Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Awaremba Watu Wake kwa Kuwapa Nuru

Yehova Awaremba Watu Wake kwa Kuwapa Nuru

Yehova Awaremba Watu Wake kwa Kuwapa Nuru

“Ondoka [“inuka,” “NW”], uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja, na utukufu wa BWANA umekuzukia.”—ISAYA 60:1.

1, 2. (a) Hali ya wanadamu ikoje? (b) Ni nani wanaosababisha giza la wanadamu?

“LAITI tungekuwa na mtu kama Isaya au Mtakatifu Paulo!” Hivyo ndivyo Rais Harry Truman wa Marekani alivyoomboleza kule nyuma katika miaka ya 1940. Kwa nini alisema hivyo? Ni kwa sababu aliona uhitaji wa kuwa na viongozi wenye maadili bora ulimwenguni katika siku zake. Wanadamu walikuwa wamepitia kipindi cha giza zito lisilo na kifani katika karne ya 20, yaani, vita ya pili ya ulimwengu. Lakini, ingawa vita hiyo ilikuwa imekwisha, ulimwengu haukuwa na amani, giza liliendelea. Naam, hata sasa, miaka 57 baada ya vita hiyo, bado ulimwengu umo gizani. Kama Rais Truman angekuwa hai leo, bila shaka bado angeona uhitaji wa kuwa na viongozi wenye maadili kama Isaya au mtume Paulo.

2 Iwe Rais Truman alijua au hakujua, mtume Paulo alizungumzia giza linalowakumba wanadamu, naye alitoa onyo kulihusu katika maandiko yake. Kwa mfano, aliwaonya waamini wenzake hivi: “Tuna kushindana mwereka, si dhidi ya damu na mwili, bali dhidi ya serikali, dhidi ya mamlaka, dhidi ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, dhidi ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12) Kwa maneno hayo Paulo alionyesha kwamba mbali na kutambua giza la kiroho linalofunika ulimwengu, alijua pia chanzo chake, yaani, mashetani wenye nguvu wanaofafanuliwa kuwa “watawala wa ulimwengu.” Basi, ikiwa viumbe wa roho wenye nguvu ndio chanzo cha giza hili, wanadamu wanaweza kufanya nini ili kuliondoa?

3. Licha ya giza linalokumba wanadamu, Isaya alitabiri nini kuhusu waaminifu?

3 Isaya pia alitaja giza linalowakumba wanadamu. (Isaya 8:22; 59:9) Hata hivyo, Isaya alipotabiri kuhusu siku zetu, Mungu alimwongoza kuandika kwamba hata katika siku hizi zenye giza, Yehova angewapa tumaini wale wanaopenda nuru. Ndiyo, ijapokuwa Paulo na Isaya hawako leo, maandishi yao yanaweza kutuongoza. Ili tuone jinsi Maandiko hayo ni baraka kwa wale wanaompenda Yehova, na tuchunguze maneno ya kiunabii ya Isaya katika sura ya 60 ya kitabu chake.

Mwanamke wa Kiunabii Aangaza Nuru

4, 5. (a) Yehova anamwamuru mwanamke afanye nini, naye anatoa ahadi gani? (b) Sura ya 60 ya Isaya ina habari gani yenye kusisimua?

4 Mwanamke aliye katika hali mbaya sana ndiye anayeambiwa maneno ya kwanza ya sura ya 60 ya Isaya. Amelala chini kifudifudi katika giza tititi. Ghafula, nuru inalipenya lile giza, naye Yehova anaita kwa sauti kubwa: “Ondoka [“inuka,” NW], uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja, na utukufu wa BWANA umekuzukia.” (Isaya 60:1) Wakati umewadia kwa mwanamke huyo kusimama ili aangaze nuru ya Mungu, yaani, utukufu wake. Kwa nini? Tunapata jibu katika mstari unaofuata: “Tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu; bali BWANA atakuzukia wewe, na utukufu wake utaonekana juu yako.” (Isaya 60:2) Mwanamke huyo anapotii agizo la Yehova anahakikishiwa kwamba kutakuwa na matokeo mazuri ajabu. Yehova anasema hivi: “Mataifa wataijilia nuru yako, na wafalme kuujia mwanga wa kuzuka kwako.”—Isaya 60:3.

