Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naimarishwa na Udugu Wetu wa Ulimwenguni Pote

Naimarishwa na Udugu Wetu wa Ulimwenguni Pote

Simulizi la Maisha

Naimarishwa na Udugu Wetu wa Ulimwenguni Pote

LIMESIMULIWA NA THOMSON KANGALE

Katika Aprili 24, 1993, nilialikwa kuhudhuria programu ya kuwekwa wakfu kwa ofisi mpya ya tawi, ambayo ilikuwa na majengo 13, huko Lusaka, Zambia. Kwa kuwa ilikuwa vigumu kwangu kutembea, dada Mkristo ambaye alikuwa akitutembeza kwenye majengo hayo aliniuliza hivi kwa fadhili, “Ungependa nikubebee kiti ili uweze kupumzika mara kwa mara?” Mimi ni Mwafrika naye ni Mzungu, lakini hakujali hilo. Nilimshukuru sana, kwa kuwa fadhili yake iliniwezesha kutembea katika majengo yote ya ofisi ya tawi.

KWA miaka mingi, mambo kama hayo yamechangamsha moyo wangu, yakihakikisha usadikisho wangu kwamba miongoni mwa ushirika wa Kikristo wa Mashahidi wa Yehova, kuna upendo ambao Kristo alisema ungetambulisha wafuasi wake wa kweli. (Yohana 13:35; 1 Petro 2:17) Acheni niwaambie jinsi nilivyokuja kujuana na Wakristo hao mwaka wa 1931, mwaka ambao walitangaza tamaa yao ya kutaka wajulikane kwa jina linalotoka katika Biblia Mashahidi wa Yehova.—Isaya 43:12.

Huduma ya Mapema Katika Afrika

Katika Novemba 1931, nilikuwa na umri wa miaka 22 na nilikuwa nikiishi Kitwe, katika eneo la Copperbelt huko Northern Rhodesia (ambayo sasa ni Zambia). Rafiki yangu mmoja ambaye nilikuwa nikicheza naye kandanda alinijulisha kwa Mashahidi. Nilihudhuria baadhi ya mikutano yao na nikaandikia ofisi ya tawi huko Cape Town, Afrika Kusini, nikiomba kichapo cha kujifunzia Biblia, The Harp of God. * Kitabu hicho kilikuwa cha Kiingereza, nami sikukielewa kwa kuwa sikujua lugha hiyo vizuri.

Eneo la Copperbelt, lililoko karibu kilometa 240 kusini-magharibi ya Ziwa Bangweulu, karibu na eneo nilimokulia, lilikuwa na wafanyakazi wengi kutoka mikoa mingine walioajiriwa kufanya kazi katika migodi ya shaba. Vikundi kadhaa vya Mashahidi vilikutana huko kwa ukawaida kwa ajili ya funzo la Biblia. Baada ya muda fulani, nilihamia Kitwe katika mji ulioko karibu na Ndola kisha nikaanza kushirikiana na kikundi cha Mashahidi huko. Wakati huo, nilikuwa kapteni wa timu ya kandanda iliyoitwa Prince of Wales. Pia nilikuwa mfanyakazi wa nyumbani kwa meneja Mzungu wa Shirika la Maziwa ya Afrika, kampuni ambayo ilikuwa na maduka mengi mbalimbali huko Afrika ya kati.

Sikusoma sana, kwa hiyo nilijua Kiingereza kidogo nilichojifunza kutoka kwa Wazungu niliokuwa nikiwafanyia kazi. Hata hivyo, nilikuwa na tamaa ya kuendelea kujifunza katika shule huko Plumtree, Southern Rhodesia (ambayo sasa ni Zimbabwe). Hata hivyo, katika kipindi hicho, niliandikia ofisi ya tawi ya Cape Town kwa mara ya pili. Niliwajulisha kwamba nimepokea kitabu The Harp of God na nilitaka kumtumikia Yehova kwa wakati wote.

Nilishangaa kupokea jibu lao, ambalo lilisema: “Twakupongeza kwa tamaa yako ya kumtumikia Yehova. Tungependa kukutia moyo usali kuhusu jambo hilo, na Yehova atakusaidia uelewe kweli zaidi, na kukusaidia umtumikie.” Baada ya kusoma barua hiyo mara kadhaa, niliuliza Mashahidi kadhaa jambo ambalo ningefanya. Walisema hivi: “Ikiwa kweli una tamaa ya kumtumikia Yehova, anza sasa.”

Nilisali kuhusu jambo hilo kwa juma zima na hatimaye nikaamua kuacha elimu yangu ya kilimwengu na kuendelea na funzo langu la Biblia pamoja na Mashahidi. Mwaka uliofuata, katika Januari 1932, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova Mungu kwa ubatizo wa maji. Baada ya kuhama kutoka Ndola kuelekea jiji la karibu la Luanshya, nilikutana na Jeanette, mwamini mwenzangu, na tukaoana Septemba 1934. Tulipooana, tayari Jeanette alikuwa na mwana na binti.

