Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utukufu wa Yehova Unaangazia Watu Wake

Utukufu wa Yehova Unaangazia Watu Wake

Utukufu wa Yehova Unaangazia Watu Wake

“BWANA mwenyewe atakuwa nuru yako ya milele.”—ISAYA 60:20.

1. Yehova anawabariki watu wake waaminifu jinsi gani?

“BWANA awaridhia watu wake, huwapamba [“huwaremba,” NW] wenye upole kwa wokovu.” (Zaburi 149:4) Hivyo ndivyo alivyosema mtunga-zaburi wa kale, na maneno yake yamethibitishwa kuwa ya kweli. Yehova huwatunza, kuwafanikisha, na kuwalinda watu wake walio waaminifu. Nyakati za kale aliwapa ushindi juu ya adui zao. Leo, anawasaidia kuwa wenye nguvu kiroho na kuwahakikishia kwamba watapata wokovu kupitia dhabihu ya Yesu. (Waroma 5:9) Anafanya hivyo kwa kuwa wanapendeza machoni pake.

2. Ijapokuwa watu wa Mungu hupata upinzani, wana uhakika gani?

2 Bila shaka, wale ‘wanaoishi kwa ujitoaji-kimungu’ katika ulimwengu wenye giza watapata upinzani. (2 Timotheo 3:12) Hata hivyo, Yehova anawaona wapinzani, naye anawaonya hivi: “Kila taifa na ufalme wa watu wasiotaka kukutumikia wataangamia; naam, mataifa hayo wataharibiwa kabisa.” (Isaya 60:12) Leo, Wakristo hupingwa kwa njia nyingi. Katika nchi fulani, wapinzani hujaribu kuzuia au kupiga marufuku ibada ambayo Wakristo wa kweli humtolea Yehova. Katika nchi nyingine, watu washupavu hushambulia waabudu wa Yehova na kuteketeza mali zao. Hata hivyo, kumbukeni kwamba tayari Yehova ameamua kile kitakachowapata wote wanaopinga mapenzi yake. Wapinzani watashindwa. Wale wanaopigana na Sayuni, kwa kuwapinga watoto wake duniani, hawatafanikiwa. Je, huo si uhakikishio wenye kutia moyo kutoka kwa Mungu wetu mkuu, Yehova?

Baraka Nyingi Zisizotarajiwa

3. Uzuri na mafanikio ya waabudu wa Yehova yalifananishwa na nini?

3 Katika siku za mwisho za ulimwengu huu, Yehova amewapa watu wake baraka nyingi zisizotarajiwa. Ameremba hasa mahali pake pa ibada na wale waliomo wanaoitwa kwa jina lake. Kulingana na unabii wa Isaya, anamwambia Sayuni hivi: “Utukufu wa Lebanoni utakujia wewe, mberoshi na mtidhari na mteashuri pamoja; ili kupapamba [“kuparemba,” NW] mahali pangu patakatifu, nami nitapatukuza mahali pa miguu yangu.” (Isaya 60:13) Milima iliyofunikwa kwa misitu inayositawi inavutia sana. Kwa hiyo, miti inayositawi ni mfano unaofaa wa uzuri na ufanisi wa waabudu wa Yehova.—Isaya 41:19; 55:13.

4. “Patakatifu” na “mahali pa miguu [ya Yehova]” panamaanisha nini, na pamerembwa kwa njia gani?

4 Mahali “patakatifu” na “mahali pa miguu [ya Yehova]” panapotajwa katika Isaya 60:13 panamaanisha nini? Panamaanisha nyua za lile hekalu kuu la kiroho la Yehova, yaani, mpango wa kumkaribia Yehova katika ibada kupitia Yesu Kristo. (Waebrania 8:1-5; 9:2-10, 23) Yehova ameamua kutukuza hekalu hilo la kiroho kwa kuwakusanya watu wa mataifa yote waje wakaabudu humo. (Hagai 2:7) Hapo awali, Isaya mwenyewe aliona halaiki ya watu kutoka mataifa yote wakiuendea mlima ulioinuliwa wa ibada ya Yehova. (Isaya 2:1-4) Mamia ya miaka baadaye, mtume Yohana aliona katika njozi “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” Hao walisimama ‘mbele ya kiti cha ufalme cha Mungu wakimtolea utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.’ (Ufunuo 7:9, 15) Unabii huo mbalimbali umetimizwa katika siku zetu. Kwa hiyo, tumejionea kwamba nyumba ya Yehova imerembwa.

