Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fuata Kielelezo cha Wafalme

Fuata Kielelezo cha Wafalme

Fuata Kielelezo cha Wafalme

“Ajiandikie nakala ya torati hii katika chuo, . . . na awe nayo, asome humo siku zote atakazoishi.” —KUMBUKUMBU LA TORATI 17:18, 19.

1. Huenda Mkristo akataka kuwa kama nani?

HAIELEKEI kwamba ungejilinganisha na mfalme au malkia. Ni Mkristo gani mwaminifu aliye mwanafunzi wa Biblia ambaye angewazia akitenda kwa mamlaka ya kifalme kama vile Wafalme waaminifu Daudi, Yosia, Hezekia, au Yehoshafati? Hata hivyo, unaweza na unapaswa kuwa kama wao katika njia moja ya pekee. Njia gani hiyo? Na kwa nini utake kuwa kama wao?

2, 3. Yehova alijua nini kimbele kuhusiana na mfalme wa kibinadamu, na mfalme huyo alipaswa kufanya nini?

2 Katika siku za Musa, muda mrefu kabla Mungu hajawaruhusu Waisraeli wawe na mfalme wa kibinadamu, Yeye alijua kimbele kwamba kuna wakati watu Wake wangetamani kuwa na mfalme. Kwa hiyo alimwongoza Musa kwa roho yake ili atie ndani maagizo fulani yafaayo alipoandika Sheria ya agano. Hayo yalikuwa maagizo kwa ajili ya mfalme.

3 Mungu alisema: “Utakapokwisha kuingia katika nchi akupayo BWANA, Mungu wako, . . . nawe utakaposema, Nitaweka mfalme juu yangu mfano wa mataifa yote yaliyo kando-kando yangu; usiache kumweka yule atakayechaguliwa na BWANA, Mungu wako. . . . Tena na iwe, zamani aketipo juu ya kiti cha ufalme wake, ajiandikie nakala ya torati hii katika chuo, . . . na awe nayo, asome humo siku zote atakazoishi; ili apate kujifunza kumcha BWANA, Mungu wake, ayashike maneno yote ya torati hii na amri hizi, kwa kuyafanya.”—Kumbukumbu la Torati 17:14-19.

4. Maagizo ya Mungu kwa wafalme yalihusisha nini?

4 Naam, mfalme ambaye Yehova angechagua kwa ajili ya waabudu wake alipaswa kuandika nakala yake mwenyewe ya maandishi ambayo sasa yanapatikana katika Biblia yako. Mfalme huyo alipaswa kusoma nakala hiyo kila siku, kwa kurudia-rudia. Hilo si jambo alilofanya ili kuchemsha bongo tu bali alijifunza akiwa na kusudi lenye manufaa. Ili mfalme akubaliwe na Yehova alihitaji kuendelea na funzo hilo ili kusitawisha na kudumisha maoni yanayofaa. Pia alihitaji kujifunza maandishi hayo yaliyoandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu ili awe mfalme mwenye busara na ufahamu.—2 Wafalme 22:8-13; Mithali 1:1-4.

Jifunze Kama Mfalme

5. Mfalme Daudi angeweza kunakili na kusoma vitabu gani vya Biblia, naye alihisije kuhusu jambo hilo?

5 Unafikiri Daudi alipaswa kufanya nini alipokuwa mfalme wa Israeli? Alipaswa kunakili vitabu vya kwanza vitano vya Biblia (Mwanzo, Kutoka, Mambo ya Walawi, Hesabu, Kumbukumbu la Torati). Wazia jinsi Daudi alivyohisi akilini na moyoni alipotumia macho na mikono yake mwenyewe kunakili Sheria. Yaelekea pia Musa aliandika kitabu cha Ayubu na vilevile Zaburi ya 90 na 91. Je, Daudi alinakili vitabu hivyo pia? Labda alifanya hivyo. Yaelekea pia angeweza kupata vitabu vya Yoshua, Waamuzi, na Ruthu. Kwa hiyo unaweza kuona kwamba Mfalme Daudi angeweza kusoma na kutafakari sehemu kubwa ya Biblia. Yale Daudi aliyosema kuhusu Sheria ya Mungu katika andiko la Zaburi 19:7-11 yanaonyesha kwamba inawezekana alifanya hivyo.

