Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Panda kwa Uadilifu, Vuna Fadhili-Upendo za Mungu

Panda kwa Uadilifu, Vuna Fadhili-Upendo za Mungu

Panda kwa Uadilifu, Vuna Fadhili-Upendo za Mungu

“AMDHAMINIYE mgeni hakosi ataumia; achukiaye mambo ya dhamana [“kufanya mapatano kwa kupeana mkono,” “NW”] yu salama.” (Mithali 11:15) Mithali hii fupi inatutia moyo kwa njia yenye kusadikisha kwamba tunapaswa kuwa watu wanaochukua mambo kwa uzito. Ukimkopesha pesa mtu usiyemjua vizuri, unajitafutia matatizo ya kifedha. Epuka kufanya mapatano kwa kupeana mkono—ishara ambayo katika Israeli la kale ilikuwa sawa na kutia sahihi makubaliano—na hivyo kuepuka matatizo ya kifedha.

Bila shaka kanuni ya msingi inayotumika hapa ni: “Lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia.” (Wagalatia 6:7) Nabii Hosea alisema: “Jipandieni katika haki [“uadilifu” NW], vuneni kwa fadhili [“fadhili-upendo,” NW].” (Hosea 10:12) Naam, panda kwa uadilifu kwa kufanya mambo kwa njia ya Mungu na kuvuna fadhili-upendo zake. Kwa kutumia kanuni hii mara nyingi, Mfalme Solomoni wa Israeli anawahimiza watu kwa bidii watende mambo yanayofaa, waseme mambo yanayofaa, na kuwa na mtazamo mzuri. Tunapochunguza kwa makini maneno yake ya hekima, tutatiwa moyo kupanda mbegu kwa uadilifu.—Mithali 11:15-31.

Panda “Adabu,” Vuna ‘Heshima’

“Mwanamke wa adabu huheshimiwa daima; na watu wakali hushika mali siku zote,” asema mfalme mwenye hekima. (Mithali 11:16) Mstari huu unaonyesha tofauti iliyopo kati ya heshima anayopata “mwanamke wa adabu” na mali zisizodumu za mtu mkali.

Mtu anawezaje kujipatia adabu ambayo humletea heshima? Solomoni alitoa shauri hili: “Shika hekima kamili na busara, basi yatakuwa . . . neema shingoni mwako.” (Mithali 3:21, 22) Naye mtunga-zaburi alizungumza kuhusu ‘neema kumiminwa mdomoni mwa mfalme.’ (Zaburi 45:1, 2) Naam, hekima kamili, uwezo wa kufikiri, na kutumia ulimi ifaavyo hufanya mtu awe na adabu na athaminiwe zaidi. Ndivyo ilivyo na mwanamke mwenye busara. Mfano mmoja ni Abigaili, mke wa Nabali mpumbavu. Abigaili alikuwa “mwenye akili njema, mzuri wa uso,” naye Mfalme Daudi alimsifu kwa kuwa alikuwa mwenye “busara.”—1 Samweli 25:3, 33.

Mwanamke anayemwogopa Mungu na mwenye adabu bila shaka ataheshimiwa. Atasifiwa na wengine. Ikiwa ameolewa, ataheshimiwa na mumewe. Kwa kweli, atafanya familia yote iheshimiwe. Heshima yake itadumu. “Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi; na neema kuliko fedha na dhahabu.” (Mithali 22:1) Jina zuri analojifanyia pamoja na Mungu litadumu.

Hali ya mtu mkali au ‘mkatili’ ni tofauti kabisa. (Mithali 11:16, New International Version) Mtu mkali anahesabiwa pamoja na waovu na maadui wa waabudu wa Yehova. (Ayubu 6:23; 27:13) Mtu wa namna hiyo ‘hamweki Mungu mbele zake.’ (Zaburi 54:3) Kwa kukandamiza na kuwatumia vibaya watu wasio na hatia, mtu huyo anaweza ‘kukusanya fedha kama mavumbi.’ (Ayubu 27:16) Hata hivyo, huenda siku moja akalala na kukosa kuamka, ikawa ndiyo siku yake ya mwisho. (Ayubu 27:19) Kisha mali na mafanikio yake yote yatakuwa bure.—Luka 12:16-21.

