Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimezeeka na Kushiba Siku

Nimezeeka na Kushiba Siku

Simulizi la Maisha

Nimezeeka na Kushiba Siku

LIMESIMULIWA NA MURIEL SMITH

Mlango wa mbele wa nyumba yangu ulitikiswa baada ya kubishwa kwa nguvu. Nilikuwa tu nimerudi nyumbani kupata chakula cha mchana baada ya asubuhi yenye shughuli nyingi katika kazi ya kuhubiri. Kama ilivyokuwa desturi yangu, nilikuwa ninatayarisha chai baadaye nipumzike kwa nusu-saa. Mlango uliendelea kubishwa na nilipokuwa nikielekea mlangoni nilishangaa ni nani aliyenitembelea wakati huo. Mara moja nikatambua. Wanaume wawili waliosimama mlangoni walijitambulisha kuwa maofisa wa polisi. Walisema kwamba wamekuja kusaka nyumba yangu ili kutafuta vichapo vinavyochapishwa na Mashahidi wa Yehova—tengenezo lililokuwa limepigwa marufuku.

Kwa nini Mashahidi wa Yehova walipigwa marufuku huko Australia, nilipataje kuwa mmoja wao? Yote hayo yalianza mnamo mwaka wa 1910 nilipopokea zawadi kutoka kwa mama yangu, nikiwa na umri wa miaka kumi.

FAMILIA yetu iliishi katika nyumba ya mbao katika kitongoji cha Crows Nest kilicho Kaskazini ya Sydney. Siku moja nilitoka shuleni nikamkuta mama yangu akizungumza na mwanamume fulani mlangoni. Nilitaka kujua mtu huyo aliyevalia suti na kubeba mkoba uliojaa vitabu ni nani. Kwa sababu ya woga niliomba radhi kisha nikaingia ndani ya nyumba. Hata hivyo, dakika chache baadaye, Mama aliniita. Akasema: “Mtu huyu ana vitabu vizuri, na vyote vinazungumzia Maandiko. Na sasa, kwa sababu karibuni utasherehekea siku yako ya kuzaliwa, ninaweza kukununulia ama nguo mpya au vitabu hivi. Unapenda nini?”

Nami nikamjibu, “O, asante Mama, nitachukua vitabu.”

Kwa hiyo, nikiwa na umri wa miaka kumi, nikawa na mabuku matatu ya kwanza ya Studies in the Scriptures yaliyoandikwa na Charles Taze Russell. Kwa sababu singeweza kuelewa vitabu hivyo kwa urahisi, yule mwanamume alieleza kwamba mama alihitaji kunisaidia kuvielewa. Mama akasema kwamba angefurahi kufanya hivyo. La kuhuzunisha ni kwamba, punde tu baada ya hapo, Mama akafa. Baba alijitahidi kunitunza mimi, ndugu, na dada yangu mdogo, lakini wakati huo mimi pia nikawa na madaraka zaidi ambayo yalielekea kunilemea. Hata hivyo, msiba mwingine ulikuwa unakaribia.

Mwaka mmoja baada ya vita ya kwanza ya ulimwengu kuanza mwaka wa 1914, baba yetu mpendwa aliuawa. Tukiwa mayatima, ndugu na dada yangu walipelekwa kuishi na watu wa ukoo, nami nikapelekwa katika chuo cha bweni cha Katoliki. Wakati mwingine nilifadhaishwa na upweke. Na bado, nashukuru kwa kupata fursa ya kuendelea kufuatia muziki, hasa kupiga piano. Baada ya miaka kadhaa, nilihitimu kutoka hicho chuo cha bweni. Mnamo mwaka wa 1919, nikaolewa na Roy Smith, mwuzaji wa vyombo vya muziki. Mnamo mwaka wa 1920, tukawa na mtoto, nikaanza tena shughuli za kila siku za maisha. Lakini vipi vile vitabu?