5 Maneno yenye kusisimua yaliyo katika mistari hii mitatu ni utangulizi wa Isaya sura ya 60 na vilevile muhtasari wa mambo makuu ya sura hiyo. Sura hiyo inatabiri yale yatakayompata yule mwanamke wa kiunabii, na inaeleza jinsi tunavyoweza kukaa katika nuru ya Yehova licha ya giza linalofunika wanadamu. Lakini mifano inayotajwa katika mistari hiyo mitatu ya utangulizi inamaanisha nini?

6. Mwanamke anayetajwa katika sura ya 60 ya Isaya ni nani, naye anawakilishwa na nani duniani?

6 Mwanamke anayetajwa katika Isaya 60:1-3 ni Sayuni, tengenezo la kimbingu la Yehova la viumbe wa roho. Leo, Sayuni anawakilishwa duniani na mabaki ya “Israeli wa Mungu,” lile kutaniko la kimataifa la Wakristo ambao wametiwa mafuta kwa roho. Wao wana tumaini la kutawala pamoja na Kristo mbinguni. (Wagalatia 6:16) Taifa hilo la kiroho lina washiriki 144,000, na utimizo wa kisasa wa Isaya sura ya 60 unahusu hasa wale walio hai duniani katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1; Ufunuo 14:1) Unabii huo una maelezo mengi pia kuhusu ule “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” waandamani wa hao Wakristo watiwa-mafuta.—Ufunuo 7:9; Yohana 10:16.

7. Hali ya Sayuni ilikuwaje mwaka wa 1918, na hali hiyo ilikuwa imetabiriwa jinsi gani?

7 Je, “Israeli wa Mungu” alikuwa amelala gizani wakati fulani, kama yule mwanamke wa kiunabii? Ndiyo, jambo hilo lilitukia zaidi ya miaka 80 iliyopita. Wakati wa vita ya kwanza ya ulimwengu, Wakristo watiwa-mafuta walijitahidi sana kuendeleza kazi ya kutoa ushahidi. Lakini mwaka wa 1918, mwaka wa mwisho wa vita, kazi ya kuhubiri karibu ikomeshwe kabisa. Joseph F. Rutherford, aliyesimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote, na Wakristo wengine mashuhuri walihukumiwa vifungo virefu gerezani kwa mashtaka bandia. Katika kitabu cha Ufunuo, Wakristo watiwa-mafuta waliokuwa duniani wakati huo walitajwa katika unabii huo kuwa maiti zilizolala “juu ya njia pana ya jiji kubwa ambalo katika maana ya kiroho laitwa Sodoma na Misri.” (Ufunuo 11:8) Kwa kweli huo ulikuwa wakati wenye giza kwa Sayuni aliyewakilishwa na watoto wake watiwa-mafuta duniani.

8. Ni badiliko gani kubwa lililotukia mwaka wa 1919, na matokeo yalikuwa nini?

8 Hata hivyo, mwaka wa 1919 kukawa na badiliko kubwa. Yehova aliangaza nuru juu ya Sayuni! Washiriki wa Israeli wa Mungu waliokuwa duniani walianza kuangaza nuru ya Mungu, wakaanza tena kuzitangaza habari njema kwa ujasiri. (Mathayo 5:14-16) Kwa sababu ya bidii hiyo mpya ya Wakristo hao, wengine walivutwa kwenye nuru ya Yehova. Mwanzoni, wapya waliokuja walitiwa mafuta ili wawe washiriki wa Israeli wa Mungu. Katika Isaya 60:3 wanaitwa wafalme, kwa kuwa wataurithi Ufalme wa kimbingu wa Mungu pamoja na Kristo. (Ufunuo 20:6) Baadaye, umati mkubwa wa kondoo wengine walivutwa kwenye nuru ya Yehova. Hao ndio “mataifa” yanayotajwa katika unabii huo.

