Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ongezeni Kwenye Uvumilivu Wenu Ujitoaji-kimungu

Ongezeni Kwenye Uvumilivu Wenu Ujitoaji-kimungu

Ongezeni Kwenye Uvumilivu Wenu Ujitoaji-kimungu

“Jazeni kwenye imani yenu . . . uvumilivu, kwenye uvumilivu wenu ujitoaji-kimungu.”—2 PETRO 1:5, 6.

1, 2. (a) Ni ukuzi wa aina gani unaotazamiwa kwa mtoto? (b) Ukuzi wa kiroho ni muhimu kadiri gani?

UKUZI wa kimwili ni muhimu kwa mtoto. Hata hivyo, inatazamiwa kwamba mtoto huyo atakua kiakili na kihisia-moyo pia. Baada ya muda, mtoto ataacha tabia zake za kitoto na akue kuwa mtu mzima. Mtume Paulo alizungumzia jambo hilo alipoandika: “Nilipokuwa kitoto, nilikuwa nikisema kama kitoto, nikifikiri kama kitoto, nikiwazawaza kama kitoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mtu mzima, nimeziondolea mbali tabia za kitoto.”—1 Wakorintho 13:11.

2 Paulo anataja jambo muhimu kuhusu ukuzi wa kiroho. Wakristo wanahitaji kukua na wawe “watu wazima katika nguvu za kuelewa” na kuacha kuwa vitoto kiroho. (1 Wakorintho 14:20) Wanapaswa kujitahidi sana kufikia “kipimo cha kimo ambacho ni cha ujao wa Kristo.” Hivyo hawatakuwa ‘vitoto, wakirushwa huku na huku kama vile na mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho.’—Waefeso 4:13, 14.

3, 4. (a) Tunapaswa kufanya nini ili tukue na kuwa watu wazima kiroho? (b) Ni sifa gani zinazompendeza Mungu tunazopaswa kuonyesha, nazo ni muhimu kadiri gani?

3 Tunawezaje kukua na kuwa watu wazima kiroho? Chini ya hali za kawaida, ukuzi wa kimwili hutokea wenyewe tu, lakini ukuzi wa kiroho huhitaji jitihada. Ukuzi wa kiroho huanza kwa kupata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu na kutenda kulingana na ujuzi huo. (Waebrania 5:14; 2 Petro 1:3) Kufanya hivyo hutuwezesha kuwa na sifa zinazompendeza Mungu. Kama vile viungo mbalimbali vya mwili hukua wakati uleule, ndivyo na sifa mbalimbali zinazompendeza Mungu husitawi wakati uleule. Mtume Petro aliandika: “Mkiitikia kwa kuchanga kwenu jitihada yote yenye bidii, jazeni kwenye imani yenu wema wa adili, kwenye wema wa adili wenu ujuzi, kwenye ujuzi wenu kujidhibiti, kwenye kujidhibiti kwenu uvumilivu, kwenye uvumilivu wenu ujitoaji-kimungu, kwenye ujitoaji-kimungu wenu shauku ya kidugu, kwenye shauku ya kidugu yenu upendo.”—2 Petro 1:5-7.

4 Sifa zote anazotaja Petro ni muhimu, na hakuna moja inayoweza kuachwa. Anaendelea kusema: “Ikiwa mambo haya yakaa ndani yenu na kufurika, yatawazuia kuwa ama wasiotenda ama wasiozaa matunda kuhusu ujuzi sahihi juu ya Bwana wetu Yesu Kristo.” (2 Petro 1:8) Na tukazie fikira uhitaji wa kuongeza ujitoaji-kimungu kwenye uvumilivu wetu.

Uhitaji wa Kuvumilia

5. Kwa nini tunahitaji kuwa wavumilivu?

5 Petro na Paulo wanahusianisha ujitoaji-kimungu na uvumilivu. (1 Timotheo 6:11) Kuwa mvumilivu hakumaanishi tu kuendelea kustahimili chini ya magumu. Kunatia ndani subira, ujasiri, na kuwa imara bila kukata tamaa tunapokabiliwa na majaribu, vikwazo, vishawishi, au mnyanyaso. Kwa kuwa tunaishi kwa “ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu,” tunatazamia kunyanyaswa. (2 Timotheo 3:12) Ni lazima tuvumilie ili kuthibitisha kwamba tunampenda Yehova na kusitawisha sifa zinazohitajiwa ili kupata wokovu. (Waroma 5:3-5; 2 Timotheo 4:7, 8; Yakobo 1:3, 4, 12) Tunahitaji kuwa wavumilivu ili kupata uhai udumuo milele.—Waroma 2:6, 7; Waebrania 10:36.