5. Hali ya watoto wa Sayuni ilibadilika kuwa nzuri jinsi gani?

5 Hayo yote yamemletea Sayuni hali nzuri iliyoje! Yehova anasema hivi: “Kwa kuwa [uliachwa] na kuchukiwa, hata ikawa hapana mtu aliyepita ndani yako, nitakufanya kuwa fahari ya milele, furaha ya vizazi vingi.” (Isaya 60:15) Mwishoni mwa vita ya kwanza ya ulimwengu, “Israeli wa Mungu” alipatwa na kipindi cha ukiwa. (Wagalatia 6:16) Alihisi akiwa ‘ameachwa,’ kwa kuwa watoto wake duniani hawakutambua waziwazi mapenzi ya Mungu kwao. Halafu, mwaka wa 1919, Yehova aliwapa watumishi wake watiwa-mafuta nguvu mpya, na tangu wakati huo amewabariki kwa ufanisi mzuri ajabu wa kiroho. Isitoshe, mstari huo una ahadi yenye kusisimua sana. Ndiyo, Yehova mwenyewe na watoto wa Sayuni watamwonea Sayuni “fahari.” Sayuni atakuwa “furaha” tele. Na si kwa muda mfupi tu. Hali ya kupendelewa ya Sayuni, inayoonekana katika watoto wake duniani, itadumu kwa “vizazi vingi.” Haitakoma kamwe.

6. Wakristo wa kweli hutumiaje mali za thamani kutoka kwa mataifa?

6 Sikiliza sasa Mungu anapotoa ahadi nyingine. Yehova anamwambia Sayuni hivi: “Utanyonya maziwa ya mataifa, utanyonya matiti ya wafalme; nawe utajua ya kuwa mimi, BWANA, ni mwokozi wako, na mkombozi wako, Mwenye enzi wa Yakobo.” (Isaya 60:16) Sayuni hunyonya “maziwa ya mataifa” na “matiti ya wafalme” jinsi gani? Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao ambao ni “kondoo wengine” wanafanya hivyo kwa kutumia mali za thamani kutoka kwa mataifa ili kuendeleza ibada safi. (Yohana 10:16) Michango ya hiari inatumiwa kutimiza kazi kubwa ya kuhubiri na kufundisha ulimwenguni pote. Wao hutumia kwa hekima vifaa vya kisasa vya uchapishaji. Hivyo, Biblia na vitabu vya Biblia huchapishwa katika mamia ya lugha. Leo, watu wengi zaidi wana nafasi ya kujifunza kweli ya Biblia kuliko wakati mwingine wowote. Watu wa mataifa mengi sana wanajifunza kwamba Yehova ndiye Mwokozi aliyewakomboa watumishi wake watiwa-mafuta waliokuwa mateka wa kiroho.

Maendeleo ya Kitengenezo

7. Watoto wa Sayuni wamekuwa na maendeleo gani makubwa?

7 Yehova amewaremba watu wake kwa njia nyingine. Amewabariki kwa maendeleo ya kitengenezo. Tunasoma hivi kwenye Isaya 60:17: ‘Badala ya shaba nitaleta dhahabu, na badala ya chuma nitaleta fedha, na badala ya mti, shaba, na badala ya mawe, chuma; tena nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na hao wakutozao fedha kuwa haki.’ Kubadilisha shaba kwa dhahabu ni maendeleo, na ndivyo ilivyo na vitu vinginevyo vinavyotajwa. Kwa kupatana na andiko hilo, Israeli wa Mungu amefanya maendeleo ya kitengenezo muda wote wa siku hizi za mwisho. Fikiria mifano michache.

8-10. Taja maendeleo mbalimbali ya kitengenezo ambayo yamefanywa tangu mwaka wa 1919.