Jirani Aniambia Kweli za Kiroho

Kwa miaka yote hiyo, nilisafiri na “vitabu vya Biblia.” Ijapokuwa sikuwa nimevisoma, moyoni mwangu nilijua kwamba vilikuwa na ujumbe wa maana. Halafu, siku moja mwishoni mwa miaka ya 1920, jirani yetu Lil Bimsom, alitutembelea. Tukaenda mezani, tukaketi na kunywa chai.

Ghafula alishangaa na kusema, “Kumbe una vitabu hivyo!”

Vitabu vipi? nikauliza kwa mshangao.

Akaelekezea kidole vitabu Studies in the Scriptures vilivyokuwa kwenye maktaba. Lil aliviomba akaenda navyo nyumbani na kuvisoma kwa makini. Punde si punde, msisimuko wake kuhusu aliyosoma ukawa wazi. Lil alipata vitabu vingine zaidi kutoka kwa Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Na zaidi, hakukosa kutuambia mambo yote aliyokuwa akijifunza. Kimoja cha vitabu alivyopata ni The Harp of God ambacho baadaye kililetwa kwetu. Hatimaye maisha yangu katika utumishi wa Yehova yakaanza nilipotenga wakati kusoma vitabu hivi vinavyozungumzia habari ya Biblia. Mwishowe, nikapata majibu kwa maswali muhimu sana ambayo kanisa letu halikuweza kunipa.

Jambo la kupendeza ni kwamba Roy alitilia maanani ujumbe wa Biblia, na sote wawili tukawa wanafunzi wenye bidii wa Biblia. Hapo awali, Roy alikuwa mshiriki wa Freemasons. Wakati huo familia yetu iliungana katika ibada ya kweli, na mara mbili kila juma ndugu fulani aliongoza funzo la Biblia na familia yetu. Tulipata kitia-moyo zaidi tulipoanza kuhudhuria mikutano iliyofanywa na Wanafunzi wa Biblia. Mikutano huko Sydney ilifanywa katika jumba dogo la kupanga katika kitongoji cha Newtown. Ndugu wengi waliohudhuria mikutano wakati huo walihitaji kusafiri mwendo mrefu kwa sababu wakati huo kulikuwa na Mashahidi wanaopungua 400 nchini kote.

Kwa kawaida ili kuhudhuria mikutano, familia yetu ilivuka Bandari ya Sydney. Kabla ya kujengwa kwa Daraja la Bandari ya Sydney mnamo mwaka wa 1932, kila aliyevuka alitumia mashua ya kuvushia. Licha ya gharama na muda uliohusika katika safari hiyo, tulijitahidi kutokosa chakula chochote cha kiroho kilichoandaliwa na Yehova. Jitihada ya kuweka msingi imara katika kweli ilikuwa ya maana kwani vita ya pili ya ulimwengu ilikuwa inakaribia, na suala la kutokuwamo lingeathiri familia yetu moja kwa moja.

Wakati wa Majaribu na Baraka

Ile miaka ya mapema ya 1930 ilikuwa yenye kusisimua kwangu na kwa familia yetu. Nilibatizwa mnamo mwaka wa 1930, na 1931, nikahudhuria kusanyiko lisiloweza kusahaulika ambapo sote tulisimama na kukubali kuitwa jina zuri, Mashahidi wa Yehova. Mimi na Roy tuliazimia kuishi kwa jina hilo kwa kushiriki katika njia na kampeni zote za kuhubiri ambazo tengenezo lilipendekeza. Kwa mfano, mnamo mwaka wa 1932 tulikuwa na kampeni ya kijitabu cha pekee kilichokusudiwa kuwafikia watu wengi waliokuja kushuhudia kufunguliwa kwa Daraja la Bandari ya Sydney. Jambo kuu lilikuwa kutumia magari yenye vikuza-sauti, nasi tulikuwa na pendeleo la pekee kuwekewa vikuza-sauti katika gari la familia yetu. Kwa kutumia tekinolojia hiyo, tulieneza ujumbe wa hotuba za Biblia zilizorekodiwa za Ndugu Rutherford katika barabara zote za Sydney.

