumisha usafi na utaratibu kuhusiana na kila jambo maishani mwetu?

13 Bila shaka si rahisi kudumisha miili yetu, vitu vyetu, na makao yetu yakiwa safi na yenye utaratibu. Hatuhitaji kuwa na vifaa ghali au vya hali ya juu, bali tunahitaji tu kupanga vitu vizuri na kujitahidi kufanya hivyo daima. Lazima tutenge wakati wa kuoga, kufua nguo, kusafisha nyumba, gari, na kadhalika. Hata ingawa tuna mengi ya kufanya kuhusiana na huduma, kuhudhuria mikutano, funzo la kibinafsi, na madaraka mengine maishani, twapaswa kudumisha usafi ili tuendelee kukubalika machoni pa Mungu na wanadamu. Kanuni inayojulikana sana kwamba “kwa kila jambo kuna majira yake” yahusu pia sehemu hii ya maisha yetu.—Mhubiri 3:1.

Moyo Ambao Haujatiwa Unajisi

14. Kwa nini tunaweza kusema kwamba usafi wa kiadili na wa kiroho ni muhimu zaidi ya usafi wa kimwili?

14 Kama vile ilivyo muhimu kuhangaikia usafi wa kimwili, ni muhimu pia kuhangaikia usafi wa kiadili na wa kiroho. Twafikia mkataa huo kwa kukumbuka kwamba taifa la Israeli lilikataliwa na Yehova, si kwa sababu halikuwa safi kimwili, bali kwa sababu lilikuwa chafu kiadili na kiroho. Kupitia nabii Isaya, Yehova aliwaambia kwamba kwa sababu walikuwa “taifa lenye dhambi, watu wanaochukua mzigo wa uovu,” dhabihu zao, kuadhimisha mwezi mpya na sabato, naam, hata sala zao zilikuwa mzigo kwa Yehova. Walipaswa kufanya nini ili kupata kibali cha Mungu tena? Yehova alisema: “Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya.”—Isaya 1:4, 11-16.

15, 16. Yesu alisema ni nini ambacho humtia mtu unajisi, nasi tunaweza kunufaikaje na maneno ya Yesu?

15 Ili kuelewa zaidi kwa nini usafi wa kiadili na wa kiroho ni muhimu, fikiria mambo aliyosema Yesu wakati Mafarisayo na waandishi walipodai kwamba wanafunzi wa Yesu hawakuwa safi kwa sababu hawakunawa mikono yao kabla ya kula. Yesu aliwasahihisha kwa kusema: “Si kile kiingiacho ndani ya kinywa chake hutia mtu unajisi; bali ni kile kitokacho katika kinywa chake ndicho hutia mtu unajisi.” Kisha Yesu akatoa maelezo haya: “Mambo yanayotoka katika kinywa hutoka moyoni, na mambo hayo hutia mtu unajisi. Kwa kielelezo, kutoka moyoni huja mawazowazo maovu, mauaji-kimakusudi, uzinzi, uasherati, wizi, shuhuda zisizo za kweli, makufuru. Hayo ndiyo mambo yanayotia mtu unajisi; lakini kula mlo bila kuosha mikono hakutii mtu unajisi.”—Mathayo 15:11, 18-20.

16 Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno ya Yesu? Yesu alikuwa akisema kwamba matendo maovu, yasiyo ya adili, na yasiyo safi hutokana na maelekeo ya moyoni yaliyo maovu, yasiyo ya adili, na yasiyo safi. Kama alivyosema mwanafunzi Yakobo, “kila mmoja hujaribiwa kwa kuvutwa na kutongozwa na tamaa yake mwenyewe.” (Yakobo 1:14, 15) Kwa hiyo, iwapo hatutaki kutenda dhambi nzito alizotaja Yesu, lazima tuondoe kabisa maelekeo hayo katika mioyo yetu. Hiyo yamaanisha kwamba lazima tuwe waangalifu kuhusu habari tunazosoma, picha tunazotazama, na muziki tunaosikiliza. Leo, mashirika ya vitumbuizo na utangazaji yanatumia uhuru wa kusema na uhuru wa wasanii kuwa udhuru wa kupuuza viwango vya wema, na hivyo kutokeza muziki na sinema zinazokusudiwa kuamsha tamaa za mwili wenye dhambi. Twapaswa kuazimia kukataa kabisa mawazo hayo yasisitawi mioyoni mwetu. Jambo lililo muhimu ni kwamba ili tumpendeze Mungu na kukubalika kwake, lazima tuwe macho daima kudumisha moyo usio na unajisi.—Mithali 4:23.