6. Ni nini kinachotuhakikishia kwamba Yesu alipendezwa na Maandiko kama babu yake Daudi?

6 Daudi Mkuu—Yesu, Mwana wa Daudi—alifuata kielelezo hicho. Yesu alikuwa na desturi ya kwenda kwenye hekalu la kwao kila juma. Huko alisikia Maandiko yakisomwa na kuelezwa. Zaidi ya hayo, kuna pindi ambapo Yesu mwenyewe alisoma Neno la Mungu kwa sauti kubwa hadharani na kueleza jinsi lilivyotumika. (Luka 4:16-21) Ni rahisi kuona kwamba Yesu aliyafahamu Maandiko. Soma tu masimulizi ya Injili, na utaona kwamba mara nyingi Yesu alisema “imeandikwa” au kutaja mistari fulani hususa ya Maandiko. Kwa mfano, katika Mahubiri yake ya Mlimani kwenye kitabu cha Mathayo, Yesu alinukuu Maandiko ya Kiebrania mara 21.—Mathayo 4:4-10; 7:29; 11:10; 21:13; 26:24, 31; Yohana 6:31, 45; 8:17.

7. Yesu alitofautianaje na viongozi wa kidini?

7 Yesu alifuata ushauri ulio katika andiko la Zaburi 1:1-3: “Heri mtu yule asiyekwenda katika shauri la wasio haki. . . . Bali sheria ya BWANA ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku. . . . Kila alitendalo litafanikiwa.” Yesu alikuwa tofauti kama nini na viongozi wa kidini wa siku zake, ‘waliojiketisha wenyewe katika kiti cha Musa’ lakini wakapuuza “sheria ya BWANA”! —Mathayo 23:2-4.

8. Kwa nini viongozi wa kidini Wayahudi hawakunufaika kutokana na kusoma na kujifunza Biblia?

8 Hata hivyo, huenda wengine wakashangazwa na mistari fulani ya Biblia inayoweza kueleweka kimakosa kwamba Yesu aliwavunja moyo wasikilizaji wake wasijifunze Biblia. Kwenye andiko la Yohana 5:39, 40, tunasoma maneno ambayo Yesu aliwaambia watu fulani katika siku zake: “Nyinyi mnayachunguza Maandiko, kwa sababu mwafikiri kwamba kwa njia yayo mtakuwa na uhai udumuo milele; na hayo yenyewe ndiyo yatoayo ushahidi juu yangu. Na bado hamtaki kuja kwangu ili mpate kuwa na uhai.” Kwa kusema hivyo, Yesu hakuwavunja moyo Wayahudi waliomsikiliza wasijifunze Maandiko. Badala yake, alikuwa akionyesha kwamba hawakuwa wanyofu, bali walifuata Maandiko yaliyowapendeza na kupuuza mengine. Walijua kwamba Maandiko yangewawezesha kupata uhai udumuo milele, lakini Maandiko hayohayo waliyochunguza yangepaswa kuwaelekeza kwa Mesiya, Yesu. Hata hivyo, walikataa kumkubali. Hivyo, kwa sababu hawakuwa wanyofu wala wenye kufundishika, hawakunufaika na funzo lao la Biblia.—Kumbukumbu la Torati 18:15; Luka 11:52; Yohana 7:47, 48.

9. Mitume na manabii wa kale waliweka mfano gani bora?

9 Wanafunzi wa Yesu, kutia ndani mitume, walikuwa tofauti kabisa na viongozi hao. Walijifunza ‘maandishi matakatifu, yawezayo kufanya mtu awe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu.’ (2 Timotheo 3:15) Walikuwa kama manabii wa kale ‘walioulizia habari kwa bidii yenye kuendelea na kutafuta kwa uangalifu sana.’ Manabii hao hawakuona kuyachunguza Maandiko kuwa jambo la kufanywa kwa bidii kwa miezi michache au mwaka mmoja tu. Mtume Petro anasema kwamba “walifuliza kupeleleza-peleleza,” hasa kuhusu Kristo na utukufu uliohusika katika daraka lake la kuokoa wanadamu. Katika barua yake ya kwanza, Petro alinukuu vitabu kumi vya Biblia mara 34.—1 Petro 1:10, 11.

10. Kwa nini sisi sote tunapaswa kupendezwa na funzo la Biblia?

10 Basi, ni wazi kwamba wafalme wa kale wa Israeli walipaswa kujifunza Neno la Mungu kwa makini. Yesu alifuata kielelezo hicho. Nao wale watakaokuwa wafalme pamoja na Kristo mbinguni wanapaswa kujifunza Neno la Mungu pia. (Luka 22:28-30; Waroma 8:17; 2 Timotheo 2:12; Ufunuo 5:10; 20:6) Leo, kielelezo hicho cha wafalme ni muhimu pia kwa wote wanaotazamia kupata baraka duniani chini ya utawala wa Ufalme.—Mathayo 25:34, 46.

