Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Kuna Mahali Penye Moto wa Mateso?

Je, Kweli Kuna Mahali Penye Moto wa Mateso?

Je, Kweli Kuna Mahali Penye Moto wa Mateso?

HATA iwe unafikiri nini unaposikia maneno “kuzimu” na “gehena,” watu wengi hufikiri kwamba waovu watateseka motoni kwa sababu ya dhambi walizotenda. Biblia inasema hivi kuhusu dhambi na matokeo yake: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Pia Maandiko husema: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Kwa kuwa adhabu ya dhambi ni kifo, swali muhimu litakalotusaidia kujua kama kuna mahali penye moto wa mateso ni: Ni nini hutupata tunapokufa?

Je, kuna kitu fulani kilicho hai ambacho huendelea kuishi baada ya kifo? Kuzimu au gehena ni nini, na ni watu gani huenda huko? Je, watu wanaoenda huko wana tumaini lolote? Biblia hutoa majibu ya kweli na yenye kuridhisha kwa maswali hayo.

Je, Kuna Uhai Baada ya Kifo?

Je, kuna kitu fulani ndani yetu kama vile nafsi au roho ambacho huendelea kuishi baada ya mwili kufa? Ebu fikiria jinsi mwanadamu wa kwanza, Adamu, alivyopata kuwa hai. Biblia inasema: “BWANA Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai.” (Mwanzo 2:7) Ijapokuwa uhai wake ulitegemea kupumua, kupuliza “pumzi ya uhai” puani mwake kulihusisha mengi zaidi ya kupuliza tu hewa ndani ya mapafu yake. Kulimaanisha kwamba Mungu alianzisha uhai katika mwili wa Adamu usio na uhai—“kani ya uhai,” ambayo hutenda kazi ndani ya viumbe wote wa kidunia. (Mwanzo 6:17; 7:22, NW) Biblia huitaja kani hiyo ya uhai kuwa “roho.” (Yakobo 2:26) Roho hiyo inaweza kulinganishwa na umeme ambao huendesha mashine au kifaa fulani na kukiwezesha kufanya kazi. Kama vile umeme usivyofanana na kifaa unachoendesha, kani ya uhai haifanani na kiumbe inachokihuisha. Haina utu wala uwezo wa kufikiri.

Ni nini huipata roho ya mtu anapokufa? Andiko la Zaburi 146:4 husema: “Pumzi [“roho,” NW] yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” Mtu anapokufa, roho yake isiyo na umbo haiendelei kuishi mahali pengine ikiwa kiumbe cha roho, bali ‘humrudia Mungu aliyeitoa.’ (Mhubiri 12:7) Hiyo inamaanisha kwamba tumaini lolote la wakati ujao la mtu huyo linategemea Mungu pekee yake.

Wanafalsafa wa kale Wagiriki, Socrates na Plato waliamini kwamba nafsi iliyo ndani ya mtu haifi kamwe bali huendelea kuishi baada ya mtu huyo kufa. Biblia inafundisha nini kuhusu nafsi? Andiko la Mwanzo 2:7 linasema, Adamu “akawa nafsi hai.” Hakupewa nafsi; alikuwa nafsi, yaani, mtu. Maandiko husema kwamba nafsi huzaliwa, hufunga, hushiba, huzimia, na kadhalika. (Mwanzo 46:18; Zaburi 35:13; Mithali 27:7; Yona 2:7, Zaire Swahili Bible) Naam, mtu ni nafsi. Mtu anapokufa, nafsi hiyo hufa.—Ezekieli 18:4, ZSB.

Kwa hiyo, wafu wako katika hali gani? Yehova alisema hivi alipomhukumu Adamu: “U mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Adamu alikuwa wapi kabla Yehova hajamwumba kutokana na mavumbi ya ardhi na kumpa uhai? Hakuwepo! Adamu hakuendelea kuwapo baada ya kufa. Hali ya wafu inaonyeshwa wazi katika andiko la Mhubiri 9:5, 10, ambapo tunasoma: “Wafu hawajui neno lolote . . . Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu uendako wewe.” Kulingana na Biblia, kifo ni kinyume cha uhai. Wafu hawajui neno lolote, hawana hisia zozote, hawafikiri chochote.

Je, Mtu Anapokufa Anateseka Milele au Anakuwa Kaburini Tu?

Kwa kuwa wafu hawajui neno lolote, kuzimu wala gehena si mahali penye moto wa mateso ambapo waovu huteseka baada ya kufa. Kwa hiyo kuzimu ni nini? Tunaweza kupata jibu la swali hilo kwa kuchunguza kilichompata Yesu baada ya kufa. Luka, mwandishi wa Biblia anasema: “[Yesu] hakuachiliwa mbali katika Hadesi (“kuzimu” UV) wala mwili wake haukuona uharibifu.” * (Matendo 2:31) Kuzimu alikoenda Yesu ni wapi? Mtume Paulo aliandika hivi: “Niliwapa nyinyi . . . kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba amefufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko.” (1 Wakorintho 15:3, 4) Kwa hiyo Yesu alikuwa kuzimu, yaani, kaburini, lakini hakuachwa huko, kwa kuwa alifufuliwa.

