Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze na Uwafundishe Wengine Maadili ya Kikristo

Jifunze na Uwafundishe Wengine Maadili ya Kikristo

Jifunze na Uwafundishe Wengine Maadili ya Kikristo

“Je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe?”—WAROMA 2:21.

1, 2. Una sababu zipi za kutaka kujifunza Biblia?

UNA sababu nyingi za kutaka kujifunza Neno la Mungu. Yaelekea unataka kujua Neno la Mungu linasema nini kuhusu watu, matukio, sehemu mbalimbali, na kadhalika. Unataka kujua mafundisho ya kweli, yanayotofautiana na mafundisho ya kidini yasiyo ya kweli kama vile Utatu au moto wa mateso. (Yohana 8:32) Pia ungetaka kumjua Yehova vizuri zaidi ili uweze kumwiga na kujiendesha kwa unyofu mbele zake.—1 Wafalme 15:4, 5.

2 Sababu nyingine muhimu ya kujifunza Neno la Mungu ni ili kujiandaa kufundisha wengine—wapendwa wako, marafiki, na hata wale usiowajua. Kuwafundisha wengine Neno la Mungu ni jambo la lazima kwa Wakristo wa kweli. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.”—Mathayo 28:19, 20.

3, 4. Kwa nini inafaa kufundisha kama Yesu alivyoamuru?

3 Kujifunza Biblia ili uweze kufundisha wengine ni jambo linalofaa na lenye kuleta uradhi unaodumu. Kazi ya ualimu imeheshimiwa kwa muda mrefu. Kichapo Encarta Encyclopedia kinasema: “Wayahudi wengi waliwaona walimu kuwa viongozi waliowaelekeza watu kwenye wokovu nao waliwatia watoto wao moyo wawaheshimu walimu zaidi ya wazazi wao.” Inafaa hasa Wakristo wajifunze Biblia kwanza, kisha wawafundishe wengine.

4 “Kazi ya ualimu hufanywa na watu wengi zaidi kuliko kazi nyingine yoyote ya utaalamu. Kuna walimu wapatao milioni 48 ulimwenguni pote.” (The World Book Encyclopedia) Mwalimu wa kawaida ana daraka la kuwafundisha vijana, na mambo anayowafundisha yanaweza kuathiri maisha yao baadaye. Kazi hiyo inakuwa na matokeo makubwa hata zaidi unapotii amri ya Yesu ya kuwafundisha wengine, kwa kuwa ufundishaji wako utaathiri wakati wao ujao. Mtume Paulo alikazia jambo hilo alipomhimiza Timotheo hivi: “Kaza uangalifu kwako mwenyewe na kwa kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivi utajiokoa wewe mwenyewe na wale wakusikilizao pia.” (1 Timotheo 4:16) Naam, ufundishaji wako unahusiana na wokovu.

5. Kwa nini ufundishaji unaofanywa na Wakristo ndio bora zaidi?

5 Kujifunza na kufundisha wengine kumeagizwa na kunaelekezwa na Mtawala wa ulimwengu wote ambaye ndiye Chanzo kikuu zaidi cha ufundishaji. Jambo hilo hufanya kazi hiyo ya kufundisha iwe muhimu zaidi kuliko kazi nyingine yoyote ya kufundisha, kama vile kufundisha mambo ya msingi shuleni, kufundisha watu kazi fulani, au kufundisha utaalamu fulani katika mambo ya kitiba. Mkristo humfundisha mwanafunzi kumwiga Mwana wa Mungu, Kristo Yesu, na pia aweze kuwafundisha wengine kufanya hivyo.—Yohana 15:10.

Kwa Nini Ujifunze?

6, 7. (a) Kwa nini tunapaswa kujifunza wenyewe kwanza? (b) Ni katika njia gani Wayahudi wa karne ya kwanza walishindwa kufundisha?

6 Kwa nini tunapaswa kujifunza wenyewe kwanza? Kwa sababu hatuwezi kuwafundisha wengine ifaavyo tusipojifunza wenyewe kwanza. Paulo alikazia jambo hilo katika andiko lenye kuamsha fikira ambalo lilikuwa na ujumbe wa maana kwa Wayahudi wa siku zake. Andiko hilo lina ujumbe mzito kwa Wakristo leo. Paulo aliuliza: “Je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe? Wewe, unayehubiri ‘Usiibe,’ je, wewe huiba? Wewe, unayesema ‘Usifanye uzinzi,’ je, wewe hufanya uzinzi? Wewe, unayeonyesha chukio kubwa la sanamu, je, wewe hupokonya mahekalu? Wewe, uonaye fahari katika sheria, je, kwa ukiukaji wako wa Sheria wewe huvunjia Mungu heshima?”—Waroma 2:21-23.

