Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Wanauonaje Moto wa Mateso Leo?

Watu Wanauonaje Moto wa Mateso Leo?

Watu Wanauonaje Moto wa Mateso Leo?

WAOVU huenda wapi wanapokufa? Je, wao huenda kuzimu, mahali ambapo wengi huamini pana moto wa mateso yasiyo na mwisho? Au je, hukumu itakayotekelezwa dhidi ya waovu ni ile hali ya kutengwa na Mungu?

Kwa karne nyingi, viongozi wa Jumuiya ya Wakristo wamewazia kwamba watenda dhambi watatupwa katika moto wa mateso na kuteswa vikali. Imani hiyo ingali inafundishwa na dini nyingi. Gazeti U.S.News & World Report lasema, ‘huenda dini zinazojiita za Kikristo zilieneza imani hiyo, hata hivyo dini nyingine zisizo za Kikristo zinashikilia imani hiyo pia. Karibu dini zote kubwa na ndogo ulimwenguni zinaamini kwamba kutakuwa na adhabu kali baada ya kufa.’ Wahindu, Wabudha, Waislamu, Wajaini, na Watao wanaamini kwamba kuna mahali fulani penye moto wa mateso.

Hata hivyo, leo watu wana maoni tofauti kuhusu moto wa mateso. ‘Ingawa bado kuna watu wanaoamini kwamba kuna moto wa mateso,’ linasema gazeti lililonukuliwa juu, ‘leo kuna watu wanaoamini kwamba kuna uharibifu wa milele, jambo linalodokeza kwamba huenda waovu wasiadhibiwe kwa kutupwa katika moto wa mateso.’

Gazeti la Wajesuti La Civiltà Cattolica lilisema hivi: “Inapotosha . . . kufikiri kwamba Mungu hutumia roho waovu kutesa watu waliohukumiwa kwa kutumia moto.” Liliendelea kusema: “Waovu hawatatupwa mahali halisi penye mateso bali ni hali ya msononeko ambayo itawapata watu waliotengwa na Mungu.” Papa John Paul wa Pili alisema hivi katika mwaka wa 1999: “Moto wa mateso si mahali halisi bali ni hali itakayowapata wale ambao kwa hiari hujitenga kabisa na Mungu, aliye chanzo cha uhai na furaha.” Papa huyo alisema hivi kuhusu picha zinazoonyesha mahali penye moto wa mateso: “Zinaonyesha hali ya kukata tamaa na maisha yasiyo na kusudi ya wale wanaojitenga na Mungu.” Mwanahistoria wa masuala ya kanisa, Martin Marty alisema kwamba iwapo papa angefafanua moto wa mateso kuwa mahali penye “miale ya moto na ibilisi aliye na uma, watu hawangeamini.”

Dini nyingine zina maoni kama hayo. Ripoti moja ya tume inayochunguza mafundisho ya Kanisa la Anglikana ilisema: “Waovu hawataadhibiwa kwa kuteswa milele, bali watatoweka milele kwa sababu ya kuamua kumpinga Mungu kabisa.”

Mafundisho ya Kanisa la Episkopali la Marekani yanafafanua adhabu ya waovu kuwa ‘kifo cha milele kwa sababu ya kumkataa Mungu.’ Gazeti U.S.News & World Report linasema kwamba watu wengi zaidi wanaunga mkono wazo hilo, kwamba “mwisho wa waovu ni uharibifu si kuteseka milele. . . . Wanasisitiza kwamba wale ambao hatimaye watamkataa Mungu wataharibiwa ‘kwa moto wenye kuteketeza kabisa.’”

Ingawa watu wengi sasa wanakataa wazo la moto na salfa, wengi wanaendelea kuamini kwamba kuna mahali halisi penye moto wa mateso. “Maandiko husema waziwazi kuhusu mahali halisi pa mateso,” asema Albert Mohler wa Southern Baptist Theological Seminary huko Louisville, Kentucky, Marekani. Nayo ripoti The Nature of Hell, iliyotayarishwa na shirika la Evangelical Alliance Commission, inasema: ‘Mahali pa mateso ni kule kuteseka kunakotokana na kutambua kwamba umekataliwa.’ Inaongeza kusema: “Kuna adhabu na mateso ya aina mbalimbali yanayolingana na dhambi ambazo mtu alitenda akiwa duniani.”

Je, kuna mahali halisi penye moto wa mateso au pa uharibifu wa milele? Au ni ile hali ya kutengwa tu na Mungu? Waovu waliokufa wako katika hali gani?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]

Historia Fupi Kuhusu Moto wa Mateso

WATU wanaodai kuwa Wakristo walianza kuamini kwamba kuna moto wa mateso lini? Muda mrefu baada ya kipindi alichoishi Yesu Kristo na mitume wake. “Kichapo Apocalypse of Peter (karne ya pili W.K.) ndicho kichapo cha kwanza cha Kikristo [si sehemu ya Biblia] kueleza jinsi watenda dhambi watakavyoadhibiwa na kuteswa katika moto,” yasema Encyclopædia Universalis ya Kifaransa.

Hata hivyo, Mababa wa Kanisa wa mapema hawakukubaliana kuhusu adhabu ya waovu. Justin Martyr, Clement wa Alexandria, Tertullian, na Cyprian waliamini kwamba waovu watateswa katika moto. Origen na mwanatheolojia Gregory wa Nyssa walifikiri kwamba adhabu hiyo ni kule kutenganishwa na Mungu—kuteseka kiroho. Kwa upande mwingine, Augustine wa Hippo aliamini kwamba waovu watateseka kiroho na kimwili—maoni ambayo yalikuja kukubaliwa na wengi. “Kufikia karne ya tano fundisho thabiti kwamba watenda dhambi hawatapewa nafasi nyingine katika maisha ya sasa na kwamba moto utakaowateketeza hautazimwa kamwe lilienea kila mahali,” akaandika Profesa J.N.D. Kelly.

Katika karne ya 16, watu kama vile Martin Luther na John Calvin ambao walileta marekebisho makubwa ya Kiprotestanti walielewa kwamba kuteswa motoni kulifananisha kutengwa na Mungu milele. Hata hivyo, watu walianza kuamini tena kwamba kuna moto wa mateso karne mbili zilizofuata. Mhubiri Mprotestanti, Jonathan Edwards, alikuwa akiwatisha Wamarekani wakati wa ukoloni katika karne ya 18 kwa picha zilizoonyesha waziwazi watenda dhambi wakiteseka motoni.

Hata hivyo, muda mfupi baadaye, ni watu wachache tu walioendelea kuamini kwamba kuna moto wa mateso. “Imani ya kwamba kuna mahali pa kuwatesa waovu ilikuwa karibu kufifia kabisa katika karne ya 20,” linasema gazeti U.S.News & World Report.

[Picha]

Justin Martyr aliamini kwamba waovu watateswa katika moto

Augustine wa Hippo alifundisha kwamba waovu watateseka kiroho na kimwili