8 Kabla ya mwaka wa 1919, makutaniko ya watu wa Mungu yalisimamiwa na wazee na mashemasi waliochaguliwa na washiriki wa kutaniko kupitia kura. Kuanzia mwaka huo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aliweka mkurugenzi wa utumishi katika kila kutaniko ili kusimamia utumishi wa shambani. (Mathayo 24:45-47) Hata hivyo, mpango huo haukufanikiwa sana katika makutaniko mengi kwa kuwa baadhi ya wazee waliochaguliwa kwa kura hawakuunga mkono kazi ya kuhubiri habari njema. Kwa hiyo, katika mwaka wa 1932, makutaniko yaliagizwa yaache kuchagua kwa kura wazee na mashemasi. Badala yake, walipaswa kuchagua wanaume ambao wangetumikia katika halmashauri ya utumishi pamoja na mkurugenzi wa utumishi. Jambo hilo lilikuwa kama “shaba” badala ya “mti,” na yakawa maendeleo makubwa!

9 Katika mwaka wa 1938, makutaniko ulimwenguni pote yalikubali mpango bora uliopatana zaidi na Maandiko. Usimamizi wa kutaniko ukakabidhiwa mtumishi wa shirika na watumishi wengine, ambao waliteuliwa chini ya usimamizi wa mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Tangu wakati huo mambo ya kura yakaisha! Kwa hiyo, watumishi wote katika kutaniko waliwekwa kulingana na kanuni za Mungu. Hiyo ilikuwa kama “chuma” badala ya “mawe” au “dhahabu” badala ya “shaba.”

10 Tangu wakati huo, kumekuwa na maendeleo. Kwa mfano, katika mwaka wa 1972 ilieleweka kwamba makutaniko yalipaswa kusimamiwa na baraza la wazee waliowekwa kulingana na kanuni za Mungu, na hakuna mzee aliyepaswa kuwa na mamlaka juu ya wale wengine. Utaratibu huo ulipatana hata zaidi na jinsi makutaniko ya Kikristo ya karne ya kwanza yalivyosimamiwa. Isitoshe, yapata miaka miwili iliyopita, hatua nyingine ilichukuliwa. Rekebisho lilifanywa katika usimamizi wa mashirika fulani ya kisheria, na hivyo kuwezesha Baraza Linaloongoza kukaza fikira kwa ukamili juu ya masilahi ya kiroho ya watu wa Mungu badala ya kukengeushwa na mambo ya kisheria.

11. Ni nani ambaye ameleta maendeleo ya kitengenezo miongoni mwa watu wa Yehova, na matokeo yamekuwa nini?

11 Ni nani anayeleta maendeleo hayo? Ni Yehova Mungu. Yeye ndiye anayesema hivi: “Nitaleta dhahabu.” (Italiki ni zetu.) Na anaongeza hivi: “Nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na hao wakutozao fedha kuwa haki.” (Italiki ni zetu.) Ndiyo, Yehova ndiye anayeongoza usimamizi juu ya watu wake. Yehova anawaremba watu wake kwa maendeleo hayo ya kitengenezo ambayo yalitabiriwa. Na kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova wamebarikiwa katika njia nyingi. Tunasoma hivi kwenye Isaya 60:18: “Jeuri haitasikiwa tena katika nchi yako, ukiwa na uharibifu hazitakuwa mipakani mwako; bali utaziita kuta zako, Wokovu, na malango yako, Sifa.” Maneno hayo yanapendeza sana. Lakini yametimizwaje?

12. Wakristo wa kweli wamepata amani nyingi jinsi gani?

12 Wakristo wa kweli wanamtegemea Yehova kabisa ili awape maagizo na mwongozo, na matokeo yalitabiriwa na Isaya: “Watoto wako wote watafundishwa na BWANA; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” (Isaya 54:13) Isitoshe, roho ya Yehova i juu ya watu wake na mojawapo ya matunda ya roho hiyo ni amani. (Wagalatia 5:22, 23) Amani ya watu wa Yehova inawafanya wawe kimbilio katika ulimwengu huu wenye jeuri. Hali yao yenye amani inayotokana na upendo ambao Wakristo wa kweli huonyeshana, inaonyesha jinsi maisha yatakavyokuwa katika ulimwengu mpya. (Yohana 15:17; Wakolosai 3:14) Bila shaka sisi sote tunafurahia sana kuwa na amani hiyo na kuiendeleza, kwa kuwa inaleta sifa na utukufu kwa Mungu wetu, nayo ni muhimu sana katika paradiso yetu ya kiroho.—Isaya 11:9.

