Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakristo Huabudu kwa Roho na Kweli

Wakristo Huabudu kwa Roho na Kweli

Wakristo Huabudu kwa Roho na Kweli

“Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yeye lazima waabudu kwa roho na kweli.”—YOHANA 4:24.

1. Mungu hupendezwa na ibada ya aina gani?

YESU KRISTO, Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova alionyesha waziwazi ibada ambayo inampendeza Baba yake wa mbinguni. Alipokuwa akimtolea ushahidi wenye kusisimua mwanamke mmoja Msamaria kwenye kisima kimoja karibu na jiji la Sikari, Yesu alisema: “Nyinyi mwaabudu kile msichojua; sisi twaabudu kile tujuacho, kwa sababu wokovu hutokana na Wayahudi. Hata hivyo, saa inakuja, nayo ipo sasa, wakati waabudu wa kweli watakapomwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta wa namna hiyo wamwabudu yeye. Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yeye lazima waabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:22-24) Maneno hayo yanamaanisha nini?

2. Ibada ya Wasamaria ilitegemea nini?

2 Wasamaria walikuwa na maoni ya kidini yasiyo ya kweli. Walikubali tu vitabu vitano vya kwanza vya Maandiko Matakatifu kuwa ndivyo vilivyoandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Lakini walikubali tafsiri yao wenyewe ya vitabu hivyo, iliyoitwa Pentateuki ya Wasamaria. Ingawa Wasamaria hawakumjua Mungu, Wayahudi walikuwa wamefundishwa Maandiko. (Waroma 3:1, 2) Wayahudi waaminifu na watu wengineo wangeweza kupata kibali cha Yehova. Lakini walipaswa kufanya nini?

3. Ni nini kinachohitajiwa ili kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli”?

3 Wayahudi, Wasamaria, na watu wengine walipaswa kufanya nini ili kumpendeza Yehova? Walipaswa kumwabudu “kwa roho na kweli.” Nasi tunapaswa kufanya hivyo. Ingawa tunapaswa kumtumikia Mungu kwa bidii na kuchochewa na moyo uliojaa upendo na imani, kumwabudu Mungu kwa roho hasa huhitaji tuwe na roho yake takatifu na kuiruhusu ituongoze. Kujifunza na kufuata Neno la Mungu kunapaswa kutusaidia kuwa na mtazamo kama wa Mungu. (1 Wakorintho 2:8-12) Ili Yehova akubali ibada yetu, ni lazima pia tumwabudu katika kweli. Lazima ibada hiyo ipatane na yale ambayo Neno la Mungu, Biblia, hufunua kumhusu na kuhusu makusudi yake.

Kweli Inaweza Kupatikana

4. Watu wengine huionaje kweli?

4 Watu fulani wanaojifunza falsafa wamekuwa na maoni kwamba wanadamu hawawezi kupata kweli kamili. Hata mwandishi Alf Ahlberg kutoka Sweden aliandika hivi: “Kuna maswali mengi ya kifalsafa ambayo hayawezi kujibiwa kikamili.” Ingawa wengine husema kwamba hakuna kweli inayoweza kutegemeka kabisa, je, ndivyo ilivyo? Yesu Kristo hakuwa na maoni hayo.

5. Kwa nini Yesu alikuja ulimwenguni?

5 Na tuwazie kwamba tunatazama tukio lifuatalo: Ni mapema mwaka wa 33 W.K., na Yesu amesimama mbele ya Gavana Mroma Pontio Pilato. Yesu anamwambia Pilato hivi: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” Kisha Pilato anamwuliza hivi: “Kweli ni nini?” Lakini hangojei Yesu aeleze zaidi.—Yohana 18:36-38.

6. (a) “Kweli” imefafanuliwaje? (b) Yesu aliwapa wafuasi wake mgawo gani?