Hatua kwa hatua nikafanya maendeleo ya kiroho na mwaka wa 1937, nikaanza utumishi wa wakati wote. Muda mfupi baada ya hapo nikawa mhudumu anayesafiri ambaye sasa anaitwa mwangalizi wa mzunguko. Waangalizi wasafirio hutembelea makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ili kuyaimarisha kiroho.

Kuhubiri Miaka ya Mapema

Katika Januari 1938, nilielekezwa kwa chifu Mwafrika aitwaye Sokontwe, ambaye alikuwa ameomba Mashahidi wa Yehova wamtembelee. Niliendesha baiskeli kwa siku mbili ili kufika huko. Nilipomwambia kwamba nilikuwa nimetumwa kumtembelea kwa sababu ya barua yake aliyoandikia ofisi yetu ya tawi ya Cape Town, alishukuru sana.

Niliwatembelea watu wake nyumba hadi nyumba na kuwaalika kwenye insaka (kibanda cha watu wote). Walipokusanyika niliwatolea hotuba. Hiyo ilitokeza mafunzo mengi ya Biblia. Chifu wa kijiji hicho na karani wake walikuwa wa kwanza kuwa waangalizi wa makutaniko huko. Leo, kuna makutaniko zaidi ya 50 katika eneo hilo, ambalo sasa lajulikana kama wilaya ya Samfya.

Kuanzia mwaka wa 1942 hadi 1947, nilitumikia katika eneo la karibu na Ziwa Bangweulu. Nilikaa siku kumi katika kila kutaniko. Kwa kuwa wafanyakazi wa mavuno ya kiroho walikuwa wachache, tulihisi tu kama vile Bwana wetu Yesu Kristo, alivyohisi aliposema hivi: “Ndiyo, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, ombeni Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mathayo 9:36-38) Katika siku hizo za mapema, haikuwa rahisi kusafiri, kwa hiyo mara nyingi Jeanette alibaki Luanshya na watoto nilipotembelea makutaniko. Wakati huo, Jeanette na mimi tulipata watoto wengine wawili, lakini mmoja wao akafa akiwa na umri wa miezi kumi.

Siku hizo, kulikuwa na magari machache tu, na pia hakukuwa na barabara nyingi. Siku moja, nilianza safari ya zaidi ya kilometa 200 nikiendesha baiskeli ya Jeanette. Nyakati nyingine nilipolazimika kuvuka mto mdogo, niliibeba baiskeli hiyo kwenye mabega yangu, nikaishikilia kwa mkono mmoja na kuogelea kwa mkono ule mwingine. Idadi ya Mashahidi iliongezeka sana katika Luanshya, na mwaka wa 1946, watu 1,850 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo.

Kazi Yetu Yapingwa

Katika pindi moja wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu, mkuu wa wilaya huko Kawambwa aliniita na kuniambia: “Nataka uache kutumia vitabu vya Watch Tower Society kwa sababu sasa vimepigwa marufuku. Lakini naweza kukupa vichapo unavyoweza kutumia ili kuandika vitabu vingine vya kutumia katika kazi yako.”

Nikamjibu “Nimeridhika na vichapo tulivyo navyo na sihitaji vingine.”

“Wewe hujui Wamarekani. Watakupoteza,” akasema (vichapo vyetu vilikuwa vikichapiwa Marekani).

“La, wale ninaoshirikiana nao hawatanipoteza,” nikamjibu.

Kisha akaniuliza: “Huwezi kutia moyo makutaniko yenu yatoe michango ya kusaidia vitani kama vile dini nyingine zinavyofanya?”

Nikamjibu, “Hiyo ni kazi ya watumishi wa serikali.”

Akasema, “Kwa nini usiende nyumbani na ufikirie kuhusu jambo hilo?”

Nilimwambia hivi, “Kwenye Kutoka 20:13 na 2 Timotheo 2:24, Biblia hutuamuru tusiue wala kupigana.”

Ingawa niliruhusiwa kuondoka, baadaye niliitwa na mkuu wa wilaya huko Fort Rosebery, mji ambao sasa unaitwa Mansa. “Nimekuita hapa kukujulisha kwamba serikali imepiga marufuku vitabu vyenu,” akasema.

Nikamwambia, “Naam. Nimesikia jambo hilo.”

“Kwa hiyo uende kwenye makutaniko yenu yote na uwaambie watu mnaoabudu pamoja walete vitabu vyote hapa. Umesikia?”

“Hiyo si kazi yangu,” nikamjibu. “Ni kazi ya watumishi wa serikali.”

