Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Neno la Mungu Hukazia Nguvu’

‘Neno la Mungu Hukazia Nguvu’

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

‘Neno la Mungu Hukazia Nguvu’

KATIKA kisiwa chenye jua cha Jamaika, huko Karibea, watu wengi wanaijua Biblia. Karibu kila familia ina tafsiri ya King James Version, na watu fulani wameona kwamba “neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu.” (Waebrania 4:12) Nguvu hiyo inaweza kubadili maisha ya watu, kama inavyoonyeshwa na jambo lililoonwa linalofuata.

Mwanamume aitwaye Cleveland alitembelewa na mmoja wa Mashahidi wa Yehova baada tu ya kurudi nyumbani kutoka kazini. Baada ya kuzungumzia Maandiko fulani, Shahidi huyo alimwachia kitabu cha kujifunzia Biblia, Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Cleveland hakujua jinsi Neno la Mungu lingekazia nguvu katika maisha yake.

Cleveland alikuwa akisali mara tatu kwa siku, akimwomba Mungu amsaidie ili amwabudu kwa njia inayofaa. Cleveland alikuwa na uhakika kwamba wazazi wake hawakumwabudu Mungu kwa njia inayofaa, lakini baada ya kuchunguza dini mbalimbali, alikata tamaa. Ingawa alikuwa amesikia juu ya Mashahidi wa Yehova, Cleveland hakuwa na uhakika kwamba walifundisha kweli. Ingawa alikuwa na shaka, Cleveland alikubali kujifunza Biblia na Shahidi aliyemtembelea. Kwa nini? Kwa sababu alitaka kuthibitisha kwamba Mashahidi hawafundishi kweli!

Muda si muda, Cleveland alijifunza kwamba uhusiano wa kingono kati yake na wanawake wawili tofauti haukumpendeza Mungu. (1 Wakorintho 6:9, 10) Baada ya kujifunza mara mbili tu, alipiga moyo konde kuachana na wanawake hao. Pia alianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwenye Jumba la Ufalme. Lakini hilo likawa jaribu lingine.

Cleveland alikuwa mchezaji mwenye bidii katika timu ya kwao ya kandanda, na alikuwa akikosa mikutano wakati timu hiyo ilipokuwa ikicheza. Angefanya nini? Ingawa wachezaji wenzake, mkufunzi, na marafiki walimkaza sana, Cleveland aliamua kuacha timu hiyo. Naam, Neno la Mungu lilikuwa limeanza kukazia nguvu, likimnufaisha!

Nguvu ya Neno la Mungu ilidhihirika tena wakati Cleveland alipoanza kuhubiria wengine yale aliyokuwa akijifunza katika Biblia. (Matendo 1:8) Kwa sababu hiyo, wawili kati ya wachezaji wenzake walianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Cleveland alipostahili kuwa mhubiri asiyebatizwa wa habari njema, alifurahia sana kuhubiri, akitumia Neno la Mungu kuwasaidia wengine.

Cleveland aliendelea kuchochewa na nguvu ya Neno la Mungu na hatimaye akaonyesha wakfu wake kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Sasa ana pendeleo la kutumikia akiwa mhudumu wa wakati wote na mtumishi wa huduma katika kutaniko.

Huko Jamaika na ulimwenguni kote, maelfu ya watu wamejifunza kwamba Neno la Mungu kwa kweli “liko hai na hukazia nguvu.”

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 8]

 

JAMAIKA

[Hisani]

Ramani na tufe: Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.