6 “Kweli” imefafanuliwa kuwa “kinyume cha uongo.” (Kamusi ya Kiswahili Sanifu) Hata hivyo, je, Yesu alitoa ushahidi juu ya kweli kwa ujumla? La. Yesu alikuwa anazungumzia kweli hususa. Aliwapa wafuasi wake mgawo wa kuitangaza kweli hiyo, kwa kuwa aliwaambia hivi: ‘Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.’ (Mathayo 28:19, 20) Kabla “ya umalizio wa mfumo wa mambo,” wafuasi wa kweli wa Yesu wangetangaza “kweli ya habari njema” duniani pote. (Mathayo 24:3; Wagalatia 2:14) Kwa kufanya hivyo wangetimiza maneno haya ya Yesu: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Kwa hiyo, ni muhimu kuwatambua wale wanaofundisha mataifa ile kweli kwa kuhubiri habari njema ya Ufalme.

Jinsi Tunavyoweza Kujifunza Kweli

7. Unaweza kuthibitishaje kwamba Yehova ndiye Chanzo cha ile kweli?

7 Yehova ndiye Chanzo cha ile kweli ya kiroho. Hata mtunga-zaburi Daudi alimwita Yehova “Mungu wa kweli.” (Zaburi 31:5; 43:3) Yesu alikubali kwamba neno la Baba yake ni kweli, na pia akatangaza hivi: “Imeandikwa katika Manabii, ‘Na wote watafundishwa na Yehova.’ Kila mtu ambaye amesikia kutoka kwa Baba na ambaye amejifunza huja kwangu.” (Yohana 6:45; 17:17; Isaya 54:13) Hivyo basi, lazima wale wanaotafuta kweli wafundishwe na Yehova, yule Mfunzi Mtukufu. (Isaya 30:20, 21, NW) Wale wanaotafuta kweli wanahitaji “kumjua Mungu.” (Mithali 2:5) Na kwa upendo Yehova amefundisha au kutupatia kweli kwa njia mbalimbali.

8. Mungu amefundisha au kutupatia ile kweli kwa njia zipi?

8 Kwa mfano, Mungu aliwapa Waisraeli Sheria yake kupitia malaika. (Wagalatia 3:19) Kupitia ndoto, aliahidi kuwabariki wazee wa ukoo, Abrahamu na Yakobo. (Mwanzo 15:12-16; 28:10-19) Mungu hata alizungumza kutoka mbinguni, kama wakati wa ubatizo wa Yesu ambapo maneno haya yenye kusisimua yalisikiwa duniani: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Tunaweza pia kushukuru kwamba Mungu ametupatia kweli yake kwa kutumia roho yake takatifu kuwaongoza waandikaji wa Biblia. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa kujifunza Neno la Mungu tunaweza kuwa na ‘imani katika kweli.’—2 Wathesalonike 2:13.

Kweli na Mwana wa Mungu

9. Mungu amemtumiaje Mwana wake ili kuifunua ile kweli?

9 Mungu ametumia hasa Mwana wake, Yesu Kristo kuwafunulia wanadamu ile kweli. (Waebrania 1:1-3) Kwa kweli, Yesu alifundisha kweli kwa njia isiyo na kifani. (Yohana 7:46) Hata baada ya kupaa mbinguni, alifunua kweli kutoka kwa Baba yake. Kwa mfano, mtume Yohana alipokea “ufunuo kupitia Yesu Kristo, ambao Mungu alimpa, kuonyesha watumwa wake mambo ambayo lazima yatukie upesi.”—Ufunuo 1:1-3.

10, 11. (a) Kweli ambayo Yesu alitoa ushahidi juu yake inahusiana na nini? (b) Yesu aliifanya kweli iwe halisi jinsi gani?

10 Yesu alimwambia Pontio Pilato kwamba Alikuja duniani kutoa ushahidi juu ya ile kweli. Wakati wa huduma yake, Yesu alifunua kwamba kweli hiyo ilihusiana na kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova kupitia Ufalme wake chini ya Kristo akiwa Mfalme. Ili kutoa ushahidi juu ya ile kweli, Yesu alihitaji kufanya mengi zaidi ya kuhubiri na kufundisha. Yesu alifanya kweli hiyo iwe halisi kwa kuifuata katika maisha yake. Kwa hiyo, mtume Paulo aliandika: “Msiache mtu yeyote awahukumu nyinyi katika kula na kunywa au kwa habari ya msherehekeo au mwadhimisho wa mwezi mpya au wa sabato; kwa maana mambo haya ni kivuli cha mambo yajayo, bali uhalisi ni wa Kristo.”—Wakolosai 2:16, 17.