6. Kuvumilia hadi mwisho humaanisha kufanya nini?

6 Hata hali yetu iwe nzuri kadiri gani mwanzoni, jambo lililo muhimu zaidi hasa ni kuwa na uvumilivu. Yesu alisema: “Yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:13) Naam, ni lazima tuvumilie hadi mwisho, hata ikiwa mwisho huo utamaanisha mwisho wa maisha yetu ya sasa au mwisho wa ulimwengu huu mwovu. Vyovyote vile, tunapaswa kudumisha uaminifu-maadili wetu kwa Mungu. Hata hivyo, tusipoongeza ujitoaji-kimungu kwenye uvumilivu wetu, hatutaweza kumpendeza Yehova, na hatutapata uhai udumuo milele. Lakini ujitoaji-kimungu ni nini?

Ujitoaji-Kimungu Humaanisha Nini?

7. Ujitoaji-kimungu ni nini, nao hutuchochea kufanya nini?

7 Ujitoaji-kimungu humaanisha kumheshimu Yehova Mungu, kumwabudu na kumtumikia ili kuonyesha kwamba tu waaminifu-washikamanifu kwake akiwa mtawala wa ulimwengu wote. Ili tuwe wenye ujitoaji-kimungu kuelekea Yehova, tunahitaji kupata ujuzi sahihi kumhusu yeye na kuhusu njia zake. Tunahitaji kumjua Mungu kwa undani zaidi. Kwa kufanya hivyo tutachochewa kusitawisha uhusiano wa karibu naye, ambao utaonyeshwa kwa matendo na mwenendo wetu. Tunapaswa kujitahidi iwezekanavyo kuwa kama Yehova—kuiga njia zake na kuwa na sifa na utu kama wake. (Waefeso 5:1) Naam, ujitoaji-kimungu hutuchochea kutaka kumpendeza Mungu katika yote tunayofanya.—1 Wakorintho 10:31.

8. Kuna uhusiano gani kati ya ujitoaji-kimungu na kujitoa kwa Yehova peke yake?

8 Ili tuwe na ujitoaji-kimungu wa kweli, ni lazima tumwabudu Yehova peke yake na kumtanguliza katika mioyo yetu. Tunapaswa kujitoa kwa Yehova peke yake kwa kuwa yeye ndiye Muumba wetu. (Kumbukumbu la Torati 4:24; Isaya 42:8) Hata hivyo, Yehova hatulazimishi tumwabudu. Yeye hutaka tujitoe kwake kwa hiari. Kumjua Mungu na kumpenda hutuchochea tuwe safi kimwili na kiadili, tujiweke wakfu kwake kwa hiari, na kuishi kupatana na wakfu huo.

Sitawisha Uhusiano Pamoja na Mungu

9, 10. Tunawezaje kusitawisha na kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu?

9 Baada ya kuonyesha wakfu wetu kwa Mungu kupitia ubatizo, bado tunahitaji kusitawisha uhusiano wa karibu sana pamoja naye. Kwa hiyo, tamaa yetu ya kufanya hivyo na kumtumikia Yehova kwa uaminifu hutuchochea kujifunza na kutafakari Neno lake. Tunaporuhusu roho ya Mungu itende kazi katika akili na mioyo yetu kupitia kujifunza na kutafakari, upendo wetu kwa Yehova huongezeka zaidi. Uhusiano wetu pamoja naye huendelea kuwa jambo muhimu zaidi maishani mwetu, nasi humwona Yehova kuwa Rafiki yetu mkubwa na kutaka kumpendeza nyakati zote. (1 Yohana 5:3) Furaha inayotokana na kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu inaongezeka, na tunashukuru kwamba yeye hutufunza na kutusahihisha inapohitajika.—Kumbukumbu la Torati 8:5.