Mkutano Usiotazamiwa Waleta Matokeo Mazuri

Baada ya vita, tuliendelea kuhubiri. Mwaka wa 1947, nilikuwa tu nimetoka kumaliza kutumikia kutaniko moja kwenye kijiji cha Mwanza nilipouliza ni wapi ningenunua chai. Nilielekezwa kwenye nyumba ya Bwa. Nkonde, ambapo kulikuwa na mkahawa. Bwa. Nkonde na mke wake walinikaribisha kwa uchangamfu. Nilipokuwa nikinywa chai yangu, nilimwuliza Bwa. Nkonde kama angependa kusoma sura iliyokuwa ikizungumza juu ya “Hell, a Place of Rest in Hope” katika kitabu “Let God Be True.”

“Kwa hiyo waielewa hell kuwa nini?” nikamwuliza baada ya kumaliza chai. Akishangazwa na yale aliyosoma, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi na baadaye akabatizwa pamoja na mke wake. Ijapokuwa hakuendelea kuwa Shahidi, mke wake na watoto wake kadhaa waliendelea kuwa Mashahidi. Hata, mmoja wa watoto wake Pilney, angali anatumikia katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Zambia. Na ijapokuwa mama ya Pilney sasa ni mzee sana, angali Shahidi mwaminifu.

Nakaa Afrika Mashariki kwa Muda Mfupi

Ofisi yetu ya tawi huko Northern Rhodesia, ambayo ilianzishwa mapema mwaka wa 1948 huko Lusaka, ilinipa mgawo wa kwenda Tanganyika (ambayo sasa ni Tanzania). Shahidi mwingine aliandamana nami pamoja na mke wangu kwenye safari yetu tulipotembea katika eneo lenye milima mingi kwa miguu. Safari hiyo ilichukua muda wa siku tatu nayo ilikuwa yenye kuchosha sana. Nilibeba vifurushi vya vitabu, mke wangu akabeba nguo zetu, na yule Shahidi mwingine akabeba matandiko yetu.

Tulipofika Mbeya mwezi wa Machi 1948, kulikuwa na kazi nyingi ya kusaidia akina ndugu wafanye marekebisho ili wajipatanishe kabisa na mafundisho ya Biblia. Kwanza, katika eneo hilo tulijulikana kama watu wa Watchtower. Ijapokuwa jina Mashahidi wa Yehova lilikuwa limekubaliwa na akina ndugu, halikuwa limejulishwa hadharani. Kwa kuongezea, Mashahidi fulani walihitaji kuacha desturi kadhaa zilizohusiana na kuheshimu wafu. Lakini labda rekebisho ambalo lilikuwa gumu zaidi kwa wengi lilikuwa kuhalalisha ndoa zao ili ziheshimike miongoni mwa watu wote.—Waebrania 13:4.

Baadaye, nilikuwa na pendeleo la kutumikia maeneo mengine ya Afrika Mashariki kutia ndani Uganda. Nilitumia majuma sita huko Entebbe na Kampala, ambapo watu wengi walisaidiwa kupata ujuzi wa kweli za Biblia.

Mwaliko wa Kwenda New York City

Baada ya kutumikia huko Uganda kwa muda fulani, mapema mwaka wa 1956 nilifika Dar es Salaam, jiji kuu la Tanganyika. Barua kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa ikiningoja. Ilikuwa na maagizo ya kuniarifu nianze kujitayarisha kwenda New York ili kuhudhuria kusanyiko la kimataifa ambalo lingefanywa kuanzia Julai 27 hadi Agosti 3, 1958. Nilisisimuka sana.

Wakati ulipowadia, mimi na mwangalizi mwingine anayesafiri, Luka Mwango, tulisafiri kwa ndege kutoka Ndola hadi Salisbury (ambalo sasa ni Harare), Southern Rhodesia, kisha hadi Nairobi, Kenya. Kutoka huko tulisafiri hadi London, Uingereza, ambako tulipokewa kwa uchangamfu. Tulipokwenda kulala usiku huo, tulisisimuka na tukaendelea kuongea jinsi sisi Waafrika tulivyopokewa kwa ukarimu na Wazungu. Tulitiwa moyo kwelikweli na jambo hilo.

Hatimaye, tulifika New York, mahali ambapo kusanyiko lilifanyiwa. Siku moja, wakati wa kusanyiko, nilitoa ripoti juu ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika Northern Rhodesia. Siku hiyo wahudhuriaji 200,000 walikusanyika katika uwanja wa Polo Grounds na Yankee Stadium huko New York City. Sikuweza kulala usiku huo kwa sababu ya kufikiria jinsi nilivyofurahia pendeleo hilo kubwa.