7 Kwa kutumia maswali hayo yasiyohitaji majibu, Paulo alionyesha makosa mawili yaliyotajwa katika Amri Kumi: Usiibe na usizini. (Kutoka 20:14, 15) Wayahudi fulani wa siku za Paulo walijivunia kuwa na Sheria ya Mungu. ‘Walifundishwa kwa mdomo kutokana na Sheria na wakashawishwa kwamba walikuwa viongozi wa walio vipofu, na nuru kwa wale walio katika giza, walimu wa vitoto.’ (Waroma 2:17-20) Hata hivyo, wengine walikuwa wanafiki kwa sababu walikuwa wakiiba au kuzini kisiri. Matendo hayo hayakuiheshimu Sheria wala kumheshimu Mtungaji wa Sheria hiyo aliye mbinguni. Unaweza kuona kwamba hawakustahili kuwafundisha wengine kwa kuwa wao wenyewe hawakuwa wakijifunza.

8. Huenda Wayahudi fulani wa siku za Paulo ‘waliyapokonya mahekalu’ kwa njia gani?

8 Paulo alizungumza kuhusu kupokonya mahekalu. Je, Wayahudi fulani walifanya hivyo kihalisi? Paulo alikuwa akimaanisha nini? Kulingana na habari chache zinazopatikana katika andiko hilo, hatuwezi kusema kwa uhakika jinsi Wayahudi fulani ‘walivyopokonya mahekalu.’ Mapema kidogo, karani wa jiji la Efeso alisema kwamba Paulo na wenzake hawakuwa “wapokonya-mahekalu,” jambo linalodokeza kwamba watu fulani walifikiri kwamba Wayahudi walipokonya mahekalu. (Matendo 19:29-37) Je, walikuwa wakitumia au kuuza vitu fulani vya thamani kutoka kwa mahekalu ya wapagani ambayo yalikuwa yameporwa na watekaji au wafuasi shupavu wa dini ya Kiyahudi? Kulingana na Sheria ya Mungu, dhahabu na fedha iliyotengeneza sanamu ingepaswa kuharibiwa, wala si kuchukuliwa kwa matumizi ya kibinafsi. (Kumbukumbu la Torati 7:25) * Kwa hiyo huenda Paulo alikuwa akizungumza kuhusu Wayahudi waliopuuza amri ya Mungu na kutumia au kufaidika na vitu vilivyotoka katika mahekalu ya wapagani.

9. Ni mambo gani yasiyofaa yaliyofanywa hekaluni huko Yerusalemu ambayo huenda yangekuwa sawa na kupokonya hekalu?

9 Kwa upande mwingine, Josephus alitaja kashfa nyingine huko Roma iliyosababishwa na Wayahudi wanne wakioongozwa na mwalimu wa Sheria. Wayahudi hao wanne walimshawishi mwanamke Mroma, aliyekuwa amegeuzwa imani akawa mfuasi wa dini ya Kiyahudi, achange dhahabu na vitu vingine vya thamani kwenye hekalu huko Yerusalemu. Walipopata vitu hivyo kutoka kwake, walivitumia kujitajirisha. Jambo hilo lilikuwa sawa na kupokonya hekalu. * Wengine walikuwa wakipokonya hekalu la Mungu kwa kutoa dhabihu zenye kasoro na kuendeleza biashara yenye pupa hekaluni, hivyo kulifanya kuwa “pango la wapokonyaji.”—Mathayo 21:12, 13; Malaki 1:12-14; 3:8, 9.

Fundisha Maadili ya Kikristo

10. Ni jambo gani kuu lililozungumziwa na Paulo kwenye Waroma 2:21-23 ambalo hatupaswi kupuuza?

10 Hata Paulo awe alikuwa akigusia mazoea gani katika karne ya kwanza ambayo yalihusiana na wizi, uzinzi, na kupokonya mahekalu, na tusipuuze jambo kuu katika mazungumzo yake. Aliuliza: “Je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe?” Inafaa tuzingatie kwamba mifano ambayo Paulo alitumia ilihusu maadili. Hapa mtume hakukazia mafundisho au historia ya Biblia. Paulo alizungumza juu ya kujifunza na kufundisha wengine maadili ya Kikristo.