Andiko la Mithali 11:16 linatufundisha somo zuri kama nini! Kwa kutuonyesha kwa maneno machache yale ambayo tunaweza kuvuna kwa kuwa wenye adabu au kwa kuwa wakali, mfalme wa Israeli atuhimiza tupande kwa uadilifu.

“Fadhili-Upendo” Huthawabisha

Akitufundisha somo jingine juu ya uhusiano wa kibinadamu, Solomoni asema: “Mwenye rehema [“mwenye fadhili-upendo,” “NW”] huitendea mema nafsi yake; aliye mkali hujisumbua mwili wake.” (Mithali 11:17) Msomi mmoja asema kwamba ‘jambo kuu katika mithali hiyo ni kwamba mtu atapatwa na matokeo hata kama hakukusudia au hakuyatarajia ikitegemea jinsi anavyowatendea wengine iwe ni kwa njia inayofaa au isiyofaa.’ Mfikirie mwanamke kijana anayeitwa Lisa. * Ijapokuwa ana nia njema, yeye huchelewa kila mara anapopanga kukutana na wengine. Ni kawaida yake kuchelewa dakika 30 au zaidi anapopanga kukutana na watangazaji wengine wa Ufalme ili kwenda kuhubiri. Lisa hajitendei mema. Je, anaweza kuwalaumu wengine iwapo watachoka kupoteza wakati wao wenye thamani na kukataa kukutana naye wakati ujao?

Mtu ambaye hutaka kufanya mambo kikamilifu—mtu anayejiwekea viwango vya juu—hujitendea kikatili. Sikuzote yeye hujitahidi kutimiza miradi isiyoweza kufikiwa ambayo amejiwekea na hivyo huchoka na kukata tamaa. Kwa upande mwingine, tunapojiwekea miradi ya kiasi na tunayoweza kufikia, tunajitendea mema. Labda sisi huelewa mambo polepole. Au labda hatuwezi kufanya mambo fulani kwa sababu ya ugonjwa au uzee. Tusifadhaike kamwe kwa sababu ya maendeleo ya kiroho tunayofanya, lakini sikuzote tuendelee kuwa na kiasi tunapokabiliana na udhaifu wetu. Tutakuwa wenye furaha ‘tukifanya yote tuwezayo’ kulingana na uwezo wetu.—2 Timotheo 2:15; Wafilipi 4:5.

Akieleza kindani kwamba mtu mwadilifu hujinufaisha ilhali mtu mkali hujiumiza, mfalme mwenye hekima asema: “Mtu mwovu hupata mshahara wa udanganyifu; apandaye haki [“uadilifu,” “NW”] ana thawabu ya hakika. Haki huelekea uzima; afuataye maovu hufuata mauti yake mwenyewe. Wenye kuhalifu moyoni ni chukizo kwa BWANA; walio wakamilifu katika njia zao humpendeza. [“Wajaposhikana mkono kwa mkono,” “NW”] hakika mtu mwovu hatakosa adhabu, bali wazao wa wenye haki wataokoka.”Mithali 11:18-21.

Mistari hii inakazia jambo hili muhimu katika njia mbalimbali: Panda kwa uadilifu na kuvuna thawabu. Huenda mwovu akaamua kudanganya au kucheza kamari ili apate pesa pasipo kutoa jasho. Kwa kuwa mshahara huo ni wa udanganyifu, huenda akakata tamaa. Mtu anayefanya kazi kwa bidii hupata thawabu hakika, yaani atakuwa na usalama. Kwa sababu ya kuwa na kibali cha Mungu, mtu asiye na lawama ana tumaini la kuishi milele. Lakini mtu mbaya atapatwa na nini? “Wajaposhikana mkono kwa mkono” kupanga mambo ya uhaini, mwovu hataepuka adhabu. (Mithali 2:21, 22) Hilo ni himizo zuri kama nini la kupanda kwa uadilifu!