Hata hivyo, hali zilianza kubadilika tena na kuendelea kuwa ngumu. Kufikia mwaka wa 1932 Australia ililemewa na ule Mshuko Mkubwa wa Kiuchumi, basi mimi na Roy tukaamua kuishi maisha sahili zaidi. Njia moja ilikuwa kuhamia eneo lililokuwa karibu na kutaniko na hivyo tukapunguza sana gharama za usafiri. Hata hivyo, hofu ya Vita ya Pili ya Ulimwengu ilipoenea ulimwenguni pote, mikazo ya kiuchumi ikawa si kitu.

Australia kama vile kwingineko, iliwanyanyasa Mashahidi wa Yehova ambao walikuwa shabaha ya minyanyaso ulimwenguni pote kwa sababu ya kutii amri ya Yesu ya kutokuwa sehemu ya ulimwengu. Wakichochewa na hasira wakati huo wa vita, wengine walituita Wakomunisti. Wapinzani hao walidai kwa uwongo kwamba Mashahidi wa Yehova walitumia vituo vyao vinne vya redio vilivyokuwa huko Australia kutuma habari kwa jeshi la Japan.

Ndugu wachanga walioitwa wakatumikie jeshini walikabiliana na mikazo mingi. Ninafurahi kusema kwamba wana wetu watatu walikuwa na imani thabiti na walidumisha kutokuwamo. Mwana wetu mkubwa, Richard, alihukumiwa kifungo cha miezi 18 gerezani. Mwana wetu wa pili, Kevin, alieleza wazi msimamo wake wa kutotumikia katika jeshi kwa sababu ya imani yake. Hata hivyo, jambo la kusikitisha ni kwamba, mwana wetu mdogo Stuart alikufa katika aksidenti ya pikipiki akienda kortini kujitetea kuhusu suala la kutokuwamo. Kwa kweli msiba huo ulikuwa wenye kufadhaisha sana. Lakini, kukazia fikira Ufalme na ahadi ya Yehova ya ufufuo kulitusaidia kuvumilia.

Walikosa Kitu Chenye Thamani

Mnamo Januari 1941, Mashahidi wa Yehova huko Australia walipigwa marufuku. Lakini, kwa miaka miwili na nusu, mimi na Roy kama vile mitume wa Yesu, tulitii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu, tukaendelea kuhubiri kisiri. Na ni wakati huo wale polisi wawili niliotangulia kutaja walipobisha hodi mlangoni. Ni nini kilichotokea?

Niliwakaribisha ndani. Walipoingia nikawauliza, “Je, ninaweza kumaliza kunywa chai kabla hamjaanza kusaka nyumba?” Inashangaza kwamba walikubali, kisha nikaenda jikoni nikasali kwa Yehova na kwa utulivu nikafikiria jinsi ya kufanya. Niliporudi, polisi mmoja aliingia kwenye maktaba yetu na kuchukua kila kitu kilichokuwa na ishara ya Watchtower, kutia ndani Biblia na vichapo vyote vilivyokuwa ndani ya mkoba wangu wa mahubiri.

“Una hakika kwamba hujaficha vichapo vingine ndani ya katoni?” akaniuliza. “Tumejulishwa kwamba wewe huhudhuria mkutano kila juma katika jumba lililo mwisho wa barabara hii na hupeleka vichapo vingi huko.”

“Hiyo ni kweli,” nikajibu, “lakini haliko huko sasa.”

“Ndiyo, tunajua hivyo, Bi. Smith,” akasema. “Tunajua pia kwamba vichapo hivyo vimewekwa katika nyumba za watu kotekote katika eneo hili.”

Katika chumba cha kulala cha mwana wetu, walipata katoni tano za kijitabu Freedom or Romanism.

Kisha akaniuliza, “Una hakika hakuna chochote kingine ndani ya gereji?”

“La, hakuna chochote humo,” nikamjibu.