11. Kwa nini ukazie fikira maadili ya Kikristo unapojifunza Neno la Mungu?

11 Ili tuweze kufuata yale tunayojifunza kwenye Waroma 2:21-23 tunahitaji kujifunza maadili ya Kikristo yaliyo katika Neno la Mungu, tutende kupatana na tunayojifunza, kisha kuwafundisha wengine kufanya vivyo hivyo. Kwa hiyo, unapojifunza Biblia, uwe macho kutambua viwango vya Yehova, ambavyo ndivyo msingi wa maadili ya Kikristo. Tafakari juu ya ushauri na mafundisho unayopata katika Biblia. Kisha ufuate yale unayojifunza. Ili kufanya hivyo, unahitaji kuwa jasiri na mwenye kuazimia. Ni rahisi kwa wanadamu wasio wakamilifu kutoa sababu za kuonyesha ni kwa nini hali fulani inawaruhusu au kuwafanya wapuuze maadili ya Kikristo. Labda Wayahudi ambao Paulo alitaja walitumia sababu hizo za kijanja ili kupunguza uzito wa maadili ya Kikristo au kupotosha wengine. Hata hivyo, maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba hatupaswi kupunguza uzito wa maadili ya Kikristo kwa sababu ya mapendezi yetu.

12. Mwenendo wetu huathirije maoni ya watu kumhusu Yehova Mungu, na kwa nini inafaa kukumbuka jambo hilo?

12 Mtume alikazia sababu moja muhimu ya kujifunza na kufuata maadili ya Biblia. Mwenendo usiofaa wa Wayahudi ulimvunjia Yehova heshima: “Wewe, uonaye fahari katika sheria, je, kwa ukiukaji wako wa Sheria wewe huvunjia Mungu heshima? Kwa maana ‘jina la Mungu linafanyiwa kufuru miongoni mwa mataifa kwa sababu ya nyinyi watu.’” (Waroma 2:23, 24) Hali iko hivyo leo. Tunapopuuza maadili ya Kikristo, tunamvunjia heshima yule aliye Chanzo cha maadili hayo. Kinyume cha hilo, tunapofuata viwango vyake bila kuyumbayumba tunamletea Mungu heshima. (Isaya 52:5; Ezekieli 36:20) Kufahamu jambo hilo kunaweza kutia nguvu azimio lako unapokabili majaribu au hali ambazo zinaweza kukufanya ufikiri kwamba kupuuza maadili ya Kikristo ndilo jambo rahisi au lifaalo zaidi kufanya. Maneno ya Paulo yanatufundisha jambo lingine pia. Mbali na kujua kwamba mwenendo wako mzuri humletea Mungu heshima, wasaidie watu unaowafundisha waelewe kwamba wanamletea Yehova heshima wanapofuata viwango vya maadili wanavyojifunza. Mbali na kuleta uradhi na kulinda afya ya mtu, maadili ya Kikristo humletea heshima Yule aliyeyaanzisha ambaye huwatia moyo watu wayafuate.—Zaburi 74:10; Yakobo 3:17.

13. (a) Biblia inatusaidiaje kuhusiana na maadili? (b) Onyesha jambo kuu katika ushauri uliotolewa kwenye 1 Wathesalonike 4:3-7.

13 Maadili huathiri watu wengine pia. Kuna mifano katika Neno la Mungu inayoonyesha manufaa ya kufuata viwango vya Mungu vya maadili na matokeo ya kuvipuuza. (Mwanzo 39:1-9, 21; Yoshua 7:1-25) Unaweza pia kupata ushauri ulio wazi kuhusu maadili kama huu: “Haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kule kutakaswa kwenu, kwamba mjiepushe na uasherati; kwamba kila mmoja wenu apaswe kujua jinsi ya kupata umiliki wa chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima, si katika hamu yenye tamaa ya ngono kama ile waliyo nayo pia mataifa wale wasiomjua Mungu; kwamba yeyote asifikie hatua ya kudhuru na kuziingilia haki za ndugu yake katika jambo hilo, . . . kwa maana Mungu alituita sisi, si kwa kuruhusu ukosefu wa usafi, bali kwa kuhusiana na utakaso.”—1 Wathesalonike 4:3-7.

