Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Makusanyiko ya Kimataifa Katika Mwaka wa 2003

Makusanyiko ya Kimataifa Katika Mwaka wa 2003

Makusanyiko ya Kimataifa Katika Mwaka wa 2003

MKUTANO wa kila mwaka wa washiriki wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania ulifanywa Jumamosi, Oktoba 6, 2001, huko Jersey City, New Jersey, Marekani. Baada ya mkutano huo, washiriki pamoja na wageni wao walifurahia programu ya pekee. Siku iliyofuata, kwenye mikutano ya ziada iliyofanywa huko Kanada na Marekani, washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova walitoa tangazo lifuatalo baada ya hotuba yao ya mwisho:

“Tunapotazamia wakati ujao, inafaa sana watu wote wa Mungu wasiache kukutanika pamoja. Mtume Paulo alituhimiza tuendelee kukutanika pamoja na pia kutiana moyo hata zaidi kwa kuwa siku kuu ya Yehova yenye kutisha inazidi kukaribia. (Waebrania 10:24, 25) Kupatana na amri hiyo ya Kimaandiko, tunatumaini kuwa na makusanyiko ya wilaya ulimwenguni pote mwaka ujao [2002]. Kisha katika mwaka wa 2003, ikiwa ni mapenzi ya Yehova, huenda tukawa na makusanyiko ya kimataifa ya pekee katika sehemu fulani za ulimwengu. Sasa ndio wakati wa kuwa macho na kufuliza kulinda, na kutambua jinsi matukio ya ulimwengu yanavyodhihirika.”

Lazima utendaji wa watu wa Mungu uendelee licha ya kuongezeka kwa misukosuko na wasiwasi wa ulimwengu huu unaokaribia kwisha. Lazima habari njema ya Ufalme, inayotia ndani ujumbe wa Biblia wa kuonya watu, itangaziwe kila taifa, kabila, lugha, na watu, na kuwahimiza ‘wamhofu Mungu na kumpa utukufu kwa sababu saa ya hukumu yake inazidi kukaribia.’ (Ufunuo 14:6, 7) Kwa hiyo, kulingana na mapenzi ya Baba yetu wa kimbingu, mipango inafanywa kuwe na makusanyiko ya kimataifa katika sehemu mbalimbali za ulimwengu mwaka wa 2003.

Kwanza, mipango inafanywa kuwe na makusanyiko hayo katika majiji machache huko Amerika Kaskazini, na muda mfupi baadaye huko Ulaya. Baadaye kidogo katika mwaka wa 2003, mipango itafanywa ili wajumbe wasafiri wakiwa vikundi kwenda majiji machache ya Asia; na karibu mwisho wa mwaka, vikundi zaidi vitasafiri kwenda Afrika, Amerika Kusini, na eneo la Pasifiki. Ofisi fulani za tawi zitaombwa zitume wajumbe wachache kwenye makusanyiko hususa, kwa hiyo haitawezekana kualika kila mtu. Hata hivyo, itatia moyo kuwa na wajumbe wachache wanaowakilisha nchi mbalimbali kila mahali.

Hivi karibuni makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yatapokea habari kuhusu makusanyiko hayo. Habari kuhusu tarehe na majiji hususa ambako wajumbe walioalikwa wanaweza kuhudhuria itatolewa na ofisi ya tawi ya nchi wanamoishi. Kwa hiyo, mnaombwa msiandike barua au kuuliza maswali wakati huu kuhusiana na habari hiyo.

Wale watakaochaguliwa kuwa wajumbe wanapaswa kuwa Mashahidi waliojiweka wakfu na kubatizwa, ambao ni kielelezo kizuri na watakaowaonyesha ndugu wenyeji shauku ya kidugu. Ndugu wenyeji nao watapata fursa nzuri za kuwakaribisha wageni kwa upendo na kuwaonyesha ukarimu wa kutoka moyoni. (Waebrania 13:1, 2) Hilo litatokeza “badilishano la kitia-moyo.” (Waroma 1:11, 12) Habari zaidi kuhusu mipango hii itatolewa na ofisi za tawi zitakazoombwa zitume wajumbe katika nchi hususa.

Katika nchi nyingi kutakuwa na makusanyiko ya wilaya ya siku tatu kama kawaida mnamo mwaka wa 2003. Kwa kukutanika pamoja, wote watakuwa na fursa ya ‘kusikia, kujifunza, na kutiwa moyo.’ (Kumbukumbu la Torati 31:12; 1 Wakorintho 14:31) Makusanyiko hayo yatawapa watu wa Mungu fursa ya ‘kuonja na kuona ya kuwa BWANA yu mwema.’ (Zaburi 34:8) Mishonari watakuwepo, na baadhi yao watakuwa na sehemu katika programu kwenye makusanyiko yote ya kimataifa, na vilevile kwenye makusanyiko mengi ya wilaya.

Mwaka huu wa 2002, tunafurahia Makusanyiko ya Wilaya ya “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii” yanayotuchochea kuhubiri hata zaidi. Tunapoendelea kufanya hivyo, bila shaka tutakuwa na hamu nyingi hata zaidi ya kujua mambo ambayo Yehova ametuandalia mwaka ujao. Hilo litatusaidia ‘tufulize kulinda, kuwa macho, na kujithibitisha kuwa tayari’ tunapofikiria nyakati hizi hatari na muhimu.—Mathayo 24:42-44.