Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Epuka Kudanganywa

Epuka Kudanganywa

Epuka Kudanganywa

DANGANYIFU ni zoea la zamani sana. Ni mojawapo ya matukio ya kwanza kabisa kuandikwa katika historia, wakati Shetani alipomdanganya Hawa katika bustani ya Edeni.—Mwanzo 3:13; 1 Timotheo 2:14.

Tangu wakati huo udanganyifu umeenea sana duniani, hasa siku hizi. Ikitabiri kuhusu wakati huu Biblia ilionya: “Watu waovu na walaghai wataendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi, wakiongoza vibaya na kuwa wenye kuongozwa vibaya.”—2 Timotheo 3:13.

Watu hudanganywa kwa sababu mbalimbali. Walaghai na wahuni hudanganya watu ili waibe pesa zao. Wanasiasa fulani huwadanganya wapiga kura kwa nia ya kubaki mamlakani kwa njia yoyote ile. Watu hata hujidanganya wenyewe. Hawataki kukubali ukweli wa mambo, badala yake wao hujidanganya kwamba hawatapatwa na madhara hata wakijiingiza katika mazoea hatari kama vile kuvuta sigara, kutumia madawa ya kulevya, au kufanya uasherati.

Watu pia hudanganywa katika mambo ya kidini. Viongozi wa kidini wa siku za Yesu waliwadanganya watu. Yesu alisema hivi kuhusu wadanganyifu hao: “Viongozi vipofu ndivyo walivyo. Basi, ikiwa kipofu aongoza kipofu, wote wawili wataanguka ndani ya shimo.” (Mathayo 15:14) Hata watu wenyewe hujidanganya katika mambo ya kidini. Andiko la Mithali 14:12 linasema: “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, lakini mwisho wake ni njia za mauti.”

Kama ilivyokuwa siku za Yesu, si ajabu kwamba watu wengi leo hudanganywa katika mambo ya kidini! Mtume Paulo alisema kwamba Shetani “amepofusha akili za wasioamini, ili mmuliko wa habari njema yenye utukufu juu ya Kristo, aliye mfano wa Mungu, usipate kung’aa kwa kupenya.”—2 Wakorintho 4:4.

Tunapodanganywa na mlaghai, tunapoteza pesa. Tunapodanganywa na mwanasiasa, huenda tukapoteza kiasi fulani cha uhuru. Lakini Shetani akitudanganya tukatae kweli kumhusu Yesu Kristo, tunapoteza uhai udumuo milele! Kwa hiyo, epuka kudanganywa. Jifunze Biblia ambayo ndiyo chanzo pekee cha mafundisho ya kweli ya kidini. Utapata manufaa nyingi ukifanya hivyo.—Yohana 17:3.