Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unafundisha kwa Matokeo?

Je, Unafundisha kwa Matokeo?

Je, Unafundisha kwa Matokeo?

WAZAZI, wazee, na wahubiri wa habari njema wanapaswa kuwa walimu. Wazazi hufundisha watoto wao, wazee hufundisha washiriki wa kutaniko la Kikristo, na wahubiri wa habari njema hufundisha watu wanaopendezwa. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Mathayo 28:19, 20; 1 Timotheo 4:13, 16) Unaweza kufanya nini ili ufundishaji wako uwe na matokeo mazuri zaidi? Njia moja ni kwa kuwaiga walimu stadi wanaotajwa katika Neno la Mungu. Ezra alikuwa mmoja wao.

Kujifunza Kutoka kwa Mfano wa Ezra

Ezra alikuwa kuhani wa ukoo wa Haruni aliyeishi yapata miaka 2,500 iliyopita huko Babiloni. Katika mwaka wa 468 K.W.K., alisafiri hadi Yerusalemu ili kuendeleza ibada safi miongoni mwa Wayahudi walioishi huko. (Ezra 7:1, 6, 12, 13) Ili kutimiza kazi hiyo ilimpasa kuwafundisha watu Sheria ya Mungu. Ezra alifanya nini kuhakikisha kwamba ufundishaji wake ulikuwa na matokeo mazuri. Alichukua hatua kadhaa za lazima. Hatua hizo zimetajwa katika Ezra 7:10:

“Ezra alikuwa [1] ameuelekeza [“tayarisha,” “NW”] moyo wake [2] kuitafuta sheria ya BWANA, na [3] kuitenda, na [4] kufundisha maagizo na hukumu [“haki,” NW] katika Israeli.”(Italiki ni zetu.) Tuchunguze kwa ufupi kila mojawapo ya hatua hizo na tuone kile tunachoweza kujifunza.

‘Ezra Alikuwa Ameutayarisha Moyo Wake’

Kama vile mkulima anavyotayarisha udongo kwa kulima kabla ya kupanda mbegu, Ezra alitayarisha moyo wake kwa kusali ili akubali neno la Mungu. (Ezra 10:1) Yaani, ‘aliuelekeza moyo wake’ kupokea mafundisho ya Yehova.—Mithali 2:2.

Vivyo hivyo, Biblia inasema kwamba Mfalme Yehoshafati ‘alitayarisha, moyo wake kumtafuta Mungu.’ (2 Mambo ya Nyakati 19:3) Kwa upande mwingine, kizazi kimoja cha Waisraeli kinafafanuliwa kuwa “cha ukaidi na uasi” kwa sababu ‘hakikujitengeneza moyo.’ (Zaburi 78:8) Yehova anamwona “yule mtu wa siri wa moyoni.” (1 Petro 3:4) Naam, ‘atawafundisha wenye upole njia yake.’ (Zaburi 25:9) Kwa hiyo, ni muhimu sana kwamba walimu leo wafuate mfano wa Ezra kwa kutoa sala ili wawe na hali nzuri ya moyoni.

“Kuitafuta Sheria ya BWANA”

Ili awe mwalimu stadi, Ezra alitafuta ushauri kutoka kwa Neno la Mungu. Ikiwa ungemwendea daktari ili kutafuta ushauri, bila shaka ungemsikiliza kwa makini na kuhakikisha kwamba umeelewa yote anayokuambia na kupendekeza. Ungefanya hivyo kwa sababu unajali afya yako. Hivyo, basi, tunapaswa kusikiliza hata zaidi yale ambayo Yehova anatuambia au kupendekeza katika Neno lake, Biblia, na kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Tunapaswa kufanya hivyo kwa sababu ushauri wake unahusu maisha yetu! (Mathayo 4:4; 24:45-47) Daktari anaweza kukosea, lakini “sheria ya BWANA ni kamilifu.” (Zaburi 19:7) Hatuhitaji kamwe kutilia shaka sheria ya Yehova.