11 Kweli ilipata kuwa halisi Yesu alipozaliwa Bethlehemu kama ilivyokuwa imetabiriwa. (Mika 5:2; Luka 2:4-11) Kweli pia ilipata kuwa halisi wakati unabii wa Danieli kuhusu kutokea kwa Mesiya ulipotimizwa baada ya ‘majuma 69 ya miaka.’ Jambo hilo lilitukia Yesu alipojitoa kwa Mungu wakati wa ubatizo na kutiwa mafuta kwa roho takatifu mwaka wa 29 W.K., wakati barabara uliokuwa umetabiriwa. (Danieli 9:25; Luka 3:1, 21, 22) Kweli pia ilipata kuwa halisi kupitia huduma ya Yesu ya kuelimisha watu akiwa mtangazaji wa Ufalme. (Isaya 9:1, 2, 6, 7; 61:1, 2; Mathayo 4:13-17; Luka 4:18-21) Pia kweli ilipata kuwa halisi kupitia kifo na ufufuo wake.—Zaburi 16:8-11; Isaya 53:5, 8, 11, 12; Mathayo 20:28; Yohana 1:29; Matendo 2:25-31.

12. Kwa nini Yesu angeweza kusema, ‘Mimi ndiyo kweli’?

12 Kwa kuwa kweli ilikazia Yesu Kristo, yeye angeweza kusema hivi: “Mimi ndiyo njia na kweli na uhai. Hakuna ajaye kwa Baba ila kupitia mimi.” (Yohana 14:6) Watu huwekwa huru kiroho wanaposimama “upande wa ile kweli” kwa kukubali daraka la Yesu kuhusiana na kusudi la Mungu. (Yohana 8:32-36; 18:37) Watu wenye mfano wa kondoo watapata uhai udumuo milele kwa sababu wao huikubali kweli na humfuata Kristo kwa imani.—Yohana 10:24-28.

13. Tutachunguza kweli ya Kimaandiko katika maeneo gani matatu?

13 Kweli iliyofundishwa na Yesu na wanafunzi wake walioongozwa na roho ya Mungu, ndiyo hufanyiza mafundisho ya Wakristo wa kweli. Kwa hiyo, wale ‘walio watiifu kwa imani huendelea kutembea katika kweli.’ (Matendo 6:7; 3 Yohana 3, 4) Hivyo basi, ni nani wanaotembea katika kweli leo? Ni nani hasa wanaofundisha mataifa ile kweli? Ili kujibu maswali hayo, tutakazia fikira Wakristo wa mapema na kuchunguza kweli ya Kimaandiko kuhusiana na (1) imani, (2) njia ya kuabudu, na (3) mwenendo wa mtu binafsi.

Kweli na Imani

14, 15. Ungesema Wakristo wa mapema na Mashahidi wa Yehova wana maoni gani kuhusu Maandiko?

14 Wakristo wa mapema waliliheshimu sana Neno la Yehova lililoandikwa. (Yohana 17:17) Walilitumia kuamua ni imani na desturi gani zinazofaa na zisizofaa. Clement wa Alexandria aliyeishi katika karne ya pili na ya tatu alisema: “Wale wanaojitahidi kupata sifa bora hawataacha kuitafuta kweli hadi watakapothibitishiwa imani yao kupitia Maandiko.”

15 Kama Wakristo wa mapema, Mashahidi wa Yehova wanaiheshimu sana Biblia. Wanaamini kwamba “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha.” (2 Timotheo 3:16) Kwa hiyo, na tuchunguze mambo kadhaa ambayo Wakristo wa mapema waliamini na kuyalinganisha na yale ambayo watumishi wa Yehova wa siku hizi wamejifunza kwa sababu Biblia ndicho kitabu chao kikuu cha mafundisho.

