Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, Abeli alijua kwamba dhabihu ya mnyama ilihitajika ili kupata kibali cha Mungu?

Biblia inataja mambo machache sana kuhusu dhabihu za Kaini na Abeli. Katika andiko la Mwanzo 4:3-5, BHN, tunasoma: “Baada ya muda fulani, Kaini alimtolea Mwenyezi-Mungu dhabihu kutokana na mazao ya shambani, naye Abeli akamtolea Mungu dhabihu ya wazawa wa kwanza wa kondoo wake na nyama nono. Mwenyezi-Mungu akapendezwa na Abeli na dhabihu yake, lakini hakupendezwa na Kaini wala na dhabihu yake.”

Biblia haitaji kama kabla ya kutoa dhabihu hizo Yehova alikuwa amewaambia jambo lolote hususa kuhusu dhabihu wala kuhusu aina ya dhabihu ambazo angekubali. Hivyo, yaonekana Kaini na Abeli walijiamulia wenyewe aina ya dhabihu walizotoa. Walizuiwa kuingia katika makao ya Kiparadiso yaliyokuwa ya wazazi wao; wakaanza kupatwa na matokeo ya dhambi; nao walikuwa wametengwa na Mungu. Ni lazima hali hiyo yenye kusikitisha ya dhambi iwe iliwachochea sana kumgeukia Mungu ili awasaidie. Yaelekea walimtolea Mungu zawadi kwa hiari ili kupata kibali chake.

Kwa hiyo, Mungu alikubali dhabihu ya Abeli lakini akakataa ya Kaini. Kwa nini? Je, ni kwa sababu Abeli alitoa dhabihu inayofaa naye Kaini akatoa isiyofaa? Hatuwezi kuwa na uhakika kwamba aina ya dhabihu walizotoa ndizo zilizomfanya Mungu akubali moja na kukataa nyingine kwa kuwa hawakuwa wameambiwa ni dhabihu za aina gani zinazokubalika na zisizokubalika. Hata hivyo, yaelekea kwamba dhabihu walizotoa zilikubalika. Katika Sheria ambayo mwishowe Yehova alilipa taifa la Israeli, dhabihu zilizokubalika zilitia ndani wanyama, sehemu za wanyama, na pia nafaka iliyochomwa, miganda ya shayiri, unga mwembamba, vitu vilivyookwa, na divai. (Mambo ya Walawi 6:19-23; 7:11-13; 23:10-13) Yaonekana kwamba si vitu walivyotoa tu vilivyofanya Mungu akubali dhabihu ya Abeli na kukataa ya Kaini.—Linganisha Isaya 1:11; Amosi 5:22.

Karne kadhaa baadaye, mtume Paulo alisema: “Kwa imani Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko Kaini, imani ambayo kupitia hiyo alitolewa ushahidi kwamba yeye alikuwa mwadilifu, Mungu akitoa ushahidi kwa habari ya zawadi zake.” (Waebrania 11:4) Hivyo, Abeli alitambuliwa na Mungu kuwa mwadilifu kwa sababu ya imani. Lakini aliamini nini? Alikuwa na imani katika ahadi ya Yehova kwamba angetoa Mbegu, ambaye ‘angeponda kichwa cha nyoka’ na kurudisha amani na ukamilifu ambao wanadamu walifurahia hapo awali. Huenda maneno kwamba Mbegu ‘angepondwa kisigino’ ndiyo yaliyomsaidia Abeli kuamua kwamba dhabihu iliyohitajiwa ingehusisha kumwaga damu. (Mwanzo 3:15) Hata hivyo, ukweli ni kwamba imani ya Abeli ndiyo iliyofanya ‘dhabihu yake iwe ya thamani kubwa zaidi kuliko ya Kaini.’

Vivyo hivyo, Kaini alikataliwa kwa sababu alikosa imani, kama matendo yake yalivyoonyesha, bali si kwa sababu alitoa dhabihu isiyofaa. Yehova alikuwa amemweleza Kaini waziwazi hivi: “Kama ukitenda vyema, hutapata kibali?” (Mwanzo 4:7) Mungu hakumkataa Kaini kwa sababu alichukizwa na dhabihu yake, bali alimkataa kwa sababu “kazi zake mwenyewe zilikuwa mbovu.” Kaini alikuwa mwenye wivu, chuki, na hatimaye akawa mwuaji.—1 Yohana 3:12.