Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanaendelea Kutembea Katika Kweli

Wanaendelea Kutembea Katika Kweli

Wanaendelea Kutembea Katika Kweli

“Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.”—3 YOHANA 4.

1. “Kweli ya habari njema” hukazia nini?

YEHOVA huwakubali tu wale wanaomwabudu “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Wao hutii kweli na kukubali mafundisho yote ya Kikristo yanayotokana na Neno la Mungu. ‘Kweli hii ya habari njema’ hukazia Yesu Kristo na kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova kupitia Ufalme. (Wagalatia 2:14) Mungu huruhusu “utendaji wa kosa” uwaendee wale wanaopendelea uwongo, lakini wokovu unategemea kuwa na imani katika habari njema na kutembea katika kweli.—2 Wathesalonike 2:9-12; Waefeso 1:13, 14.

2. Mtume Yohana alikuwa mwenye shukrani kwa mambo gani hasa, naye alikuwa na uhusiano gani pamoja na Gayo?

2 Watangazaji wa Ufalme ni “wafanyakazi wenzi katika kweli.” Kama mtume Yohana na rafikiye Gayo, wao hufuata kweli bila kuyumbayumba na hutembea katika kweli. Huku akimfikiria Gayo, Yohana aliandika: “Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.” (3 Yohana 3-8) Hata ingawa Yohana hakumfundisha Gayo kweli, mwanamume huyo, ambaye yaonekana alikuwa na umri mdogo, alifaa kuitwa mtoto wa kiroho wa Yohana. Hiyo ni kwa sababu mtume huyo alikuwa mzee kwa umri na alikuwa Mkristo mkomavu mwenye upendo kama wa baba.

Kweli na Ibada ya Kikristo

3. Mikutano iliyofanywa na Wakristo wa mapema ilikuwa na kusudi na manufaa gani?

3 Ili kujifunza kweli, Wakristo wa mapema walikutana pamoja wakiwa kutaniko. Mara nyingi walikutana katika nyumba za watu. (Waroma 16:3-5) Kwa hiyo, walitiana moyo na kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora. (Waebrania 10:24, 25) Kuhusu wale waliodai kuwa Wakristo nyakati za baadaye, Tertullian (wapata mwaka wa 155 W.K.–baada ya mwaka wa 220 W.K.) aliandika hivi: “Tunakutana ili kusoma vitabu vya Mungu . . . Kwa maneno hayo matakatifu tunajenga imani yetu, tunakuza tumaini letu, na kuimarisha uhakika wetu.”—Apology, sura ya 39.

4. Kuimba kumetimiza fungu gani katika mikutano ya Kikristo?

4 Yaelekea Wakristo wa mapema waliimba kwenye mikutano. (Waefeso 5:19; Wakolosai 3:16) Profesa Henry Chadwick aandika kwamba Celsus, mchambuzi mmoja wa karne ya pili, aligundua kwamba nyimbo tamu zilizoimbwa na wale waliodai kuwa Wakristo ‘zilikuwa nzuri sana hivi kwamba alichukizwa na jinsi zilivyovutia hisia za watu.’ Naye Chadwick anaongeza kusema: “Clement wa Alexandria, ndiye mwandikaji Mkristo wa mapema zaidi kuandika kuhusu aina ya muziki unaofaa kwa Wakristo. Anasema kwamba muziki huo haupaswi kuhusisha dansi yenye kuchochea hisia za kingono.” (The Early Church, ukurasa wa 274-275) Inaonekana wazi kwamba Wakristo wa mapema waliimba walipokutana pamoja. Vivyo hivyo Mashahidi wa Yehova huimba nyimbo zilizotungwa kutoka kwa Biblia, ambazo zina maneno yenye nguvu ya kumtukuza Mungu na Ufalme.

5. (a) Mwongozo wa kiroho ulitolewaje katika makutaniko ya Wakristo wa mapema? (b) Wakristo wa kweli wamefuataje maneno ya Yesu kwenye Mathayo 23:8, 9?

5 Katika makutaniko ya Wakristo wa mapema, wazee walifundisha kweli, nao watumishi wa huduma waliwasaidia waamini wenzao katika njia mbalimbali. (Wafilipi 1:1) Baraza linaloongoza ambalo lilitegemea Neno la Mungu na roho takatifu liliandaa mwongozo wa kiroho. (Matendo 15:6, 23-31) Hakukuwa na vyeo vya kidini kwa kuwa Yesu aliamuru wanafunzi wake hivi: “Msiitwe Rabi, kwa maana mmoja ni mwalimu wenu, lakini nyinyi nyote ni akina ndugu. Zaidi ya hayo, msiite yeyote baba yenu duniani, kwa maana mmoja ni Baba yenu, Aliye wa kimbingu.” (Mathayo 23:8, 9) Katika njia hiyo na njia nyingine mbalimbali, kuna ufanani kati ya Wakristo wa mapema na Mashahidi wa Yehova.