Kweli Kuhusu Nafsi

16. Ukweli ni nini kuhusu nafsi?

16 Kwa kuwa waliyaamini Maandiko, Wakristo wa mapema walifundisha kweli kuhusu nafsi. Walijua kwamba ‘mtu alipata kuwa nafsi hai’ Mungu alipomwumba. (Mwanzo 2:7) Zaidi ya hayo, walijua kwamba nafsi ya mwanadamu hufa. (Ezekieli 18:4, ZSB; Yakobo 5:20) Pia walijua kwamba “wafu hawajui neno lo lote.”—Mhubiri 9:5, 10.

17. Unaweza kuelezaje tumaini la wafu?

17 Wanafunzi wa mapema wa Yesu walikuwa na tumaini hakika kwamba wafu walio katika kumbukumbu la Mungu watafufuliwa waishi tena. Imani yao ilidhihirishwa na Paulo aliyesema: “Nina tumaini kuelekea Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Hata Minucius Felix, aliyedai kuwa Mkristo, aliandika hivi baadaye: ‘Ni nani ambaye ni mpumbavu au amekosa akili sana hivi kwamba angethubutu kudai kuwa Mungu ambaye alimwumba mwanadamu hawezi kumwumba tena upya?’ Kama Wakristo wa mapema, Mashahidi wa Yehova wanaamini kweli ya Maandiko kuhusu nafsi ya mwanadamu, kifo, na ufufuo. Hebu sasa tuchunguze Mungu ni nani na Kristo ni nani?

Kweli na Utatu

18, 19. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Utatu si fundisho la Kimaandiko?

18 Wakristo wa mapema hawakuamini kwamba Mungu, Kristo, na roho takatifu ni Utatu. Kichapo The Encyclopædia Britannica kinasema: “Hakuna neno Utatu wala fundisho lililo wazi kuhusu Utatu katika Agano Jipya. Hata Yesu na wafuasi wake hawakutaka kupinga Shema [sala ya Waebrania] katika Agano la Kale inayosema: ‘Sikiliza, Ee Israeli; Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja’ (Kum. 6:4).” Wakristo hawakuabudu utatu wa Waroma au miungu mingine yoyote. Walikubali maneno ya Yesu kwamba Yehova peke yake ndiye anayepaswa kuabudiwa. (Mathayo 4:10) Zaidi ya hayo, waliamini maneno haya ya Kristo: “Baba ni mkubwa zaidi kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Mashahidi wa Yehova wanaamini vivyo hivyo leo.

19 Wakristo wa mapema walijua vizuri tofauti kati ya Mungu, Kristo, na roho takatifu. Hata waliwabatiza wanafunzi (1) kwa jina la Baba, (2) kwa jina la Mwana, na (3) kwa jina la roho takatifu, bali si kwa jina la Utatu. Mashahidi wa Yehova pia hufundisha kweli hiyo ya Kimaandiko na hivyo wao huonyesha tofauti kati ya Mungu, Mwana wake, na roho takatifu.—Mathayo 28:19.

Kweli na Ubatizo

20. Wale wanaotaka kubatizwa wanahitaji kujua nini?

20 Yesu aliwapa wafuasi wake mgawo wa kuwafanya watu kuwa wanafunzi kwa kuwafundisha ile kweli. Ili wastahili kubatizwa, wanahitaji kuwa na ujuzi wa msingi wa Maandiko. Kwa mfano, ni lazima wajue cheo na mamlaka ya Baba na ya Mwana wake, Yesu Kristo. (Yohana 3:16) Wale wanaotaka kubatizwa wanahitaji kujua kwamba roho takatifu si mtu bali ni nguvu ya utendaji ya Mungu.—Matendo 2:1-4.

21, 22. Kwa nini unaweza kusema kwamba ubatizo ni wa wale wanaoamini?