Kisha akafungua kabati katika chumba cha kulia. Akapata fomu zilizokuwa zikitumiwa kujaza ripoti ya kutaniko lakini ambazo hazikuwa zimejazwa. Alizichukua na akasisitiza kuisaka gereji.

Nikamwambia, “Haya njoo huku basi.”

Walinifuata mpaka kwenye gereji na baada ya kuisaka, wakaondoka.

Polisi hao walifikiri wamepata kitu chenye thamani sana baada ya kuchukua hizo katoni tano! Lakini, walikosa kitu chenye thamani hasa. Wakati huo, nilitumikia nikiwa mwandishi wa kutaniko, na nilikuwa na majina ya wahubiri wa kutaniko na habari nyinginezo muhimu nyumbani. Nashukuru kwamba akina ndugu walitutahadharisha mapema kuhusu msako wa aina hiyo, nami nilikuwa nimezificha hati hizo kwa makini. Niliziingiza ndani ya bahasha na kuzitia ndani ya mikebe ya majani chai, sukari, na unga. Nyingine nilizitia mahali pa kufugia ndege palipokuwa karibu na gereji. Kwa hiyo polisi hao walipita bila kuona habari muhimu walizokuwa wakitafuta.

Kuanza Utumishi wa Wakati Wote

Kufikia mwaka wa 1947, watoto wetu wakubwa walikuwa tayari na familia zao wenyewe. Wakati huo mimi na Roy tukaamua kuanza utumishi wa wakati wote. Kwa sababu kulikuwa na uhitaji katika eneo la Kusini ya Australia, tuliuza makao yetu na kununua nyumba ya trela tuliyoiita Mispa, linalomaanisha “Watchtower.” Kuishi hivi kulituwezesha kuhubiri katika maeneo ya mbali. Mara nyingi tulihubiri katika maeneo ya mashambani yasiyogawiwa mtu. Ninakumbuka mambo mengi mazuri ya wakati huo. Mojawapo ya mafunzo niliyokuwa nayo ni mwanamke fulani aliyeitwa Beverly. Kabla ya kufanya maendeleo kufikia ubatizo alihama kutoka eneo hilo. Wazia shangwe niliyokuwa nayo miaka mingi baadaye dada mmoja aliponijia kusanyikoni na kujitambulisha kuwa Beverly! Nilifurahi sana kumwona baada ya miaka mingi akimtumikia Yehova pamoja na mume na watoto wake.

Katika mwaka wa 1979, nilipata pendeleo la kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia. Kati ya mambo yaliyokaziwa katika shule hiyo ni kwamba ili kuvumilia katika utumishi wa painia lazima uwe na ratiba nzuri ya funzo la kibinafsi. Bila shaka niliona hilo kuwa kweli. Maisha yangu yote nimeyatumia katika funzo, mikutano na kuhubiri. Ninaliona kuwa pendeleo kutumikia kwa zaidi ya miaka 50 nikiwa painia wa kawaida.

Kukabiliana na Matatizo ya Afya

Hata hivyo, kwa miaka mingi iliyopita, nimekuwa na magumu yasiyo na kifani. Katika mwaka wa 1962, nilipimwa na kupatikana kuwa nina ugonjwa wa macho unaoitwa glakoma. Wakati huo hakukuwapo matibabu yanayofaa, na macho yangu yaliendelea kudhoofika upesi. Afya ya Roy pia iliendelea kudhoofika, na katika mwaka wa 1983 alipata ugonjwa wa kiharusi ambao ulimfanya apooze na kushindwa kuzungumza. Akafa mwaka wa 1986. Alinisaidia sana nilipokuwa katika utumishi wa wakati wote, na kwa kweli ninamkosa.

