Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwabudu Mungu “Katika Roho”

Mwabudu Mungu “Katika Roho”

Mwabudu Mungu “Katika Roho”

“Basi, mtamlinganisha Mungu na nani? Au mtamfananisha na mfano [“sanamu,” NW] wa aina gani?” ISAYA 40:18

LABDA unaamini kabisa kwamba kutumia sanamu za kuchorwa kunakubalika katika kumwabudu Mungu. Huenda ukaona kwamba sanamu hizo zinaweza kuboresha uhusiano wako na Msikiaji wa sala, ambaye anaweza kufikiriwa kwamba hana utu kwa kuwa haonekani.

Lakini je, sisi tu huru kabisa kuamua jinsi tutakavyomwabudu Mungu? Je, si Mungu ndiye mwenye mamlaka ya kuamua njia inayokubalika na isiyokubalika? Yesu alieleza maoni ya Mungu kuhusu jambo hilo aliposema: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” (Yohana 14:6) * Maneno hayo yanaonyesha kwamba hatupaswi kutumia sanamu za kuchorwa au vitu vingine vitakatifu katika ibada.

Naam, kuna ibada fulani hususa ambayo Yehova Mungu hukubali. Ibada ipi? Katika pindi nyingine, Yesu alisema hivi: “Saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.”—Yohana 4:23, 24.

Je, Mungu ambaye “ni roho” anaweza kuwakilishwa na sanamu? La. Hata sanamu ya kuchorwa iwe nzuri namna gani, haiwezi kuufikia utukufu wa Mungu. Kwa hiyo sanamu inayosemekana inamwakilisha Mungu haiwezi kuonyesha kikweli jinsi alivyo. (Waroma 1:22, 23) Je, mtu anaweza kuwa ‘anaabudu katika kweli’ ikiwa anamwabudu Mungu kupitia picha fulani iliyochorwa na binadamu?

Fundisho la Biblia Lililo Wazi

Sheria ya Mungu ilikataza kutengeneza sanamu kwa ajili ya ibada. Amri ya pili katika zile Amri Kumi inasema: “Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu chochote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia.” (Kutoka 20:4, 5) Pia Maandiko ya Kikristo yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu yanaamuru hivi: “Ikimbieni ibada ya sanamu.”—1 Wakorintho 10:14.

Kwa kweli, wengi husisitiza kwamba hawaabudu sanamu wanapozitumia katika ibada. Kwa mfano, mara nyingi Wakristo wa Kanisa la Othodoksi husema kwamba hawaabudu sanamu za kuchorwa ambazo wao huzisujudia, kuzipigia magoti, na kusali mbele yake. Kasisi mmoja wa Kanisa la Othodoksi aliandika: “Sisi hutukuza sanamu hizo kwa sababu ni takatifu, na kwa sababu tunaheshimu yule zinayemwakilisha.”

Hata hivyo, swali linabaki: Je, Mungu hukubali sanamu za kuchorwa zitumiwe kwa kusudi la kumtukuza? Biblia haisemi tunapaswa kufanya hivyo. Waisraeli walipotengeneza sanamu ya ndama, wakidai eti walikusudia kumwabudu Yehova, yeye alikataa kabisa ibada hiyo na kusema kwamba walikuwa wameasi imani.—Kutoka 32:4-7.

Hatari Iliyofichika

Ni hatari kutumia sanamu katika ibada. Huenda kufanya hivyo kukawashawishi watu waanze kuabudu sanamu inayosemekana inamwakilisha Mungu badala ya kumwabudu Mungu mwenyewe. Yaani, wanaifanya sanamu hiyo kuwa kitu cha kuabudiwa.

Vitu kadhaa vilianza kuabudiwa katika siku za Waisraeli. Kwa mfano, Musa alitengeneza nyoka ya shaba wakati Waisraeli walipokuwa wakisafiri nyikani. Mwanzoni, mfano huo wa nyoka ulikuwa wa kuponya. Wale walioadhibiwa kwa kuumwa na nyoka wangetazama nyoka hiyo ya shaba na Mungu angewasaidia. Lakini inaonekana kwamba baada ya Waisraeli kuingia katika Bara Lililoahidiwa, waligeuza nyoka hiyo ya shaba kuwa sanamu ya kuabudiwa kana kwamba nyoka yenyewe ilikuwa na uwezo wa kuponya. Waliichomea uvumba na hata kuipa jina, Nehushtani.—Hesabu 21:8, 9; 2 Wafalme 18:4.