Uzuri Halisi kwa Mwenye Busara

Solomoni aendelea kusema, “kama pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe, kadhalika mwanamke mzuri asiye na akili [“asiye na busara,” “NW”].” (Mithali 11:22) Pete zilizowekwa puani zilipendwa sana nyakati za Biblia. Pete ya dhahabu ilikuwa kito kilichoonekana kwa urahisi ilipowekwa puani mwa mwanamke. Haingefaa kutia pete nzuri kama hiyo puani mwa nguruwe. Ndivyo ilivyo na mtu mwenye sura nzuri “asiye na busara.” Haifai kwa mtu kama huyo kujipamba. Havutii hata kidogo.

Ni kweli kwamba ni jambo la kawaida kuhangaikia sura zetu. Lakini kwa nini tuhangaikie sura zetu au maumbile yetu kupita kiasi? Hatuwezi kubadili sehemu kubwa ya maumbile yetu. Kuna mambo mengine yaliyo muhimu kuliko sura. Je, si kweli kwamba watu wengi tunaowapenda na wanaotuvutia wana sura ya kawaida tu? Furaha haitegemei kuwa na sura nzuri. Jambo lenye thamani ni sifa za moyoni ambazo huonyesha utu wa Mungu. Na tuwe wenye busara na kusitawisha sifa hizo.

‘Nafsi ya Mtu Mkarimu Itafanikishwa’

Mfalme Solomoni asema, “haja ya mwenye haki ni mema tu; bali kutaraji kwake mtu mwovu ni ghadhabu.” Akieleza ukweli wa maneno hayo, yeye aendelea kusema: “Kuna atawanyaye, lakini huongezewa zaidi; kuna azuiaye isivyo haki, lakini huelekea uhitaji.”Mithali 11:23, 24.

Tunapotawanya kwa bidii—kuwapa wengine—ujuzi wa Neno la Mungu, bila shaka tunaboresha uelewevu wetu wa “upana na urefu na kimo na kina” cha neno hilo. (Waefeso 3:18) Kwa upande mwingine, mtu asiyetumia ujuzi wake huenda akaupoteza. Naam, “yeye apandaye kwa uhaba atavuna pia kwa uhaba; na yeye apandaye kwa wingi atavuna pia kwa wingi.”—2 Wakorintho 9:6.

Mfalme aendelea kusema, “nafsi ya mtu mkarimu itawandishwa; [itafanikishwa] anyweshaye atanyweshwa mwenyewe.” (Mithali 11:25) Tunapotumia wakati na mali zetu kwa ukarimu ili kuendeleza ibada ya kweli, tunamfurahisha sana Yehova. (Waebrania 13:15, 16) ‘Atatufungulia madirisha ya mbinguni, na kutumwagia baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha.’ (Malaki 3:10) Ona jinsi watumishi wake wanavyofanikiwa kiroho leo!

Akitoa mfano mwingine unaoonyesha tofauti iliyopo kati ya tamaa ya mwadilifu na mwovu, Solomoni asema: “Awanyimaye watu nafaka, watu watamlaani; auzaye nafaka, baraka itakuwa kichwani pake.” (Mithali 11:26) Mtu anaweza kupata faida kwa kununua vitu kwa bei ya chini na kuvibania hadi bei inapoongezeka. Hata ingawa huenda ikanufaisha kubania bidhaa na kubakisha kiasi fulani, kwa ujumla watu huchukia mtu anayefanya hivyo kwa sababu ya uchoyo. Kwa upande mwingine, watu humpenda mtu asiyejipatia faida kubwa wakati wa hali ya dharura.