Wanyanyaswa kwa Kuhubiri Kweli

6, 7. Ingawa wanatangaza ujumbe wa amani, Wakristo wa kweli wametendewaje?

6 Ingawa walitangaza ujumbe wa amani wa Ufalme, Wakristo wa mapema walinyanyaswa kama Yesu alivyonyanyaswa. (Yohana 15:20; 17:14) Mwanahistoria John L. von Mosheim alisema kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa ‘kikundi cha watu ambao hawakuwa hatari kwa watu wengine. Hawakuwa na uadui kuelekea serikali.’ Dakt. Mosheim alisema kwamba “Wakristo waliwakasirisha Waroma kwa sababu ya ibada yao sahili, ambayo haikufanana hata kidogo na sherehe takatifu za ibada za watu wengine.” Aliendelea kusema hivi: ‘Hawakutoa dhabihu wala hawakuwa na mahekalu, sanamu, watabiri, wala makasisi. Mambo hayo yalifanya watu wasiojua ukweli wa mambo wawashutumu kwa kuwa walifikiri kwamba hakuna dini isiyokuwa na sherehe takatifu za ibada. Hivyo Wakristo hao walionwa kuwa waatheisti, yaani, watu wasioamini kuna Mungu; na kulingana na sheria za Waroma, waatheisti walionwa kuwa watu waliosumbua jamii.’

7 Makasisi, wasanii, na watu wengineo ambao walipata riziki yao kutokana na ibada ya sanamu walichochea watu dhidi ya Wakristo ambao hawakuabudu sanamu. (Matendo 19:23-40; 1 Wakorintho 10:14) Tertullian aliandika hivi: “Wao huamini kwamba Wakristo ndio husababisha kila jambo baya linalowapata watu. Ikiwa maji ya Mto Tiber yanafurika na kufikia kuta za jiji lao, ikiwa maji ya Mto Nile si mengi kuweza kunyunyizia mashamba, ikiwa hakunyeshi, au ikiwa kuna tetemeko la ardhi, njaa, au msiba, mara moja watu hupaaza sauti: ‘Watupeni Wakristo kwa simba!’” Hata wapatwe na nini, Wakristo wa kweli ‘hujilinda wenyewe na sanamu.’—1 Yohana 5:21.

Kweli na Maadhimisho ya Kidini

8. Kwa nini wale wanaotembea katika kweli hawasherehekei Krismasi?

8 Wale wanaotembea katika kweli huepuka maadhimisho yasiyo ya Kimaandiko kwa sababu ‘nuru haina ushiriki na giza.’ (2 Wakorintho 6:14-18) Kwa mfano, hawasherehekei Krismasi, sherehe inayofanywa Desemba 25. “Hakuna mtu anayejua tarehe kamili ya kuzaliwa kwa Kristo,” kinasema kichapo The World Book Encyclopedia. Kichapo The Encyclopedia Americana (Chapa ya 1956) kinasema: ‘Desturi nyingi za kujifurahisha zinazofuatwa wakati wa Krismasi zinatokana na Saturnalia, sherehe ya Waroma iliyofanywa katikati ya mwezi wa Desemba.’ Ensaiklopedia ya M’Clintock na Strong inasema: ‘Mwadhimisho wa Krismasi haukuagizwa na Mungu, wala hautokani na Agano Jipya.’ Nacho kitabu Daily Life in the Time of Jesus kinasema: ‘Wakati wa baridi kali, makundi ya kondoo hayakutoka nje; na jambo hilo peke yake linatuonyesha kwamba haielekei kwamba tarehe iliyowekwa ya kusherehekea Krismasi wakati wa baridi kali, ni ya kweli, kwa kuwa kitabu cha Injili kinasema kwamba wachungaji walikuwa nje.’—Luka 2:8-11.

9. Kwa nini watumishi wa Yehova wa zamani na wa siku hizi hawasherehekei Ista?

9 Inasemekana kwamba Ista ni sikukuu ya kukumbuka kufufuka kwa Kristo, lakini vitabu vyenye kutegemeka vinaihusianisha na ibada isiyo ya kweli. Kamusi The Westminster Dictionary of the Bible inasema kwamba “mwanzoni Ista ilikuwa sherehe ya kumtukuza Teutonic, mungu wa kike wa Wajerumani aliyeaminika kuleta nuru na majira ya mvua nyingi. Wajerumani walioitawala Uingereza zamani walimwita Eastre,” au Eostre. Vyovyote vile, kichapo Encyclopædia Britannica (Chapa ya 11) kinasema: “Agano Jipya halitaji lolote kuhusu kuadhimishwa kwa sikukuu ya Ista.” Wakristo wa mapema hawakusherehekea Ista wala haisherehekewi na watu wa Yehova leo.