14. Unaweza kujiuliza maswali gani kuhusiana na ushauri kwenye andiko la 1 Wathesalonike 4:3-7?

14 Andiko hilo linaonyesha wazi kwamba mwenendo mchafu kingono huvunja maadili ya Kikristo. Hata hivyo, unaweza kuelewa andiko hilo kwa undani zaidi. Maandiko fulani yana mambo mengi tunayoweza kujifunza na kutafakari, na hivyo kuyafahamu kwa undani na kwa usahihi zaidi. Kwa mfano, unaweza kutafakari juu ya yale ambayo Paulo alimaanisha aliposema kwamba kufanya uasherati kunaweza kufanya mtu ‘afikie hatua ya kudhuru na kuziingilia haki za ndugu yake katika jambo hilo.’ Ni haki gani zinazotajwa, na kuelewa jambo hilo vema kunaweza kukuchocheaje zaidi udumishe maadili ya Kikristo? Matokeo ya utafiti huo yanaweza kukusaidiaje uwafundishe wengine na kuwasaidia wamheshimu Mungu?

Jifunze Ili Ufundishe

15. Ni vifaa gani unavyoweza kutumia unapojifunza?

15 Mashahidi wa Yehova wana vifaa wanavyotumia kufanya utafiti wa maswali au masuala yanayotokea wanapojifunza au wanapofundisha wengine. Kichapo Watch Tower Publications Index ni kifaa kinachopatikana katika lugha mbalimbali. Ikiwa una kifaa hicho, unaweza kukitumia kupata habari katika vichapo vya Mashahidi wa Yehova vinavyozungumzia Biblia. Unaweza kutafuta habari unayotaka kwa kutumia vichwa au orodha ya mistari ya Biblia. Kifaa kingine kinachopatikana kwa Mashahidi wa Yehova katika lugha mbalimbali kuu ni Watchtower Library. Programu hiyo ya kompyuta iliyohifadhiwa katika kifaa kiitwacho CD-ROM, inajumulisha vichapo vingi sana na husaidia mtu kufanya utafiti wa mambo mbalimbali kutia ndani habari za kimaandiko. Ikiwa unaweza kupata vifaa hivyo, vitumie kwa ukawaida unapojifunza Neno la Mungu ili uwafundishe wengine.

16, 17. (a) Unaweza kupata wapi ufafanuzi kuhusu haki zilizotajwa kwenye andiko la 1 Wathesalonike 4:6? (b) Uasherati unaweza kuingilia haki za wengine katika njia zipi?

16 Hebu tufikirie mfano uliotajwa juu kwenye andiko la 1 Wathesalonike 4:3-7. Suala lilitokea kuhusu haki. Haki za nani? Nazo haki hizo zinaweza kuingiliwa jinsi gani? Kwa kutumia vifaa vya kujifunzia vilivyotajwa, unaweza kupata maelezo yanayofafanua mistari hiyo, kutia ndani haki ambazo Paulo alitaja. Unaweza kusoma maelezo hayo katika Insight on the Scriptures, Buku la Kwanza, ukurasa wa 863-864; Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?, ukurasa wa 145; gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1989, ukurasa wa 31.

17 Ukiendelea kujifunza, utaona kwamba vichapo hivyo vinathibitisha yale ambayo Paulo alisema. Mwasherati humtenda Mungu dhambi na kujiweka katika hatari ya kupatwa na magonjwa. (1 Wakorintho 6:18, 19; Waebrania 13:4) Mwanamume anayefanya uasherati na mwanamke, huingilia haki za mwanamke huyo. Yeye huchafua maadili na dhamiri ya mwanamke huyo. Ikiwa hajaolewa, haki yake ya kufunga ndoa akiwa bikira huvunjwa, naye mtu atakayemwoa hunyimwa haki ya kufunga ndoa na bikira. Mwanamume huyo huwaumiza wazazi na mume wa mwanamke huyo ikiwa ameolewa. Mwanamume huyo asiye na maadili huinyima familia yake haki ya kuwa na sifa nzuri kiadili. Ikiwa yeye ni mshiriki wa kutaniko la Kikristo, analiaibisha na kuliharibia sifa kutaniko.—1 Wakorintho 5:1.