Akitutia moyo tuendelee kutamani mema, au mambo ya uadilifu, mfalme wa Israeli asema: “Atafutaye mema kwa bidii hutafuta fadhili; atafutaye madhara, hayo yatamjia. Azitegemeaye mali zake ataanguka; mwenye haki atasitawi kama jani.”Mithali 11:27, 28.

Mwadilifu Huvuta Watu

Akieleza jinsi tendo la upumbavu huleta matokeo mabaya, Solomoni asema: “Ataabishaye nyumba yake mwenyewe ataurithi upepo.” (Mithali 11:29a) Akani ‘alitaabishwa’ na kosa lake mwenyewe, kisha yeye pamoja na familia yake wakapigwa mawe hadi wakafa. (Yoshua, sura ya 7) Leo, kichwa cha familia ambaye ni Mkristo na washiriki wa familia yake wanaweza kufanya kosa zito linaloweza kufanya watengwe na ushirika wa kutaniko la Kikristo. Kwa kutotii amri za Mungu na kuruhusu kosa zito katika familia yake, mtu anaweza kuitaabisha familia yake. Labda yeye pamoja na wengine katika familia yake watatengwa na ushirika wa Kikristo kwa kuwa wakosaji wasiotubu. (1 Wakorintho 5:11-13) Naye atapata nini? Upepo tu—kitu kisicho na thamani yoyote.

Mstari huo waendelea kusema, “mpumbavu atakuwa mtumwa wa mtu mwenye moyo wa akili.” (Mithali 11:29b) Kwa kuwa mpumbavu hatumii hekima, hawezi kupewa madaraka makubwa. Isitoshe, kwa kuwa hawezi kusimamia mambo yake vizuri analazimika kutegemea mtu mwingine katika njia fulani. Mtu huyo mpumbavu anaweza kuwa “mtumwa wa mtu mwenye moyo wa akili.” Bila shaka, tunapaswa kutumia utambuzi na hekima katika shughuli zetu zote.

Mfalme mwenye hekima atuhakikishia hivi: “Mazao ya mwenye haki ni mti wa uzima; na mwenye hekima huvuta roho za watu [“huvuta watu,” “Biblia Habari Njema”].” (Mithali 11:30) Yeye hufanyaje hivyo? Mtu mwadilifu huwajenga wengine kiroho kupitia usemi na mwenendo wake, na huwatia moyo kumtumikia Yehova na hatimaye huenda watu hao wakapokea uhai kutoka kwa Mungu.

‘Mkosaji Atalipwa Mara Nyingi Zaidi’

Mithali ambazo zimetajwa zinatutia moyo tuonyeshe sifa ya uadilifu. Akitumia kwa njia nyingine ile kanuni ya kwamba “lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia,” Solomoni asema: “Tazama, mwenye haki atalipwa duniani; basi mwovu na mkosaji si mara nyingi zaidi?”Mithali 11:31.

Hata ingawa mtu mwadilifu hujitahidi kufanya linalofaa, yeye hukosea nyakati nyingine. (Mhubiri 7:20) Naye “atalipwa” makosa yake kwa kupewa nidhamu. Namna gani mwovu ambaye amekusudia kufuata mwenendo mbaya bila kufanya jitihada yoyote ya kufuata njia ya uadilifu? Je, hastahili kupewa ‘malipo’ makubwa zaidi, yaani, adhabu kali zaidi? Mtume Petro aliandika hivi: “Ikiwa ni kwa shida mtu mwadilifu anaokolewa, mtu asiyemwogopa Mungu na mtenda-dhambi wataonekana wapi?” (1 Petro 4:18) Na tuazimie sikuzote, kupanda mbegu kwa uadilifu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Jina limebadilishwa hapa.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Abigaili alipata ‘heshima’ kwa sababu alikuwa na “adabu”

[Picha katika ukurasa wa 30]

‘Mtu mwovu anapata mshahara wa udanganyifu, naye mwadilifu hupata thawabu ya hakika’

[Picha katika ukurasa wa 31]

‘Panda kwa wingi, vuna kwa wingi’