Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sanamu za Kuchorwa—Zilianza Kutumiwa Zamani

Sanamu za Kuchorwa—Zilianza Kutumiwa Zamani

Sanamu za Kuchorwa—Zilianza Kutumiwa Zamani

“Sanamu za kuchorwa hutusaidia kukaribia wema na utakatifu wa Mungu na Watakatifu wake.”ASKOFU MKUU WA KANISA LA OTHODOKSI LA UGIRIKI HUKO AUSTRALIA

NI SIKU yenye joto kali sana ya mwezi wa Agosti na jua linaangaza kwenye ngazi zinazoelekea kwenye nyumba ya watawa ya “Mama Mtakatifu Zaidi wa Mungu,” kwenye kisiwa cha Tínos, katika Bahari ya Aegea. Joto hilo kali halipunguzi bidii ya wahiji zaidi ya 25,000 wa Kanisa la Othodoksi la Ugiriki ambao wanatembea polepole wakijitahidi kuifikia sanamu ya kuchorwa iliyopambwa sana ya mama ya Yesu.

Msichana mdogo aliyelemaa na mwenye maumivu na mfadhaiko atembea kwa magoti yanayovuja damu nyingi. Karibu naye kuna mwanamke mzee aliyesafiri kutoka mbali na ingawa amechoka, yeye anaendelea tu kukokota miguu yake. Mwanamume wa makamo atoa jasho jingi anapojikakamua kwa hamu na kwa wasiwasi kupita katikati ya umati unaosukumana. Wote wanataka kuifikia sanamu hiyo ya Maria ili kuibusu na kuisujudia.

Bila shaka watu hawa wenye kushikilia dini sana wanataka kumwabudu Mungu kwa unyofu. Hata hivyo, ni wangapi kati yao wanaojua kwamba ibada ya sanamu za kuchorwa ilianzishwa na wapagani karne nyingi kabla ya Ukristo?

Kuenea kwa Sanamu za Kuchorwa

Katika maeneo ambako watu wanafuata imani ya Kiothodoksi, sanamu za kuchorwa zinapatikana kila mahali. Sanamu za Yesu, Maria, na “watakatifu” wengine wengi huonwa kuwa muhimu sana katika makanisa. Mara nyingi watu wa dini hutukuza sanamu hizo kwa kuzibusu, kuchoma uvumba, na kuwasha mishumaa. Zaidi ya hayo, karibu wafuasi wote wa Kanisa la Othodoksi wametenga mahali fulani pa kuweka sanamu na kutolea sala katika nyumba zao. Ni jambo la kawaida kwa wafuasi wa Kanisa la Othodoksi kusema kwamba kuabudu sanamu huwafanya wawe karibu na Mungu. Wengi huamini kwamba Mungu amezipa sanamu hizo utakatifu na uwezo wa kufanya miujiza.

Yaelekea waumini hao wangeshangaa kujua kwamba Wakristo wa karne ya kwanza hawakutumia sanamu za kuchorwa katika ibada yao. Kitabu Byzantium kinasema: ‘Wakristo wa mapema walichukia kabisa kuabudu picha za watakatifu. Waliwaiga wafuasi wa dini ya Kiyahudi ambao walichukia sana ibada ya sanamu.’ Kitabu hicho kinasema: ‘Kuanzia Karne ya Tano na kuendelea sanamu za kuchorwa ziliabudiwa sana hadharani na faraghani.’ Ikiwa Wakristo wa karne ya kwanza hawakuabudu sanamu hizo, basi zoea hilo lilianzia wapi?

Chanzo cha Sanamu za Kuchorwa

Mtafiti aitwaye Vitalij Ivanovich Petrenko aliandika: “Ibada ya sanamu na pia desturi zinazoambatana na zoea hilo zilianza kabla ya Ukristo na ‘zilianzishwa na wapagani.’” Wanahistoria wengi hukubaliana naye na kusema kwamba ibada ya sanamu za kuchorwa ilianza katika dini za kale za Babiloni, Misri, na Ugiriki. Kwa mfano, katika Ugiriki ya kale watu waliamini kwamba sanamu zilikuwa na uwezo kama wa Mungu. Wengine walifikiri kwamba baadhi ya sanamu hizo hazikutengenezwa na wanadamu bali zilishuka kutoka mbinguni. Wakati wa misherehekeo ya kipekee watu waliandamana jijini wakiwa wamebeba sanamu hizo na kuzitolea dhabihu. ‘Watu wa kidini waliziona sanamu hizo kuwa miungu ingawa jitihada zilikuwa zimefanywa kuwaeleza tofauti kati ya mungu na sanamu,’ akasema Petrenko.