18. Unafaidikaje na funzo la Biblia kuhusu maadili ya Kikristo?

18 Maelezo hayo kuhusu haki yanakusaidia kuelewa kindani zaidi mstari huo. Bila shaka, ukiendelea kujifunza kwa njia hiyo utaelewa Maandiko vizuri zaidi na utanufaika sana. Ufahamu wako kwamba ujumbe wa Mungu ni wa kweli na ni wenye nguvu utaongezeka. Utaimarisha azimio lako la kufuata maadili ya Kikristo hata ukipatwa na jaribu gani. Unaweza pia kuwa mwalimu mwenye matokeo sana. Kwa mfano, unapowafundisha wengine kweli ya Biblia, unaweza kufafanua andiko la 1 Wathesalonike 4:3-7 na kuongeza ufahamu na uthamini wao kwa maadili ya Kikristo. Hivyo, funzo lako linaweza kukusaidia na kuwasaidia wengine wengi wamheshimu Mungu. Tumetaja mfano mmoja tu kutoka katika barua ya Paulo kwa Wathesalonike. Kuna mambo mengine mengi yanayohusiana na maadili ya Kikristo, kutia ndani mifano na ushauri mwingi unaoweza kujifunza, kufuata, na kufundisha wengine.

19. Kwa nini ni muhimu kudumisha maadili ya Kikristo?

19 Bila shaka ni jambo la hekima kudumisha maadili ya Kikristo. Andiko la Yakobo 3:17 linasema kwamba “hekima ya kutoka juu,” kwa Yehova Mungu mwenyewe, “kwanza kabisa ni safi kiadili.” Bila shaka, jambo hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kufuata viwango vya Mungu vya maadili. Kwa kweli, Yehova hutaka wale wanaomwakilisha katika kufundisha Biblia waweke mfano mzuri “katika usafi wa kiadili.” (1 Timotheo 4:12) Maisha ya wanafunzi wa mapema kama Paulo na Timotheo yanaonyesha kwamba waliepuka ukosefu wa maadili. Paulo hata aliandika hivi: “Acheni uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa hata visitajwe hata miongoni mwenu, kama vile ifaavyo watu watakatifu; wala mwenendo wa aibu wala maongezi ya kipumbavu wala kufanya mzaha wenye aibu.”—Waefeso 5:3, 4.

20, 21. Kwa nini unakubaliana na maneno ya mtume Yohana kwenye 1 Yohana 5:3?

20 Viwango vya maadili vilivyo katika Neno la Mungu ni wazi na hususa na si vyenye kulemea. Yohana, mtume aliyeishi muda mrefu zaidi ya wengine alijua jambo hilo. Kutokana na mambo aliyokuwa amejionea kwa miaka mingi, Yohana alijua kwamba maadili ya Kikristo hayakuwa yenye kudhuru. Kinyume chake, yalikuwa mema, yenye kunufaisha na kuleta baraka. Yohana alikazia jambo hilo kwa kuandika: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.”—1 Yohana 5:3.

21 Hata hivyo, ona kwamba Yohana hakusema kwamba kumtii Mungu kwa kufuata maadili ya Kikristo kunafaa kwa sababu tu tutaepuka matatizo na matokeo mabaya ya kutofanya hivyo. Alionyesha maoni yafaayo kuhusu utii kwa Mungu kwa kufunua kwanza kwamba utii huo ni wonyesho wa upendo wetu kwa Yehova Mungu na ni fursa nzuri ya kudhihirisha upendo wetu kwake. Kwa kweli, ili kujifunza au kufundisha wengine wampende Mungu tunahitaji tukubali na kufuata viwango vya juu vya Mungu. Naam, tunahitaji kujifunza wenyewe na kuwafundisha wengine maadili ya Kikristo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ingawa Josephus anaonyesha kwamba Wayahudi waliheshimu vitu vitakatifu, yeye aliirudia sheria ya Mungu kwa kusema hivi: “Mtu yeyote na asikufuru miungu ambayo majiji mengine huabudu, wala kupokonya mahekalu ya kigeni, wala kuchukua vitu vya thamani ambavyo vimewekwa wakfu kwa mungu yeyote yule.” (Italiki ni zetu.)—Jewish Antiquities, Kitabu cha 4, sura ya 8, fungu la 10.

^ fu. 9 Jewish Antiquities, Kitabu cha 18, sura ya 3, fungu la 5.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini tunapaswa kujifunza kabla ya kufundisha wengine?

• Mwenendo wetu unawezaje kumletea Yehova sifa?

• Mwasherati anaweza kuwa anaingilia haki za nani?

• Wewe umeazimia kufanya nini kuhusiana na maadili ya Kikristo?

[Maswali ya Funzo]

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 22]

“Amri zake si zenye kulemea”