Vitabu vya Biblia vya Mambo ya Nyakati (vilivyoandikwa na Ezra, na vilivyokuwa kitabu kimoja awali) vinaonyesha kwamba Ezra alikuwa mwanafunzi makini sana. Alipoandika vitabu hivyo alitoa habari kutoka kwa maandishi mbalimbali. * Wayahudi, waliokuwa wamewasili kutoka Babiloni, walihitaji kujua angalau mambo makuu ya historia ya taifa lao. Hawakujua vizuri sherehe za dini yao, utumishi wa hekalu, na kazi za Walawi. Walihitaji sana orodha ya koo mbalimbali. Ezra alikazia hasa mambo hayo. Hadi kuja kwa Mesiya, Wayahudi walipaswa kudumu wakiwa taifa moja katika nchi ya kwao wakiwa na hekalu lao, ukuhani, na gavana. Habari ambazo Ezra alikuwa amekusanya zilisaidia kudumisha umoja na ibada ya kweli.

Je, wewe hujifunza kama Ezra? Kujifunza Biblia kwa bidii kutakusaidia kuifundisha kwa matokeo mazuri.

“Kuitafuta Sheria ya BWANA” Mkiwa Familia

Mbali na funzo la kibinafsi, funzo la familia ni njia nyingine nzuri ya kutafuta ushauri katika sheria ya Yehova.

Jan na Julia, wenzi wa ndoa huko Uholanzi, wamewasomea wana wao wawili kwa sauti tangu watoto hao walipozaliwa. Leo, Ivo ana miaka 15 naye Edo ana miaka 14. Bado wao huwa na funzo la familia kila juma. Jan anasema hivi: “Lengo letu kuu si kumaliza kusoma kitabu fulani, bali ni kuwasaidia wavulana waelewe yale tunayojifunza.” Anaongeza hivi: “Wavulana hufanya utafiti mwingi. Wao huchunguza maana ya maneno magumu. Nao hufanya utafiti kuwahusu watu wanaotajwa katika Biblia wasiowajua, ili kujua kipindi walichoishi, wao walikuwa nani, kazi yao, na kadhalika. Tangu walipojua kusoma, wamefanya utafiti katika vitabu kama vile Insight on the Scriptures, kamusi mbalimbali, na vitabu vinginevyo vya wasomi. Jambo hilo hufanya funzo la familia lipendeze zaidi. Sikuzote, wavulana hutarajia kwa hamu funzo la familia.” Faida nyingine ni kwamba wavulana wote wawili wana ufasaha wa kusema kuliko wanadarasa wenzao.

John na Tini, wenzi wengine wa ndoa huko Uholanzi, walijifunza na mwana wao, Esli, (sasa ana miaka 24 naye ni painia katika kutaniko lingine), na binti yao, Linda (sasa ana miaka 20, naye ameolewa na ndugu mwenye sifa nzuri. Hata hivyo, badala ya kutumia maswali yaliyochapishwa, walibadili njia ya kujifunza ili ipatane na umri na mahitaji ya watoto wao. Walifanyaje hivyo?

John anaeleza kwamba binti na mwana wake walichagua habari inayopendeza katika makala za “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” (katika gazeti la Mnara wa Mlinzi) na “Maoni ya Biblia” (katika gazeti la Amkeni!). Baadaye walieleza yale waliyokuwa wametayarisha na kila tulipojifunza tulikuwa na mazungumzo ya familia yenye kupendeza. Kwa njia hiyo vijana wetu walizoea kufanya utafiti na kuzungumzia yale ambayo wamejifunza. Je, wewe ‘unaitafuta sheria ya Yehova’ pamoja na watoto wako? Ukifanya hivyo, utafanya maendeleo katika ufundishaji wako, na pia utawasaidia watoto wako kuwa na matokeo mazuri zaidi wanapowafundisha wengine.