Waliosafishwa kwa Kazi Zilizo Bora

17. Kwa nini Yehova amewasafisha watu wake?

17 Bila shaka, ni baraka na pia ni ulinzi kuwa na msimamo safi mbele za Yehova kupitia msaada anaotupatia. (2 Wakorintho 6:14-18) Hata hivyo, pia tunafahamu kwamba Yehova amewasafisha watu wake akiwa na kusudi hususa. Paulo alimwambia Tito kwamba Kristo Yesu ‘alijitoa mwenyewe kwa ajili yetu ili apate kutukomboa sisi kutoka kwenye kila namna ya uasi-sheria na kujisafishia mwenyewe watu walio wake mwenyewe pekee, wenye bidii kwa kazi zilizo bora.’ (Tito 2:14) Tukiwa watu waliosafishwa, tunapaswa kuwa wenye bidii katika kazi zipi?

18. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna bidii kwa kazi zilizo bora?

18 Tunapaswa kujitahidi sana kutangaza hadharani habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Kwa kufanya hivyo, tunawatolea watu kila mahali tumaini la kuishi milele katika dunia ambayo haitakuwa na uchafuzi wa aina yoyote. (2 Petro 3:13) Kazi zetu bora zatia ndani kudhihirisha matunda ya roho ya Mungu katika maisha yetu ya kila siku, na hivyo kumtukuza Baba yetu wa kimbingu. (Wagalatia 5:22, 23; 1 Petro 2:12) Pia tunawakumbuka wale ambao hawaijui kweli na ambao huenda wakapatwa na misiba ya asili au misiba mingine inayosababishwa na wanadamu. Tunakumbuka shauri hili la Paulo: “Basi, kwa kweli maadamu tuna wakati wenye kufaa kwa ajili ya hilo, acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Tunapotoa utumishi huo wote kwa moyo safi na nia safi, tunampendeza Mungu.—1 Timotheo 1:5.

19. Tutapata baraka gani kwa kuendelea kudumisha kiwango cha juu cha usafi wa kimwili, kiadili, na kiroho?

19 Tukiwa watumishi wa Mungu Aliye Juu Zaidi, twatii maneno haya ya Paulo: “Nawasihi sana nyinyi kwa huruma za Mungu, akina ndugu, mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri kuzuri.” (Waroma 12:1) Na tuendelee kuthamini pendeleo la kusafishwa na Yehova na kufanya yote tuwezayo kudumisha kiwango cha juu cha usafi wa kimwili, kiadili, na kiroho. Tukifanya hivyo tutakuwa wenye kujistahi na wenye uradhi na pia tumaini la kuona “mambo ya zamani”—mfumo wa sasa ulio mwovu na uliopotoka—ukipitilia mbali wakati Mungu ‘afanyapo vitu vyote kuwa vipya.’—Ufunuo 21:4, 5.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini Waisraeli walipewa sheria nyingi kuhusu usafi

• Usafi wa kimwili hufanyaje ujumbe tunaohubiri uvutie hata zaidi?

• Kwa nini usafi wa kiadili na wa kiroho ni muhimu zaidi ya usafi wa kimwili?

• Tunaweza kuonyeshaje kwamba sisi ni watu “wenye bidii kwa kazi zilizo bora”?

[Mawali ya Funzo]

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 21]

Usafi wa kimwili hufanya ujumbe tunaohubiri uvutie hata zaidi

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 22]

Yesu alionya kwamba mawazo maovu huongoza kwenye matendo maovu

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 23]

Wakiwa watu waliosafishwa, Mashahidi wa Yehova ni wenye bidii kwa kazi zilizo bora