Waisraeli pia walijaribu kutumia sanduku la agano kama kifaa cha uchawi dhidi ya maadui wao, lakini wakashindwa vibaya. (1 Samweli 4:3, 4; 5:11) Katika siku za Yeremia, raia wa Yerusalemu walijali zaidi hekalu kuliko walivyojali ibada ya Mungu iliyofanywa humo hekaluni.—Yeremia 7:12-15.

Leo watu wengi bado wana maelekeo ya kuabudu vitu badala ya kumwabudu Mungu. Mtafiti aitwaye Vitalij Ivanovich Petrenko alisema: ‘Mtu anapoanza kuabudu sanamu ya kuchorwa, anakabiliwa na hatari ya kuwa mwabudu sanamu. Ni wazi kwamba kuabudu vitu ni zoea la kipagani ambalo limegeuzwa kuwa ibada ya sanamu za kuchorwa kupitia mafundisho yanayopendwa na wengi.’ Vivyo hivyo, kasisi wa Kanisa la Othodoksi la Ugiriki Demetrios Constantelos anasema hivi katika kitabu chake Understanding the Greek Orthodox Church: ‘Inawezekana kwa Mkristo kuanza kuabudu sanamu ya kuchora.’

Yale madai kwamba sanamu za kuchorwa husaidia tu watu katika ibada yanatiliwa shaka sana. Kwa nini? Je, si kweli kwamba sanamu fulani za Maria au za “watakatifu” zinaonwa kuwa zinastahili ujitoaji zaidi na zina uwezo mkubwa zaidi ya sanamu nyingine za watu haohao waliokufa zamani? Kwa mfano, huko Tínos, Ugiriki, kuna wafuasi fulani wa Kanisa la Othodoksi ambao wamejitoa kwa sanamu moja ya kuchorwa ya Maria, na kuna wengine ambao wamejitoa kwa sanamu nyingine ya Maria huko Soumela, kaskazini mwa Ugiriki. Vikundi hivyo viwili vinaamini kwamba sanamu yao ndiyo ina uwezo zaidi wa kufanya miujiza, ingawa sanamu zote mbili zinawakilisha mtu yuleyule aliyekufa zamani. Hivyo, kihalisi watu huona kwamba sanamu fulani za kuchorwa zina nguvu nao huziabudu.

Kusali kwa “Watakatifu” au Maria?

Namna gani kuabudu watu fulani kama Maria au “watakatifu”? Yesu alipojaribiwa na Shetani, alimjibu hivi akitumia andiko la Kumbukumbu la Torati 6:13: “Uabudu Bwana Mungu wako, umutumikie yeye peke yake.” (Mathayo 4:10, Zaire Swahili Bible) Baadaye alisema kwamba waabudu wa kweli watamwabudu “Baba,” peke yake. (Yohana 4:23) Kwa kujua hayo, malaika mmoja alimkemea mtume Yohana aliyejaribu kumwabudu, akisema: “Usifanye hivi, . . . abudu Mungu.”—Ufunuo 22:9, ZSB.

Je, inafaa kusali kwa Maria, mama ya Yesu, au kusali kwa “watakatifu” fulani, ukiwataka wakuombee kwa Mungu? Biblia inatoa jibu lililo wazi kabisa: “Mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, mwanadamu Kristo Yesu.”—1 Timotheo 2:5.

Linda Uhusiano Wako Pamoja na Mungu

Kutumia sanamu za kuchorwa katika ibada, ni kinyume cha mafundisho ya Biblia na hakuwezi kuwasaidia watu kupata kibali cha Mungu au kupata wokovu. Kinyume cha hilo, Yesu alisema kwamba tunaweza kupata uhai wa milele kwa kumjua Mungu wa pekee wa kweli, kufahamu utu wake usio na kifani, na pia makusudi yake na jinsi anavyoshughulika na wanadamu. (Yohana 17:3) Sanamu za kuchorwa ambazo hazina uwezo wa kuona, kuhisi, au hata kuongea haziwezi kumsaidia mtu amjue Mungu ili kumwabudu kwa njia inayokubalika. (Zaburi 115:4-8) Tunaweza kujifunza mambo muhimu sana kumhusu Mungu wa pekee wa kweli kupitia Neno lake, Biblia.

Kuabudu sanamu za kuchorwa hakutunufaishi, bali kunaweza kuleta hatari ya kiroho. Namna gani? Kwanza kabisa jambo hilo linaweza kuharibu uhusiano wetu na Yehova. Kuhusu Waisraeli ‘waliomkasirisha kwa sanamu zenye kuchukiza,’ Mungu alitabiri hivi: “Nitaficha uso wangu.” (Kumbukumbu la Torati 32:16, 20The New American Bible) Ili kurudisha uhusiano wao pamoja na Mungu walihitaji ‘kutupa sanamu zao.’—Isaya 31:6, 7.