Watoto wa Mwanamke Wanakuja Nyumbani!

9, 10. (a) Mwanamke huyo aliona jambo gani la kustaajabisha, na hilo lilikuwa ishara ya matukio gani ya wakati ujao? (b) Sayuni amekuwa na sababu gani ya kuwa na shangwe?

9 Sasa, Yehova anaanza kutoa maelezo zaidi kuhusu Isaya 60:1-3. Anampa yule mwanamke amri nyingine. Sikiliza maneno yake: “Inua macho yako, utazame pande zote!” Mwanamke huyo anatii, na lo, anaona jambo la kuchangamsha moyo kama nini! Watoto wake wanakuja nyumbani. Andiko linaendelea kusema hivi: “Wote wanakusanyana; wanakujia wewe; wana wako watakuja kutoka mbali. Na binti zako watabebwa nyongani.” (Isaya 60:4) Kazi ya kuutangaza Ufalme ulimwenguni pote, iliyoanza mwaka wa 1919, iliwavuta maelfu ya watu wapya kwenye utumishi wa Yehova. Hao pia wakawa “wana” na “binti” za Sayuni, washiriki waliotiwa mafuta wa Israeli wa Mungu. Hivyo, Yehova ameremba Sayuni kwa kuwapa nuru washiriki wa mwisho wa wale 144,000.

10 Je, unaweza kuwazia furaha ya Sayuni watoto wake wanapomjia? Na bado Yehova anampa Sayuni sababu nyingine za kushangilia. Tunasoma hivi: “Ndipo utakapoona na kutiwa nuru, na moyo wako utatetemeka na kukunjuka; kwa kuwa wingi wa bahari utageuzwa kukujia, utajiri wa mataifa utakuwasilia.” (Isaya 60:5) Kwa kupatana na maneno hayo ya unabii, tangu miaka ya 1930, Wakristo wengi wenye tumaini la kuishi duniani, wamemwendea Sayuni. Wametoka katika “bahari” ya wanadamu wasio na kibali cha Mungu, nao ndio utajiri wa mataifa. Wao ni “vitu vinavyotamaniwa na mataifa [“vya mataifa,” NW].” (Hagai 2:7; Isaya 57:20) Ona pia, kwamba “vitu [hivyo] vinavyotamaniwa” hawaendi zao wakamtumikie Yehova kila mtu kivyake. Bali wao huongeza uzuri wa Sayuni wanapokuja kuabudu pamoja na ndugu zao waliotiwa mafuta, na hivyo kuwa “kundi moja” lenye “mchungaji mmoja.”—Yohana 10:16.

Wafanyabiashara na Wachungaji Waja Sayuni

11, 12. Fafanua makundi yanayomwendea Sayuni.

11 Kule kukusanywa kulikotabiriwa kumetokeza ongezeko kubwa la watu wanaomsifu Yehova. Maneno yanayofuata ya unabii huo yanaonyesha jambo hilo. Wazia kwamba umesimama pamoja na mwanamke huyo wa kiunabii kwenye Mlima Sayuni. Unaona nini unapotazama upande wa mashariki? “Wingi wa ngamia utakufunika, ngamia vijana wa Midiani na Efa; wote watakuja kutoka Sheba; wataleta dhahabu na uvumba; na kuzitangaza sifa za BWANA.” (Isaya 60:6) Wafanyabiashara wengi wanaongoza misafara ya ngamia kwenye njia zinazoelekea Yerusalemu. Ngamia hao ni wengi hivi kwamba ni kama wanaifunika nchi! Wafanyabiashara hao wamebeba zawadi zenye thamani, “dhahabu na uvumba.” Nao wanakuja kwenye nuru ya Mungu ili “kuzitangaza sifa za BWANA,” yaani, kumtukuza mbele za watu.