Daraka kwa Wafalme na Kwako Pia

11. (a) Ni hatari gani inayowakabili Wakristo kuhusiana na funzo la kibinafsi? (b) Tunapaswa kujiuliza maswali gani?

11 Tunaweza kukazia kwa unyofu kwamba kila Mkristo wa kweli anapaswa kuichunguza Biblia. Mtu hapaswi kufanya hivyo tu wakati anapojifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Kila mmoja wetu anapaswa kuazimia asiwe kama watu fulani katika siku ya Paulo walioanza kupuuza funzo la kibinafsi baada ya muda mfupi. Walijifunza “mambo ya msingi ya matamko matakatifu ya Mungu,” kama vile “fundisho la msingi juu ya Kristo.” Watu hao walishindwa “kusonga mbele kwenye ukomavu” kwa kuwa waliacha kujifunza. (Waebrania 5:12–6:3) Hivyo tunaweza kujiuliza hivi: ‘Ninahisije kuhusu funzo la kibinafsi la Neno la Mungu, bila kujali muda ambao nimekuwa mshiriki wa kutaniko la Kikristo? Paulo alisali kwamba Wakristo wa siku zake waendelee “kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.” Je, ninaonyesha kwamba nina tamaa kama hiyo?’—Wakolosai 1:9, 10.

12. Kwa nini ni muhimu kuendelea kulipenda Neno la Mungu?

12 Ili uwe na mazoea mazuri ya kujifunza ni muhimu kusitawisha upendo kwa Neno la Mungu. Andiko la Zaburi 119:14-16 linaonyesha kwamba ili tulipende Neno la Mungu tunahitaji kulitafakari kwa ukawaida tukiwa na kusudi fulani. Naam, unapaswa kufanya hivyo hata uwe umekuwa Mkristo kwa muda mrefu kadiri gani. Kwa kukazia jambo hilo, kumbuka mfano wa Timotheo. Ingawa Mkristo huyo aliyekuwa mzee wa kutaniko alikuwa tayari anatumikia akiwa “askari-jeshi mwema wa Kristo Yesu,” Paulo alimtia moyo afanye yote awezayo ‘kulitumia sawasawa neno la ile kweli.’ (2 Timotheo 2:3, 15; 1 Timotheo 4:15) Ni wazi kwamba kufanya ‘yote uwezayo’ kunahusisha kuwa na mazoea ya kujifunza Biblia kwa ukawaida.

13. (a) Unawezaje kupata muda zaidi kwa ajili ya funzo la Biblia? (b) Unaweza kufanya marekebisho gani ili kupata wakati wa kujifunza?

13 Kutenga wakati wa kujifunza Biblia kwa ukawaida ni njia moja ya kusitawisha mazoea mazuri ya kujifunza. Umefanikiwa kadiri gani katika jambo hilo? Hata jibu lako la unyofu liwe nini, je, unafikiri kwamba unaweza kunufaika kwa kutumia muda mwingi zaidi katika funzo la kibinafsi? Huenda ukajiuliza, ‘Ninawezaje kutenga wakati kwa ajili ya funzo la kibinafsi?’ Wengine wameongeza muda wanaotumia kujifunza Biblia kwa kuamka mapema kidogo asubuhi. Huenda wakasoma Biblia kwa dakika 15 au kufanya utafiti fulani katika funzo lao la kibinafsi. Unaweza pia kufanya mabadiliko fulani katika ratiba yako ya kila juma. Kwa mfano, ikiwa una zoea la kusoma gazeti karibu kila siku au kutazama habari kwenye televisheni jioni, je, unaweza kuacha kufanya hivyo siku moja tu kwa juma? Unaweza kutumia muda huo kujifunza Biblia zaidi. Kama kila juma ungetenga dakika 30 hivi unazotumia kutazama habari kwenye televisheni kila siku, kisha uzitumie katika funzo la kibinafsi, ungeongeza muda wako wa kujifunza kwa saa 25 kwa mwaka. Hebu wazia jinsi ambavyo ungenufaika kwa kuwa na muda wa saa 25 zaidi wa kusoma na kujifunza Biblia! Kuna dokezo lingine: Katika juma lijalo, jaribu kuchanganua shughuli zako za kila siku. Ona kama kuna jambo fulani unaloweza kuacha au kukatiza ili uwe na muda zaidi wa kusoma au kujifunza Biblia.—Waefeso 5:15, 16.