Imani na mazoea hayo yalipenyaje katika Ukristo? Mtafiti huyo alisema kwamba, karne kadhaa baada ya kifo cha mitume wa Kristo, “imani ya Kikristo, hasa huko Misri, ilikabiliwa na ‘imani mbalimbali za kipagani’ ambazo zilitokana na desturi na imani za Wamisri, Wagiriki, Wayahudi, na watu wa Mashariki na Waroma. Imani hizo zilichanganywa na mafundisho na desturi za Kikristo.’” Kwa sababu hiyo, ‘watengenezaji stadi wa sanamu za Kikristo walianza kuchanganya mafundisho ya dini mbalimbali kwa kutengeneza sanamu ambazo walizifanya zionekane kama za Kikristo ingawa bado zilikuwa za kipagani.’

Muda si muda watu walianza kuabudu sanamu hizo faraghani na hadharani. Katika kitabu The Age of Faith mwanahistoria Will Durant anaeleza jinsi jambo hilo lilivyotukia kwa kusema: ‘Idadi ya watakatifu wenye kuabudiwa ilipoongezeka, ilihitajika kuwatambulisha na kuwakumbuka. Kwa hiyo picha zilichorwa kwa wingi kuwakilisha watakatifu hao kutia ndani na Maria. Sanamu za Kristo zenye sura ya kuwaziwa tu pamoja na msalaba wake zilianza kuabudiwa. Watu wa kawaida walitumia sanamu hizo kama hirizi. Watu walianza kufikiri kwamba sanamu na picha za watakatifu wa zamani zingepasa kutukuzwa. Hata walianza kuziabudu kwa kuzisujudu, kuzibusu, kuwasha mishumaa, na kuchoma uvumba. Walizipamba kwa maua na kuzitazamia zifanye miujiza. Mara nyingi Mababa na vilevile washiriki wa mabaraza ya Kanisa waliwaeleza watu kwamba sanamu hizo hazikuwa miungu bali ziliwakumbusha tu miungu yao, lakini watu hawakujali.’

Leo, huenda watu wengi wanaotumia sanamu hizo za kuchorwa wakasema kwamba wanaziheshimu tu, hawaziabudu. Huenda wakasema kwamba sanamu hizo zinafaa na huwasaidia sana kumwabudu Mungu. Labda hata wewe una maoni kama hayo. Lakini swali ni, Mungu ana maoni gani kuhusu sanamu za kuchorwa? Je, huenda ikawa kutukuza sanamu hizo ni sawa na kuziabudu? Je, mazoea hayo yanaweza kukuathiri bila kujua?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]

Sanamu za Kuchorwa Ni Nini?

Tofauti na sanamu za kuchongwa ambazo Wakatoliki hutumia sana katika ibada yao, kuna picha au sanamu za kuchorwa za Kristo, Maria, “watakatifu,” malaika, watu, na matukio fulani katika Biblia au katika historia ya Kanisa la Othodoksi. Kwa kawaida picha hizo huchorwa kwenye ubao unaoweza kubebeka.

Kulingana na Kanisa la Othodoksi “michoro hiyo ya Watakatifu ni tofauti na picha za wanadamu wa kawaida.” Pia, picha hizo zilichorwa bila kuonyesha kama vitu fulani vilikuwa mbali na vingine vilikuwa karibu. Kwa kawaida ‘michoro hiyo haina vivuli wala haionyeshi kama ni mchana au ni usiku.’ Pia inaaminiwa kwamba Mungu ‘anaweza kuwa ndani’ ya mbao na rangi ya picha hizo.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Matumizi ya sanamu yalitokana na wapagani

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

© AFP/CORBIS