12 Si wafanyabiashara peke yao walio safarini. Wachungaji wengi wanamwendea Sayuni pia. Unabii unasema hivi: “Makundi yote ya Kedari yatakusanyika kwako, kondoo waume wa Nebayothi watakutumikia.” (Isaya 60:7a) Makabila yanayofuga mifugo yanakuja hadi jiji takatifu ili kumtolea Yehova wanyama bora kutoka katika makundi yao. Hata wanajitoa kumtumikia Sayuni! Yehova anawakaribishaje wageni hao? Mungu mwenyewe anajibu hivi: “Watapanda juu ya madhabahu yangu kwa kibali, nami nitaitukuza [“nitairemba,” NW] nyumba ya utukufu wangu.” (Isaya 60:7b) Yehova anakubali kwa fadhili matoleo na utumishi wa wageni hao. Wanaliremba hekalu lake.

13, 14. Ni nini kinachoonekana kikija kutoka upande wa magharibi?

13 Sasa geuka utazame upande wa magharibi. Unaona nini? Kule mbali kuna wingu jeupe linaloonekana kana kwamba linafunika uso wa bahari. Yehova anauliza swali ambalo unataka kuuliza: “Ni nani hawa warukao kama wingu, na kama njiwa waendao madirishani kwao?” (Isaya 60:8) Yehova anajibu swali lake mwenyewe: “Visiwa vitaningojea, na merikebu za Tarshishi kwanza, ili kuleta wana wako kutoka mbali, na fedha yao na dhahabu yao pamoja nao, kwa ajili ya jina la BWANA, Mungu wako, kwa ajili yake Mtakatifu wa Israeli, kwa kuwa amekutukuza wewe.”—Isaya 60:9.

14 Je, unaweza kuwazia jambo hilo? Lile wingu jeupe limekaribia zaidi na sasa linaonekana kama madoa mengi kule mbali upande wa magharibi. Madoa hayo yanaonekana kama ndege wanaoruka juu tu ya mawimbi ya bahari. Lakini yanapokaribia zaidi, unaona kwamba kumbe ni merikebu zenye matanga yaliyofunguliwa. Merikebu zinazosafiri kuelekea Yerusalemu ni nyingi sana hivi kwamba zinaonekana kama kundi la njiwa. Kundi hilo la merikebu limetoka bandari za mbali na linasafiri kwa kasi kuwapeleka waamini hadi Yerusalemu ili wamwabudu Yehova.

Tengenezo la Yehova Lapanuka

15. (a) Maneno ya Isaya 60:4-9 yanatabiri ongezeko gani? (b) Wakristo wa kweli wana moyo gani?

15 Mstari wa 4 hadi 9 unatabiri waziwazi mpanuko ambao umeendelea ulimwenguni pote tangu mwaka wa 1919. Kwa nini Yehova alimbariki Sayuni kwa ongezeko hilo? Kwa sababu tangu mwaka wa 1919, Israeli wa Mungu ameonyesha utii na kuangaza nuru ya Yehova bila kuacha. Hata hivyo, je, uliona kwamba mstari wa 7 unasema kwamba wapya hao wanaowasili ‘hupanda juu ya madhabahu ya Mungu’? Madhabahu ni mahali pa kutolea dhabihu, na maneno hayo ya unabii yanatukumbusha kwamba kumtumikia Yehova kunahusisha kujidhabihu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Nawasihi sana . . . mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri kuzuri.” (Waroma 12:1) Kwa kupatana na maneno ya Paulo, Wakristo wa kweli hawatosheki tu kwenda kumwabudu Mungu mara moja kwa juma. Wanatumia wakati wao, nguvu na mali zao ili kuendeleza ibada safi. Je, waabudu hao wanaojitoa, wanairemba nyumba ya Yehova? Unabii wa Isaya unajibu, ndiyo. Na tunaweza kuwa na uhakika kwamba waabudu hao wenye bidii pia wamerembwa vizuri machoni pa Yehova.