14, 15. (a) Kwa nini ni muhimu kuweka miradi kuhusiana na funzo la kibinafsi? (b) Ni miradi gani unayoweza kuweka kuhusiana na usomaji wa Biblia?

14 Ni nini kitakachofanya funzo lako liwe rahisi na lenye kupendeza? Ni kuweka miradi. Unaweza kuweka miradi gani ya kujifunza unayoweza kuifikia? Wengi huona inafaa kuweka mradi wa kusoma Biblia nzima kwanza. Labda mpaka sasa umenufaika kusoma sehemu fulani za Biblia mara kwa mara. Je, unaweza kuazimia kusoma Biblia nzima? Ili uweze kuisoma Biblia nzima, huenda ukaweka mradi wa kusoma kwanza vitabu vinne vya Injili, kisha usome vitabu vinavyobaki vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Baada ya kuona jinsi kusoma Biblia kunavyoridhisha na kunufaisha, huenda ukaweka mradi mwingine wa kusoma kwa kufuatanisha vitabu vya Musa na vya historia, kutia ndani kitabu cha Esta. Baada ya kusoma vitabu hivyo, utaona kwamba inawezekana kumalizia vitabu vilivyobaki vya Biblia. Mwanamke mmoja, aliyekuwa Mkristo alipokuwa na umri wa miaka 65 hivi, aliandika ndani ya jalada la Biblia yake tarehe aliyoanza kusoma Biblia na tarehe aliyomaliza. Sasa ameisoma Biblia mara tano! (Kumbukumbu la Torati 32:45-47) Yeye alisoma Biblia yenyewe badala ya kuisoma kwenye kompyuta au nakala zilizochapwa.

15 Wengi ambao tayari wameisoma Biblia nzima huchukua hatua nyinginezo ili kufanya funzo lao lenye kuendelea linufaishe na kuthawabisha zaidi. Njia moja ya kufanya hivyo ni kusoma kichapo kingine kinachofafanua kitabu cha Biblia watakachosoma. Vitabu Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa na Insight on the Scriptures, vina habari nyingi kuhusu historia, mtindo wa uandishi, na manufaa ambazo mtu anaweza kupata kwa kusoma kila kitabu cha Biblia. *

16. Tunapaswa kuepuka kufuata kielelezo cha watu gani tunapojifunza Biblia?

16 Unapojifunza, usiwe kama wale waitwao eti wasomi wa Biblia. Wao hujishughulisha kupita kiasi na uchanganuzi wa maandiko kana kwamba Biblia ilitoka kwa wanadamu. Baadhi yao hujaribu kuonyesha kwamba kila kitabu katika Biblia kiliandikiwa watu fulani hususa au kujaribu kuonyesha kusudi na maoni ya waandikaji. Kusababu huko kwa kibinadamu kunaweza kufanya Biblia ionekane kama kitabu cha historia tu au kufanya vitabu vya Biblia vionekane kama njia tu ya kuonyesha jinsi mafundisho ya kidini yalivyobadilika hatua kwa hatua. Wasomi wengine hujishughulisha sana na utafiti wa maneno, kama vile utafiti kuhusu ukuzi wa lugha iliyotumiwa kuandika Biblia. Badala ya kujishughulisha na umuhimu wa ujumbe wa Mungu, wao hujishughulisha zaidi na kuchunguza vyanzo vya maneno, wakionyesha maana ya maneno hayo katika Kiebrania na Kigiriki. Je, unafikiri kwamba kufanya hivyo kunaweza kumsaidia mtu awe na imani yenye nguvu, inayomchochea kutenda?—1 Wathesalonike 2:13.

17. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Biblia ina ujumbe unaofaa kila mtu?

17 Je, maoni ya wasomi hao ni ya kweli? Je, ni kweli kwamba kila kitabu kinakazia jambo moja tu au kiliandikiwa watu fulani hususa? (1 Wakorintho 1:19-21) Hapana shaka kwamba vitabu vya Neno la Mungu vina manufaa ya kudumu kwa watu wa umri na malezi yote. Hata ikiwa mwanzoni kitabu kilikusudiwa mtu mmoja kama vile Timotheo au Tito, au kikundi fulani hususa, labda Wagalatia au Wafilipi, sote tunaweza na tunapaswa kujifunza vitabu hivyo. Vitabu hivyo ni muhimu kwa kila mmoja wetu. Kitabu kimoja kinaweza kuzungumzia mambo mengi na kunufaisha wasomaji wengi. Naam, ujumbe wa Biblia unafaa kwa kila mtu, na jambo hilo hutusaidia kuelewa ni kwa nini Biblia imetafsiriwa katika lugha za watu mbalimbali kote ulimwenguni.—Waroma 15:4.