Kwa hiyo, ushauri huu wa Kimaandiko unafaa: “Watoto wadogo, jilindeni nafsi zenu na sanamu.”—1 Yohana 5:21.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Isipokuwa iwe imeonyeshwa vingine, Maandiko yote yamenukuliwa katika Biblia ya Union Version.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Watu Waliosaidiwa Kuabudu “Katika Roho”

Olivera alikuwa mfuasi mwenye bidii wa Kanisa la Othodoksi la Albania. Wakati nchi hiyo ilipopiga dini marufuku mwaka wa 1967, Olivera aliendelea kuabudu kisiri. Alitumia malipo yake kidogo ya uzeeni kununua uvumba, mishumaa, na sanamu za kuchorwa za dhahabu na fedha. Alificha vitu hivyo kitandani mwake na mara nyingi alilala kwenye kiti fulani kilichokuwa karibu na kitanda chake kwa kuwa hakutaka vitu hivyo vionekane au viibwe. Alipotembelewa na Mashahidi wa Yehova mapema miaka ya 1990, Olivera alitambua kwamba ujumbe wao ulikuwa wa kweli na ulitoka katika Biblia. Alielewa maana ya kuabudu “katika roho” kulingana na Biblia, na akajifunza maoni ya Mungu kuhusu kutumia sanamu za kuchorwa. (Yohana 4:24) Shahidi aliyejifunza Biblia pamoja naye aligundua kwamba idadi ya sanamu zilizokuwa nyumbani kwa Olivera ilizidi kupungua kila mara alipomtembelea. Mwishowe Olivera hakuwa na sanamu yoyote. Baada ya kubatizwa, Olivera alisema: “Leo, badala ya kuwa na sanamu za kuchorwa zisizoweza kunisaidia, nina roho takatifu ya Yehova. Ninashukuru sana kwa kuwa ninaweza kupata roho yake bila kutumia sanamu.”

Athena, kutoka kisiwa cha Lesbos, huko Ugiriki, alikuwa mfuasi mwenye bidii sana wa Kanisa la Othodoksi. Alikuwa mmoja wa wanakwaya na alifuata mapokeo ya kanisa kwa makini sana kutia ndani kuabudu sanamu za kuchorwa. Mashahidi wa Yehova walimsaidia Athena kufahamu kwamba kuna mambo fulani aliyofunzwa ambayo yalikuwa kinyume cha Biblia. Mambo hayo yalitia ndani kuabudu sanamu za kuchorwa na misalaba. Athena aliamua kufanya uchunguzi wake mwenyewe kuhusu chanzo cha sanamu hizo. Baada ya kuchunguza kwa kina katika vitabu fulani vinavyozungumzia sanamu, alipata uthibitisho wa kwamba chanzo cha sanamu hizo si cha Kikristo. Kwa kuchochewa na tamaa ya kumwabudu Mungu “katika roho,” Athena aliharibu sanamu zake, ingawa zilikuwa za pesa nyingi. Hata hivyo, Athena hakujali hasara aliyopata mradi tu angeweza kumwabudu Mungu katika njia inayokubalika na safi kiroho.—Matendo 19:19.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Je, Sanamu za Kuchorwa Ni Kazi ya Sanaa Tu?

Katika miaka ya hivi majuzi, sanamu za kuchorwa za Kanisa la Othodoksi zimekusanywa kote ulimwenguni. Wanaokusanya sanamu hizo huziona kuwa vitu vya sanaa tu vinavyoonyesha utamaduni wa Byzantium wala hawavioni kuwa vitu vitakatifu vya kidini. Ni kawaida kuona mtu asiyeamini kuwa kuna Mungu amepamba nyumba au ofisi yake kwa sanamu hizo.

Hata hivyo, Wakristo wa kweli hawasahau kusudi kuu la sanamu ambalo ni ibada. Ingawa Wakristo hawawakatazi wengine kuweka sanamu, wao hawaziweki hata kama ni kwa kusudi la kuzikusanya tu. Jambo hilo linapatana na kanuni inayopatikana kwenye andiko la Kumbukumbu la Torati 7:26: “Machukizo [sanamu zinazotumiwa katika ibada] usitie ndani ya nyumba yako, usije wewe kuwa kitu cha haramu mfano wake; ukichukie kabisa, na kukikataa kabisa.”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mungu hakukubali sanamu zitumiwe katika ibada

[Picha katika ukurasa wa 8]

Ujuzi wa Biblia hutusaidia kumwabudu Mungu katika roho