Nuru ya Yehova Itazidi Kuangaza

13. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova hatakoma kamwe kuwaangazia watu wake nuru?

13 Je, Yehova ataendelea kuwaangazia watu wake nuru? Ndiyo! Tunasoma hivi kwenye Isaya 60:19, 20: “Jua halitakuwa nuru yako tena wakati wa mchana, wala mwezi hautakupa nuru kwa mwangaza wake; bali BWANA atakuwa nuru ya milele kwako, na Mungu wako atakuwa utukufu wako. Jua lako halitashuka tena, wala mwezi wako hautajitenga [‘hautafifia,’ Biblia Habari Njema]; kwa kuwa BWANA mwenyewe atakuwa nuru yako ya milele; na siku za kuomboleza kwako zitakoma.” Nuru ya Yehova ilianza kuwaangazia watu hao mwaka wa 1919, baada ya ‘maombolezo’ yao kukoma walipotoka katika uhamisho wa kiroho. Zaidi ya miaka 80 baadaye, bado wana kibali cha Yehova huku nuru yake ikiendelea kuwaangazia. Na nuru hiyo itaendelea kuwaangazia daima. Kuhusiana na waabudu wake, Mungu wetu ‘hatashuka’ kama jua wala “kufifia” kama mwezi. Badala yake, ataendelea kuwaangazia watu wake nuru kwa umilele wote. Huo ni uhakikisho mzuri kama nini kwetu sisi tunaoishi katika siku za mwisho za ulimwengu huu wenye giza!

14, 15. (a) Watu wote wa Mungu ni “waadilifu” kwa njia gani? (b) Kondoo wengine wanatazamia kuona utimizo gani muhimu wa Isaya 60:21?

14 Sikia sasa ahadi nyingine ambayo Yehova anatoa kuhusu mwakilishi wa kidunia wa Sayuni, Israeli wa Mungu. Andiko la Isaya 60:21 linasema hivi: “Watu wako nao watakuwa wenye haki wote, nao watairithi nchi milele; chipukizi nililolipanda mimi mwenyewe, kazi ya mikono yangu mwenyewe, ili mimi nitukuzwe.” Mwaka wa 1919, wakati Wakristo watiwa-mafuta walipoanza kutenda tena, walikuwa tofauti na watu wengine. Katika ulimwengu wenye dhambi, wao walikuwa ‘wametangazwa kuwa waadilifu’ kwa sababu ya imani yao thabiti katika dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu. (Waroma 3:24; 5:1) Halafu, kama vile Waisraeli walioachwa huru kutoka katika Babiloni, walianza kumiliki “nchi” ya kiroho, au utendaji wa kiroho, ambamo wangefurahia paradiso ya kiroho. (Isaya 66:8) Hali ya kiparadiso ya nchi hiyo haitafifia kamwe, kwa sababu, tofauti na Israeli la kale, taifa la Israeli wa Mungu halitamwasi Yehova. Imani yao, uvumilivu wao, na bidii yao zitaleta sifa kwa jina la Mungu daima.

15 Washiriki wote wa taifa hilo la kiroho wamo katika agano jipya. Wote wana sheria ya Yehova mioyoni mwao, na Yehova amewasamehe dhambi zao kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu. (Yeremia 31:31-34) Amewatangaza kuwa waadilifu wakiwa “wana” na kuwashughulikia kana kwamba wao ni wakamilifu. (Waroma 8:15, 16, 29, 30) Waandamani wao ambao ni kondoo wengine, pia wamesamehewa dhambi zao kwa msingi wa dhabihu ya Yesu, na kama vile Abrahamu, wametangazwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Mungu kwa sababu ya imani yao. “Wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Na waandamani hao wa kondoo wengine wanatazamia kwa hamu baraka nyingine ya ajabu. Baada ya kuokoka “dhiki kubwa” au baada ya kufufuliwa, wataona utimizo halisi wa maneno ya Isaya 60:21 wakati dunia yote itakapokuwa paradiso. (Ufunuo 7:14; Waroma 4:1-3) Wakati huo, “wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:11, 29.