16. Ni nani waliojitolea kusaidia katika ujenzi siku za kale, na ni nani ambao wamefanya hivyo katika siku zetu?

16 Wapya hao wanaokuja wanataka kufanya kazi. Unabii unaendelea kusema hivi: “Wageni watajenga kuta zako, na wafalme wao watakuhudumu.” (Isaya 60:10) Maneno hayo yalitimizwa mara ya kwanza wakati Wayahudi waliporudi kutoka uhamishoni huko Babiloni. Wafalme na watu wengine wa mataifa walisaidia kujenga upya hekalu na jiji la Yerusalemu. (Ezra 3:7; Nehemia 3:26) Katika utimizo wa siku zetu, umati mkubwa umewaunga mkono mabaki ya watiwa-mafuta ili kuendeleza ibada ya kweli. Wamesaidia kuanzisha na kuimarisha makutaniko ya Kikristo, na hivyo kuzitia nguvu “kuta” za tengenezo la Yehova lililo kama jiji. Wanashiriki pia katika ujenzi halisi wa Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na majengo ya Betheli. Kwa njia hizi zote, wanawaunga mkono ndugu zao waliotiwa mafuta ili kuyatimiza mahitaji ya tengenezo la Yehova linalopanuka!

17. Taja njia moja ambayo Yehova anawaremba watu wake.

17 Maneno ya kumalizia ya Isaya 60:10 yanatia moyo sana. Yehova anasema hivi: “Katika ghadhabu yangu nalikupiga, lakini katika upendeleo wangu nimekurehemu.” Ndiyo, huko nyuma, mwaka wa 1918 na 1919, Yehova aliwatia watu wake nidhamu. Lakini jambo hilo limekwisha pita. Sasa, wakati umewadia kwa Yehova kuwarehemu watumishi wake waliotiwa mafuta na waandamani wao wa kondoo wengine. Na ongezeko kubwa ajabu ambalo wamepata linaonyesha kwamba anawabariki, yaani ‘anawaremba.’

18, 19. (a) Yehova anaahidi nini kuwahusu wapya wanaoingia katika tengenezo lake? (b) Mistari inayobaki ya sura ya 60 ya Isaya inatueleza nini?

18 Kila mwaka, mamia ya maelfu ya “wageni” huja kwenye tengenezo la Yehova, na njia itabaki wazi ili wengine wengi waje. Yehova anamwambia Sayuni hivi: “Malango yako nayo yatakuwa wazi daima; hayatafungwa mchana wala usiku; ili watu wapate kukuletea utajiri wa mataifa, na wafalme wao wakiongozwa pamoja nao.” (Isaya 60:11) Wapinzani fulani wanajaribu kufunga “malango” hayo, lakini tunajua kwamba hawatafanikiwa. Yehova mwenyewe amesema kwamba kwa njia moja au nyingine malango hayo yatabaki wazi. Ongezeko litaendelea.

19 Yehova amewabariki, au amewaremba, watu wake kwa njia nyingine pia katika siku hizi za mwisho. Mistari inayobaki ya sura ya 60 ya Isaya inatabiri njia hizo.

Je, Unaweza Kueleza?

• “Mwanamke” wa Mungu ni nani, na anawakilishwa na nani duniani?

• Watoto wa Sayuni walikuwa wamelala chini kifudifudi wakati gani, nao ‘walisimama’ lini na vipi?

• Kwa kutumia mifano, Yehova alitabirije ongezeko la leo la idadi ya wahubiri wa Ufalme?

• Yehova amewaangazia watu wake nuru katika njia zipi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

“Mwanamke” wa Yehova anaambiwa ainuke

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kundi la merikebu linaonekana kama njiwa kwa mbali