10 Uhusiano wetu wenye thamani pamoja na Yehova unaweza kufifia tusipoendelea kujitahidi kuuimarisha daima. Hatuwezi kumlaumu Mungu ikiwa uhusiano huo utafifia kwa kuwa “yeye hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Tunafurahi kama nini kwamba Yehova hufanya iwe rahisi kwetu kumfikia! (1 Yohana 5:14, 15) Bila shaka, ni lazima tujitahidi kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Hata hivyo, yeye hutusaidia tumkaribie kwa kutuandalia yote tunayohitaji ili kusitawisha na kudumisha ujitoaji-kimungu. (Yakobo 4:8) Tunawezaje kutumia kikamili maandalizi hayo yote yenye upendo?

Endelea Kuwa Imara Kiroho

11. Ni mambo gani yanayoonyesha kwamba tuna sifa ya ujitoaji-kimungu?

11 Upendo wetu mwingi kwa Mungu utatuchochea kuonyesha kina cha ujitoaji wetu kwake kupatana na ushauri huu wa Paulo: “Fanya yote uwezayo kabisa ili ujionyeshe mwenyewe kuwa mwenye kukubaliwa na Mungu, mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli.” (2 Timotheo 2:15) Ili kufanya hivyo, tunahitaji kuwa na ratiba nzuri ya kujifunza Biblia kwa ukawaida, kuhudhuria mikutano, na kuhubiri. Tunaweza pia kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kwa ‘kusali bila kukoma.’ (1 Wathesalonike 5:17) Hayo ni mambo muhimu yanayoonyesha tuna sifa ya ujitoaji-kimungu. Tukipuuza mojawapo ya mambo hayo tunaweza kuwa wagonjwa kiroho na kufanya iwe rahisi kushambuliwa na Shetani.—1 Petro 5:8.

12. Tunaweza kufanikiwaje kukabiliana na majaribu?

12 Pia, kudumu tukiwa wenye nguvu na bidii kiroho hutusaidia kukabiliana na majaribu mengi yanayotupata. Majaribu fulani yanaweza kuwa magumu sana ikitegemea chanzo chake. Inaweza kuwa vigumu sana kuvumilia ubaridi, upinzani, kunyanyaswa na watu wa familia, watu wa ukoo, au majirani. Huenda tukashawishiwa hatua kwa hatua kuacha kufuata kanuni za Kikristo kazini au shuleni. Kuvunjika moyo, ugonjwa, na mshuko-moyo unaweza kutudhoofisha kimwili na kufanya iwe vigumu sana kuvumilia majaribu ya imani. Lakini tunaweza kufanikiwa kuvumilia majaribu yote tukidumu ‘katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, tukingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.’ (2 Petro 3:11, 12) Na pia tunaweza kufanya hivyo kwa furaha tukiwa na uhakika kwamba Mungu atatubariki.—Mithali 10:22.

13. Tunapaswa kufanya nini ili tuendelee kuonyesha sifa ya ujitoaji-kimungu?

13 Ingawa Shetani hushambulia wale wanaoonyesha sifa ya ujitoaji-kimungu, hatuna haja ya kuogopa. Kwa nini? Kwa sababu “Yehova ajua jinsi ya kukomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.” (2 Petro 2:9) Ili kuvumilia majaribu na kukombolewa, ni lazima “tukatae katakata kukosa kumwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na tuishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mfumo uliopo wa mambo.” (Tito 2:12) Tukiwa Wakristo, tunapaswa kujihadhari tusiruhusu udhaifu wowote unaohusisha tamaa na matendo ya kimwili uharibu sifa yetu ya ujitoaji-kimungu. Hebu tuchunguze baadhi ya mambo yanayoweza kuharibu sifa yetu ya ujitoaji-kimungu.