“Kuitenda”

Ezra alitenda yale ambayo alijifunza. Kwa mfano, alipokuwa Babiloni, yaelekea alikuwa na maisha ya starehe. Hata hivyo, alipotambua kwamba angeweza kuwasaidia watu wake katika nchi nyingine, aliacha starehe za Babiloni na kusafiri hadi Yerusalemu, jiji la mbali lenye magumu, taabu, na hatari. Ni wazi kwamba Ezra hakujifunza tu Biblia bali alikuwa tayari kutenda kupatana na yale aliyokuwa amejifunza.—1 Timotheo 3:13.

Baadaye, alipokuwa akiishi Yerusalemu, Ezra alionyesha tena kwamba alitenda kupatana na yale aliyofundisha aliposikia kwamba wanaume Waisraeli walikuwa wamewaoa wanawake wapagani. Biblia inasema kwamba ‘alirarua nguo yake na joho yake, akang’oa nywele za kichwa chake, na ndevu zake, akaketi kwa mshangao.’ Hata ‘alitahayari, na kuona haya kuinua uso wake’ mbele za Yehova.—Ezra 9:1-6.

Ezra alifaidika alipojifunza Sheria ya Mungu. Alielewa waziwazi matokeo mabaya ya kutotii. Wayahudi waliorudi kwenye nchi yao walikuwa wachache. Kama wangalioa wanawake wa mataifa mengine, huenda hatimaye wangaliungana na mataifa ya kipagani yaliyowazunguka, na ibada safi ingaliweza kutoweka duniani kwa urahisi!

Jambo la kufurahisha ni kwamba, Waisraeli walirekebisha njia zao walipoona hofu ya kimungu na bidii ya Ezra. Iliwachukua miezi mitatu tu kuwafukuza wake zao wa kigeni. Ufundishaji wa Ezra ulikuwa na matokeo mazuri kwa sababu yeye mwenyewe alifuata kwa uaminifu Sheria ya Mungu.

Hali kadhalika leo tunaweza kupata faida tukifuata sheria ya Mungu. Baba mmoja Mkristo alisema hivi: “Watoto hufuata mfano wako wala si maneno yako.” Hivyo ndivyo ilivyo katika kutaniko la Kikristo. Wazee walio na mwenendo mzuri wanaweza kutarajia kwamba kutaniko litafuata mafundisho yao.

‘Kufundisha Maagizo na Haki Katika Israeli’

Kuna jambo lingine lililofanya ufundishaji wa Ezra uwe na matokeo mazuri. Hakufundisha maoni yake mwenyewe, bali alifundisha ‘maagizo na haki.’ Yaani, alifundisha maagizo, au sheria ya Yehova. Hilo lilikuwa jukumu lake kwa sababu alikuwa kuhani. (Malaki 2:7) Pia alifundisha haki, na alitenda kupatana na yale aliyofundisha kwa kufuata sheria kikamilifu bila kuonyesha ubaguzi wala upendeleo. Watu wenye mamlaka wanapotenda kwa haki, kunakuwa na uthabiti na faida ya kudumu. (Mithali 29:4) Vivyo hivyo, wazee Wakristo, wazazi, na wahubiri wa Ufalme wanaojua Neno la Mungu vizuri huwaimarisha kiroho washiriki wa kutaniko, familia, na watu wanaopendezwa, wanapowafundisha maagizo na haki ya Yehova.

Je, unakubali kwamba ufundishaji wako unaweza kuwa wenye matokeo mazuri zaidi ukifuata mfano wa Ezra? Kwa hiyo, ‘tayarisha moyo wako, itafute sheria ya Yehova, uitende, na ufundishe maagizo na haki ya Yehova.’—Ezra 7:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Orodha ya maandiko 20 inapatikana katika kichapo cha Insight on the Scriptures, Buku la I, ukurasa wa 444-445, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

NI NINI KILICHOFANYA UFUNDISHAJI WA EZRA UWE NA MATOKEO MAZURI?

1. Alitayarisha moyo wake ili uwe na hali nzuri

2. Alitafuta ushauri katika Sheria ya Yehova

3. Alitenda yale aliyojifunza

4. Alijitahidi kujifunza ili kufundisha Maandiko wala si maoni yake