Licha ya vizuizi vyote hivyo, nilijaribu kuwa na ratiba nzuri ya kiroho. Nilinunua gari ambalo ningeweza kutumia katika utumishi wa shambani katika eneo letu la mashambani, na nikisaidiwa na binti yangu Joyce, niliendelea na utumishi wa painia. Uwezo wangu wa kuona ulidhoofika hatua kwa hatua mpaka jicho moja likaacha kuona kabisa. Madaktari waliniwekea jicho bandia. Hata hivyo, kwa kutumia miwani yenye kuongeza ukubwa wa maandishi na vichapo vya chapa kubwa, nilitumia muda wa saa tatu hadi tano kujifunza kwa kutumia jicho moja lililokuwa limedhoofika sana.

Wakati wa kujifunza umekuwa wenye thamani sana kwangu sikuzote. Kwa hiyo unaweza kuwazia jinsi nilivyofadhaika wakati nilipopoteza uwezo wangu wa kuona kwa ghafula siku moja nikiwa ninajifunza. Ni kana kwamba taa ilizimika. Sasa nilikuwa nimepoteza kabisa uwezo wangu wa kuona. Nimefanya nini ili kuendelea kujifunza? Ijapokuwa siwezi kusikia vizuri, ili niendelee kuwa na nguvu kiroho, ninategemea sana msaada wenye upendo wa familia yangu na kusikiliza kaseti.

Kuvumilia Hadi Mwisho

Sasa nikiwa na zaidi ya miaka 100, afya yangu imeendelea kudhoofika na imenibidi kupunguza utumishi wangu. Wakati mwingine mimi huhisi nikiwa nimechanganyikiwa kidogo. Na sasa kwa sababu siwezi kuona kabisa, wakati mwingine mimi hupotea kihalisi! Ningependa kuongoza mafunzo ya Biblia tena, lakini kwa sababu ya afya yangu, siwezi kwenda kuwatafuta. Mwanzoni hali hii ilinihuzunisha sana. Ilibidi nijifunze kuishi kulingana na vizuizi nilivyo navyo na kuridhika na mambo ninayoweza kutimiza. Hilo halijawa rahisi. Hata hivyo, ni pendeleo lililoje kwamba kila mwezi, ninaweza kutoa ripoti ya wakati niliotumia kuongea kuhusu Mungu wetu mkuu, Yehova. Ninapopata fursa ya kuongea kuhusu Biblia, kama vile wakati wauguzi, wafanyabiashara au wengineo wanapotutembelea nyumbani, mimi huzungumza nao kwa busara.

Jambo lenye kuniridhisha zaidi ni kuona vizazi vinne katika familia yangu, wakimwabudu Yehova kwa uaminifu. Baadhi yao wamejitahidi kutumikia sehemu zenye uhitaji wakiwa mapainia, watumishi wa huduma au wazee, na katika utumishi wa Betheli. Bila shaka kama vile wengi wa kizazi changu, nilitazamia kwamba mwisho wa mfumo huu ungekuwa umefika kitambo. Lakini nimefurahia kuona ongezeko kubwa katika hiki kipindi cha miaka 70 ambayo nimetumia katika utumishi. Ninafurahi kwamba nimeshiriki katika kazi hii kubwa.

Wauguzi wanaonitembelea husema kwamba imani yangu imeniweka hai. Nami ninakubaliana nao. Kuwa na bidii katika utumishi wa Yehova huboresha maisha. Kwa kweli, ninaweza kusema kama Mfalme Daudi kwamba nimezeeka na kushiba siku.—1 Mambo ya Nyakati 29:28.

(Dada Muriel Smith alikufa Aprili 1, 2002, makala hii ilipokuwa ikikamilishwa. Alikuwa amebakisha mwezi mmoja tu afikishe umri wa miaka 102. Kwa kweli alikuwa kielelezo bora cha uaminifu na uvumilivu.)

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nilipokuwa na umri wa miaka mitano hivi na nikiwa na umri wa miaka 19, nilipoolewa na mume wangu, Roy

[Picha katika ukurasa wa 26]

Gari letu na trela tuliyoiita Mispa

[Picha katika ukurasa wa 27]

Nikiwa na mume wangu Roy, mwaka wa 1971