Jihadhari na Mambo Yanayohatarisha Sifa ya Ujitoaji-Kimungu

14. Tunapaswa kukumbuka nini tunaposhawishiwa kuingia katika mtego wa kufuatia vitu vya kimwili?

14 Ufuatiaji wa vitu vya kimwili hunasa wengi. Huenda tukajidanganya kwa ‘kufikiri kwamba ujitoaji-kimungu ni njia ya kupata faida.’ Hivyo tunaweza kuchochewa kuwatumia vibaya waamini wenzetu ambao wanatutumaini. (1 Timotheo 6:5) Huenda hata tukaamua kimakosa kwamba ni sawa tu kumkaza Mkristo tajiri atukopeshe pesa ambazo yaelekea hatutaweza kulipa. (Zaburi 37:21) “Ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja” haitokani na kuwa na vitu vya kimwili bali inatokana na kuwa na ujitoaji-kimungu. (1 Timotheo 4:8) Kwa kuwa “hatukuleta kitu katika ulimwengu, wala hatuwezi kupeleka kitu chochote nje,” na tufuatie kwa bidii “ujitoaji-kimungu huu pamoja na ujitoshelevu” na ‘turidhike na riziki na cha kujifunika.’—1 Timotheo 6:6-11.

15. Tunaweza kufanya nini ikiwa kufuatia raha kunatuzuia tusiwe na sifa ya ujitoaji-kimungu?

15 Kufuatia raha kunaweza kutuzuia tusiwe na sifa ya ujitoaji-kimungu. Huenda tukahitaji kufanya marekebisho fulani mara moja kuhusiana na jambo hilo. Ni kweli kwamba tunaweza kupata faida fulani kutokana na mazoezi ya kimwili na tafrija. Hata hivyo, faida hizo ni kidogo sana zikilinganishwa na uhai udumuo milele. (1 Yohana 2:25) Leo, watu wengi ni “wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu, wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakithibitika kuwa si kweli kwa nguvu ya hiyo.” Tunapaswa kujiepusha na watu kama hawa. (2 Timotheo 3:4, 5) Wale wanaokazia ujitoaji-kimungu ‘wanajiwekea wenyewe kuwa hazina salama msingi bora kwa ajili ya wakati ujao, ili wao wapate kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi.’—1 Timotheo 6:19.

16. Ni tamaa zipi zenye dhambi ambazo huzuia wengine wasiishi kupatana na matakwa ya Mungu ya uadilifu, na tunaweza kuzishindaje?

16 Sifa yetu ya ujitoaji-kimungu inaweza kuharibiwa na ulevi, madawa ya kulevya, ukosefu wa maadili, na tamaa zenye dhambi. Kushindwa na mambo hayo kunaweza kutuzuia tusiishi kupatana na matakwa ya Mungu ya uadilifu. (1 Wakorintho 6:9, 10; 2 Wakorintho 7:1) Hata Paulo alilazimika kuvumilia pambano lenye kuendelea katika mwili wake wenye dhambi. (Waroma 7:21-25) Tunahitaji kuchukua hatua madhubuti ili kuondoa tamaa zisizofaa. Kwanza kabisa, ni lazima tuazimie kuwa safi kiadili. Paulo anatuambia hivi: “Fisheni viungo vya mwili wenu vilivyo juu ya dunia kwa habari ya uasherati, ukosefu wa usafi, hamu ya ngono, tamaa yenye kuumiza, na tamaa, ambako ni ibada ya sanamu.” (Wakolosai 3:5) Ili kufisha viungo vya mwili wetu kuhusiana na mambo hayo yenye dhambi, tunahitaji kuazimia kuyaondoa kabisa. Kusali kwa bidii ili kupata msaada wa Mungu kutatuwezesha kukataa kabisa tamaa mbaya na kufuatia uadilifu na ujitoaji-kimungu katika ulimwengu huu mwovu.

17. Tunapaswa kuionaje nidhamu?

17 Kuvunjika moyo kunaweza kudhoofisha uwezo wetu wa kuvumilia na kuhatarisha sifa yetu ya ujitoaji-kimungu. Watumishi wengi wa Yehova wamewahi kuvunjika moyo pindi fulani. (Hesabu 11:11-15; Ezra 4:4; Yona 4:3) Kuvunjika moyo kunaweza kuwa na matokeo mabaya sana ikiwa kunaandamana na kinyongo kwa sababu tunahisi kwamba tulikosewa, au kwa sababu tulikaripiwa, au kupewa nidhamu kali. Hata hivyo, karipio na nidhamu huonyesha kwamba Mungu anatupenda na anatujali. (Waebrania 12:5-7, 10, 11) Nidhamu haipaswi kuonwa tu kuwa adhabu bali njia ya kutuzoeza uadilifu. Ikiwa sisi ni wanyenyekevu, tutathamini na kukubali ushauri, tukitambua kwamba “makaripio ya nidhamu ndiyo njia ya uzima.” (Mithali 6:23, NW) Jambo hilo linaweza kutusaidia kufanya maendeleo ya kiroho katika kufuatia ujitoaji-kimungu.