10. Ni mwadhimisho gani ambao Yesu alianzisha, na ni nani wanaouadhimisha ifaavyo?

10 Yesu hakuwaamuru wafuasi wake waadhimishe kuzaliwa kwake wala kufufuka kwake, lakini alianzisha Ukumbusho wa kifo chake cha kidhabihu. (Waroma 5:8) Kwa kweli, hili ndilo tukio pekee ambalo aliwaamuru wanafunzi wake waadhimishe. (Luka 22:19, 20) Mashahidi wa Yehova bado huadhimisha mwadhimisho huo wa kila mwaka, ambao pia unaitwa Mlo wa Jioni wa Bwana.—1 Wakorintho 11:20-26.

Kweli Yatangazwa Ulimwenguni Pote

11, 12. Wale wanaotembea katika kweli hutegemezaje kazi yao ya kuhubiri?

11 Wale wanaoijua kweli huona kuwa ni pendeleo kutumia wakati wao, nguvu, na rasilimali zao nyingine katika kazi ya kuhubiri habari njema. (Marko 13:10) Kazi ya kuhubiri ya Wakristo wa mapema ilitegemezwa kwa michango ya hiari. (2 Wakorintho 8:12; 9:7) Tertullian aliandika: “Hata ikiwa kuna kisanduku cha michango, michango hiyo haitokani na pesa ambazo zinalipwa mlangoni ili kuingia, kana kwamba dini ni biashara. Kila mtu huleta kiasi kidogo cha pesa mara moja kila mwezi—au wakati wowote anaotaka, na ikiwa tu anataka na anaweza; kwa kuwa hakuna anayelazimishwa; ni utoaji wa hiari.”—Apology, sura ya 39.

12 Kazi ya kuhubiri Ufalme ambayo Mashahidi wa Yehova hufanya ulimwenguni pote hutegemezwa pia kwa michango ya hiari. Mashahidi na pia watu wanaopendezwa na wenye shukrani huliona kuwa pendeleo kutegemeza kazi hii kwa michango yao. Katika jambo hilo pia, kuna ufanani kati ya Wakristo wa mapema na Mashahidi wa Yehova.

Kweli na Mwenendo Wako

13. Kuhusiana na mwenendo, Petro alitoa ushauri gani ambao Mashahidi wa Yehova hufuata?

13 Wakristo wa mapema walitembea katika kweli nao walifuata ushauri huu wa mtume Petro: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa bora miongoni mwa mataifa, ili, katika jambo ambalo katika hilo wao wanasema dhidi yenu kuwa watenda-maovu, likiwa tokeo la kazi zenu bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea wapate kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.” (1 Petro 2:12) Mashahidi wa Yehova huchukua kwa uzito maneno hayo.

14. Wakristo wana maoni gani kuhusu vitumbuizo visivyo vya adili?

14 Hata baada ya uasi-imani kuenea, watu waliokuwa Wakristo kwa jina tu waliepuka vitendo vya ukosefu wa maadili. W. D. Killen, profesa wa historia ya makanisa ya Kikristo, aliandika hivi: ‘Katika karne ya pili na ya tatu, watu walipenda sana kwenda katika majumba ya michezo ya kuigiza yaliyokuwa katika kila mji mkubwa; na ingawa kwa ujumla waigizaji walikuwa watu wenye maadili mabaya sana, maonyesho yao yenye kuchochea hisia yaliendelea kutimiza tamaa zilizopotoka za watu wa kizazi hicho. Wakristo wote wa kweli walichukia maonyesho hayo. . . . Walichukia sana mambo ya aibu yaliyofanywa huko; na waliona maombi yaliyofanywa daima kwa miungu ya kipagani, ya kiume na ya kike kuwa kinyume kabisa na imani yao.’ (The Ancient Church, ukurasa wa 318-319) Leo wafuasi wa kweli wa Yesu pia huepuka vitumbuizo vyenye aibu, vinavyoshusha maadili.—Waefeso 5:3-5.

Kweli na “Mamlaka Zilizo Kubwa”

15, 16. “Mamlaka zilizo kubwa” ni nani, nao wanaotembea katika kweli huwaonaje?