21 Wakristo wa mapema walibatiza tu watu waliokuwa na ujuzi, waliotubu, na ambao walikuwa wamejiweka wakfu kwa Mungu bila masharti yoyote ili kufanya mapenzi yake. Wayahudi na wageuzwa imani ambao walikusanyika Yerusalemu kwenye Pentekoste 33 W.K., walijua Maandiko ya Kiebrania. Walipomsikia mtume Petro akizungumza kuhusu Mesiya, watu 3,000 hivi ‘walikubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo’ na ‘kubatizwa.’—Matendo 2:41; 3:19–4:4; 10:34-38.

22 Ubatizo wa Kikristo ni wa wale wanaoamini. Watu wa Samaria walikubali kweli, na “walipomwamini Filipo, aliyekuwa akitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu na juu ya jina la Yesu Kristo, waliendelea kubatizwa, wanaume na pia wanawake.” (Matendo 8:12) Akiwa mgeuzwa imani mwenye bidii na aliyemjua Yehova, towashi Mwethiopia kwanza alikubali maelezo ya Filipo kuhusu utimizo wa unabii wa Kimesiya, kisha akabatizwa. (Matendo 8:34-36) Baadaye, Petro alimwambia Kornelio na watu wengine wasio Wayahudi kwamba “mtu ambaye humhofu [Mungu] na kutenda uadilifu akubalika kwake” na kwamba kila mtu anayemwamini Yesu Kristo husamehewa dhambi. (Matendo 10:35, 43; 11:18) Mambo hayo yote yanapatana na amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo aliamuru.’ (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8) Mashahidi wa Yehova hufanya vivyo hivyo, nao hukubali tu kubatiza watu ambao wana ujuzi wa msingi wa Maandiko na ambao wamejiweka wakfu kwa Mungu.

23, 24. Ubatizo wa Kikristo unaofaa ni gani?

23 Wanaoamini wanapaswa kubatizwa kwa kuzamishwa kabisa katika maji. Baada ya Yesu kubatizwa katika Mto Yordani, “alipanda kutoka majini.” (Marko 1:10) Yule towashi Mwethiopia alibatizwa katika “maji fulani.” Yeye na Filipo ‘waliteremka na kuingia katika maji’ kisha ‘wakapanda kutoka kwenye maji.’ (Matendo 8:36-40) Maandiko yanafananisha ubatizo na kuzikwa, jambo ambalo pia linaonyesha kuzamishwa kabisa katika maji.—Waroma 6:4-6; Wakolosai 2:12.

24 Kichapo The Oxford Companion to the Bible kinasema: ‘Maelezo katika Agano Jipya kuhusu ubatizo yanaonyesha kwamba mtu aliyebatizwa alichovywa ndani ya maji.’ Kitabu cha Kifaransa Larousse du XXe Siècle (Paris, 1928) kinasema kwamba, “Wakristo wa mapema walibatizwa kwa kuzamishwa mahali popote ambapo maji yalipatikana.” Nacho kitabu After Jesus—The Triumph of Christianity kinasema: ‘Kwa kawaida, yule anayetaka kubatizwa alipaswa kutangaza imani, kisha kuzamishwa kabisa katika maji katika jina la Yesu.’

25. Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

25 Mambo yaliyotajwa kuhusu imani na desturi za Wakristo wa mapema ambazo zilitegemea Biblia ni mifano tu. Tunaweza kutaja mambo mengine ambayo Wakristo hao wa mapema waliamini ambayo Mashahidi wa Yehova wanaamini pia. Katika makala inayofuata, tutazungumzia njia nyingine za kuwatambua wale wanaofundisha watu ile kweli.

Ungejibuje?

• Mungu anataka ibada ya aina gani?

• Kweli ilipataje kuwa halisi kupitia Yesu Kristo?

• Ukweli ni nini kuhusu nafsi na kifo?

• Ubatizo wa Kikristo hufanywaje, nao wanaotaka kubatizwa wanapaswa kufanya nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yesu alimwambia Pilato hivi: ‘Nimekuja kutoa ushahidi juu ya ile kweli’

[Picha katika ukurasa wa 17]

Unaweza kueleza ni kwa nini Yesu alisema: ‘Mimi ndiyo kweli’?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ukweli ni nini kuhusu ubatizo wa Kikristo?