18. Tunapaswa kufanya nini tunapokosewa au kukosea wengine?

18 Huenda hali za kutoelewana, kukosewa au kukosea wengine zikafanya iwe vigumu kwetu kuonyesha sifa ya ujitoaji-kimungu. Huenda mambo hayo yakasababisha hangaiko au kufanya wengine wajitenge na ndugu na dada zao wa kiroho. (Mithali 18:1) Lakini tunapaswa kukumbuka kwamba kuwawekea wengine kinyongo kunaweza kuathiri vibaya sana uhusiano wetu na Yehova. (Mambo ya Walawi 19:18) Kwa kweli, “yeye ambaye hapendi ndugu yake, ambaye ameona, hawezi kuwa anapenda Mungu, ambaye hajaona.” (1 Yohana 4:20) Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alikazia uhitaji wa kuchukua hatua mara moja kusuluhisha mambo tunapokosewa na wengine. Aliwaambia wasikilizaji wake hivi: “Basi, ikiwa wewe unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na huko wakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, toa zawadi yako.” (Mathayo 5:23, 24) Huenda kuomba msamaha kukatuliza maumivu yaliyosababishwa na maneno au matendo yasiyo ya fadhili. Kuomba msamaha na kukubali kwamba tulitenda isivyofaa, kunaweza kusuluhisha mambo na kurudisha uhusiano wenye amani. Yesu pia alitoa ushauri mwingine kuhusu jinsi ya kutatua matatizo. (Mathayo 18:15-17) Tunafurahi kama nini wakati jitihada zetu za kutatua matatizo zinapofanikiwa!—Waroma 12:18; Waefeso 4:26, 27.

Fuata Kielelezo cha Yesu

19. Kwa nini ni muhimu sana kuiga kielelezo cha Yesu?

19 Bila shaka, tutapatwa na majaribu, lakini majaribu hayo hayapaswi kutuzuia kuendelea katika shindano la mbio la kupata uhai udumuo milele. Kumbuka kwamba Yehova anaweza kutuokoa katika jaribu. ‘Tunapoondoa kila uzito’ na ‘kukimbia kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu,’ na ‘tumkazie macho Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.’ (Waebrania 12:1-3) Kuchunguza kielelezo cha Yesu kwa makini na kujitahidi kumwiga kwa maneno na matendo kutatusaidia tusitawishe ujitoaji-kimungu na kuonyesha sifa hiyo kwa kadiri kubwa zaidi.

20. Tunapata thawabu gani kwa kuonyesha uvumilivu na ujitoaji-kimungu?

20 Sifa za uvumilivu na ujitoaji-kimungu zinahusiana sana katika kutusaidia kufanya wokovu wetu kuwa hakika. Kwa kuonyesha sifa hizo nzuri, tunaweza kuendelea kumtolea Mungu utumishi mtakatifu kwa uaminifu. Hata tukipatwa na majaribu, tutakuwa wenye furaha Yehova anapotuonyesha shauku nyororo na kutubariki kwa sababu tumevumilia na tu wenye ujitoaji-kimungu. (Yakobo 5:11) Zaidi ya hayo, Yesu mwenyewe anatuhakikishia hivi: “Kwa uvumilivu kwa upande wenu mtajipatia nafsi zenu.”—Luka 21:19.

Ungejibuje?

• Kwa nini uvumilivu ni muhimu?

• Ujitoaji-kimungu ni nini, nao huonyeshwaje?

• Tunawezaje kusitawisha na kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu?

• Ni mambo gani yanayohatarisha sifa yetu ya ujitoaji-kimungu, nasi tunaweza kuyaepukaje?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Ujitoaji-kimungu huonyeshwa kwa njia mbalimbali

[Picha katika ukurasa wa 14]

Jihadhari na mambo yanayohatarisha sifa yako ya ujitoaji-kimungu