15 Ingawa Wakristo wa mapema walikuwa na mwenendo mzuri, wafalme fulani Waroma waliwaelewa vibaya. Mwanahistoria E. G. Hardy anasema kwamba wafalme hao waliwaona kuwa “watu wa kudharauliwa kwa sababu walishikilia sana dini.” Barua ambazo Gavana Pliny the Younger wa Bithinia na Mfalme Trajan waliandikiana, zinaonyesha kwamba, kwa ujumla watawala hawakuujua Ukristo vizuri. Wakristo wana maoni gani kuhusu Serikali?

16 Kama wafuasi wa mapema wa Yesu, Mashahidi wa Yehova hujitiisha kwa kadiri fulani kwa “mamlaka zilizo kubwa” za kiserikali. (Waroma 13:1-7) Ikiwa matakwa ya wanadamu yanapingana na ya Mungu, wao huchukua msimamo huu: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Kitabu After Jesus—The Triumph of Christianity kinasema: ‘Ingawa Wakristo hawakuabudu mfalme, wao hawakuchochea watu wafanye fujo, nayo dini yao haikuwa hatari kwa ufalme ingawa wapagani waliiona kuwa tofauti na nyakati nyingine yenye kuchukiza.’

17. (a) Wakristo wa mapema walitetea serikali gani? (b) Wafuasi wa kweli wa Kristo wamefuataje andiko la Isaya 2:4 katika maisha yao?

17 Wakristo wa mapema walitetea Ufalme wa Mungu, kama vile wazee wa ukoo Abrahamu, Isaka, na Yakobo walivyoonyesha imani katika ‘jiji lililoahidiwa ambalo limefanywa na Mungu.’ (Waebrania 11:8-10) Kama Bwana-Mkubwa wao, wanafunzi wa Yesu ‘hawakuwa sehemu ya ulimwengu.’ (Yohana 17:14-16) Na kuhusiana na vita na ugomvi, wao walifuatia amani kwa ‘kufua panga zao kuwa majembe.’ (Isaya 2:4) Geoffrey F. Nuttall, mwalimu wa historia ya kanisa, alisema hivi kuhusu ufanani huu wenye kutokeza: ‘Mtazamo wa Wakristo wa mapema kuelekea vita ulikuwa kama wa watu ambao hujiita Mashahidi wa Yehova, na ingawa jambo hilo ni kweli, sisi hulikubali shingo upande.’

18. Kwa nini hakuna haja kwa serikali yoyote kuwaogopa Mashahidi wa Yehova?

18 Kwa kuwa Wakristo wa mapema walichukua msimamo wa kutokuwamo na walijitiisha kwa “mamlaka zilizo kubwa,” wao hawakuwa tisho kwa serikali yoyote, na ndivyo ilivyo na Mashahidi wa Yehova. ‘Mtu aliye na ubaguzi na mwenye kutia shaka ndiye tu anayeweza kuamini kwamba Mashahidi wa Yehova ni tisho kwa serikali yoyote,’ akaandika mhariri mmoja kutoka Amerika ya Kaskazini. ‘Wao wanapenda amani kama vile kikundi cha kidini kinavyotazamiwa kuwa, na hawajaribu kupindua serikali.’ Serikali zinazowafahamu vizuri zinajua kwamba hakuna haja ya kuwaogopa Mashahidi wa Yehova.

19. Tunaweza kusema nini kuhusu Wakristo wa mapema na Mashahidi wa Yehova kuhusu kulipa kodi?

19 Njia moja ambayo Wakristo wa mapema waliheshimu “mamlaka zilizo kubwa” ni kwa kulipa kodi. Alipomwandikia Antoninus Pius, Mtawala Mroma (138-161 W.K.), Justin Martyr alisema kwamba Wakristo walilipa kodi zao ‘kwa utayari zaidi kuliko watu wengine wote.’ (First Apology, sura ya 17) Naye Tertullian aliwaambia watawala Waroma kwamba wakusanya-kodi wao ‘walistahili kuwashukuru Wakristo’ kwa kuwa walilipa kodi zao kwa kuongozwa na dhamiri. (Apology, sura ya 42) Wakristo walinufaika wakati wa Pax Romana, au Amani ya Roma, kwa kuwa kulikuwa na sheria na utengamano, barabara nzuri, na usafiri wa baharini ambao kwa kadiri fulani ulikuwa salama. Kwa kuwa walitambua kwamba walikuwa na deni kwa jamii, walitii maneno haya ya Yesu: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.” (Marko 12:17) Watu wa Yehova leo hufuata ushauri huo, nao wamepongezwa kwa unyofu wao, kama katika kulipa kodi.—Waebrania 13:18.

