Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Acheni Sisi Tufanye Lililo Jema Kuelekea Wote”

“Acheni Sisi Tufanye Lililo Jema Kuelekea Wote”

“Njoni Kwangu, Nami Hakika Nitawaburudisha Nyinyi”

“Acheni Sisi Tufanye Lililo Jema Kuelekea Wote”

KAZI muhimu ya Yesu ilikuwa kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Marko 1:14; Luka 8:1) Kwa kuwa wafuasi wa Kristo wangependa kumwiga, wao huona kazi ya kufundisha ujumbe wa Biblia kuhusu Ufalme wa Mungu kuwa kazi muhimu zaidi maishani mwao. (Luka 6:40) Kwa kweli Mashahidi wa Yehova huchangamka moyoni kuona jinsi ambavyo ujumbe wa Ufalme huleta burudiko la kudumu kwa wale wanaoukubali—kama ulivyowaburudisha watu wakati Yesu alipokuwa duniani.—Mathayo 11:28-30.

Mbali na kufundisha Neno la Mungu, Yesu alifanya kazi nyingine nzuri, kama vile kuponya wagonjwa na kulisha wenye njaa. (Mathayo 14:14-21) Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova hufundisha watu Biblia na vilevile kuwasaidia walio na uhitaji. Kwa kweli, Maandiko huwaandaa Wakristo “kwa ajili ya kila kazi njema” na kuwahimiza wafanye “lililo jema kuelekea wote.”2 Timotheo 3:16, 17; Wagalatia 6:10.

“Ndugu Zetu Walikuja Kutusaidia”

Mnamo Septemba 1999, nchi ya Taiwan ilikumbwa na tetemeko baya sana la ardhi. Miezi michache baadaye, mvua nyingi sana na maporomoko ya theluji yalisababisha msiba mbaya zaidi wa asili katika historia ya Venezuela. Hivi karibuni, nchi ya Msumbiji ilikumbwa na mafuriko mabaya sana. Katika visa vyote vitatu, Mashahidi wa Yehova walikuja mara moja na kuwaletea wale waliokumbwa na msiba huo chakula, maji, dawa, mavazi, mahema, na vifaa vya kupikia. Wafanyakazi wa kujitolea waliokuwa na ujuzi wa kitiba walijenga hospitali ndogo za muda ili kutibu wagonjwa, nao wajenzi wa kujitolea wakajenga nyumba mpya kwa ajili ya wale walioachwa bila makao.

Watu waliopatwa na misiba hiyo waliguswa moyo kupokea msaada huo kwa wakati unaofaa. “Tulikuwa tumekata tamaa sana wakati ndugu zetu walipokuja kutusaidia.” asema Malyori, ambaye nyumba yake ilibomolewa na maporomoko ya theluji nchini Venezuela. Malyori alisema hivi baada ya wafanyakazi wa kujitolea kujengea familia yake nyumba mpya: “Tunamshukuru Yehova sana kwa yote ambayo ametufanyia!” Na wakati watu waliokumbwa na mafuriko nchini Msumbiji walipopokea funguo za nyumba mpya walizojengewa, wote walianza kuimba wimbo wa Ufalme “Yehova Ni Kimbilio Letu.” *

Pia wafanyakazi wa kujitolea walipata burudiko kwa kuwasaidia walio na uhitaji. “Nilifurahi kusaidia ndugu hao walioteseka sana,” akasema Marcelo, aliyekuwa muuguzi katika kambi moja ya wakimbizi nchini Msumbiji. Huang ambaye ni mfanyakazi wa kujitolea nchini Taiwan, alisema hivi: “Ilifurahisha sana kushiriki kazi ya kupeleka chakula na mahema kwa akina ndugu walio na uhitaji. Ilikuwa kazi yenye kuimarisha imani.”

Programu Yenye Manufaa ya Wafanyakazi wa Kujitolea

Pia kazi ya kujitolea imeleta burudiko la kiroho kwa makumi ya maelfu ya wafungwa ulimwenguni pote. Jinsi gani? Katika miaka ya hivi majuzi, Mashahidi wa Yehova wamegawanya vichapo vinavyozungumzia Biblia kwa wafungwa zaidi ya 30,000 katika magereza yapatayo 4,000 nchini Marekani pekee. Isitoshe, inapowezekana, Mashahidi hutembelea wafungwa katika magereza ili kujifunza Biblia pamoja nao na kuongoza mikutano ya Kikristo. Je, wafungwa hunufaika?

Wafungwa fulani wanaojifunza Biblia huanza kuwaeleza wafungwa wenzao mafundisho yanayoburudisha ya Neno la Mungu. Kwa sababu hiyo, sasa katika magereza kadhaa ulimwenguni pote kuna vikundi vya wafungwa wanaomwabudu Yehova pamoja. “Kikundi chetu kinaendelea kukua,” akaripoti mfungwa mmoja huko Oregon, Marekani mwaka wa 2001. “Tuna watangazaji wa Ufalme 7 ambao wanaongoza mafunzo ya Biblia 38. Watu zaidi ya 25 huhudhuria hotuba ya watu wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi, na watu 39 walihudhuria Ukumbusho [wa kifo cha Kristo]. Watu watatu zaidi watabatizwa hivi karibuni!”

Manufaa na Shangwe

Maofisa wa gereza wameona manufaa ya programu hii ya wafanyakazi wa kujitolea. Jambo linalowavutia sana maofisa ni manufaa ya kudumu ya programu hii ya wafanyakazi wa kujitolea. Ripoti moja inasema: “Katika miaka kumi ambayo programu hii imekuwako, hakuna mfungwa aliyebatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova akiwa bado gerezani amewahi kurudi huko tena baada ya kuachiliwa—tofauti na asilimia 50-60 ya wafungwa wengine ambao hurudi gerezani tena.” Kwa kuona matokeo ambayo Mashahidi wa kujitolea walipata, kasisi mmoja wa gereza huko Idaho alisema hivi katika barua aliyoandikia makao makuu ya Mashahidi wa Yehova: “Hata ingawa sikubaliani na imani yenu ya kidini, nimevutiwa sana na tengenezo lenu.”

Wafanyakazi wa kujitolea wanathawabishwa pia kwa kusaidia wafungwa. Baada ya kuongoza mkutano pamoja na kikundi cha wafungwa walioimba wimbo wa Ufalme kwa mara ya kwanza, mfanyakazi mmoja wa kujitolea aliandika hivi: “Ilitia moyo kuona wanaume 28 wakiungana pamoja kumwimbia Yehova sifa. Nao waliimba kwa sauti kubwa! Ni pendeleo lililoje kuwepo kwenye tukio kama hilo!” Mfanyakazi mmoja wa kujitolea aliyekuwa akitembelea magereza huko Arizona alisema hivi: “Tumethawabishwa kama nini kwa kufanya kazi hii ya pekee!”

Mashahidi wa kujitolea ulimwenguni pote wanakubaliana na maneno ya Yesu aliyesema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Pia wanathibitisha kwamba kufuata shauri la Biblia la kuwatendea watu wote mema kunaburudisha kwelikweli.—Mithali 11:25.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona wimbo namba 85 katika kitabu Mwimbieni Yehova Sifa, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Venezuela

[Picha katika ukurasa wa 8]

Taiwan

[Picha katika ukurasa wa 8]

Msumbiji