Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Matatizo ya Wanadamu Yatapata Kwisha?

Je, Matatizo ya Wanadamu Yatapata Kwisha?

Je, Matatizo ya Wanadamu Yatapata Kwisha?

“ROBO ya wakazi wa dunia wanaishi katika hali ya umaskini, watu bilioni 1.3 wana mapato yanayopungua dola moja kwa siku, bilioni 1 hawajui kusoma na kuandika, bilioni 1.3 hawana maji safi ya kunywa na bilioni 1 hukosa chakula kila siku.” Ndivyo isemavyo ripoti moja kutoka Ireland kuhusu hali ya ulimwengu.

Inahuzunisha kama nini kwamba wanadamu wameshindwa kupata suluhisho la kudumu kwa matatizo ya ulimwengu! Matatizo hayo yanahuzunisha hata zaidi unapotambua kwamba watu wengi wanaotajwa katika ripoti hiyo ni wanawake na watoto dhaifu. Je, si jambo lenye kufadhaisha kwamba hata leo katika karne ya 21, ‘haki za binadamu wengi sana zinaendelea kukiukwa kila siku’?—The State of the World’s Children 2000.

“Ulimwengu Mpya Katika Kizazi Kimoja”

Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa imesema kwa uhakika kwamba ‘hali ya kukatisha tamaa ambayo imesababishwa na kukiukwa kwa haki za binadamu ulimwenguni pote yaweza kukomeshwa.’ Shirika hilo linasema kwamba hali hizo mbaya zinazowapata mabilioni ya watu sasa “haziwezi kuepukika wala kubadilishwa.” Hata shirika hilo limetoa mwito “watu wote watokeze ulimwengu mpya katika kizazi kimoja.” Shirika hilo linatumaini kwamba ulimwengu huo “hautakuwa na umaskini, ubaguzi, jeuri wala magonjwa.”

Watu wanaosema hivyo wanatiwa moyo wanapoona kwamba hata sasa kuna watu wanaojali na wanaofanya kazi kubwa sana ili kupunguza mateso yanayoletwa na “vita na mizozo inayoendelea bila kukoma.” Kwa mfano, katika miaka 15 iliyopita, Mradi wa Kusaidia Watoto wa Chernobyl “umesaidia kupunguza mateso ya mamia ya watoto wanaopatwa na kansa inayosababishwa na miali ya nyuklia.” (The Irish Examiner, April 4, 2000) Mashirika ya kutoa misaada makubwa kwa madogo kwa kweli husaidia sana mamia ya watu waliokumbwa na vita na msiba.

Hata hivyo, watu wanaoshiriki kazi hiyo ya kutoa misaada wanaelewa jinsi hali ilivyo kikweli. Wanajua kwamba matatizo yaliyopo ‘yameenea sana kuliko ilivyokuwa miaka kumi iliyopita.’ David Begg, mkuu wa Shirika la Kutoa Misaada la Ireland, asema kwamba “wafanyakazi, na wafadhili walisaidia sana” wakati Msumbiji ilipokumbwa na mafuriko mabaya. “Lakini,” aongeza kusema, “hatuwezi kukabiliana na misiba mikubwa kama hiyo tukiwa peke yetu.” Anasema hivi waziwazi kuhusu misaada inayotolewa barani Afrika: “Zile sababu chache zinazofanya tuwe na tumaini ni kama nuru ya mishumaa inayoendelea kuzimika.” Wengi wangefikiri kwamba anazungumzia hali zilizopo duniani pote.

Je, ni jambo la hekima kutazamia “ulimwengu mpya katika kizazi kimoja”? Ijapokuwa jitihada zinazofanywa sasa kusaidia watu ni nzuri, bila shaka ni jambo la hekima kutumainia ulimwengu mpya wenye haki na amani kutoka chanzo kingine. Biblia inazungumzia tumaini hilo, kama tutakavyoona katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 2]

Ukurasa wa 3, watoto: UN/DPI Photo by James Bu