Pia mfikirie Yobu mwaminifu, aliyeteseka sana. Akitamani kuepuka mateso yaliyompata, alisihi hivi: “Laiti ungenificha kuzimuni, ukanilinda kwa siri, hata ghadhabu zako zitakapopita.” * (Ayubu 14:13) Je, lingekuwa jambo la akili kufikiri kwamba Yobu alitamani kwenda mahali penye moto wa mateso ili kulindwa? Yobu alijua kwamba mateso yake yangeisha akienda “kuzimu” au kaburini. Kwa hiyo kulingana na Biblia, kuzimu ni kaburi la kawaida la wanadamu ambapo watu wazuri na wabaya huenda.

Je, Moto wa Mateso Unafananisha Uharibifu wa Milele?

Je, inawezekana kwamba moto wa mateso unafananisha uharibifu wa milele? Yakitofautisha moto wa mateso na Hadesi, Maandiko husema: “Kifo na Hadesi vi[li]vurumishwa ndani ya ziwa la moto.” “Ziwa” linalotajwa hapa ni la mfano, kwa kuwa kifo na Hadesi ambavyo vinatupwa ndani yake haviwezi kuchomwa kihalisi. “Hili [ziwa la moto] humaanisha kifo cha pili”—ambapo hakuna tumaini la kufufuliwa.—Ufunuo 20:14.

Ziwa la moto ni sawa na “Gehena ya moto” ambayo Yesu alizungumzia. (Mathayo 5:22; Marko 9:47, 48) Neno Gehena linapatikana mara 12 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, nalo linamaanisha bonde la Hinomu, lililokuwa nje ya kuta za Yerusalemu. Yesu alipokuwa duniani, bonde hilo lilitumiwa kuwa mahali pa kutupa takataka, “ambapo miili ya wahalifu, na mizoga ya wanyama, na kila namna ya takataka ilitupwa.” (Smith’s Dictionary of the Bible) Mioto iliendelea kuwaka kwa kuongeza salfa ili kuteketeza takataka kabisa. Yesu alitumia bonde hilo kuwa mfano wa uharibifu wa milele.

Sawa na Gehena, ziwa la moto linafananisha uharibifu wa milele. Kifo na Hadesi ‘huvurumishwa humo’ katika maana ya kwamba vitaondolewa kabisa wakati wanadamu watakapokombolewa kutoka katika dhambi na adhabu ya kifo. Pia “fungu” la wakosaji wasiotubu na wa kukusudia litakuwa katika ziwa hilo. (Ufunuo 21:8) Wao pia wataharibiwa milele. Kwa upande mwingine, wale walio katika kumbukumbu la Mungu huko kuzimu—kaburi la ujumla la wanadamu—wana tumaini zuri la wakati ujao.

Walio Kuzimu Watatolewa!

Andiko la Ufunuo 20:13 linasema: “Bahari ikawatoa hao wafu waliokuwa ndani yayo, na kifo na Hadesi vikawatoa wafu ndani yavyo.” Naam, wale walio katika kuzimu inayotajwa na Biblia watatolewa. Kama Yesu alivyoahidi, “saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti [ya Yesu] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Mamilioni ya wafu walio katika kumbukumbu la Yehova Mungu watafufuliwa katika dunia itakayofanywa kuwa paradiso tena.—Luka 23:43; Matendo 24:15.

Katika ulimwengu mpya wa Mungu, wanadamu waliofufuliwa ambao watatii sheria zake adilifu hawatakufa tena. (Isaya 25:8) Yehova “atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.” Kwa kweli “mambo ya zamani [yatakuwa] yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Ni tumaini zuri kama nini kwa wale walio katika kuzimu—“makaburi ya ukumbusho”! Kwa kweli tumaini hilo ni sababu ya kutosha kutufanya tujifunze zaidi kuhusu Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo.—Yohana 17:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Katika tafsiri ya Union Version, neno la Kigiriki Hades limetafsiriwa kuzimu mara zote kumi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Andiko la Luka 16:19-31 linataja mateso, lakini simulizi lote lina maana ya ufananisho. Ona sura ya 88 ya kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 11 Neno la Kiebrania Sheol linapatikana mara 65 katika Maandiko ya Kiebrania, nalo limetafsiriwa “kuzimu” katika Biblia ya Union Version na Biblia Habari Njema.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yobu alisali alindwe kuzimuni

[Picha katika ukurasa wa 6]

Gehena yenye moto inafananisha uharibifu wa milele

[Picha katika ukurasa wa 7]

‘Wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka’