Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wote Waliangamia

Wote Waliangamia

Wote Waliangamia

“Vilindi vimewafunikiza, walizama vilindini kama jiwe.”

MANENO hayo yanatajwa katika wimbo ulioimbwa na Musa na Waisraeli ili kusherehekea kuokolewa kwao kupitia Bahari Nyekundu na kuangamizwa kwa maadui wao Wamisri—Farao na majeshi yake—waliokuwa wakiwafuata.—Kutoka 15:4, 5.

Wale walioona tukio hilo la kustaajabisha walijifunza jambo fulani dhahiri. Hakuna anayeweza kupinga mamlaka ya Yehova na aishi. Hata hivyo, miezi kadhaa baadaye Waisraeli mashuhuri—Kora, Dathani, Abiramu, na watu wengine 250 waliowaunga mkono—walipinga waziwazi mamlaka ya Musa na Aroni waliyopewa na Mungu.—Hesabu 16:1-3.

Yehova alimwagiza Musa awaonye Waisraeli wajitenge na waasi hao. Dathani na Abiramu, pamoja na watu wa jamaa zao waliowaunga mkono, walikataa kwa ukaidi kubadili msimamo wao wa uasi. Ndipo Musa akasema kwamba Yehova angetumia njia fulani kuwadhihirishia Waisraeli kwamba wanaume hao walikuwa “wamemdharau BWANA.” Mara, Yehova akapasua nchi chini ya miguu yao. “Basi wao, na wote waliokuwa nao, wakashukia shimoni wali hai; nayo nchi ikawafunika.” Namna gani Kora na waasi wale wengine? ‘Moto ulitoka kwa BWANA, ukawateketeza hao watu mia mbili hamsini waliofukiza uvumba.’—Hesabu 16:23-35; 26:10.

Farao na majeshi yake, na pia watu hao walioasi nyikani, waliangamia kwa sababu hawakutambua mamlaka ya Yehova na jinsi anavyojali watu wake. Kwa hiyo, ni jambo la haraka kwa wale wanaotaka kulindwa na Yehova katika siku hizi hatari wajifunze juu yake, na kumtii akiwa Mungu “Aliye Juu Zaidi” na “Mweza-Yote.” Wakifanya hivyo, maneno haya ya Yehova yanaweza kuwapa uhakikisho wenye nguvu: “Ijapo watu elfu waanguka ubavuni pako. Naam, kumi elfu mkono wako wa kuume! Hata hivyo hautakukaribia wewe. Ila kwa macho yako utatazama, na kuyaona malipo ya wasio haki. Kwa kuwa Wewe BWANA ndiwe kimbilio langu; umemfanya Aliye juu kuwa makao yako.”—Zaburi 91:1, 7-9, NW.