Upesi kusanyiko likaisha nasi tukarudi nyumbani. Tulipokuwa tukirudi nyumbani, tulifurahia tena ukarimu wenye upendo wa ndugu na dada zetu wa Uingereza. Muungano wa watu wa Yehova wajapokuwa wametoka katika jamii gani au taifa gani, ulionyeshwa kwa njia isiyoweza kusahaulika katika safari hiyo!

Naendelea na Utumishi Licha ya Majaribu

Katika mwaka wa 1967, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa wilaya—mhudumu ambaye husafiri kutoka mzunguko hadi mzunguko. Kufikia wakati huo idadi ya Mashahidi katika Zambia iliongezeka hadi kufikia 35,000. Baadaye, kwa sababu ya hali mbaya ya afya, nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko tena huko Copperbelt. Hatimaye, Jeanette alipata matatizo ya afya na akafa Desemba 1984 akiwa mwaminifu kwa Yehova.

Baada ya kifo chake, niliumia kihisia sana wakati watu wa ukoo wa Jeanette wasioamini waliponilaumu kuwa nimesababisha kifo chake kwa kuwa mchawi. Lakini wengine ambao walijua ugonjwa wa Jeanette na waliokuwa wameongea na daktari wake waliwaeleza jamaa hao ukweli wa mambo. Kisha likaja jaribu jingine. Watu fulani wa ukoo walitaka nifuate desturi ya kienyeji inayoitwa ukupyanika. Katika eneo ninalotoka, desturi hii hutaka mwenzi wa yule aliyekufa, afanye ngono pamoja na mtu wa ukoo wa karibu wa mwenzi wake. Bila shaka nilikataa.

Hatimaye, msongo kutoka kwa watu hao wa ukoo ukakoma. Nilishukuru kwamba Yehova alinisaidia kusimama imara. Mwezi mmoja baada ya mazishi ya mke wangu, ndugu mmoja alinijia akisema: “Ndugu Kangale, ulitutia moyo sana wakati mke wako alipokufa kwa sababu hukukubali hata desturi moja ya kienyeji. Twataka kukushukuru sana.”

Mavuno ya Ajabu

Sasa imetimia miaka 65 tangu nilipoanza huduma yangu ya wakati wote nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Imekuwa shangwe kama nini miaka hii yote kuona mamia ya makutaniko yakianzishwa na Majumba ya Ufalme mengi yakijengwa katika maeneo ambayo nilitumikia nikiwa mwangalizi asafiriye wakati mmoja! Tulikuwa Mashahidi wapatao 2,800 mwaka wa 1943, na sasa tumeongezeka hadi kuwa watangazaji wa Ufalme zaidi ya 122,000 nchini Zambia. Mwaka jana zaidi ya watu 514,000 walihudhuria Ukumbusho katika nchi hii, ambayo ina idadi ya watu isiyozidi milioni 11.

Kwa sasa, Yehova ananitunza. Ninapohitaji matibabu, ndugu Mkristo hunipeleka hospitalini. Makutaniko bado hunialika nitoe hotuba za watu wote, na hilo hunitia moyo sana. Kutaniko ninaloshirikiana nalo limepanga kwamba akina dada Wakristo wawe na zamu za kusafisha nyumba yangu, na akina ndugu wanajitolea kuandamana nami kwenye mikutano kila juma. Najua kwamba singeweza kufurahia utunzi huo kama singekuwa ninamtumikia Yehova. Namshukuru sana kwa kuendelea kunitumia katika huduma ya wakati wote na kwa madaraka mengi ambayo nimepewa nitimize hadi sasa.

Macho yangu hayaoni vizuri, na ninapokwenda kwenye Jumba la Ufalme, lazima nipumzike mara nyingi. Mkoba wangu waonekana kuwa mzito siku hizi, kwa hiyo ninaufanya uwe mwepesi kwa kupunguza vitabu ambavyo sivihitaji mkutanoni. Huduma yangu ya shambani hasa ni kuongoza mafunzo ya Biblia na wale ambao wanakuja nyumbani kwangu. Lakini nina shangwe kama nini kukumbuka miaka ya hapo nyuma na kuweza kutafakari ukuzi wa ajabu ambao umetokea! Nimetumikia katika shamba ambalo maneno ya Yehova yanayopatikana kwenye andiko la Isaya 60:22 yana utimizo mkubwa. Andiko hilo lasema: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, BWANA, nitayahimiza hayo wakati wake.” Kwa kweli, nimeishi kuona utimizo huo ukitokea Zambia na pia ulimwenguni pote. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.

^ fu. 50 Kwa kusikitisha, Ndugu Kangale alidhoofika, na akafa akiwa mwaminifu wakati simulizi hili lilipokuwa likitayarishwa.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Thomson na ofisi ya tawi ya Zambia ikionyeshwa nyuma

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ofisi ya tawi ya Zambia leo