Manufaa Kwako na kwa Wengine

18. Unaposoma Neno la Mungu, unapaswa kutafakari juu ya nini?

18 Unapojifunza, utaona kwamba inanufaisha sana kujitahidi kuielewa Biblia na pia kujitahidi kuona jinsi mambo madogo-madogo ya Biblia yanavyohusiana. (Mithali 2:3-5; 4:7) Yale ambayo Yehova amefunua katika Neno lake yanahusiana sana na kusudi lake. Kwa hiyo, jaribu kuona jinsi mambo na ushauri unaosoma katika Neno la Mungu unavyohusiana na kusudi lake. Unaweza kutafakari juu ya jinsi tukio, wazo, au unabii fulani unavyohusiana na kusudi la Yehova. Jiulize: ‘Habari hii inanieleza nini kumhusu Yehova? Inahusianaje na kusudi la Mungu linalotimizwa kupitia Ufalme wake?’ Unaweza kutafakari pia juu ya maswali haya: ‘Ninaweza kutumiaje habari hii? Je, ninaweza kuitumia kufundisha au kutolea wengine ushauri unaotegemea Maandiko?’—Yoshua 1:8.

19. Ni nani anayenufaika unapoeleza wengine mambo unayojifunza? Eleza.

19 Kuwafikiria wengine kunanufaisha kwa njia nyingine pia. Unaposoma Biblia, utajifunza mambo mapya na kuwa na maoni mapya. Jaribu kutumia mambo hayo katika mazungumzo yenye kujenga pamoja na watu wa familia yako au watu wengine. Ukifanya hivyo nyakati zifaazo na kwa kiasi, bila shaka mazungumzo hayo yatakuwa yenye kuthawabisha. Ukiwaeleza wengine kwa unyofu na kwa uchangamfu mambo uliyojifunza au yaliyokupendeza, yaelekea utawachochea wavutiwe zaidi na mambo hayo. Zaidi ya hilo, wewe pia utanufaika. Kwa njia gani? Wataalamu wamesema kwamba mtu atakumbuka kwa muda mrefu zaidi mambo aliyojifunza ikiwa atayatumia au kuyarudia-rudia kwa kuwaeleza wengine mara tu baada ya kuyasoma. *

20. Kwa nini tutanufaika kwa kuisoma Biblia tena na tena?

20 Bila shaka, kila wakati unaposoma kitabu cha Biblia utajifunza jambo jipya. Utavutiwa sana na mistari fulani ambayo awali haikukuvutia. Utaifahamu vema zaidi. Jambo hilo linapaswa kukazia kwamba vitabu vya Biblia si maandishi tu ya wanadamu, bali ni hazina na inafaa tuvisome tena na tena ili tunufaike. Kumbuka kwamba mfalme kama Daudi alipaswa ‘kuisoma siku zote za maisha yake.’

21. Unaweza kutazamia kupata manufaa gani ukitumia wakati mwingi zaidi kujifunza Neno la Mungu?

21 Naam, wale wanaotenga wakati ili kujifunza Biblia kwa undani hunufaika sana. Wanapata ufahamu mwingi sana wa mambo ya kiroho. Wanakuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu. Pia wananufaisha sana familia zao, ndugu na dada zao katika kutaniko la Kikristo, na wale wanaotazamiwa kuwa waabudu wa Yehova baadaye.—Waroma 10:9-14; 1 Timotheo 4:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Vichapo hivi vinavyosaidia mtu kujifunza Biblia vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova na vinapatikana katika lugha mbalimbali.

^ fu. 19 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1993, ukurasa wa 13-14.

Je, Unakumbuka?

• Wafalme wa Israeli walipaswa kufanya nini?

• Yesu na mitume wake walitoa kielelezo gani kuhusiana na funzo la Biblia?

• Unaweza kufanya marekebisho gani ili kuongeza muda unaotumia kwa ajili ya funzo la kibinafsi?

• Unapaswa kusoma Neno la Mungu ukiwa na mtazamo gani?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 15]

‘Isome Biblia Yenyewe’

‘Ikiwa tunatafuta habari fulani katika Biblia, Internet inaweza kutusaidia sana. Lakini ikiwa tunataka kusoma, kujifunza, na kutafakari juu ya habari zilizo katika Biblia, tunapaswa kuisoma Biblia yenyewe. Hiyo ndiyo njia pekee ya kuielewa vizuri.’—Gertrude Himmelfarb, profesa aliyestaafu wa Chuo Kikuu cha City, New York.