Ongezeko Linazidi

16. Yehova alitoa ahadi gani ya pekee, na imetimizwa kwa njia gani?

16 Katika mstari wa mwisho wa Isaya sura ya 60, tunasoma kuhusu ahadi ya mwisho ya Yehova katika sura hiyo. Anamwambia Sayuni hivi: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, BWANA, nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isaya 60:22) Yehova ametimiza ahadi yake katika wakati wetu. Wakati watiwa-mafuta walipoanza kutenda tena mwaka wa 1919, walikuwa wachache, yaani “mdogo.” Idadi yao iliongezeka wakati Waisraeli wengine wa kiroho walipokusanywa. Halafu wale kondoo wengine wakaanza kujiunga nao, na idadi yao inaongezeka daima. Hali ya amani ya watu wa Mungu, paradiso ya kiroho iliyo katika “nchi” yao, imewavuta watu wengi sana wenye mioyo minyofu hivi kwamba yule “mnyonge” kwa kweli amekuwa “taifa hodari.” Wakati huu “taifa” hili, ambalo ni Israeli wa Mungu pamoja na “wageni” zaidi ya milioni sita waliojiweka wakfu, lina watu wengi kuliko mataifa mengi duniani. (Isaya 60:10) Raia wake wote hushiriki pia kuangaza nuru inayotoka kwa Yehova, na kwa hiyo wanapendeza machoni pake.

17. Mazungumzo haya kuhusu Isaya sura ya 60 yamekutia moyo jinsi gani?

17 Ndiyo, imani yetu inaimarishwa tunapochunguza mambo makuu ya Isaya sura ya 60. Inatia moyo kuona kwamba Yehova alijua zamani sana kwamba watu wake wangepelekwa kwenye uhamisho wa kiroho kisha kurudishwa. Tunashangazwa kuona kwamba zamani sana Yehova alitabiri ongezeko kubwa la idadi ya waabudu wa kweli ambalo tunaona katika siku hizi zetu. Isitoshe, inatia moyo sana kujua kwamba Yehova hatatuacha kamwe! Kwa upendo mwingi anahakikisha kwamba malango ya “jiji” yatakuwa wazi daima ili wale walio na “mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele” waweze kukaribishwa kwa ukarimu. (Matendo 13:48) Yehova ataendelea kuwaangazia watu wake nuru. Sayuni ataendelea kuwa mwenye fahari watoto wake wanapozidi kuangaza nuru yao. (Mathayo 5:16) Bila shaka tumetiwa moyo hata zaidi kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Israeli wa Mungu na kuthamini pendeleo letu la kuangaza nuru ya Yehova!

Je, Unaweza Kueleza?

• Sisi tuna uhakika gani kuhusu upinzani?

• Watoto wa Sayuni ‘wamenyonya maziwa ya mataifa’ jinsi gani?

• Yehova ‘ameleta shaba badala ya mti’ kwa njia zipi?

• Ni sifa gani mbili zinazozungumziwa katika Isaya 60:17, 21?

• “Mdogo” amekuwa “taifa hodari” kwa njia gani?

[Maswali Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

UNABII WA ISAYA—Nuru kwa Wanadamu Wote

Mambo makuu ya makala hizi yalizungumziwa katika hotuba kwenye Kusanyiko la Wilaya la mwaka wa 2001/2002 lenye kichwa “Walimu wa Neno la Mungu.” Katika makusanyiko mengi, msemaji alipomalizia hotuba yake, alitangaza kutolewa kwa kitabu kipya chenye kichwa Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote, Buku la Pili. Mwaka uliotangulia, kitabu Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote, Buku la Kwanza, kilitolewa. Vitabu hivyo viwili vina maelezo kuhusu karibu kila mstari katika kitabu cha Isaya. Vitabu hivyo vinatusaidia sana kuelewa na kuthamini kitabu cha unabii cha Isaya kinachoimarisha imani.

[Picha katika ukurasa wa 15]

‘Yehova huwaremba wenye upole kwa wokovu’ wanapokabili upinzani mkali

[Picha katika ukurasa wa 16]

Watu wa Mungu hutumia vitu vyenye thamani kutoka kwa mataifa ili kuendeleza ibada safi

[Picha katika ukurasa wa 17]

Yehova amewabariki watu wake kwa maendeleo ya kitengenezo na kwa kuwapa amani