Kweli Ni Kifungo cha Muungano

20, 21. Kuhusiana na udugu wenye amani, kuna ufanani gani kati ya Wakristo wa mapema na watumishi wa Yehova leo?

20 Kwa sababu walitembea katika kweli, Wakristo wa mapema waliunganishwa katika udugu wenye amani, kama vile Mashahidi wa Yehova leo. (Matendo 10:34, 35) Barua moja iliyochapwa katika gazeti The Moscow Times inasema: ‘Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kuwa watu wema, wenye fadhili, na wanyenyekevu. Ni rahisi sana kushughulika nao. Wao hawalazimishi wengine kufanya mambo, na siku zote hujaribu kudumisha uhusiano wenye amani pamoja na wengine. Hawachukui hongo, wala hawalewi wala kutumia dawa za kulevya na ni rahisi kuelewa ni kwa nini hawafanyi hivyo: Katika yote wafanyayo, wao hujaribu kufuata imani yao inayotegemea Biblia. Kama watu wote ulimwenguni wangejaribu kufuata Biblia maishani mwao kama vile Mashahidi wa Yehova, ulimwengu wetu mkatili ungekuwa tofauti kabisa.’

21 Kichapo Encyclopedia of Early Christianity kinasema: ‘Washiriki wa kanisa la mapema walijiona kuwa jamii yenye uelewevu mpya, na Wayahudi na watu wasio Wayahudi ambao hapo awali walikuwa maadui wangeweza kuishi katika jamii hii kwa amani.’ Mashahidi wa Yehova pia ni udugu wa ulimwenguni pote wenye kupenda amani—kwa kweli jamii ya ulimwengu mpya. (Waefeso 2:11-18; 1 Petro 5:9; 2 Petro 3:13) Wakati ofisa mkuu wa usalama kwenye uwanja wa maonyesho wa Pretoria, huko Afrika Kusini, alipoona jinsi Mashahidi wa jamii zote walivyofanya kusanyiko lao kwa amani, alisema hivi: ‘Katika siku hizi chache zilizopita, kila mtu alikuwa mwenye adabu, watu walisemezana vizuri, na walionyesha mtazamo mzuri. Mambo hayo yathibitisha kwamba watu wenu wana maadili bora, na kwamba wote wanaishi pamoja kama familia moja yenye furaha.’

Wabarikiwa kwa Kufundisha Kweli

22. Ni nini ambacho kimetukia kwa sababu Wakristo wamefanya kweli iwe dhahiri?

22 Paulo na Wakristo wengine ‘walifanya kweli iwe dhahiri’ kupitia mwenendo wao na kazi ya kuhubiri. (2 Wakorintho 4:2) Je, hukubali kwamba Mashahidi wa Yehova wanafanya vivyo hivyo na wanafundisha mataifa yote ile kweli? Watu kotekote duniani wanaikubali ibada ya kweli na wanaendelea kumiminika kwa wingi kwenye “mlima wa nyumba ya BWANA.” (Isaya 2:2, 3) Kila mwaka, maelfu hubatizwa ili kuonyesha wakfu wao kwa Mungu na hivyo makutaniko mengi huanzishwa.

23. Una maoni gani kuhusu wale wanaofundisha mataifa yote ile kweli?

23 Ingawa Mashahidi wa Yehova wana malezi mbalimbali, wao wana umoja katika ibada ya kweli. Upendo wanaoonyesha huwatambulisha kuwa wanafunzi wa Yesu. (Yohana 13:35) Je, unaweza kuona kwamba ‘Mungu kwa kweli yumo miongoni mwao’? (1 Wakorintho 14:25) Je, umejiunga na wale wanaofundisha mataifa yote ile kweli? Ikiwa ndivyo, na uwe mwenye shukrani daima kwa ajili ya kweli na upate pendeleo la kutembea katika kweli hiyo milele.

Ungejibuje?

• Kuna ufanani gani kati ya Wakristo wa mapema na Mashahidi wa Yehova kuhusu namna ya kuabudu?

• Ni mwadhimisho gani pekee wa kidini ambao huadhimishwa na wale wanaotembea katika kweli?

• “Mamlaka zilizo kubwa” ni nani, nao Wakristo huwaonaje?

• Kweli inakuwa kifungo cha muungano jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Sikuzote mikutano ya Kikristo imewanufaisha wale wanaotembea katika kweli

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yesu aliwaamuru wafuasi wake waadhimishe Ukumbusho wa kifo chake cha kidhabihu

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kama Wakristo wa mapema, Mashahidi wa Yehova huheshimu “mamlaka zilizo kubwa”